Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utakuwepo Katika Ulimwengu Mpya?

Je, Utakuwepo Katika Ulimwengu Mpya?

Je, Utakuwepo Katika Ulimwengu Mpya?

“Hakuna jema kwao kupita kufurahi, na kufanya mema maadamu wanaishi. Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—MHUBIRI 3:12, 13.

1. Kwa nini twaweza kutarajia mema wakati ujao?

WATU wengi humfikiria Mungu Mweza Yote kuwa mkali na mkatili. Lakini andiko lililo juu ni kweli utakayoipata katika Neno lake lililopuliziwa. Kweli hiyo yapatana na kuwa kwake “Mungu mwenye furaha” na yapatana pia na kule kuwaweka wazazi wetu wa kwanza katika paradiso ya kidunia. (1 Timotheo 1:11; Mwanzo 2:7-9) Tunapotafuta ufahamu wenye kina juu ya wakati ujao ambao Mungu huahidi watu wake, tusishangae kupata kujua hali zitakazotuletea furaha ya kudumu.

2. Unatazamia mambo gani?

2 Katika makala iliyotangulia, tulichunguza matabiri matatu kati ya manne ambapo Biblia hutabiri juu ya “mbingu mpya na nchi [“dunia,” NW] mpya.” (Isaya 65:17) Utabiri mmoja kati ya matabiri hayo yenye kutegemeka umerekodiwa kwenye Ufunuo 21:1. Mistari inayofuata inataja wakati ambapo Mungu Mweza Yote atabadili kabisa hali duniani ziwe bora. Atafuta machozi ya huzuni. Watu hawatakufa tena kutokana na uzee, ugonjwa, au aksidenti. Maombolezo, kilio, na maumivu yatatoweka. Ni matazamio yenye kupendeza kama nini! Lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba matazamio hayo yatatimizwa, nayo yaweza kuwa na matokeo gani juu yetu wakati huu?

Sababu za Kuwa na Uhakika

3. Kwa nini twaweza kutumaini ahadi za Biblia kuhusu wakati ujao?

3 Ona jinsi Ufunuo 21:5 linavyoendelea kusema. Lamnukuu Mungu, aketiye katika kiti chake cha ufalme mbinguni akitangaza hivi: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Ahadi hiyo ya Mungu ni bora kuliko tangazo lolote la kitaifa la uhuru, kuliko sheria yoyote ya leo ya haki za binadamu, au lengo lolote la wanadamu la wakati ujao. Ni tangazo linalotegemeka kabisa kutoka kwa Mmoja ambaye Biblia husema ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Inaeleweka kwamba huenda ukahisi hakuna kitu kingine kinachohitajiwa ila kuendelea tu kufurahia matazamio hayo mazuri sana na kumtumaini Mungu. Lakini si lazima tukomee hapo. Kuna mengi bado tuwezayo kujifunza juu ya wakati wetu ujao.

4, 5. Ni unabii gani mbalimbali wa Biblia tuliochunguza tayari ambao waweza kuimarisha tumaini letu juu ya mambo yatakayotukia wakati ujao?

4 Fikiria mambo ambayo makala iliyotangulia ilithibitisha kuhusu ahadi za Biblia juu ya mbingu mpya na dunia mpya. Isaya alitabiri mfumo huo mpya, na unabii wake ulitimizwa Wayahudi waliporudi katika nchi yao na kuanzisha tena ibada ya kweli. (Ezra 1:1-3; 2:1, 2; 3:12, 13) Hata hivyo, je, unabii wa Isaya ulirejezea tukio hilo tu? Bila shaka la! Mambo aliyotabiri yangetimizwa pia katika njia kubwa zaidi muda mrefu baadaye. Kwa nini tukate kauli hiyo? Kwa sababu ya mambo tusomayo katika 2 Petro 3:13 na Ufunuo 21:1-5. Maandiko hayo yarejezea mbingu mpya na dunia mpya zitakazowanufaisha Wakristo ulimwenguni pote.

