Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Farijiwa na Nguvu za Yehova

Farijiwa na Nguvu za Yehova

Farijiwa na Nguvu za Yehova

“Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.”—ZABURI 94:19.

BIBLIA ina maneno yenye kufariji watu wote wanaotamani kupata faraja. Basi, si ajabu kwamba The World Book Encyclopedia chasema kwamba “watu wengi sana wameigeukia Biblia ili wapate faraja, tumaini, na mwongozo nyakati za matatizo na wasiwasi.” Kwa nini?

Kwa sababu Biblia imepuliziwa na Muumba wetu mwenye upendo, “Mungu wa faraja yote ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Yeye ni ‘Mungu apaye faraja.’ (Waroma 15:5) Yehova ameweka mfano kwa kutuandalia sisi sote kitulizo. Alituma Mwana wake wa pekee, Kristo Yesu, aje duniani kutupa tumaini na kutuliwaza. Yesu alifundisha: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Biblia inasema Yehova ni Mungu ambaye ‘siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu; na ndiye Mungu wa wokovu wetu.’ (Zaburi 68:19) Wanadamu wenye kumhofu Mungu wanaweza kusema hivi kwa uhakika: “Nimemweka BWANA mbele yangu daima, kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa.”—Zaburi 16:8.

Mafungu kama hayo ya Biblia huonyesha jinsi Yehova Mungu anavyotupenda sana sisi wanadamu. Ni wazi kwamba ana tamaa ya kutoka moyoni—na vilevile ana uwezo—wa kutufariji sana na kupunguza maumivu yetu nyakati za taabu. “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.” (Isaya 40:29) Basi, twawezaje kufarijiwa na nguvu za Yehova?

Matokeo Yenye Kutuliza ya Utunzaji wa Yehova

Mtunga-zaburi aliandika: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Ndiyo, Yehova Mungu anapendezwa na wanadamu. Mtume Petro aliwahakikishia Wakristo wa karne ya kwanza hivi: “Yeye [Mungu] huwajali nyinyi.” (1 Petro 5:7) Yesu Kristo alikazia jinsi Mungu anavyowathamini wanadamu aliposema hivi: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao hupata kusahaulika mbele ya Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiwe na hofu; nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Luka 12:6, 7) Mungu anatuthamini sana hivi kwamba yeye huona hata mambo madogo-madogo sana yanayotuhusu. Yuajua mambo ambayo sisi wenyewe hatuyajui kwa sababu anapendezwa sana nasi.

Svetlana, yule kahaba mdogo aliyetajwa katika makala iliyotangulia, alifarijiwa sana alipotambua kwamba Yehova anapendezwa naye binafsi. Mashahidi wa Yehova walimpata alipokuwa karibu kujiua. Kisha akakubali funzo la Biblia, ambalo lilimsaidia kumfahamu Yehova akiwa mtu halisi ambaye anapendezwa na hali njema yake. Jambo hilo lilimgusa moyo na kumchochea abadili maisha yake na kujiweka wakfu kwa Mungu. Pia lilimfanya Svetlana ajiheshimu na kumsaidia kuvumilia na kuwa na mtazamo mzuri maishani licha ya matatizo yake. “Nina hakika,” yeye asema sasa, “kwamba Yehova hataniacha kamwe. Nimeona ukweli wa maneno ya 1 Petro 5:7. Andiko hilo linasema: ‘Tupeni hangaiko lenu lote juu [ya Yehova], kwa sababu yeye huwajali nyinyi.’”

Tumaini Linalotegemea Biblia Hutufariji

Njia moja hususa ambayo Mungu hutufariji ni kupitia Neno lake lililoandikwa ambalo lina tumaini zuri ajabu la wakati ujao. Mtume Paulo aliandika: “Mambo yote yaliyoandikwa wakati wa mbele yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Paulo alionyesha wazi uhusiano uliopo kati ya tumaini la kweli na faraja alipoandika: “Mungu Baba yetu, aliyetupenda sisi na aliyetupa faraja idumuyo milele na tumaini jema kwa njia ya fadhili isiyostahiliwa na, afariji mioyo yenu na kuwafanya nyinyi kuwa imara katika kila kitendo chema na neno jema.” (2 Wathesalonike 2:16, 17) Hilo “tumaini jema” lahusisha tazamio la kuishi maisha makamilifu na yenye furaha na yasiyokoma katika dunia paradiso.—2 Petro 3:13.

Tumaini hakika na jangavu kama hilo lilimtia moyo Laimonis, yule kilema mzoevu wa kileo ambaye alitajwa katika makala iliyotangulia. Aliposoma vichapo vinavyotegemea Biblia vya Mashahidi wa Yehova, alifurahi kujifunza juu ya ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu, ambamo angekuwa na afya bora kabisa. Alisoma katika Biblia ahadi nzuri ifuatayo ya kuponywa kimuujiza: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isaya 35:5, 6) Ili astahili kuishi katika Paradiso hiyo, Laimonis alifanya mabadiliko makubwa. Aliacha kunywa pombe, na majirani na watu wanaomfahamu wameona mabadiliko hayo. Sasa anaongoza mafunzo kadhaa ya Biblia, akiwapa wengine faraja inayotokana na tumaini linalotegemea Biblia.

