Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waaminifu na Wenye Ujasiri-Japo Mnyanyaso wa Nazi

Waaminifu na Wenye Ujasiri-Japo Mnyanyaso wa Nazi

Waaminifu na Wenye Ujasiri-Japo Mnyanyaso wa Nazi

Mnamo Juni 17, 1946, Malkia Wilhelmina wa Uholanzi aliipelekea risala za rambirambi familia moja ya Mashahidi wa Yehova jijini Amsterdam. Alipeleka risala hizo kwa sababu alivutiwa na mwana wa familia hiyo, Jacob van Bennekom, ambaye aliuawa na wafuasi wa Nazi wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Miaka kadhaa awali, baraza la mji wa Doetinchem, ambao uko upande wa mashariki wa Uholanzi, liliamua kuipa barabara moja jina la Bernard Polman, aliyekuwa pia Shahidi wa Yehova ambaye aliuawa wakati wa vita hiyo.

KWA nini wafuasi wa Nazi waliwanyanyasa Jacob, Bernard, na Mashahidi wa Yehova wengine nchini Uholanzi wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili? Na ni nini kilichowawezesha Mashahidi hao waendelee kuwa waaminifu japo mnyanyaso mkatili wa miaka mingi na hatimaye kupata heshima na staha ya malkia na wananchi wenzao? Ili tupate jibu, ebu tupitie matukio fulani yaliyosababisha mapambano hayo, yaliyo kama yale ya Daudi na Goliathi, kati ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa wachache na chama cha Nazi chenye nguvu nyingi.

Marufuku—Lakini Wenye Kutenda Hata Zaidi

Mnamo Mei 10, 1940, jeshi la Nazi lilishambulia Uholanzi kwa ghafula. Kwa kuwa vichapo vilivyogawanywa na Mashahidi wa Yehova vilifichua matendo maovu ya Unazi na kutetea Ufalme wa Mungu, wafuasi wa Nazi walijaribu kukomesha mara moja utendaji wa Mashahidi. Katika muda unaopungua majuma matatu baada ya Nazi kushambulia Uholanzi, walitoa amri ya siri ya kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Mnamo Machi 10, 1941, gazeti moja lilitangaza hadharani marufuku hiyo, likiwashutumu Mashahidi kwa kupinga “taifa na makanisa.” Hivyo, msako wa Mashahidi ukaongezeka.

Jambo la kutokeza ni kwamba, ingawa kikosi chenye sifa mbaya cha Gestapo, au polisi wa siri, kilipeleleza makanisa yote, kilinyanyasa kikatili shirika moja tu la Kikristo. “Mnyanyaso hadi kifo,” asema mwanahistoria Mholanzi Dakt. Louis de Jong, “ulikipata kikundi kimoja tu cha kidini—Mashahidi wa Yehova.”—Het Koninkrik der Nederlanden in de Tweede Wereldoorlog (Ufalme wa Uholanzi Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili).

Polisi wa Gestapo walishirikiana na polisi wa Uholanzi katika kuwasaka na kuwakamata Mashahidi. Isitoshe, mwangalizi mmoja asafiriye ambaye alishikwa na hofu na kuasi imani aliwapasha wafuasi wa Nazi habari kuhusu wale waliokuwa waamini wenzake. Kufikia mwisho wa Aprili 1941, Mashahidi 113 walikuwa wamekamatwa. Je, shambulio hilo kali lilikomesha kazi ya kuhubiri?

Jibu lapatikana katika ile iitwayo Meldungen aus den Niederlanden (Ripoti Kutoka Uholanzi), hati ya siri ambayo Sicherheitspolizei (Polisi wa Usalama) wa Ujerumani waliandika mnamo Aprili 1941. Ripoti hiyo yasema hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Madhehebu hiyo iliyopigwa marufuku inaendelea na utendaji wenye bidii katika nchi yote, ikifanya mikutano na kubandika karatasi zinazotangaza maneno kama ‘Kunyanyasa Mashahidi wa Mungu ni uhalifu’ na ‘Yehova atawaadhibu wanyanyasaji kwa uharibifu wa milele.’” Majuma mawili baadaye polisi haohao waliripoti kwamba “licha ya Polisi wa Usalama kuchukua hatua kali zaidi dhidi ya utendaji wa Wanafunzi wa Biblia, utendaji wao unaendelea kuongezeka.” Naam, licha ya hatari ya kukamatwa, Mashahidi waliendelea na kazi yao, wakiwagawia watu vichapo zaidi ya 350,000 katika mwaka wa 1941 pekee!

