Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unawaona Wenye Jeuri Kama Mungu Awaonavyo?

Je, Unawaona Wenye Jeuri Kama Mungu Awaonavyo?

Je, Unawaona Wenye Jeuri Kama Mungu Awaonavyo?

Tangu kale watu wamevutiwa na kuwaheshimu watu hodari, wale wenye nguvu nyingi za kimwili na wenye ujasiri. Mmoja wao ni shujaa katika hekaya za Ugiriki ya kale, aliyeitwa Heracles, au Hercules kwa jina la Kiroma.

HERACLES alikuwa shujaa hodari mwenye kusifiwa sana, mpiganaji mwenye nguvu zaidi kuliko wengine. Hekaya zasema alikuwa mungu-mwanadamu, mwana wa Zeusi mungu wa Wagiriki, na Alcmene, mama wa kibinadamu. Matendo yake ya kishujaa yalianza angali mtoto katika kitanda cha watoto. Wakati mungu wa kike mwenye wivu alipotuma majoka mawili yamuue, Heracles aliyanyonga. Baadaye maishani alipigana vita, akayashinda majitu, na kupambana na kifo ili kumwokoa rafikiye. Pia aliharibu miji, akabaka wanawake, akamrusha mvulana fulani kutoka orofani, na kumwua mke na watoto wake mwenyewe.

Ingawa Heracles anayetajwa katika hekaya hakuwa mtu halisi, tangu zamani za kale alitajwa katika hadithi za nchi za kale ambazo Wagiriki walizijua. Waroma walimwabudu kama mungu; wafanya-biashara na wasafiri walimwomba ili wapate ufanisi na ulinzi kutokana na hatari. Hadithi za matendo yake ya kishujaa zimewasisimua watu kwa maelfu ya miaka.

Chanzo cha Hekaya Hiyo

Je, hadithi za Heracles na mashujaa wengine katika hekaya ni za kweli? Labda kwa njia fulani. Biblia hutaja wakati fulani, mapema katika historia ya mwanadamu, ambapo kwa kweli “miungu” na “miungu-wanadamu” iliishi duniani.

Musa aliandika haya kuhusu enzi hiyo: “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.”—Mwanzo 6:1, 2.

“Wana wa Mungu” hawakuwa wanadamu; walikuwa malaika, wana wa Mungu. (Linganisha Ayubu 1:6; 2:1; 38:4, 7.) Yuda, mwandikaji wa Biblia, asema kwamba malaika fulani “hawakutunza cheo chao cha awali bali wakaachilia mbali mahali pao wenyewe pa kukaa penye kufaa.” (Yuda 6) Yaani, waliacha mahali walipogawiwa katika tengenezo la Mungu la mbinguni kwa kupendelea kuishi na wanawake warembo duniani. Yuda aongeza kwamba malaika hao waasi walikuwa kama watu wa Sodoma na Gomora, ‘waliofanya uasherati kwa kuzidi mno na kutoka kwenda kufuatia mwili kwa ajili ya utumizi usio wa asili.’—Yuda 7.

Biblia haitoi habari kamili ya matendo ya malaika hao waasi. Hata hivyo, hekaya za kale za Ugiriki na kwingineko zaonyesha miungu mingi ambayo iliishi kati ya wanadamu, ama kwa kuonekana au kwa kutoonekana. Ilipojitwalia maumbo ya wanadamu, ilionekana mizuri mno. Ilikula, ikanywa, ikalala, na kufanya ngono kati yao na binadamu pia. Ingawa ilidhaniwa kuwa mitakatifu na isiyoweza kufa, ilisema uwongo na kudanganya, ikagombana na kupigana, ikatongoza na kubaka. Hekaya hizo huenda zikaonyesha, ijapokuwa kwa njia iliyoongezwa chumvi na kupotoshwa, hali halisi zilizokuwepo kabla ya Furiko linalotajwa katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo.