Fungu la Sala

Moyo wetu ukiugua kwa sababu fulani, tunaweza kufarijiwa tukisali kwa Yehova. Sala inaweza kutuondolea mzigo. Tunaposali kwa bidii, tunaweza kufarijiwa tukikumbuka mambo yasemwayo katika Neno la Mungu. Zaburi iliyo ndefu zaidi katika Biblia ni kama sala nzuri. Mtungaji wake aliimba: “Nimezikumbuka hukumu zako za kale, Ee BWANA, nikajifariji.” (Zaburi 119:52) Katika hali ngumu sana, hasa zile zinazohusu ugonjwa, mara nyingi huwezi kupata suluhisho moja kwa mambo yote. Huenda tusijue vizuri jinsi tuwezavyo kupata suluhisho tukitegemea nguvu zetu wenyewe. Wengi wameona kwamba kama yote yawezekanayo yamefanywa, kumwendea Mungu katika sala kulitokeza faraja na, nyakati nyingine, kulitokeza masuluhisho ambayo hayakutarajiwa.—1 Wakorintho 10:13.

Pat, ambaye alipelekwa haraka hospitalini kwenye chumba cha wagonjwa mahututi, alipata faraja hiyo kutokana na sala. Baada ya kupata nafuu, alisema: “Nilimwomba Yehova na kutambua kwelikweli kwamba ni lazima niache uhai wangu mikononi mwake, nikitumaini atafanya mapenzi yake. Wakati huo wote nilikuwa mtulivu; nilikuwa na amani ya Mungu inayotajwa kwenye Wafilipi 4:6, 7.” Mistari hiyo inaweza kutufariji kama nini sisi sote! Paulo atuonya hivi katika andiko hilo: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”

Roho Takatifu Ikiwa Mfariji

Usiku ule kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia wazi mitume wake kwamba karibuni angewaacha. Wakasumbuka na kuhuzunika. (Yohana 13:33, 36; 14:27-31) Akitambua kwamba walihitaji kuendelea kufarijiwa, Yesu akawaahidi: “Nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji [au, mfariji] mwingine awe pamoja nanyi milele.” (Yohana 14:16; kielezi-chini) Katika andiko hilo Yesu alikuwa akirejezea roho takatifu ya Mungu. Miongoni mwa mambo mengine, roho ya Mungu iliwafariji mitume walipojaribiwa na kuwaimarisha waendelee kufanya mapenzi ya Mungu.—Matendo 4:31.

Angie, ambaye mume wake nusura afe katika aksidenti mbaya, aliweza kukabiliana na hali kwa mafanikio japo msononeko na maumivu aliyopata. Ni nini kilichomsaidia? Asema hivi: “Bila utegemezo wa roho takatifu ya Yehova, hatungefaulu kushinda mambo yaliyotupata na kuendelea kubaki imara. Kwa kweli nguvu za Yehova zimedhihirika kupitia udhaifu wetu, naye amekuwa ngome katika wakati wetu wa taabu.”

Udugu Wenye Kufariji

Hata mtu apatwe na hali gani maishani, hata hali zenye kuumiza kadiri gani zitokee, anaweza kufarijiwa katika udugu uliopo katika kutaniko la Yehova. Udugu huo huandaa utegemezo wa kiroho na msaada kwa wale wanaoshirikiana nalo. Humo, mtu aweza kupata marafiki wenye upendo, wenye kujali, na wenye kufariji, ambao wako tayari kusaidia na kuwafariji wengine katika nyakati za taabu.—2 Wakorintho 7:5-7.

Washiriki wa kutaniko la Kikristo hufundishwa ‘kufanya lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zao.’ (Wagalatia 6:10) Elimu ya Biblia wanayopokea huwasukuma waonyeshane upendo wa kidugu na shauku-nyororo. (Waroma 12:10; 1 Petro 3:8) Ndugu na dada wa kiroho kutanikoni husukumwa kuwa wafadhili, wenye kufariji, na wenye huruma nyororo.—Waefeso 4:32.

Joe na Rebecca, ambao walifiwa na mwana wao, walipata utegemezo kama huo wenye kufariji kutoka kwa washiriki wa kutaniko la Kikristo. Wao wasema: “Yehova na kutaniko lake lenye upendo wametusaidia kuvumilia wakati mgumu. Tumepokea mamia ya kadi, barua, na simu. Jambo hilo latufanya tuthamini jinsi udugu wetu ulivyo wenye thamani. Tulipokuwa bado tumechanganyikiwa kwa sababu ya msiba huo, washiriki wa makutaniko mengi ya karibu walikuja kutusaidia, wakiandaa chakula na kutusafishia nyumba.”

Ufarijike!

Taabu zituandamapo kama upepo mkali, na msononeko utupigapo daima kama mvua ya mawe isiyo na huruma, Mungu yu tayari kutupatia ulinzi wenye kuliwaza. Hivi ndivyo mojawapo ya zaburi inavyofafanua jinsi aandaavyo kinga yenye kufariji: “Kwa manyoya yake atakufunika, chini ya mbawa zake utapata kimbilio.” (Zaburi 91:4) Huo huenda ukawa mfano wa tai. Ni mfano wa ndege ambaye aona hatari kisha apanua mabawa yake kufunika makinda yake ili ayalinde. Kwa maana kubwa zaidi, Yehova huwa Mlinzi wa kweli wa wale wote wanaomkimbilia.—Zaburi 7:1.

Ukipenda kujifunza mengi kumhusu Mungu, utu wake, makusudi yake, na uwezo wake wa kufariji, twakuomba ujifunze Neno lake. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza. Ndiyo, wewe pia unaweza kufarijiwa na nguvu za Yehova!

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tumaini la wakati ujao linalotegemea Biblia laweza kufariji