5 Kama ilivyotajwa awali, Biblia hutumia usemi “mbingu mpya na dunia mpya” mara nne. Tumechunguza semi tatu kati ya hizo nne nasi tumekata kauli yenye kutia moyo sana. Biblia hutabiri waziwazi kwamba Mungu ataondoa uovu na mambo mengine yanayosababisha kuteseka na kwamba atazidi kuwabariki wanadamu katika mfumo wake mpya ulioahidiwa.

6. Unabii wa nne unaotaja “mbingu mpya na dunia mpya” watabiri nini?

6 Sasa na tuchunguze usemi unaosalia wa “mbingu mpya na dunia mpya,” kwenye Isaya 66:22-24: “Kama vile mbingu mpya na nchi [“dunia,”NW] mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa. Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema BWANA. Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.”

7. Kwa nini tufikie mkataa wa kwamba andiko la Isaya 66:22-24 litatimizwa wakati ujao?

7 Unabii huo ulitimizwa miongoni mwa Wayahudi waliorudishwa katika nchi yao, lakini kungekuwa na utimizo mwingine. Lazima utimizo huo ungetokea baadaye sana, baada ya barua ya pili ya Petro na Ufunuo kuandikwa, kwa kuwa barua hizo zataja ‘mbingu na dunia mpya’ za wakati ujao. Twaweza kutarajia utimizo huo mkubwa na ulio kamili katika mfumo mpya. Fikiria baadhi ya mambo tuwezayo kutazamia kufurahia.

8, 9. (a) Ni katika maana gani watu wa Mungu wataendelea ‘kukaa’? (b) Ni nini maana ya unabii kwamba watumishi wa Yehova wataabudu “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato”?

8 Andiko la Ufunuo 21:4 laonyesha kwamba kifo hakitakuwapo tena kamwe. Maneno ya Isaya sura ya 66 yakubaliana na ahadi hiyo. Twaweza kuona kuanzia mstari wa 22 kwamba Yehova anajua ya kwamba mbingu mpya na dunia mpya hazitakuwa za muda mfupi tu. Isitoshe, watu wake watadumu; wataendelea ‘kukaa’ mbele zake. Yale ambayo tayari Mungu amewafanyia wateule wake yatupa uhakika. Wakristo wa kweli wamekabili mnyanyaso mkali, hata wamekabili jitihada za kishupavu za kuwaangamiza. (Yohana 16:2; Matendo 8:1) Lakini, hata maadui wenye nguvu sana wa watu wa Mungu, kama vile Maliki Nero wa Roma na Adolf Hitler, hawajaweza kuwaondolea mbali waaminifu-washikamanifu wa Mungu, wanaoitwa kwa jina lake. Yehova amehifadhi kutaniko la watu wake, nasi tuna hakika kwamba anaweza kuendelea kulifanya likae hata milele.

9 Vivyo hivyo, wakiwa mtu mmoja-mmoja, wale walio waaminifu kwa Mungu, wakiwa sehemu ya dunia mpya, jamii ya waabudu wa kweli katika ulimwengu mpya, watakaa daima kwa kuwa watakuwa wakimtolea Muumba wa vitu vyote ibada safi. Ibada hiyo haitakuwa ya pindi kwa pindi au isiyo na utaratibu. Sheria ya Mungu, ambayo Waisraeli walipewa kupitia Musa, ilitaka matendo fulani ya ibada yafanywe kila mwezi, uliotiwa alama na mwezi mpya, na kila juma, lililotiwa alama na siku ya Sabato. (Mambo ya Walawi 24:5-9; Hesabu 10:10; 28:9, 10; 2 Mambo ya Nyakati 2:4) Kwa hiyo, Isaya 66:23 lataja ibada ya kawaida na yenye kuendelea ya Mungu, juma baada ya juma, mwezi baada ya mwezi. Kutoamini kuwepo kwa Mungu na unafiki wa kidini hazitakuwako wakati huo. “Wanadamu wote watakuja kuabudu mbele” za Yehova.

10. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba ulimwengu mpya hautaharibiwa daima na waovu?

