Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupambana na Ufisadi kwa Kutumia Upanga wa Roho

Kupambana na Ufisadi kwa Kutumia Upanga wa Roho

Kupambana na Ufisadi kwa Kutumia Upanga wa Roho

“Mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”—Waefeso 4:24.

MILKI ya Roma ilipofikia upeo wake wa maendeleo, ilikuwa ndiyo utawala mkuu zaidi wa binadamu uliopata kutawala duniani. Sheria za Roma zilikuwa nzuri sana hivi kwamba zingali zinatumiwa kama msingi wa sheria za nchi nyingi. Hata hivyo, licha ya maendeleo ya Roma, majeshi yake hayakuweza kushinda adui fulani wa siri: ufisadi. Hatimaye, ufisadi uliharakisha kuanguka kwa Roma.

Mtume Paulo ni baadhi ya wale walioteseka chini ya maofisa fisadi wa Roma. Yaonekana Feliksi, gavana Mroma aliyemhoji, alitambua kuwa Paulo hana hatia. Lakini Feliksi, mmoja wa magavana fisadi zaidi wa wakati wake, aliahirisha kesi ya Paulo, akitumaini Paulo angempa fedha ili aachiliwe huru.—Matendo 24:22-26.

Badala ya kumpa Feliksi rushwa, Paulo alisema naye waziwazi kuhusu “uadilifu na kujidhibiti.” Feliksi hakubadili tabia yake, na Paulo akakaa gerezani badala ya kujaribu kukiuka sheria kwa kutoa rushwa. Alihubiri ujumbe wa kweli na wenye kufuata haki, naye akautekeleza. “Sisi twaitibari tuna dhamiri yenye kufuata haki,” akawaandikia Wakristo Wayahudi, “kwa kuwa twataka kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

Msimamo wake ulikuwa kinyume kabisa cha maadili ya wakati huo. Ndugu ya Feliksi, Palasi, alikuwa mmojawapo wa watu matajiri zaidi katika ulimwengu wa kale, na mali yake—inayokadiriwa kuwa dola milioni 45—ilikusanywa kwa rushwa na kutoza watu kwa nguvu. Hata hivyo, mali yake si kitu ilinganishwapo na mabilioni ya dola ambazo watawala fulani fisadi wa karne ya 20 wamehifadhi katika akaunti za siri za mabenki. Kwa wazi, wajinga pekee ndio wawezao kuamini kwamba serikali za leo zimeshinda pambano dhidi ya ufisadi.

Kwa kuwa ufisadi umekuwepo tangu kale, je, tuamue kwamba ni sehemu tu ya maumbile ya mwanadamu? Au je, hatua fulani yaweza kuchukuliwa ili kuuzuia?

Ufisadi Waweza Kuzuiwaje?

Hatua ya kwanza ya wazi ya kuzuia ufisadi ni kutambua kuwa ufisadi huangamiza na ni mbaya, kwa maana huwanufaisha mafidhuli kwa hasara ya wengine. Hapana shaka maendeleo fulani yamefanywa katika kupambana nao. James Foley, naibu waziri wa mambo ya nje wa Marekani, alisema: “Sote twatambua kwamba rushwa huleta hasara kubwa. Rushwa huharibu utawala mwema, huathiri vibaya maendeleo ya uchumi, huvuruga biashara, na kuwadhuru raia ulimwenguni kote.” Wengi wana maoni kama yake. Siku ya Desemba 17, 1997, nchi kubwa-kubwa 34 zilitia sahihi “mkataba wa rushwa” unaokusudiwa “kuwa na matokeo makubwa katika pambano dhidi ya ufisadi ulimwenguni kote.” Mkataba huo “huharimisha kumpa au kumwahidi ofisa wa serikali rushwa ili kupata au kuendelea kudumisha mapatano ya kibiashara ya kimataifa.”