Ni nini kilichowezesha kikundi hiki kidogo lakini chenye kuongezeka cha Mashahidi mamia kadhaa kuwa na ujasiri wa kukabili adui zao wenye kuogofya? Kama Isaya, nabii mwaminifu wa kale, Mashahidi walimhofu Mungu, si mwanadamu. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa na hakika katika maneno haya yenye kufariji ambayo Yehova alimwambia Isaya: “Mimi, naam, mimi, ndimi niwafarijiye; wewe u nani hata ukamwogopa mtu atakayekufa?”—Isaya 51:12.

Ujasiri Wahitaji Staha

Kufikia mwisho wa mwaka wa 1941, idadi ya Mashahidi waliokamatwa ilipanda kufikia watu 241. Hata hivyo, wachache walishindwa na hofu ya mwanadamu. Willy Lages, aliyekuwa askari mwenye sifa mbaya wa polisi wa siri wa Ujerumani, amenukuliwa akisema kwamba “asilimia 90 ya Mashahidi wa Yehova walikataa kufunua jambo lolote, lakini watu wachache tu wa dini zile nyingine ndio waliokuwa na ujasiri wa kunyamaza.” Jambo alilojionea Johannes J. Buskes, kasisi wa Uholanzi aliyefungwa pamoja na Mashahidi, lathibitisha maneno ya Lages. Buskes aliandika hivi mwaka wa 1951:

“Wakati huo, nilipata kuwastahi sana kwa sababu ya itibari yao na imani yao yenye nguvu. Sitamsahau kijana mmoja—alikuwa na umri usiozidi miaka 19—ambaye aligawanya vijitabu ambavyo vilitabiri kuanguka kwa Hitler na Utawala wa Nazi. . . . Angeachiliwa baada ya miezi sita tu kama angeahidi kuacha utendaji huo. Alikataa katakata, naye akahukumiwa kufanya kazi kwa muda usio dhahiri katika kambi ya kazi ngumu huko Ujerumani. Tulijua vizuri hukumu hiyo ilimaanisha nini. Asubuhi iliyofuata, wakati alipoondoshwa nasi tukamuaga, nilimwambia tungemkumbuka na kusali kwa ajili yake. Jibu lake lilikuwa tu: ‘Usiwe na wasiwasi juu yangu. Ufalme wa Mungu hakika utakuja.’ Huwezi kusahau jambo kama hilo, hata ikiwa hupendi kamwe mafundisho ya hawa Mashahidi wa Yehova.”

Licha ya upinzani mkatili, Mashahidi waliendelea kuongezeka. Ingawa Mashahidi walikuwa 300 punde tu kabla ya vita ya ulimwengu ya pili, walikuwa wameongezeka kufikia 1,379 mwaka wa 1943. Inasikitisha kwamba kufikia mwisho wa mwaka huohuo, Mashahidi 54 kati ya Mashahidi zaidi ya 350 waliokamatwa, walikufa katika kambi za mateso. Kufikia mwaka wa 1944 kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 141 wa Uholanzi ambao walikuwa wamefungwa katika kambi za mateso.

Mwaka wa Mwisho wa Mnyanyaso wa Nazi

Baada ya shambulio la majeshi ya Muungano la Juni 6, 1944, kunyanyaswa kwa Mashahidi kuliingia mwaka wake wa mwisho. Wafuasi wa Nazi na washirika wao walikuwa wanaelekea kushindwa kijeshi. Mtu angefikiri kwamba katika hali hiyo wafuasi wa Nazi wangeacha kunyanyasa Wakristo wasio na hatia. Lakini katika mwaka huo, Mashahidi wengine 48 wakakamatwa, na Mashahidi wengine 68 kati ya wale waliokuwa wamefungwa walikufa. Jacob van Bennekom, aliyetajwa hapo awali, alikuwa mmoja wao.