Watu Hodari wa Zamani, Watu Wenye Sifa

Malaika hao wasiotii waliotwaa miili yenye kuonekana walifanya ngono na wanawake, kisha wanawake hao wakazaa watoto. Watoto hao hawakuwa wa kawaida. Walikuwa Wanefili, nusu wanadamu na nusu malaika. Masimulizi ya Biblia yasema: “Nao Wanefili walikuwako duniani siku zile; tena, baada ya hayo, wana wa Mungu walipoingia kwa binti za wanadamu, wakazaa nao wana; hao ndio waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa.”—Mwanzo 6:4.

Neno la Kiebrania “wanefili” lamaanisha kihalisi “waangushaji,” yaani, watu wanaowaangusha wengine, au wanaofanya wengine waanguke, kupitia matendo ya jeuri. Basi, haishangazi kwamba masimulizi ya Biblia yaongezea: “Dunia ikajaa dhuluma [“jeuri,” NW].” (Mwanzo 6:11) Miungu-wanadamu katika hekaya, kama vile Heracles na shujaa wa Kibabiloni aitwaye Gilgamesh, yafanana sana na Wanefili.

Ona kwamba Wanefili waliitwa “watu hodari” na “watu wenye sifa.” Kinyume cha Noa mwadilifu, aliyeishi nyakati hizohizo, Wanefili hawakuwa na haja ya kuendeleza sifa ya Yehova. Walijali tu sifa, utukufu, na umashuhuri wao wenyewe. Kupitia matendo ya ajabu, ambayo bila shaka yalihusisha jeuri na umwagaji wa damu, walijipatia sifa waliyotamani kutoka kwa ulimwengu usiomwogopa Mungu walimoishi. Walikuwa mashujaa hodari katika siku zao—wenye kuhofiwa, kuheshimiwa, na kuonekana wasioshindika.

Ingawa huenda Wanefili na baba zao, wale malaika waliotenda dhambi, walipata sifa machoni pa watu wa siku hizo, kwa hakika hawakuwa na sifa njema machoni pa Mungu. Tabia yao ilichukiza. Basi Mungu akawachukulia hatua malaika hao waliotenda dhambi. Mtume Petro aliandika hivi: “Mungu hakuacha kuadhibu malaika waliofanya dhambi, bali, kwa kuwatupa ndani ya Tartaro, aliwatia kwenye mashimo ya giza zito ili wawekwe akiba kwa ajili ya hukumu; na hakuacha kuadhibu ulimwengu wa kale, bali alitunza salama Noa, mhubiri wa uadilifu, pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasioogopa Mungu.”—2 Petro 2:4, 5.

Wakati wa Furiko, malaika hao waasi waliivua miili yao yenye kuonekana kisha wakarudi kwa aibu kwenye makao ya roho. Mungu aliwaadhibu kwa kuwazuia kutwaa tena miili ya kibinadamu. Wanefili, wazao wa malaika wasiotii waliokuwa na nguvu zinazoshinda za wanadamu, waliangamia wote. Noa na familia yake ndogo peke yao ndio waliookoka Gharika.

Watu Wenye Sifa Leo

Hapana miungu na miungu-wanadamu inayoishi duniani leo ikiwa na umbo linaloonekana. Hata hivyo, jeuri imejaa sana. Watu wenye sifa leo wanatukuzwa katika vitabu, sinema, televisheni, na muziki. Hawawezi kamwe kugeuza shavu la pili, kuwapenda adui zao, kutafuta amani, kusamehe, wala kuacha jeuri. (Mathayo 5:39, 44; Waroma 12:17; Waefeso 4:32; 1 Petro 3:11) Badala yake, watu hodari wa leo wanapendwa kwa sababu ya nguvu na uwezo wao wa kupigana, kujilipizia kisasi, na kukabiliana na jeuri kwa kutumia jeuri kubwa zaidi. *

Maoni ya Mungu kwa watu wa aina hiyo hayajabadilika tangu siku za Noa. Yehova havutiwi na watu wanaopenda jeuri, wala hafurahii matendo yao ya kishujaa. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “BWANA humjaribu mwenye haki; bali nafsi yake humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu [“jeuri,” NW].”—Zaburi 11:5.