Hata hivyo, rushwa inayotolewa ili kupata kandarasi katika nchi nyingine ni sehemu ndogo tu ya ufisadi. Yahitajika hatua ya pili, iliyo ngumu zaidi, ili kuukomesha ufisadi kila mahali: kubadili moyo, naam, kubadili mioyo mingi. Lazima watu kila mahali wajifunze kuchukia rushwa na ufisadi. Ndipo hongo itakapokomeshwa. Ili kutimiza hilo, gazeti la Newsweek lilisema kuwa wengine huonelea kuwa serikali zapaswa “kuwaelimisha raia kwa jumla wazingatie maadili.” Vivyo hivyo, wanaharakati wa kikundi kiitwacho Transparency International kinachopambana na ufisadi hupendekeza kwamba wafuasi wao “waendeleze maadili” kazini.

Mapambano dhidi ya rushwa ni mambo ya kiadili yasiyoweza kufanikiwa kwa kutunga sheria tu au kwa “upanga” wa adhabu ya kisheria. (Waroma 13:4, 5) Yapasa maadili yaingizwe katika mioyo ya watu. Hilo lawezekana tu kwa kutumia Neno la Mungu, Biblia, ambalo mtume Paulo aliliita “upanga wa roho.”—Waefeso 6:17.

Biblia Hulaani Ufisadi

Mbona Paulo alikataa ufisadi? Kwa sababu alitaka kufanya mapenzi ya Mungu, “asiyependelea nyuso za watu, wala hakubali rushwa.” (Kumbukumbu la Torati 10:17) Isitoshe, hapana shaka Paulo alikumbuka maagizo hususa katika Sheria ya Musa: “Usipendelee uso wa mtu; wala usitwae rushwa; kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya wenye akili, na kugeuza daawa ya wenye haki.” (Kumbukumbu la Torati 16:19) Mfalme Daudi kadhalika alijua Yehova huchukia ufisadi, naye aliomba kwamba Mungu asimhesabu pamoja na watenda-dhambi, ambao “mkono wao wa kuume umejaa rushwa.”—Zaburi 26:10.

Wanaomwabudu Mungu kwa unyofu wana sababu zaidi za kuukataa ufisadi. “Mfalme akitumia haki huipatia nchi uthabiti,” akaandika Solomoni, “lakini akipenda hongo taifa huangamia.” (Mithali 29:4, Biblia Habari Njema) Haki—hasa inapotekelezwa kuanzia kwa wenye mamlaka ya juu—huleta uthabiti, ilhali ufisadi huletea nchi umaskini. Basi, gazeti la Newsweek lilisema: “Katika nchi ambamo kila mtu hutaka kujinufaisha kwa ufisadi na ajua jinsi ya kufanya hivyo, uchumi huangamia tu.”

Hata uchumi usipoangamia kabisa, wapendao haki huvunjika moyo wakati ufisadi unapoendelea pasipo kudhibitiwa. (Zaburi 73:3, 13) Muumba wetu, aliyetuumba na tamaa ya kupata haki, anakosewa pia. Yehova aliingilia kati nyakati zilizopita ili kuukomesha ufisadi uliokuwa wazi. Kwa mfano, aliwaambia waziwazi wakazi wa Yerusalemu kwa nini angewaacha mikononi mwa adui zao.

Mungu alisema hivi kupitia Mika nabii wake: “Sikieni haya, tafadhali, enyi vichwa vya nyumba ya Yakobo, mnaoitawala nyumba ya Israeli, mnaochukia hukumu, na kuipotosha adili. Wakuu wake huhukumu ili wapate rushwa, na makuhani wake hufundisha ili wapate ijara, na manabii wake hubashiri ili wapate fedha . . . Basi, kwa ajili yenu, Sayuni utalimwa kama shamba lilimwavyo, na Yerusalemu utakuwa magofu.” Ufisadi ulikuwa umeangamiza jamii ya Israeli, kama vile ulivyoangamiza Roma karne kadhaa baadaye. Kupatana na onyo la Mungu, Yerusalemu uliangamizwa na kuachwa ukiwa karibu karne moja baada ya Mika kuyaandika maneno hayo.—Mika 3:9, 11, 12.