Jacob mwenye umri wa miaka 18 alikuwa miongoni mwa watu 580 waliobatizwa kuwa Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1941. Punde baada ya kubatizwa aliacha kazi nzuri kwa sababu kazi hiyo ilimaanisha aridhiane kutokuwamo kwake kwa Kikristo. Aliajiriwa kazi ya tarishi na kuanza kutumikia akiwa mhudumu wa wakati wote. Alipokuwa akipeleka vichapo vya Biblia, aligunduliwa na kukamatwa. Mnamo Agosti 1944, Jacob mwenye umri wa miaka 21 aliandikia familia yake barua hii akiwa gerezani jijini Rotterdam:

“Mimi ni mzima na nina furaha tele. . . . Kufikia sasa nimehojiwa mara nne. Mahoji ya kwanza na ya pili yalikuwa makali sana, na nilipigwa vibaya, lakini kwa nguvu na fadhili zisizostahiliwa za Bwana, sijafunua jambo lolote hadi sasa. . . . Tayari nimeweza kutoa hotuba hapa, kwa ujumla hotuba sita, ambazo zimesikilizwa na watu 102. Baadhi yao wamependezwa na wameahidi kwamba punde waachiliwapo, wataendelea na upendezi huo.”

Mnamo Septemba 14, 1944, Jacob alipelekwa kwenye kambi ya mateso katika jiji la Uholanzi la Amersfoort. Hata huko yeye aliendelea kuhubiri. Jinsi gani? Mfungwa mwenzake akumbuka: “Wafungwa walikuwa wakiokota vipande vya sigareti zilizotupwa na walinzi na kutumia kurasa za Biblia kusokotea sigareti. Nyakati nyingine Jacob alifaulu kusoma maneno machache kutoka kwenye ukurasa wa Biblia uliokuwa tu karibu utumiwe kusokotea sigareti. Angetumia maneno hayo mara moja kuwa msingi wa kutuhubiria. Muda si muda, tukambandika Jacob jina, ‘Mtu wa Biblia.’”

Mnamo Oktoba 1944, Jacob alikuwa miongoni mwa wafungwa wengi walioamriwa wachimbe mitaro ya kutegea vifaru vya vita. Jacob alikataa kufanya kazi hiyo kwa sababu dhamiri yake haingemruhusu kuunga mkono vita. Ingawa walinzi walimtisha daima, yeye hakukubali kuchimba. Mnamo Oktoba 13 ofisa mmoja alimtoa katika seli ya upweke na kumpeleka mahali pa kazi. Kwa mara nyingine, Jacob akakataa kuchimba mitaro hiyo. Hatimaye, Jacob akaamuriwa achimbe kaburi lake mwenyewe, kisha akauawa kwa kupigwa risasi.

Msako wa Mashahidi Waendelea

Msimamo wenye ujasiri wa Jacob na wengine uliwakasirisha wafuasi wa Nazi na kufanya waanze kuwasaka Mashahidi tena. Mmoja wa Mashahidi waliyetaka kumkamata ni Evert Kettelarij mwenye umri wa miaka 18. Mwanzoni, Evert aliweza kutoroka na kujificha, lakini akakamatwa baadaye na kupigwa sana ili atoe habari kuhusu Mashahidi wengine. Alikataa, kisha akapelekwa Ujerumani kufanya kazi ngumu.

Mwezi huohuo, Oktoba 1944, polisi walianza kumtafuta Bernard Luimes, shemeji ya Evert. Walimpata akiwa na Mashahidi wengine wawili—Antonie Rehmeijer na Albertus Bos. Albertus tayari alikuwa amefungwa kwa miezi 14 katika kambi ya mateso. Hata hivyo, alipoachiliwa, alianza tena kuhubiri kwa bidii. Kwanza, hao wanaume watatu walipigwa kikatili na wafuasi wa Nazi, kisha wakauawa kwa kupigwa risasi. Miili yao ilipatikana tu baada ya vita na kuzikwa upya. Punde tu baada ya vita, magazeti kadhaa yaliripoti mauaji hayo. Gazeti moja lilisema kwamba Mashahidi hao watatu walikuwa wamekataa katakata kufanyia Nazi kazi yoyote iliyopingana na sheria ya Mungu na kuongeza kwamba “jambo hilo lilifanya wauawe.”