Nguvu ya Aina Tofauti

Yesu Kristo ni tofauti kabisa na watu hodari wenye jeuri, naye alikuwa mwanadamu mashuhuri zaidi aliyepata kuishi, mtu mwenye amani. Hakutenda “jeuri” alipokuwa duniani. (Isaya 53:9) Adui zake walipokuja kumkamata katika bustani ya Gethsemane, wafuasi wake walikuwa na panga kadhaa. (Luka 22:38, 47-51) Huenda wangeunda genge la wapiganaji ili kuzuia Wayahudi wasimkamate.—Yohana 18:36.

Hata mtume Petro alichomoa upanga wake ili kumkinga Yesu, lakini Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:51, 52) Naam, jeuri huzaa jeuri, kama vile historia ya mwanadamu imeonyesha mara nyingi. Licha ya kuwa na nafasi ya kujikinga, Yesu pia alikuwa na njia nyingine ya kujikinga. Aliendelea kumwambia Petro: “Au wafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika?”—Mathayo 26:53.

Badala ya kutumia jeuri au kutafuta ulinzi wa malaika, Yesu aliwaruhusu wale waliomwua wamkamate. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba alijua wakati wa Baba yake wa mbinguni wa kuukomesha uovu duniani haukuwa umefika. Badala ya kuchukua hatua ya kujikinga, Yesu alimtumaini Yehova.

Huo haukuwa udhaifu bali wonyesho wa nguvu kuu ya ndani. Yesu alionyesha imani yenye nguvu kwamba Yehova angenyoosha mambo kwa wakati na njia Yake mwenyewe. Kwa sababu ya utii wake, Yesu alikwezwa kwenye cheo chenye sifa, cha pili kutoka kwa Yehova mwenyewe. Mtume Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu: “Alijinyenyekeza mwenyewe akawa mtiifu hadi kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hiihii pia Mungu alimkweza kwenye cheo cha juu zaidi akampa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina jingine, ili katika jina la Yesu kila goti likunjwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya ardhi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:8-11.

Ahadi ya Mungu ya Kuikomesha Jeuri

Wakristo wa kweli huishi kulingana na kielelezo na mafundisho ya Yesu. Hawavutiwi wala kuwaiga watu wa kilimwengu wenye sifa na jeuri. Wanajua kwamba wakati wa Mungu ufikapo, watu hao wataangamizwa milele, kama vile watu waovu walivyoangamizwa katika siku za Noa.

Mungu ndiye Muumba wa dunia na wanadamu. Ndiye pia Mwenye Enzi Kuu halali. (Ufunuo 4:11) Iwapo hakimu mwanadamu ana uwezo wa kisheria wa kutoa hukumu, basi Mungu ana uwezo zaidi wa kufanya vivyo hivyo. Atakomesha uovu wote na wale wanaoutenda kwa kuwa anaziheshimu kanuni zake za uadilifu na anawapenda wale wanaompenda.—Mathayo 13:41, 42; Luka 17:26-30.

Hatua hiyo italeta amani yenye kudumu duniani, amani inayotegemea haki na uadilifu. Hayo yalitabiriwa katika unabii mashuhuri unaomhusu Yesu Kristo: “Kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele. Wivu wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”—Isaya 9:6, 7.

Basi Wakristo wana sababu halali ya kutii shauri lililopuliziwa zamani za kale: “Usimhusudu mtu mwenye jeuri, wala usiichague mojawapo ya njia zake. Maana mtu mkaidi ni chukizo kwa BWANA, bali siri yake ni pamoja na wanyofu.”—Mithali 3:31, 32.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Mara nyingi watu wenye jeuri katika michezo mingi ya vidio na sinema za ubuni wa sayansi wanaonyesha matendo hayo mabaya na yenye jeuri kwa kadiri kubwa zaidi.

[Blabu\Picha katika ukurasa wa 26, 29 zimeandaliwa na]

WATU HODARI WA LEO WANAPENDWA KWA SABABU YA NGUVU NA UWEZO WAO WA KUKABILIANA NA JEURI KWA KUTUMIA JEURI KUBWA ZAIDI

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Alinari/Art Resource, NY