Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtu Aliye Mfano Bora Ambaye Alikubali Kusahihishwa

Mtu Aliye Mfano Bora Ambaye Alikubali Kusahihishwa

Mtu Aliye Mfano Bora Ambaye Alikubali Kusahihishwa

“MAMBA wa Zambia Hula Watu 30 kwa Mwezi.” Ndivyo gazeti moja la Afrika lilivyoripoti miaka kadhaa iliyopita. Kwa mujibu wa mtaalamu mmoja wa wanyama aliyewakamata mamba hao kwa ajili ya utafiti, “ilihitaji wanaume 12 kumshikilia chini mamba mmoja.” Akiwa na mkia na mataya yenye nguvu sana, mamba anaweza kuogofya sana!

Yaonekana kwa kumwita mamba “Leviathani,” Muumba alitumia huyu “mfalme juu ya mahayawani wote wakali” ili kumfundisha mtumishi wake Yobu somo muhimu. (Ayubu 41:1, 34, NW) Jambo hilo lilitukia miaka 3,500 hivi iliyopita nchini Usi, yaelekea mahali fulani kaskazini mwa Arabia. Akimfafanua kiumbe huyu, Mungu alimwambia Yobu: “Hapana aliye mkali hata akathubutu kumwamsha; bali ni nani awezaye kusimama mbele yangu mimi?” (Ayubu 41:10) Ni kweli kabisa! Ikiwa sisi humhofu mamba, yatupasa kuhofu hata zaidi kama nini kusema dhidi ya Yule aliyemwumba! Yobu alionyesha kwamba amethamini somo hilo kwa kuungama kosa lake.—Ayubu 42:1-6.

Yobu anapotajwa, huenda tukakumbuka mfano wake mwaminifu wa kuvumilia jaribu. (Yakobo 5:11) Kwa kweli, Yehova alimfurahia Yobu hata kabla ya imani yake kujaribiwa vikali. Kwa maoni ya Mungu, wakati huo ‘hapakuwa na mmoja aliye kama Ayubu duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.’ (Ayubu 1:8) Hilo lapasa kutuchochea tujifunze mengi zaidi juu ya Yobu, kwa kuwa kufanya hivyo kutatusaidia pia kuona jinsi tuwezavyo kumpendeza Mungu.

Alitanguliza Uhusiano Wake na Mungu

Yobu alikuwa tajiri. Mbali na dhahabu, alikuwa na kondoo 7,000, ngamia 3,000, punda-majike 500, ng’ombe 1,000, na watumishi wengi sana. (Ayubu 1:3) Lakini Yobu alimtumaini Yehova wala si mali. Alisababu hivi: “Ikiwa nimeifanya dhahabu kuwa tumaini langu, na kuiambia dhahabu safi, Wewe u tegemeo langu; kama nilifurahi kwa kuwa mali yangu yalikuwa mengi, na kwa sababu mkono wangu umepata vitu vingi; . . . hilo nalo lingekuwa uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; kwani ningemwambia uongo Mungu aliye juu.” (Ayubu 31:24-28) Kama Yobu, yatupasa kuthamini zaidi uhusiano wetu wa karibu na Yehova Mungu kuliko vitu vya kimwili.

Kuwatendea Wanadamu Wenzake kwa Haki

Yobu aliwatendeaje watumishi wake? Maneno ya Yobu mwenyewe yaonyesha kwamba wao walimwona kuwa mtu asiyebagua na mwenye kufikika: “Kama nimekataa kesi ya mtumishi wangu, wa kiume au wa kike, waliponiletea malalamiko yao, nitafanya nini basi Mungu atakaponikabili? Je, akinichunguza nitamjibu nini?” (Yobu 31:13, 14, Biblia Habari Njema) Yobu alithamini rehema ya Yehova na hivyo akawarehemu watumwa wake. Ni mfano bora kama nini, hata kwa wale walio na nyadhifa za uangalizi katika kutaniko la Kikristo! Ni lazima pia wao wawe wenye haki, wasiobagua, na wenye kufikika.

Yobu alipendezwa pia na wengine wasiokuwa wa nyumbani kwake. Akionyesha kuwahangaikia wengine, yeye alisema: “Ikiwa nimewanyima maskini haja zao, au kama nimeyatia kiwi macho ya mwanamke mjane; . . . ikiwa nimewainulia mayatima mkono, nilipoona msaada wangu langoni; basi bega langu na lianguke kutoka mahali pake, na mkono wangu uvunjike mfupani mwake.” (Ayubu 31:16-22) Na tuwe wenye kuwafikiria wenye shida tunaowajua katika kutaniko.

