Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Roho ya Mungu Hutendaje Kazi Leo?

Roho ya Mungu Hutendaje Kazi Leo?

Roho ya Mungu Hutendaje Kazi Leo?

ALIKUWA mlemavu tangu kuzaliwa. Aliketi kila siku kwenye lango liitwalo Mzuri la hekalu ili apate zawadi za rehema kutoka kwa wale waliokuwa wakiingia hekaluni. Lakini wakati mmoja, mwombaji huyu kilema akapokea zawadi yenye thamani kubwa zaidi kushinda sarafu chache ndogo. Aliponywa!—Matendo 3:2-8.

Ingawa mitume Petro na Yohana ndio ‘waliomwinua’ hivi kwamba ‘miguu yake ikafanywa imara,’ wao hawakutaka wasifiwe kwa uponyaji huo. Kwa nini? Petro mwenyewe alieleza: “Wanaume wa Israeli, kwa nini mnastaajabu juu ya hili, au kwa nini mnatukodolea macho kama kwamba kwa nguvu ya binafsi au ujitoaji-kimungu tumemfanya atembee?” Kwa kweli, Petro na Yohana walitambua kwamba si kwa uwezo wao bali ni kwa roho takatifu ya Mungu kwamba wangeweza kufanya jambo kama hilo.—Matendo 3:7-16; 4:29-31.

Wakati huo, ‘kazi hizo zenye nguvu’ zilifanywa ili kuonyesha kwamba Mungu aliliunga mkono kutaniko jipya la Kikristo. (Waebrania 2:4) Lakini baada ya kutimiza kusudi lake, kazi hizo ‘zingeondolewa mbali,’ akasema mtume Paulo. * (1 Wakorintho 13:8) Hivyo, katika kutaniko la kweli la Kikristo sasa, hakuna maponyo yaliyoagizwa rasmi na Mungu wala ujumbe wa unabii wala utoaji wa roho waovu.

Je, hilo lamaanisha kwamba roho takatifu ya Mungu haitendi kazi tena? La, hasha! Ebu tuone njia nyingine ambazo roho ya Mungu ilitenda kazi katika karne ya kwanza na kutenda kazi katika wakati wetu.

“Roho ya Ile Kweli”

Utendaji mmoja wa roho takatifu ya Mungu ni kujulisha, kuelimisha, na kufunua kweli. Punde tu kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nina mambo mengi ya kuwaambia nyinyi, lakini hamwezi kuyahimili wakati wa sasa. Hata hivyo, wakati huyo awasilipo, roho ya ile kweli, atawaongoza nyinyi ndani ya kweli yote.”—Yohana 16:12, 13.

“Roho ya ile kweli” ilimwagwa siku ya Pentekoste 33 W.K. wakati wanafunzi wapatao 120 waliokusanyika katika chumba cha juu huko Yerusalemu walipobatizwa kwa roho takatifu. (Matendo 2:1-4) Mtume Petro alikuwa miongoni mwa wale waliokuwapo kwa ajili ya msherehekeo huo wa kila mwaka. Akiwa amejawa na roho takatifu, Petro ‘alisimama’ na kufafanua au kubainisha kweli fulani juu ya Yesu. Kwa mfano, alisimulia jinsi “Yesu Mnazareti” “ali[vyo]kwezwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” (Matendo 2:14, 22, 33) Roho ya Mungu pia ilimchochea Petro awatangazie kwa ujasiri Wayahudi waliomsikiliza: “Acha nyumba yote ya Israeli ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana na pia Kristo, Yesu huyu ambaye nyinyi mlimtundika mtini.” (Matendo 2:36) Kwa sababu ya ujumbe wa Petro wenye kupuliziwa kwa roho, watu wapatao elfu tatu ‘walikubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo’ na kubatizwa. Kwa njia hiyo, roho takatifu ya Mungu ikasaidia kuwaongoza kwenye kweli.—Matendo 2:37-41.

Roho takatifu ya Mungu pia ilitenda kazi kama mwalimu na mkumbushaji. Yesu alisema: “Msaidiaji, roho takatifu, ambayo Baba atapeleka katika jina langu, hiyo itawafundisha nyinyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.”—Yohana 14:26.

Roho takatifu ilitendaje kazi kama mwalimu? Roho ya Mungu iliwawezesha wanafunzi kuelewa mambo ambayo Yesu alikuwa amewaambia hapo awali ijapokuwa hawakuyaelewa kikamili. Kwa mfano, mitume walijua kwamba wakati wa kesi yake, Yesu alimwambia hivi gavana wa Yudea, Pontio Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” Lakini Yesu alipoenda mbinguni, zaidi ya siku 40 baadaye, bado mitume walikuwa na maoni yenye makosa kwamba Ufalme ungesimamishwa hapa duniani. (Yohana 18:36; Matendo 1:6) Yaonekana mitume hawakuweza kufahamu kikamili maana ya maneno ya Yesu hadi baada ya kumwagwa kwa roho takatifu ya Mungu siku ya Pentekoste 33 W.K.