10 Isaya 66:24 latuhakikishia kwamba amani na uadilifu za dunia mpya hazitakuwa hatarini kamwe. Waovu hawataiharibu dunia kamwe. Kumbuka kwamba andiko la 2 Petro 3:7 lasema kwamba tunangojea “siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.” Watakaoharibiwa ni watu wasiomwogopa Mungu. Hakuna madhara yatakayowapata wasio na hatia, tofauti na vile itukiavyo mara nyingi katika vita vya wanadamu, ambapo majeruhi walio raia huwa wengi kuliko askari. Hakimu Mkuu atuhakikishia kwamba siku yake itakuwa ya kuangamiza watu wasiomwogopa Mungu.

11. Isaya anaonyesha ni nini kitampata yeyote anayekataa Mungu na ibada yake?

11 Waokokaji waadilifu wataona kwamba neno la Mungu la kiunabii ni la kweli. Mstari wa 24 hutabiri kwamba ‘mizoga ya watu waliomwasi’ Yehova itakuwa uthibitisho wa hukumu yake. Huenda maneno ya waziwazi ambayo Isaya alitumia yakawa yenye kushtua. Hata hivyo, yanapatana na jambo hakika la kihistoria. Nje ya kuta za Yerusalemu la kale kulikuweko mahali mbalimbali pa kutupa takataka na, pindi kwa pindi, mizoga ya wahalifu walioonekana kuwa hawastahili mazishi ya heshima. * Huko funza na moto mkali zingemaliza upesi takataka hizo na mizoga hiyo. Kwa wazi, mfano wa Isaya waonyesha mfano wa hukumu ya Yehova dhidi ya waasi ambayo haiwezi kubadilishwa.

Mambo Ambayo Ameahidi

12. Isaya atoa madokezo gani zaidi kuhusu maisha katika ulimwengu mpya?

12 Ufunuo 21:4 latuambia mambo ambayo hayatakuwapo katika mfumo mpya ujao. Hata hivyo, ni mambo gani yatakayokuwapo wakati huo? Maisha yatakuwaje? Je, twaweza kupata madokezo yoyote yenye kutegemeka? Ndiyo. Isaya sura ya 65 yafafanua kiunabii hali tutakazofurahia iwapo tutakubaliwa na Yehova kuishi wakati aumbapo hatimaye mbingu mpya na dunia mpya. Waliobarikiwa kuishi daima katika dunia mpya hawatazeeka kisha wafe. Isaya 65:20 latuhakikishia hivi: “Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa.”

13. Isaya 65:20 latuhakikishiaje kwamba watu wa Mungu watakuwa salama?

13 Unabii huo ulipotimizwa mara ya kwanza kwa watu wa Isaya, ulimaanisha kwamba watoto wa nchi hiyo walikuwa salama. Hakuna adui waliokuwa wakiwajia, kama vile Wababiloni walivyofanya pindi moja, ili kunyakua watoto wanyonyao au kuangamiza wanaume wenye nguvu. (2 Mambo ya Nyakati 36:17, 20) Katika ulimwengu mpya ujao, watu watakuwa salama salimini nao wataweza kufurahia maisha. Iwapo mtu ataamua kumwasi Mungu, hataruhusiwa kuendelea kuishi. Mungu atamwondoa. Itakuwaje ikiwa mtenda-dhambi huyo mwasi ana umri wa miaka mia moja? Atakufa akiwa “mtoto wa siku chache” ikilinganishwa na kufurahia maisha yasiyo na kikomo.—1 Timotheo 1:19, 20; 2 Timotheo 2:16-19.

14, 15. Ni utendaji gani wenye kuthawabisha uwezao kutarajia kulingana na Isaya 65:21, 22?