Kwa kuwa alipendezwa bila ubinafsi na wengine, Yobu alikaribisha wageni. Hivyo, angeweza kusema: “Mgeni hakulala njiani; lakini nilimfungulia msafiri milango yangu.” (Ayubu 31:32) Huo ni mfano bora kama nini kwa watumishi wa Mungu leo! Wakati wale ambao wamependezwa na kweli ya Biblia karibuni wanapokuja kwenye Jumba la Ufalme, kuwakaribisha vizuri kwaweza kuchangia maendeleo yao ya kiroho. Bila shaka, twahitaji pia kuwakaribisha kwa upendo waangalizi wasafirio na Wakristo wengine.—1 Petro 4:9; 3 Yohana 5-8.

Yobu alikuwa na mtazamo ufaao hata kwa adui zake. Hakufurahia msiba ambao ungempata mtu mwenye kumchukia. (Ayubu 31:29, 30) Badala yake, alikuwa tayari kuwafanyia mema watu kama hao, kama inavyoonyeshwa na utayari wake wa kusali kwa ajili ya wafariji wake watatu wasio wa kweli.—Ayubu 16:2; 42:8, 9; linganisha Mathayo 5:43-48.

Alikuwa Safi Kingono

Yobu alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa mwenzi wake wa ndoa, asiruhusu kamwe moyo wake usitawishe urafiki usiofaa na mwanamke mwingine. Yobu alisema: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana? Kama moyo wangu ulishawishwa kwa mwanamke, nami nimeotea mlangoni pa jirani yangu; ndipo hapo mke wangu na asage kwa mwingine, na wengine na wainame juu yake. Kwani hilo lingekuwa kosa kuu; naam, lingekuwa ni uovu wa kuadhibiwa na waamuzi.”—Ayubu 31:1, 9-11.

Yobu hakuruhusu tamaa zisizo za adili zifisidi moyo wake. Badala yake, alifuatia mwenendo mnyofu. Si ajabu kwamba Yehova Mungu alimfurahia mtu huyu mwaminifu ambaye alipinga vishawishi vya ukosefu wa adili!—Mathayo 5:27-30.

Alihangaikia Hali ya Kiroho ya Familia

Nyakati nyingine, wana wa Yobu walitayarisha karamu ambazo wana wake wote na binti zake wote walihudhuria. Baada ya siku hizo za karamu kwisha, Yobu alihangaika sana isije ikawa watoto wake walitenda dhambi dhidi ya Yehova kwa njia fulani. Hivyo Yobu alichukua hatua kwa kuwa simulizi la Kimaandiko lasema: “Basi ilikuwa, hapo hizo siku za karamu zao zilipokuwa zimetimia, Ayubu hutuma kwao akawatakasa, kisha akaamka asubuhi na mapema, na kusongeza sadaka za kuteketezwa kama hesabu yao wote ilivyokuwa; kwani Ayubu alisema, Yumkini kwamba hawa wanangu wamefanya dhambi, na kumkufuru Mungu mioyoni mwao.” (Ayubu 1:4, 5) Jinsi jambo hilo lilivyokazia mioyoni mwa washiriki wa familia ya Yobu hangaiko lake kwamba wawe na hofu yenye staha kwa Yehova na kutembea katika njia Zake!

Leo, vichwa vya familia za Kikristo wahitaji kufundisha familia zao Neno la Mungu, Biblia. (1 Timotheo 5:8) Na kwa hakika inafaa kusali kwa ajili ya washiriki wa familia.—Waroma 12:12.

Alivumilia kwa Uaminifu Chini ya Jaribu

Wasomaji wengi wa Biblia wanafahamu majaribu makali yaliyompata Yobu. Shetani Ibilisi alidai kwamba chini ya majaribu Yobu angemlaani Mungu. Yehova alikubali mwito huo wa ushindani, na bila kukawia Shetani akamletea Yobu msiba. Akapoteza mifugo yake yote. Na jambo baya hata zaidi, watoto wake wote wakafa. Muda mfupi baadaye, Shetani akampiga Yobu kwa majipu yenye madhara toka kichwani hadi miguuni.—Ayubu, sura ya 1, 2.

Matokeo yakawa nini? Mke wake alipomsihi amlaani Mungu, Yobu alisema: “Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya?” Rekodi ya Biblia yaongeza kusema: “Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.” (Ayubu 2:10) Naam, Yobu alivumilia kwa uaminifu na hivyo akamthibitisha Ibilisi kuwa mwongo. Na tuvumilie majaribu vivyo hivyo na kuthibitisha kwamba utumishi wetu kwa Mungu huchochewa tu na upendo wetu kwa Yehova.— Mathayo 22:36-38.

Alikubali kwa Unyenyekevu Kusahihishwa

Ingawa Yobu alikuwa mfano bora katika njia nyingi, yeye hakuwa mkamilifu. Yeye mwenyewe alisema: “Ni nani awezaye kutoa kitu kilicho safi kitoke katika kitu kichafu? hapana awezaye.” (Ayubu 14:4; Waroma 5:12) Hivyo Mungu aliposema kwamba Yobu ni mkamilifu, jambo hilo lilikuwa kweli katika maana ya kwamba alitimiza yote ambayo Mungu alitarajia kutoka kwa mmojawapo wa watumishi wake wa kibinadamu wasiokamilika. Hicho ni kitia-moyo kilichoje!

