Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Biblia Ina Ujumbe wa Siri?

Je, Biblia Ina Ujumbe wa Siri?

Je, Biblia Ina Ujumbe wa Siri?

MIAKA miwili hivi baada ya Waziri Mkuu wa Israeli Yitzhak Rabin kuuawa mwaka wa 1995, mwandishi mmoja wa habari alidai kwamba kwa kutumia kompyuta amegundua utabiri wa mauaji hayo ukiwa umefichika katika maandishi ya awali ya Kiebrania ya Biblia. Mwandishi huyo, Michael Drosnin, aliandika kwamba alijaribu kumwonya waziri huyo mkuu kwa kipindi kinachozidi mwaka mmoja kwamba angeuawa lakini hakusikiliza.

Vitabu vingine na makala nyingine ambazo zimechapishwa zinadai kwamba ujumbe huo wa siri una uthibitisho kamili kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu. Je, kuna ujumbe kama huo? Je, ujumbe wa siri uwe msingi wa kuamini kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu?

Je, Ni Wazo Jipya?

Wazo la kwamba kuna ujumbe wa siri katika maandishi ya Biblia si jipya. Ndilo wazo kuu la Kabala, au mapokeo ya mafumbo ya Kiyahudi. Kulingana na walimu wa Kabala, yale yanayoonekana kuwa maana ya maandishi ya Biblia kumbe si maana ya kweli. Wanaamini kwamba Mungu alitumia herufi moja-moja za maandishi ya Biblia ya Kiebrania kama ishara ambazo zikieleweka vizuri zinatokeza kweli kubwa. Kwa maoni yao, kila herufi ya Kiebrania na mahali pake katika maandishi ya Biblia iliwekwa na Mungu kwa kusudi fulani hususa.

Kulingana na Jeffrey Satinover, mtafiti mmoja wa ujumbe huo wa siri wa Biblia, Wayahudi hao wa mafumbo huamini kwamba herufi za Kiebrania zilizotumiwa kuandika masimulizi ya uumbaji katika Mwanzo zina nguvu nyingi sana za mafumbo. Yeye aandika: “Kwa kifupi, kitabu cha Mwanzo si ufafanuzi tu; ndicho chombo hasa cha uumbaji wenyewe, mfano halisi wa akili ya Mungu ikionyeshwa katika hali halisi.”

Rabi mmoja wa karne ya 13 wa Kabala, Bachya ben Asher wa Saragossa, Hispania, aliandika juu ya herufi za siri ambazo alifunuliwa aliposoma kila herufi ya 42 katika sehemu fulani ya kitabu cha Mwanzo. Njia hiyo ya kuruka herufi kwa kufuata utaratibu fulani eti kugundua ujumbe wa siri ndiyo msingi wa wazo la kisasa la ujumbe wa siri wa Biblia.

Kompyuta “Zafunua” Ujumbe Huo

Kabla ya enzi ya kutumia kompyuta, mwanadamu hakuwa na uwezo wa kuchunguza vizuri maandishi ya Biblia kwa njia hiyo. Lakini, Agosti 1994, jarida moja la Statistical Science lilichapisha makala moja ambamo Eliyahu Rips wa chuo cha Jerusalem’s Hebrew University na watafiti wenzake walitokeza madai yaliyoshangaza sana. Walieleza kwamba kwa kuondoa nafasi zote zilizoko kati ya herufi na kuruka idadi ileile ya herufi za maandishi ya Kiebrania ya kitabu cha Mwanzo, waligundua majina 34 ya marabi mashuhuri yakiwa ndani ya maandishi hayo, pamoja na habari nyinginezo, kama vile tarehe zao za kuzaliwa au kifo, zikiwa karibu na majina yao. * Baada ya kufanya majaribio mara nyingi, watafiti hao walichapisha uamuzi wao kwamba habari iliyotiwa kwenye Mwanzo haingeweza kutukia tu yenyewe—hiyo ikiwa uthibitisho wa habari iliyopuliziwa ambayo ilifichwa kwa makusudi iwe siri katika kitabu cha Mwanzo maelfu ya miaka iliyopita.

Akitumia njia hiyo, mwandishi wa habari, Drosnin, alifanya majaribio yake mwenyewe, akitafuta habari ya siri katika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia ya Kiebrania. Kulingana na Drosnin, alipata jina la Yitzhak Rabin katika maandishi ya Biblia kwa utaratibu wa kuruka kila herufi 4,772. Akiwa amepanga maandishi ya Biblia kwa mistari yenye herufi 4,772 kila mmoja, aliona jina la Rabin (likisomwa kuelekea chini) likipitana na mstari mmoja (Kumbukumbu la Torati 4:42, unaoelekea upande) ambao Drosnin aliufasiri kuwa “muuaji ambaye ataua.”

Kumbukumbu la Torati 4:42 hasa linazungumzia mtu aliyeua bila kukusudia. Kwa hiyo wengi wamechambua mbinu ya Drosnin isiyo na msingi, wakidai kwamba mbinu zake zisizo za kisayansi zinaweza kutumiwa kupata ujumbe mwingine wowote kama huo katika maandishi yoyote. Lakini Drosnin alijitetea, akisema: “Wale wanaonichambua wakipata ujumbe unaohusu kuuawa kwa Waziri Mkuu katika [kitabu] Moby Dick, nitakubaliana nao.”

Je, Ni Uthibitisho wa Upulizio?

Profesa Brendan McKay, wa Idara ya Sayansi ya Kompyuta katika Chuo Kikuu cha Australia, alikubali mwito wa Drosnin, akatumia kompyuta sana kuchunguza maandishi ya Kiingereza ya kitabu Moby Dick. * Akitumia ile mbinu iliyotajwa na Drosnin, McKay adai kwamba alipata “matabiri” ya kuuawa kwa Indira Gandhi, Martin Luther King, Jr., John F. Kennedy, Abraham Lincoln, na wengineo. Kulingana na McKay, aligundua kwamba Moby Dick pia “ilitabiri” kuuawa kwa Yitzhak Rabin.

Akirudia maandishi ya Kiebrania ya Mwanzo, Profesa McKay na wenzake pia wamepinga matokeo ya majaribio ya Rips na wenzake. Walidai kwamba matokeo hayategemei ule ujumbe wa siri bali wategemea mbinu za utafiti za watafiti hao—watafiti wenyewe wakihusika hasa kwa kuingiza habari wanazotaka. Mjadala wa wasomi juu ya jambo hili waendelea.

Suala jingine lazuka wakati ambapo madai yanafanywa kwamba ujumbe kama huo wa siri ulifichwa kimakusudi katika maandishi “sanifu” au “ya awali” ya Kiebrania. Rips na watafiti wenzake wasema kwamba walifanya utafiti wakitumia “maandishi sanifu yaliyokubaliwa ya [kitabu cha] Mwanzo.” Drosnin aandika: “Biblia zote katika lugha ya awali ya Kiebrania ambazo zinapatikana sasa zinafanana herufi kwa herufi.” Lakini, je, kweli zinafanana? Mbali na maandishi “sanifu,” aina kadhaa za Biblia ya Kiebrania zinatumiwa leo, zikitegemea hati-kunjo tofauti-tofauti za kale. Ingawa ujumbe wa Biblia hautofautiani, hati-kunjo za awali hazifanani herufi kwa herufi.

Tafsiri nyingi leo zinategemea Kodeksi ya Leningrad—ambayo ni hati-kunjo ya Kiebrania ya Wamasora iliyo kamili na ya kale zaidi—iliyonakiliwa wapata mwaka wa 1000 W.K. Lakini Rips na Drosnin walitumia maandishi tofauti, yale ya Koren. Shlomo Sternberg, rabi wa Othodoksi aliye pia mtaalamu wa hesabu katika Chuo Kikuu cha Harvard, aeleza kwamba Kodeksi ya Leningrad “yatofautiana na chapa ya Koren iliyotumiwa na Drosnin kwa herufi 41 katika Kumbukumbu la Torati pekee.” Hati-kunjo za Bahari ya Chumvi zinatia ndani sehemu za maandishi ya Biblia zilizonakiliwa zaidi ya miaka 2,000 iliyopita. Mara nyingi mwendelezo wa maneno katika hati-kunjo hizo hutofautiana sana na maandishi ya baadaye ya Wamasora. Katika baadhi ya hati-kunjo hizo, herufi ziliongezwa kwa wingi ili kuonyesha sauti za irabu, kwa kuwa herufi za irabu hazikuwa zimevumbuliwa. Katika hati-kunjo nyinginezo, herufi chache zilitumiwa. Ulinganishi wa hati-kunjo zote za Biblia zilizoko waonyesha kwamba maana ya maandishi ya Biblia haijabadilika. Lakini ulinganishi huo pia unaonyesha waziwazi kwamba mwendelezo na idadi ya herufi zatofautiana kati ya hati-kunjo hizo.

Kutafuta ule unaosemekana kuwa ujumbe wa siri kwategemea maandishi yasiyobadilika kabisa. Badiliko la neno moja tu laweza kuharibu kabisa ule utaratibu—na ujumbe wowote ambao ungekuwapo. Mungu amehifadhi ujumbe wake kupitia Biblia. Lakini hajahifadhi kila herufi ikiwa vilevile, kana kwamba yuazingatia sana mambo madogo-madogo kama mabadiliko ya mwendelezo katika karne zilizopita. Je, jambo hilo halionyeshi kwamba hajaficha ujumbe fulani wa siri katika Biblia?—Isaya 40:8; 1 Petro 1:24, 25.

Je, Tunahitaji Ujumbe wa Siri Katika Biblia?

Mtume Paulo aliandika wazi kwamba “andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Si vigumu kutumia wala kuelewa ujumbe rahisi na wa wazi ulio katika Biblia, lakini watu wengi huamua kuupuuza. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Unabii ambao unatolewa wazi katika Biblia ni msingi imara wa kuamini upulizio wake. * Tofauti na ujumbe wa siri, unabii wa Biblia hautegemei maoni ya mtu, na ‘hauchipuki kutokana na fasiri yoyote ya faragha.’—2 Petro 1:19-21.

Mtume Petro aliandika kwamba “haikuwa kwa kufuata hadithi zisizo za kweli zilizotungwa kwa usanifu mwingi kwamba tuliwafahamisha nyinyi juu ya nguvu na kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:16) Wazo la ujumbe wa siri wa Biblia lilianzishwa na mafumbo ya Kiyahudi, yakitumia mbinu “zilizotungwa kwa usanifu” zinazoficha na kupotosha maana ya wazi ya maandishi yaliyopuliziwa ya Biblia. Maandiko yenyewe ya Kiebrania yalishutumu waziwazi utumizi kama huo wa mafumbo.—Kumbukumbu la Torati 13:1-5; 18:9-13.

Tuna furaha iliyoje kuwa na ujumbe wa wazi wa Biblia na mafundisho yake, ambao unaweza kutusaidia kumjua Mungu! Huo unafaa zaidi kuliko kujaribu kujifunza juu ya Muumba kwa kutafuta ujumbe wa siri ambao unatokezwa na fasiri ya faragha na mawazo yenye kutegemea utumizi wa kompyuta.—Mathayo 7:24, 25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Katika Kiebrania, tarakimu zaweza kuandikwa kwa kutumia herufi. Kwa hiyo, tarehe hizo ziliamuliwa kwa kutumia herufi katika maandishi ya Kiebrania badala ya tarakimu.

^ fu. 13 Lugha ya Kiebrania haina irabu. Irabu huingizwa na msomaji kulingana na muktadha. Muktadha ukipuuzwa, maana ya neno yaweza kubadilishwa kabisa kwa kuingiza irabu tofauti. Kiingereza kina irabu zisizobadilika, jambo linalofanya uchunguzi kama huo uwe mgumu sana.

^ fu. 19 Kwa habari zaidi juu ya upulizio wa Biblia na unabii wake, ona broshua ya Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.