14 Badala ya kuzungumzia sana jinsi mtenda-dhambi wa kukusudia awezavyo kuondolewa, Isaya afafanua hali za maisha zitakazokuwapo katika ulimwengu mpya. Jiwazie ukiwa katika hali hizo. Huenda mambo uwezayo kuwazia kwanza yakawa yale unayopenda sana. Isaya azungumzia mambo hayo katika mstari wa 21 na 22: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”

15 Ikiwa bado hujapata ujuzi wa kujenga au kulima, unabii wa Isaya wadokeza kwamba utaelimishwa. Hata hivyo, je, ungetaka kujifunza ukisaidiwa na wafunzi wenye uwezo, labda majirani wenye fadhili wanaofurahia kukusaidia? Isaya hakusema ikiwa nyumba yako itakuwa na madirisha makubwa yenye pazia na yasiyo na vioo ili kukuwezesha kufurahia kupunga upepo, au madirisha yenye vioo ambavyo kupitia hivyo waweza kuona majira yenye kubadilika-badilika. Je, utajenga nyumba yako ikiwa na paa yenye kuinama ili mvua na theluji zitiririke? Au tabia ya nchi ya kwenu itahitaji paa tambarare—kama mojawapo ya zile za Mashariki ya Kati—paa ambayo wewe na familia yako mwaweza kukusanyikia ili kula milo mizuri na kuwa na mazungumzo yenye kupendeza?—Kumbukumbu la Torati 22:8; Nehemia 8:16.

16. Kwa nini unaweza kutarajia ulimwengu mpya uwe wenye kuridhisha daima?

16 Jambo la maana zaidi kuliko kujua mambo hayo madogo-madogo ni kwamba utakuwa na makao yako mwenyewe. Yatakuwa yako—si kama vile leo uwezavyo kujitahidi kujenga kisha mtu mwingine akanufaika. Isaya 65:21 pia lasema kwamba utapanda na kula matunda. Ni wazi kwamba hilo laonyesha jinsi hali itakavyokuwa kwa ujumla. Utaridhishwa sana na jitihada zako, matokeo ya jasho lako mwenyewe. Nawe utaweza kufanya hivyo kwa muda mrefu—“kama siku za mti.” Bila shaka hilo lapatana na ufafanuzi wa “vitu vyote kuwa vipya”!—Zaburi 92:12-14.

17. Wazazi watatiwa moyo hasa na ahadi gani?

17 Ikiwa wewe ni mzazi, maneno haya yatakugusa moyo: “Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na BWANA, na watoto wao pamoja nao. Na itakuwa ya kwamba, kabla hawajaomba, nitajibu; na wakiwa katika kunena, nitasikia.” (Isaya 65:23, 24) Je, unajua maumivu ya ‘kuzaa kwa taabu’? Hatuhitaji kuorodhesha matatizo yawezayo kuwapata watoto ambayo huwataabisha wazazi na watu wengine. Kuhusiana na hilo, sote tumeona wazazi ambao hujishughulisha sana na kazi, utendaji, au anasa zao wenyewe hivi kwamba hawana wakati wa kutosha kwa watoto wao. Tofauti na hao, Yehova anatuhakikishia kwamba atasikia na kutosheleza mahitaji yetu, hata atayatarajia.

18. Kwa nini waweza kutarajia kufurahia wanyama katika ulimwengu mpya?

18 Ufikiriapo mambo uwezayo kufurahia katika ulimwengu mpya, wazia mandhari ambayo neno la Mungu la kiunabii lataja: “Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema BWANA.” (Isaya 65:25) Wasanii wamejaribu kuchora mandhari hiyo, lakini hiyo si mchoro wa kuwaziwa tu usioonyesha mambo kihalisi. Mandhari hiyo itakuwa halisi. Amani itaenea miongoni mwa wanadamu na pia kati yao na wanyama. Wataalamu wengi wa wanyama na watu wengi wanaopenda wanyama hutumia miaka mingi zaidi maishani mwao wakijifunza juu ya aina chache za wanyama au hata mnyama mmoja tu. Tofauti na hilo, hebu wazia mambo utakayoweza kujifunza wakati ambapo wanyama hawatakuwa wakiwaogopa wanadamu. Ndipo utakapoweza kuwakaribia hata ndege na viumbe wadogo ambao hukaa msituni—naam, uwatazame, ujifunze, na kuwafurahia. (Ayubu 12:7-9) Utaweza kufanya hivyo ukiwa salama salimini, bila hatari yoyote kutokana na mwanadamu au mnyama. Yehova asema: “Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote.” Litakuwa badiliko lililoje tofauti na hali zilizoko leo!