Wakati huohuo, Novemba 10, 1944, Bernard Polman, aliyetajwa hapo awali, alikamatwa na kupelekwa kufanya kazi kwenye mradi mmoja wa kijeshi. Yeye tu ndiye aliyekuwa Shahidi miongoni mwa watu hao waliolazimishwa kufanya kazi, naye tu ndiye aliyekataa kufanya kazi hiyo. Walinzi walitumia mbinu mbalimbali ili kumfanya aridhiane. Hakupewa chakula chochote. Pia alipigwa kikatili kwa rungu, sepeto, na tako la bunduki. Mbali na hayo, alilazimishwa kupita katika maji baridi yaliyofika magotini, kisha akafungiwa katika chumba cha chini ya ardhi chenye umajimaji ambapo alikaa usiku kucha akiwa na nguo zilizolowa maji. Hata hivyo, Bernard hakuridhiana.

Wakati huo, dada wawili wa Bernard, wasio Mashahidi wa Yehova, waliruhusiwa kumtembelea. Walimsihi abadili msimamo wake, lakini hawakuweza kamwe kumshawishi. Walipomwuliza Bernard kama kuna jambo lolote ambalo wangeweza kumfanyia, alipendekeza waende nyumbani na kujifunza Biblia. Kisha wanyanyasaji wake wakamruhusu mke wake mjamzito amtembelee, wakitumaini kwamba angemfanya abadili msimamo wake. Lakini kuwapo kwake na maneno yake ya ujasiri yalimtia Bernard moyo aendelee kuwa mwaminifu kwa Mungu. Mnamo Novemba 17, 1944, Bernard alipigwa risasi na watano kati ya wanyanyasaji wake huku wale wengine wote waliolazimishwa kufanya kazi wakitazama. Hata baada ya Bernard kufa, mwili wake ukiwa umepigwa risasi nyingi sana, ofisa msimamizi alighadhibika sana, akatoa bastola yake na kumpiga Bernard risasi kwenye kila jicho lake.

Ingawa kitendo hicho cha ukatili kiliwashtua Mashahidi waliopata habari za mauaji hayo, wao walidumisha uaminifu wao na ujasiri wao na kuendelea na utendaji wao wa Kikristo. Kutaniko moja dogo la Mashahidi wa Yehova lililokuwa karibu na mahali hapo ambapo Bernard aliuawa liliripoti hivi punde tu baada ya mauaji hayo: “Mwezi huu, licha ya hali mbaya ya hewa na matatizo ambayo Shetani ametusababishia, tumeongeza utendaji wetu. Muda uliotumiwa shambani ulipanda kutoka saa 429 hadi 765. . . . Alipokuwa akihubiri, ndugu mmoja alikutana na mtu fulani na kumtolea ushahidi mzuri. Mtu huyo alimwuliza kama yeye ni wa dini moja na mtu yule aliyepigwa risasi. Aliposikia kwamba ndugu huyo ni wa dini hiyo, mtu huyo akasema: ‘Lo! Ni mwanamume mwenye imani iliyoje! Huyo namwita shujaa wa imani!’”

Wakumbukwa na Yehova

Mnamo Mei 1945, wafuasi wa Nazi walishindwa na kufukuzwa Uholanzi. Licha ya mnyanyaso mkali wakati wa vita, Mashahidi wa Yehova waliongezeka kutoka mamia kadhaa na kufikia zaidi ya 2,000. Akizungumza kuhusu Mashahidi hao wa wakati wa vita, mwanahistoria Dakt. de Jong akiri hivi: “Wengi kati yao walikataa kukana imani yao licha ya vitisho na mateso.”

Hivyo, ni kwa sababu nzuri mamlaka za kilimwengu zimewakumbuka Mashahidi wa Yehova kwa msimamo wa ujasiri waliochukua wakati wa utawala wa Nazi. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kwamba sifa bora ya Mashahidi hao wa wakati wa vita itakumbukwa na Yehova na Yesu. (Waebrania 6:10) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo, Mashahidi hao waaminifu na wenye ujasiri ambao walikufa wakiwa katika utumishi wa Mungu watafufuliwa watoke katika makaburi ya ukumbusho, wakiwa na matazamio ya uhai udumuo milele katika dunia paradiso!—Yohana 5:28, 29.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Jacob van Bennekom

[Picha katika ukurasa wa 26]

Makala iliyotolewa katika gazeti la habari ikionyesha amri ya kupiga marufuku Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kulia: Bernard Luimes; chini: Albertus Bos (kushoto) na Antonie Rehmeijer; chini: Ofisi ya Sosaiti huko Heemstede