Roho ya Mungu pia ilitenda kazi kama mkumbushaji kwa kuwakumbusha mafundisho mbalimbali ya Yesu. Kwa mfano, roho takatifu iliwasaidia kuelewa upya unabii kuhusu kifo na ufufuo wa Kristo. (Mathayo 16:21; Yohana 12:16) Kukumbuka mafundisho ya Yesu kuliwawezesha mitume kutetea kwa ujasiri msimamo wao mbele ya wafalme, mahakimu, na viongozi wa kidini.—Marko 13:9-11; Matendo 4:5-20.

Kwa kuongezea, roho takatifu ya Mungu iliwasaidia Wakristo wa mapema katika huduma kwa kuwaelekeza kwenye maeneo yenye matokeo. (Matendo 16:6-10) Roho ya Mungu pia iliwachochea Wakristo wa mapema washiriki kuandika Neno la Mungu, Biblia, kwa manufaa ya wanadamu wote. (2 Timotheo 3:16) Basi, ni wazi kwamba roho takatifu ilitenda kazi kwa njia tofauti-tofauti katika karne ya kwanza. Haikutolewa ili kufanya miujiza peke yake.

Roho Takatifu Leo

Roho takatifu pia imekuwa ikifanya kazi kwa niaba ya Wakristo wa kweli leo. Jambo hilo lilidhihirika kwa kikundi kidogo cha wanafunzi wa Biblia huko Allegheny, Pennsylvania, Marekani, kuelekea mwishoni mwa karne ya 19. Wanafunzi hao wa Biblia wenye bidii walitaka sana kuijua “kweli.”—Yohana 8:32; 16:13.

Mshiriki mmoja wa kikundi hicho, Charles Taze Russell, alisema hivi juu ya utafutaji wake wa kweli ya Maandiko: “Nilisali . . . ili niwezeshwe kuondoa moyoni mwangu na akilini mwangu maoni yoyote yawezayo kuwa kizuizi na kusali niongozwe na roho yake kupata uelewevu ufaao.” Mungu alijibu sala hiyo ya unyenyekevu.

Russell na wenzake walifahamu mambo kadhaa walipoyachunguza Maandiko kwa bidii. “Tuligundua kwamba kwa karne nyingi,” akaeleza Russell, “madhehebu na makundi mbalimbali yalikuwa yamegawana mafundisho ya Biblia na kuyachanganya na makisio na makosa ya wanadamu.” Jambo hilo lilitokeza kile alichokiita “kupotoshwa kwa ile kweli.” Kweli za Maandiko zilifichwa katika mafundisho mengi ya kipagani ambayo kwa karne nyingi yalipenya katika Jumuiya ya Wakristo. Lakini Russell aliazimia kuijua kweli na kuitangaza.

Kupitia gazeti la Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, Russell na wenzake waliyashutumu kwa ujasiri mafundisho ya kidini yaliyomwasilisha Mungu vibaya. Walitambua kwamba—tofauti na maoni ya kidini yanayopendwa sana—nafsi inaweza kufa, na kwamba tunapokufa sisi huenda kaburini, na kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli na hivyo yeye si sehemu ya Utatu.

Hata hivyo, kama uwezavyo kutarajia, kufichuliwa kwa mafundisho ya uwongo kuliwakasirisha makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Wakiwa na hamu ya kubaki kwenye vyeo vyao mashuhuri, makasisi wengi wa Kikatoliki na wa Kiprotestanti walipanga kampeni zenye lengo la kumwaibisha Russell. Lakini yeye na wenzake hawakuacha ufichuaji huo. Waliitegemea roho ya Mungu iwaongoze wakiwa na uhakika. “Uhakikisho wa Bwana wetu,” akasema Russell, “ni kwamba . . . roho takatifu ya Baba, iliyotumwa kutokana na maombi ya Yesu aliye Mkombozi, Mpatanishi na Kichwa chetu, itakuwa mfunzi wetu.” Na bila shaka iliwafundisha! Wanafunzi hao wa Biblia wenye mioyo myeupe waliendelea kutumia maji safi ya kweli ya Biblia na kuyatangaza ulimwenguni pote.—Ufunuo 22:17.

Tengenezo la siku hizi la Mashahidi wa Yehova limeendelea kuitikia kwa utayari mwongozo wa roho takatifu ya Mungu kwa muda unaozidi karne moja sasa. Roho ya Yehova iangazapo hatua kwa hatua ufahamu wao wa kiroho, Mashahidi hufanya kwa hiari marekebisho yanayohitajika ili kujipatanisha na uelewevu mpya.—Mithali 4:18.

“Mtakuwa Mashahidi Wangu”

Yesu alitambulisha udhihirisho mwingine pia wa roho takatifu ya Mungu alipowaambia wanafunzi wake: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu iwasilipo juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8) Ahadi ya Yesu ya kuwapa wanafunzi wake “nguvu” na “roho takatifu” ili watekeleze kazi waliyopewa na Mungu bado inatimizwa leo.

Wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa kazi yao ya kuhubiri. (Ona sanduku.) Kwa kweli Mashahidi wa Yehova hutangaza ujumbe wa ile kweli katika nchi na visiwa zaidi ya 230. Wao hutetea kwa ujasiri Ufalme wa Mungu chini ya hali zozote zile, kutia ndani kuhatarisha maisha yao katika maeneo yaliyoharibiwa na vita. Bidii yao kwa ajili ya huduma ya Kikristo hutoa uthibitisho wenye nguvu kwamba roho takatifu inatenda kazi leo. Na ni wazi kwamba Yehova Mungu anabariki jitihada zao.

Kwa mfano, mwaka uliopita walitumia muda wa saa zaidi ya bilioni moja kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kukiwa na matokeo gani? Watu wapatao 323,439 walionyesha wakfu wao kwa Mungu kwa kujitoa ili kubatizwa kwa maji. Kwa kuongezea, mafunzo ya Biblia nyumbani 4,433,884 yaliongozwa kila juma pamoja na wale waliopendezwa karibuni. Kwa ujumla, vitabu 24,607,741, magazeti 631,162,309, na broshua na vijitabu 63,495,728 viligawanywa. Huo ni uthibitisho wenye nguvu kama nini wa utendaji wa roho ya Mungu!

Roho ya Mungu na Wewe

Mtu akiitikia habari njema ifaavyo, apatanishe maisha yake na viwango vya Mungu, na kuonyesha imani katika fidia iliyoandaliwa, anapata fursa ya kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Paulo aliwaambia hivi watu kama hao: ‘Mungu hutia roho takatifu yake ndani yenu.’—1 Wathesalonike 4:7, 8; 1 Wakorintho 6:9-11.

Kuwa na roho ya Mungu hutokeza baraka nyingi nzuri. Baraka za aina gani? Jambo moja ni kwamba, Neno la Mungu lililopuliziwa lasema: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, [na] kujidhibiti.” (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo, roho takatifu ya Mungu ni kani yenye nguvu inayonufaisha, ikimwezesha mtu kudhihirisha sifa za kimungu.

Kwa kuongezea, ukijifunza Biblia na kutenda unayojifunza, roho ya Mungu inaweza kukusaidia usitawishe hekima, ujuzi, ufahamu wenye kina, uwezo wa kufanya maamuzi, na uwezo wa kufikiri. Mfalme Solomoni alipokea “hekima, na akili nyingi sana, na moyo mkuu” kwa sababu alitaka kumfurahisha Mungu badala ya wanadamu. (1 Wafalme 4:29) Kwa kuwa Yehova alimpa Solomoni roho takatifu, bila shaka yeye hatawanyima roho takatifu wale wanaotaka kumfurahisha leo.

Roho takatifu ya Mungu pia huwasaidia Wakristo leo kupambana na Shetani na roho waovu, mfumo huu mwovu wa mambo, na maelekeo ya mwili wao usio mkamilifu ya kutenda dhambi. Hilo linawezekanaje? Mtume Paulo ajibu: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Wafilipi 4:13) Huenda roho takatifu isiondoe majaribu au vishawishi; lakini inaweza kukusaidia uyavumilie. Tukiitegemea roho ya Mungu, tunaweza kupokea “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili kupambana na shida au taabu zozote zile.—2 Wakorintho 4:7; 1 Wakorintho 10:13.

Ukifikiria uthibitisho wote huo, hapana shaka kwamba roho takatifu ya Mungu inatenda kazi leo. Roho ya Yehova huwatia nguvu watumishi wake kutoa ushahidi juu ya makusudi yake matukufu. Hiyo huendelea kuangaza nuru ya kiroho, na kutia imani yetu nguvu, ikitusaidia tuendelee kuwa waaminifu-washikamanifu kwa Muumba wetu. Tu wenye shukrani kama nini kwamba Mungu ametimiza ahadi yake kwa kuwapa watumishi wake waaminifu leo roho takatifu!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona makala “Why Have the Miraculous Gifts of the Spirit Ceased?” katika Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1971, ukurasa wa 501-505, la Kiingereza.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Maoni ya Wengine Kuhusu Mashahidi wa Yehova

“Ingawa makanisa mengine huajiri washauri kusudi wawashawishi watu kwenda kanisani au wapambane na masuala ya siku hizi kama ugoni-jinsia-moja na utoaji-mimba, Mashahidi hawaridhiani na ulimwengu unaobadilika. Bado wanafanya kampeni ya kuhubiri Duniani pote.”—The Orange County Register la Orange County, California, Marekani.

“Kwa habari ya kueneza imani, ni madhehebu machache yaliyo na bidii . . . kama ya Mashahidi wa Yehova.”—The Republic la Columbus, Indiana, Marekani.

“Wao peke yao ndio wanaohubiri ‘habari njema’ nyumba hadi nyumba na kutekeleza kanuni za Biblia.”—Życie Literackie, Poland.

“Katika kampeni kubwa zaidi ya kuhubiri ambayo imewahi kufanywa, Mashahidi wa Yehova wamepeleka ujumbe wa Yehova ulimwenguni pote.”—News-Observer, Tamaqua, Pennsylvania, Marekani.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Roho takatifu ya Mungu hutuelimisha kiroho,

. . . hukuza sifa bora za Kikristo,

. . . na hututegemeza katika kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri