Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanya Vitu Vyote Kuwa Vipya—Kama Ilivyotabiriwa

Kufanya Vitu Vyote Kuwa Vipya—Kama Ilivyotabiriwa

Kufanya Vitu Vyote Kuwa Vipya—Kama Ilivyotabiriwa

“Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia, husema: . . . ‘Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—UFUNUO 21:5.

1, 2. Kwa nini kwa kufaa watu wengi husita kufikiria mambo ya wakati ujao?

JE, UMEWAHI kusema au kuwaza, ‘Ni nani ajuaye kesho itakuwaje?’ Unaweza kuelewa ni kwa nini watu husita kukisia mambo ya wakati ujao au kuwatumaini watu ambao huenda wakadai kwa kimbelembele kwamba wanaweza kutabiri mambo ya wakati ujao. Ni wazi kwamba wanadamu hawana uwezo wa kutabiri kwa usahihi mambo yatakayotukia miezi au miaka kadhaa ijayo.

2 Gazeti la Forbes ASAP liliandika makala moja kuhusu wakati. Katika makala hiyo mwenyekiti wa kipindi fulani cha televisheni, Robert Cringely, aliandika hivi: “Hatimaye, wakati hutuaibisha sisi sote, lakini hakuna aaibishwaye na wakati kama watu ambao hutabiri mambo ya wakati ujao. Kujaribu kukisia mambo ya wakati ujao ni mchezo ambao sisi hushindwa karibu sikuzote. . . . Hata hivyo, waitwao eti wataalamu huendelea kutabiri.”

3, 4. (a) Watu wengine wana matarajio gani mema kuhusu milenia mpya? (b) Wengine wana matarajio gani halisi kuhusu wakati ujao?

3 Huenda umetambua kwamba kwa kuwa milenia mpya imekaziwa fikira sana, huenda ikaonekana kuwa wengi wanafikiria wakati ujao. Mwanzoni mwa mwaka uliopita, gazeti la Maclean’s lilisema: “Huenda Wakanada walio wengi wakauona mwaka wa 2000 kuwa tu kama miaka mingine kwenye kalenda, lakini mwaka huo waweza kuwa mwanzo mpya kwelikweli.” Profesa Chris Dewdney wa Chuo Kikuu cha York alitoa sababu hii ya kuwa na matarajio mema: “Milenia yamaanisha kwamba tunaweza kuachana kabisa na karne ambayo ni mbaya sana.”

4 Je, jambo hilo lasikika kuwa ndoto ya mchana? Nchini Kanada asilimia 22 pekee ya watu waliokubali kuhojiwa ndio “wanaoamini kwamba mwaka wa 2000 utatokeza mwanzo mpya wa ulimwengu.” Kwa hakika, karibu nusu ya watu hao “wanatarajia pambano jingine la ulimwengu”—vita ya ulimwengu—kabla ya miaka 50 kwisha. Ni wazi, watu wengi wanaona kwamba milenia mpya haiwezi kutatua matatizo yetu na kufanya vitu vyote kuwa vipya. Bwana Michael Atiyah, aliyekuwa mkurugenzi wa Royal Society ya Uingereza, aliandika hivi: “Ule mwendo wa kasi wa mabadiliko . . . wamaanisha kwamba karne ya ishirini na moja itatokeza masuala muhimu katika ustaarabu wetu wote. Matatizo ya ongezeko la watu, upungufu wa rasilimali, uchafuzi wa mazingira, na umaskini ambao umeenea sana, tayari yametupata nasi lazima tuyakabili kwa hima.”

5. Ni wapi tuwezapo kupata habari yenye kutegemeka kuhusu mambo ya wakati ujao?

5 Huenda ukajiuliza, ‘Kwa kuwa watu hawawezi kutabiri mambo yatakayotokea wakati ujao, basi, je, hatupaswi kuupuuza tu wakati ujao?’ Jibu ni la! Ni kweli kwamba watu hawawezi kutabiri kwa usahihi mambo ya wakati ujao, lakini hatupaswi kufikiri kwamba hakuna awezaye. Ni nani awezaye, na kwa nini tutarajie mema wakati ujao? Unaweza kupata majibu yenye kuridhisha katika matabiri manne hususa. Yamerekodiwa katika kitabu ambacho watu wengi sana wanacho na kinachosomwa na watu wengi sana, kitabu ambacho pia hueleweka vibaya na kupuuzwa sana, yaani Biblia. Hata ufikirie nini kuihusu Biblia, hata uwe waijua vizuri kadiri gani, utanufaika kwa kuyachunguza maandiko haya manne ya msingi. Kwa hakika, yanatabiri wakati ujao wenye matumaini. Isitoshe, matabiri hayo manne muhimu yaonyesha jinsi wakati wako ujao na ule wa wapendwa wako uwezavyo kuwa.

6, 7. Isaya alitabiri wakati gani, na matabiri yake yalitimizwaje kwa njia yenye kushangaza?

6 Andiko la kwanza lapatikana katika Isaya sura ya 65. Kabla ya kulisoma, zingatia akilini kikao—wakati habari hiyo ilipoandikwa na hali iliyohusika. Nabii wa Mungu Isaya, aliyeandika maneno hayo, aliishi zaidi ya karne moja kabla ya ufalme wa Yuda kukomeshwa. Mwisho huo ulikuja wakati Yehova alipoacha kuwalinda Wayahudi wasio waaminifu, akawaruhusu Wababiloni waharibu Yerusalemu na kupeleka watu wake uhamishoni. Uharibifu huo ulitokea zaidi ya miaka mia moja baada ya Isaya kuutabiri.— 2 Mambo ya Nyakati 36:15-21.

7 Kuhusu historia ya utimizo huo, kumbuka kwamba kwa kuongozwa na Mungu Isaya alitabiri jina la Mwajemi ambaye hakuwa amezaliwa, Koreshi, ambaye hatimaye alipindua Babiloni. (Isaya 45:1) Koreshi alifanya matayarisho ili Wayahudi warudi katika nchi yao mwaka wa 537 K.W.K. Kwa kushangaza, Isaya alitabiri juu ya kurudishwa huko, kama tusomavyo katika sura ya 65. Alikazia fikira hali ambayo Waisraeli wangeweza kufurahia wakirudi katika nchi yao.

8. Isaya alitabiri wakati gani ujao wenye furaha, na ni usemi gani unaopendeza hasa?

8 Twasoma hivi kwenye Isaya 65:17-19: “Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya [“dunia mpya,” NW ], na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza.” Bila shaka, Isaya alifafanua hali bora sana kuliko hali za Wayahudi wakiwa Babiloni. Alitabiri hali ya shangwe na furaha. Sasa tazama usemi ‘mbingu mpya na dunia mpya.’ Hili ndilo andiko la kwanza kati ya maandiko manne ya Biblia ambayo yataja usemi huo, na maandiko hayo manne yanaweza kuhusika moja kwa moja na wakati wetu ujao, hata yanaweza kuutabiri.

9. Wayahudi wa kale walihusikaje katika kutimizwa kwa Isaya 65:17-19?

9 Utimizo wa kwanza wa Isaya 65:17-19 ulihusisha Wayahudi wa kale ambao, kama alivyotabiri Isaya kwa usahihi, walirudi katika nchi yao, ambako walianzisha tena ibada safi. (Ezra 1:1-4; 3:1-4) Bila shaka, unatambua kwamba walirudi katika nchi yao kwenye dunia ileile wala si kwingineko katika sayari nyingine. Jambo hilo laweza kutusaidia kuelewa maana ya usemi wa Isaya alipotaja mbingu mpya na dunia mpya. Hatuhitaji kukisia-kisia, kama wafanyavyo wengine, juu ya unabii usio dhahiri wa wanadamu ambao hutabiri juu ya wakati ujao. Biblia yenyewe hufafanua alichomaanisha Isaya.

10. Tueleweje “dunia” mpya ambayo Isaya alitabiri?

10 Katika Biblia, nyakati nyingine neno “dunia” halimaanishi sayari yetu. Kwa mfano, Zaburi 96:1 husema hivi: “Mwimbieni BWANA, nchi [“dunia,”NW] yote.” Twajua kwamba dunia yetu—nchi kavu na zile bahari kubwa—haiwezi kuimba. Watu huimba. Naam, Zaburi 96:1 linarejezea watu wa dunia. * Lakini Isaya 65:17 pia hutaja “mbingu mpya.” Ikiwa “dunia” yawakilisha jamii mpya ya watu katika nchi ya Wayahudi, basi “mbingu mpya” ni nini?

11. Usemi “mbingu mpya” ulirejezea nini?

11 Kichapo Cyclopædia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature cha M’Clintock na Strong, chasema hivi: “Wakati wowote mbingu zinapotajwa katika ono la kiunabii, hizo hurejezea . . . muungano wote wa mamlaka zenye kutawala . . . zikiwa juu ya raia na kuwatawala, kama vile mbingu halisi huwa juu ya dunia na kuitawala.” Kuhusu usemi “mbingu na dunia,” Cyclopædia hiyo yasema kwamba ‘katika lugha ya kiunabii usemi huo wamaanisha hali ya kisiasa ya watu wa nyadhifa mbalimbali. Mbingu ndizo zenye enzi; nayo dunia hutawaliwa, watu ambao hutawaliwa na wakuu.’

12. Wayahudi wa kale walipataje kuona “mbingu mpya na dunia mpya”?

12 Wayahudi waliporudi katika nchi yao, walipata kile kiwezacho kuitwa mfumo mpya wa mambo. Kulikuwa na watawala wapya. Zerubabeli, mzao wa Mfalme Daudi, alikuwa gavana, naye Yoshua alikuwa kuhani wa cheo cha juu. (Hagai 1:1, 12; 2:21; Zekaria 6:11) Hao walikuwa “mbingu mpya.” Walikuwa juu ya nini? Hao “mbingu mpya” walikuwa juu ya “dunia mpya,” jamii ya binadamu waliosafishwa, waliokuwa wamerudi katika nchi yao ili kujenga upya Yerusalemu na hekalu lake kwa ajili ya kumwabudu Yehova. Kwa hiyo, katika maana hiyo halisi, kulikuwako mbingu mpya na dunia mpya katika utimizo huo uliowahusisha Wayahudi wakati huo.

13, 14. (a) Twapaswa kuchunguza andiko gani jingine ambapo usemi “mbingu mpya na dunia mpya” wapatikana? (b) Kwa nini unabii wa Petro utupendeze hasa wakati huu?

13 Angalia usije ukakosa kuelewa. Huku si kufasiri Biblia wala kutupia jicho historia ya kale tu. Waweza kuona hilo kwa kufungua andiko jingine ambapo usemi “mbingu mpya na dunia mpya” wapatikana. Katika 2 Petro sura ya 3, utapata usemi huo na kuona kwamba wakati wetu ujao wahusika.

14 Mtume Petro aliandika barua yake zaidi ya miaka 500 baada ya Wayahudi kurudi katika nchi yao. Akiwa mmoja wa mitume wa Yesu, Petro alikuwa akiwaandikia wafuasi wa Kristo, “Bwana” anayetajwa katika 2 Petro 3:2. Katika mstari wa 4, Petro ataja ‘kuwapo kulikoahidiwa’ kwa Yesu ambako kwafanya unabii huo uwe wa maana sana leo. Kuna uthibitisho wa kutosha unaoonyesha kwamba tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Yesu amekuwapo katika maana ya kuwa na mamlaka akiwa Mtawala katika Ufalme wa kimbingu wa Mungu. (Ufunuo 6:1-8; 11:15, 18) Hilo lina maana ya pekee tufikiriapo jambo jingine ambalo Petro alitabiri katika sura hiyo.

15. Unabii wa Petro kuhusu “mbingu mpya” unatimizwaje?

15 Twasoma hivi kwenye 2 Petro 3:13: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” Huenda tayari unajua kwamba Yesu ambaye yuko mbinguni ndiye Mtawala mkuu katika hizo “mbingu mpya.” (Luka 1:32, 33) Hata hivyo, maandiko mengine ya Biblia yanaonyesha kwamba hatawali akiwa peke yake. Yesu aliahidi kwamba mitume na watu wengine kama wao wangekuwa na sehemu mbinguni. Katika kitabu cha Waebrania, mtume Paulo aliwaeleza hao kuwa “washiriki wa mwito wa kimbingu.” Naye Yesu alisema kwamba wale wa kikundi hicho wangeketi katika viti vya enzi pamoja naye mbinguni. (Waebrania 3:1; Mathayo 19:28; Luka 22:28-30; Yohana 14:2, 3) Tunamaanisha kwamba watu wengine wanatawala pamoja na Yesu wakiwa sehemu ya mbingu mpya. Basi, Petro alimaanisha nini alipotumia usemi “dunia mpya”?

16. Ni “dunia [gani] mpya” iliyopo sasa?

16 Kama ilivyo katika utimizo wa kale—kurudi kwa Wayahudi katika nchi yao—utimizo wa sasa wa 2 Petro 3:13 wahusisha watu wanaojinyenyekeza chini ya utawala wa hizo mbingu mpya. Unaweza kuona mamilioni ya watu leo wanaojinyenyekeza kwa furaha chini ya utawala huo. Wananufaika kutokana na programu yake ya elimu na wanajitahidi kufuata sheria zake zipatikanazo katika Biblia. (Isaya 54:13) Hao ndio msingi wa “dunia mpya” katika maana ya kwamba wao ndio jamii ya ulimwenguni pote ya watu wa mataifa yote, lugha zote, na jamii zote, nao hufanya kazi pamoja wakijitiisha chini ya Mfalme anayetawala, Yesu Kristo. Jambo muhimu ni kwamba unaweza kuwa mmoja wao!—Mika 4:1-4.

17, 18. Kwa nini maneno yanayopatikana kwenye 2 Petro 3:13 yanatupa sababu ya kuutazamia wakati ujao?

17 Usidhani kwamba huo ndio mwisho wa mambo, kwamba hatujui barabara mambo yatakayotukia wakati ujao. Kwa kweli, ukichunguza muktadha wa 2 Petro sura ya 3 utaona mambo yanayodokeza kwamba badiliko kubwa litatukia. Katika mstari wa 5 na wa 6, Petro aandika juu ya Furiko la siku ya Noa, Gharika iliyokomesha ulimwengu mwovu wa wakati huo. Katika mstari wa 7, Petro ataja kwamba “mbingu na dunia zilizopo sasa,” mamlaka za utawala na watu pia, zimewekwa akiba kwa ajili ya “siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.” Hilo lathibitisha kwamba usemi “mbingu na dunia” haurejezei sayari yetu, ulimwengu halisi, bali wanadamu na mamlaka zao za utawala.

18 Petro aeleza katika mistari inayofuata kwamba siku ijayo ya Yehova itatokeza usafishaji mkubwa, ikifanya matayarisho kwa ajili ya mbingu mpya na dunia mpya zilizotajwa katika mstari wa 13. Ona mwisho wa mstari huo—“katika hizo uadilifu utakaa.” Je, hilo halidokezi kwamba mabadiliko makubwa mazuri lazima yatukie? Je, hilo halikuzi tazamio la mambo mapya kwelikweli, wakati ambapo wanadamu watafurahia zaidi maisha kuliko wanavyofanya leo? Ikiwa waweza kuelewa hilo, basi umepata kufahamu mambo ambayo Biblia hutabiri, ufahamu ambao ni watu wachache tu wanao.

19. Ni katika kikao gani kitabu cha Ufunuo chataja “mbingu mpya na dunia mpya” zitakazokuja?

19 Lakini acheni tulichunguze jambo hilo zaidi. Tumechunguza usemi “mbingu mpya na dunia mpya” katika Isaya sura ya 65 na pia katika 2 Petro sura ya 3. Sasa fungua Ufunuo sura ya 21, ambapo usemi huo wapatikana tena katika Biblia. Tena, kuelewa kikao kutatusaidia. Sura mbili kabla, katika Ufunuo sura ya 19, twaona vita ya ufananisho ikifafanuliwa kinaganaga—lakini si vita kati ya mataifa yenye uhasama. “Neno la Mungu” yuko kwenye upande mmoja wa vita. Yaelekea unatambua kwamba jina hilo lamrejezea Yesu Kristo. (Yohana 1:1, 14) Yeye yuko mbinguni, na katika ono hili, anaonekana akiwa na majeshi yake ya kimbingu. Akipigana na nani? Sura hiyo yataja “wafalme,” “makamanda wa kijeshi,” na watu wenye nyadhifa mbalimbali, “wadogo na wakubwa.” Pigano hilo lahusu siku ijayo ya Yehova, kuharibiwa kwa uovu. (2 Wathesalonike 1:6-10) Katika sura inayofuata, Ufunuo sura ya 20 yaanza kwa kueleza kuondolewa kwa yule “nyoka wa awali, aliye Ibilisi na Shetani.” Jambo hilo linatutayarisha kuchunguza Ufunuo sura ya 21.

20. Andiko la Ufunuo 21:1 laonyesha kutakuwa na badiliko gani muhimu wakati ujao?

20 Mtume Yohana aanza kwa maneno haya yenye kusisimua: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali, na bahari haipo tena.” Kutokana na mambo ambayo tumeona katika Isaya sura ya 65 na 2 Petro sura ya 3, tuna hakika kwamba hilo halimaanishi kuziondoa mbingu halisi na sayari yetu pamoja na vilindi vyake vya maji. Kama vile sura zinazotangulia zilivyoonyesha, watu waovu na mamlaka zao za utawala, kutia ndani mtawala asiyeonekana, Shetani, wataondolewa. Naam, kinachoahidiwa hapa ni mfumo mpya wa mambo unaohusisha watu duniani.

21, 22. Yohana anatuhakikishia baraka gani, na kufutwa kwa machozi kwamaanisha nini?

21 Tunahakikishiwa jambo hilo tuchunguzapo unabii huu wa ajabu. Mwisho wa mstari wa 3 wazungumzia wakati ambapo Mungu atakuwa na wanadamu, akiwafikiria na kuwanufaisha watu wanaofanya mapenzi yake. (Ezekieli 43:7) Yohana aendelea kusema hivi katika mstari wa 4 na 5: “Naye [Yehova] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali. Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia, husema: ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’” Ni unabii wenye kutia moyo kama nini!

22 Hebu tua ufurahie mambo ambayo Biblia inatabiri. ‘Mungu atafuta kabisa kila chozi katika macho yao.’ Hilo haliwezi kuwa larejezea machozi ya kawaida ambayo husafisha macho yetu yawezayo kudhuriwa kwa urahisi, wala haliwezi kuwa larejezea machozi ya furaha. La, Mungu atafuta kabisa machozi ambayo husababishwa na kuteseka, huzuni, kutamaushwa, kuumizwa, na maumivu makali. Twawezaje kuwa na uhakika? Ahadi hiyo ya Mungu yenye kutokeza yahusianisha kufuta kabisa machozi na ‘kutokuwepo tena kwa kifo, maombolezo, kupaaza kilio, na maumivu.’—Yohana 11:35.

23. Unabii wa Yohana watuhakikishia mwisho wa hali zipi?

23 Je, hilo halithibitishi kwamba kansa, ugonjwa wa ubongo usababishao kupooza, magonjwa ya moyo, na hata kifo zitakuwa zimeondolewa? Ni nani kati yetu ambaye hajafiwa na mpendwa kutokana na ugonjwa fulani, aksidenti, au msiba? Mungu anaahidi hapa kwamba kifo hakitakuwapo tena, jambo linalodokeza kwamba watoto wowote ambao huenda wakazaliwa wakati huo hawatalazimika kukua kisha kuzeeka na hatimaye kufa kutokana na uzee. Unabii huo pia wamaanisha kwamba ugonjwa wa kupungua akili hautakuwapo tena, wala kudhoofika kwa mifupa, magonjwa ya mji wa mimba, magonjwa ya macho—magonjwa ambayo watu huugua sana uzeeni.

24. ‘Mbingu mpya na dunia mpya’ zitakuwaje baraka, na ni nini ambacho bado tutachunguza?

24 Bila shaka, ungekubali kwamba maombolezo na kupaaza kilio kungepungua iwapo kifo, uzee, na maradhi yangeondolewa. Hata hivyo, vipi juu ya ufukara, kuwadhulumu watoto, na ubaguzi wenye uonevu kwa sababu ya malezi au rangi ya ngozi? Kama mambo hayo—yaliyo ya kawaida sana leo—yangeendelea, bado maombolezo na kupaaza kilio zingekuwako. Kwa hiyo, maisha katika “mbingu mpya na dunia mpya” hayataharibiwa na mambo yanayosababisha huzuni leo. Ni badiliko lililoje! Hata hivyo, kufikia hapo tumechunguza maandiko matatu ya Biblia kati ya manne ambayo yanataja “dunia mpya na mbingu mpya.” Kuna andiko jingine ambalo lahusiana na mambo ambayo tumechunguza nalo lakazia sababu inayofanya tutazamie kwa hamu wakati ambapo Mungu atatimiza ahadi yake ya ‘kufanya vitu vyote kuwa vipya.’ Makala inayofuata inazungumzia unabii huo na jinsi unavyochangia furaha yetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Biblia ya The New English Bible hutafsiri Zaburi 96:1 hivi: “Mwimbieni BWANA, enyi watu wote mlio duniani.” Biblia ya The Contemporary English Version husema hivi: “Kila mtu aliye duniani, amwimbie BWANA sifa.” Hilo lapatana na ule uelewevu wa kwamba Isaya alipotaja “dunia mpya,” alikuwa akirejezea watu wa Mungu wakiwa katika nchi yao.

Wakubumbuka Nini?

• Biblia inatabiri juu ya “mbingu mpya na dunia mpya” katika maandiko gani matatu?

• Wayahudi wa kale walihusikaje katika utimizo wa “mbingu mpya na dunia mpya”?

• Utimizo wa “mbingu mpya na dunia mpya” wahusisha nini kama alivyotaja Petro?

Ufunuo sura ya 21 yaonyeshaje kuwepo kwa wakati ujao ulio bora?

[Maswali ya Funzo]

Picha katika ukurasa wa 10

Kama Yehova alivyokuwa ametabiri, Koreshi alifanya matayarisho ili Wayahudi warudi katika nchi yao mwaka wa 537 K.W.K.