19, 20. Kwa nini watu wa Mungu ni tofauti kabisa na watu wengi leo?

19 Kama ilivyotajwa awali, wanadamu hawawezi kutabiri wakati ujao kwa usahihi, licha ya mahangaiko mengi sana juu ya milenia mpya. Hilo hutamausha, huvuruga, na kufanya watu wengi wakate tumaini. Peter Emberley, mkurugenzi wa chuo kikuu cha Kanada, aliandika: “Watu wengi [wazima] hatimaye wanakabili maswala muhimu ya maisha. Mimi ni nani? Kwa kweli najitahidi kufanya nini? Nakiachia kizazi kinachofuata urithi gani? Wanang’ang’ana wakiwa wenye umri wa makamo kufikia utengamano na kupata maana maishani.”

20 Unaweza kuelewa ni kwa nini watu wengi wako hivyo. Huenda wakajaribu kufurahia maisha kwa kujishughulisha na mambo ya kujifurahisha na aina nyinginezo za tafrija. Hata hivyo, hawajui mambo ya wakati ujao, kwa hiyo maisha huenda yakakosa umuhimu, utengamano au maana halisi. Sasa linganisha mambo hayo na maoni yako juu ya maisha, kwa kutegemea yale ambayo tumechunguza. Wajua kwamba katika mbingu na dunia mpya zilizoahidiwa na Yehova, tutaweza kutazama huku na huku na kusema kutoka moyoni, ‘Kwa kweli Mungu amefanya vitu vyote kuwa vipya!’ Tutafurahia hali hiyo kama nini!

21. Twaona mambo gani yanayofanana katika Isaya 65:25 na Isaya 11:9?

21 Si jambo la kimbelembele kuwazia kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. Mungu hutualika, hata kutusihi, tumwabudu katika kweli sasa na kustahili kuishi wakati ambapo ‘hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wake mtakatifu wote.’ (Isaya 65:25) Hata hivyo, je, unajua kwamba awali Isaya alitoa maelezo kama hayo, na kwamba alitia ndani jambo muhimu sana linalotuwezesha kufurahia kikweli ulimwengu mpya? Isaya 11:9 lasema hivi: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”

22. Uchunguzi wetu wa unabii wa Biblia uliotolewa mara nne wapasa kuimarisha azimio letu la kufanya nini?

22 “Kumjua BWANA.” Mungu afanyapo vitu vyote kuwa vipya, wakazi wa dunia watakuwa na ujuzi sahihi juu yake na juu ya mapenzi yake. Ujuzi huo utahusisha mengi kuliko kujifunza tu kutokana na uumbaji wa wanyama. Neno lake lililopuliziwa linahusika. Kwa mfano, fikiria mambo mengi ambayo tumefahamu kwa kuchunguza unabii uliotolewa mara nne ambao hutaja “mbingu mpya na dunia mpya.” (Isaya 65:17; 66:22; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1) Una sababu nzuri za kusoma Biblia kila siku. Je, hilo ni mojawapo ya mambo unayofanya kwa kawaida? Ikiwa sivyo, unaweza kufanya marekebisho gani ili usome kila siku baadhi ya mambo ambayo Mungu amesema? Utaona kwamba mbali na kutazamia kufurahia ulimwengu mpya, furaha yako itaongezeka wakati huu, kama ilivyokuwa na mtunga-zaburi.—Zaburi 1:1, 2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Ona kichapo Insight on the Scriptures, Buku la Kwanza, ukurasa wa 906, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

Ungejibuje?

• Kwa nini tunaweza kukata kauli kwamba Isaya 66:22-24 latabiri mambo ambayo bado yatatukia wakati ujao?

• Ni nini hasa unachotazamia kati ya mambo ambayo yametajwa katika unabii unaopatikana kwenye Isaya 66:22-24 na Isaya 65:20-25?

• Una sababu gani za kuwa na uhakika juu ya wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Isaya, Petro, na Yohana walitabiri hali zitakazokuwa katika “mbingu mpya na dunia mpya”