Yobu alivumilia jaribu lake, lakini likafunua udhaifu fulani. Waliposikia msiba uliompata, watu watatu waitwao eti wafariji wakamtembelea. (Ayubu 2:11-13) Walidai kwamba Yehova anamwadhibu Yobu kwa kutenda dhambi nzito. Bila shaka, Yobu aliumia kutokana na mashtaka hayo yasiyo ya kweli, naye akajaribu kujitetea vikali. Lakini akakosa usawaziko katika jambo hilo. Kwani, Yobu hata alidokeza kwamba alikuwa mwadilifu kuliko Mungu!—Ayubu 35:2, 3.

Kwa sababu Mungu alimpenda Yobu, Yeye alitumia mwanamume kijana kumwonyesha kosa lake. Simulizi hilo lasema: “Ndipo zikawaka hasira za huyo Elihu . . . juu ya Ayubu, kwa sababu alikuwa amejipa haki mwenyewe zaidi ya Mungu.” Kama Elihu alivyosema: “Ayubu amesema, Mimi ni mwenye haki, naye Mungu ameniondolea haki yangu.” (Ayubu 32:2; 34:5) Hata hivyo, Elihu hakujiunga na hao “wafariji” watatu katika kukata kauli kimakosa kwamba Mungu alikuwa akimwadhibu Yobu kwa dhambi zake. Badala yake Elihu alikuwa na uhakika katika uaminifu wa Yobu na kumshauri: “Kesi yako iko mbele ya [Yehova] na wewe unamngojea!” Kwa kweli Yobu alipaswa kumngojea Yehova badala ya kusema bila kufikiri akijitetea. Elihu alimhakikishia Yobu: “[Mungu] amejaa wema wala hapotoshi haki kamwe.”—Yobu 35:14; 37:23, BHN.

Maoni ya Yobu yalihitaji kusahihishwa. Hivyo, Yehova akamfunza somo juu ya uduni wa mwanadamu kwa kulinganishwa na ukuu wa Mungu. Yehova alitaja dunia, bahari, anga yenye nyota, wanyama, na maajabu mengine ya uumbaji. Hatimaye, Mungu akataja Leviathani—mamba. Kwa kukubali kwa unyenyekevu kusahihishwa, Yobu anaweka mfano zaidi.

Ingawa huenda tunafanya vizuri katika utumishi wa Yehova, tutafanya makosa. Likiwa kosa zito, Yehova anaweza kutusahihisha kwa njia fulani. (Mithali 3:11, 12) Huenda tukakumbuka andiko lenye kuchoma dhamiri yetu. Huenda Mnara wa Mlinzi au kichapo kingine cha Watch Tower Society kikasema jambo linalotuonyesha kosa. Au inawezekana Mkristo mwenzetu atatuonyesha kwa fadhili kwamba tumekosa kutumia kanuni fulani ya Biblia. Tutaitikiaje sahihisho hilo? Yobu alionyesha majuto, akisema: “Najichukia nafsi yangu, na kutubu katika mavumbi na majivu.”—Ayubu 42:6.

Alithawabishwa na Yehova

Yehova alimthawabisha Yobu, akimruhusu mtumishi wake aishi kwa miaka mingine 140. Wakati huo, alipokea mali nyingi zaidi ya ile aliyopoteza. Na ingawa Yobu alikufa hatimaye, hapana shaka kwamba atafufuliwa kwenye ulimwengu mpya wa Mungu.—Ayubu 42:12-17; Ezekieli 14:14; Yohana 5:28, 29; 2 Petro 3:13.

Sisi pia tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atatupendelea na kutubariki tukimtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu na kukubali masahihisho yenye kutegemea Biblia tuwezayo kupata. Hivyo, tutakuwa na tumaini hakika la kupata uhai katika mfumo mpya wa mambo wa Mungu. Jambo muhimu zaidi ni kwamba tutamheshimu Mungu. Mwenendo wetu wa uaminifu utathawabishwa na utakuwa uthibitisho zaidi kwamba watu wake humtumikia kwa sababu wanampenda kwa moyo wote wala si kwa sababu za kibinafsi. Tuna pendeleo lililoje kufurahisha moyo wa Yehova kama Yobu mwaminifu ambaye alikubali kwa unyenyekevu kusahihishwa!—Mithali 27:11.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yobu aliwahangaikia kwa upendo mayatima, wajane, na watu wengineo

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yobu alithawabishwa sana kwa kukubali kwa unyenyekevu kusahihishwa