Hata hivyo, si lazima mtu au taifa liwe fisadi. Mungu huwahimiza waovu waache njia zao na kubadili mawazo yao. (Isaya 55:7) Ataka kila mmoja wetu awe mkarimu badala ya kuwa mwenye pupa, awe mwadilifu badala ya kuwa fisadi. Yehova atukumbusha kwamba “amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu.”—Mithali 14:31.

Kutumia Kweli ya Biblia ili Kupambana na Ufisadi kwa Mafanikio

Ni nini kiwezacho kumchochea mtu afanye mabadiliko ya aina hiyo? Ni nguvu ile iliyomchochea Paulo kuacha Ufarisayo na kuwa mfuasi mwaminifu wa Yesu Kristo. “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu,” akaandika. (Waebrania 4:12) Leo, kweli ya Maandiko bado huendeleza ufuataji wa haki, hata miongoni mwa wale waliokuwa mafisadi sana. Ona mfano huu.

Muda mfupi baada ya kumaliza utumishi wake jeshini, Alexander, raia wa Ulaya Mashariki, alijiunga na genge lililofanya kazi ya ulaghai, upokonyaji, na ulaji rushwa. * “Kazi yangu ilikuwa kutoza kwa nguvu wanabiashara matajiri fedha za ulinzi,” asema. “Mara mwanabiashara alipopata kuniamini, washiriki wengine wa genge letu walimtisha kwa jeuri. Kisha nilijitolea kushughulikia jambo hilo—kwa kumtoza malipo ghali. ‘Wateja’ wangu walinishukuru kwa kuwasaidia kutatua matatizo yao, ilhali mimi ndiye niliyeyasababisha. Jambo hilo ndilo nililopendelea hasa kuhusiana na kazi yangu, ingawa si la kawaida.

“Pia nilifurahia msisimko na fedha nilizopata kutokana na maisha hayo. Nilikuwa na gari la bei ghali, nikaishi nyumba nzuri, nami nilikuwa na fedha za kununua chochote nilichotaka. Watu waliniogopa, jambo lililonifanya nijihisi kuwa na mamlaka. Nilidhani kwamba hakuna awezaye kunishinda na kwamba siko chini ya sheria. Iwapo matatizo yoyote yangetokea kati yangu na polisi, yangetatuliwa na mwanasheria hodari ambaye alijua mbinu za kushinda kesi mahakamani, au kupitia kutoa rushwa kwa mtu anayehusika.

“Hata hivyo, hakuna uaminifu-mshikamanifu miongoni mwa mafisadi. Mshiriki mmoja wa genge letu alianza kunichukia, nami nikakosana naye. Kwa ghafula, nikapoteza gari la anasa, pesa, na mpenzi wangu aliyependa vitu vya bei ghali. Hata nilipigwa sana. Mabadiliko hayo yalifanya nitafakari kusudi la uhai.

“Mama yangu alikuwa amejiunga na Mashahidi wa Yehova miezi michache mapema, nami nikaanza kusoma vitabu vyao. Andiko la Mithali 4:14, 15 lilifanya nitafakari: ‘Usiingie katika njia ya waovu, wala usitembee katika njia ya wabaya. Jiepushe nayo, usipite karibu nayo, igeukie mbali, ukaende zako.’ Maandiko ya aina hiyo yalinisadikisha kuwa wale wanaotaka maisha ya uhalifu hawana wakati ujao mwema. Nilianza kusali kwa Yehova na kumwomba aniongoze kwa njia inayofaa. Mashahidi wa Yehova walinifundisha Biblia, kisha nikajitoa wakfu kwa Mungu. Tangu wakati huo nimeishi kwa haki.

“Bila shaka, kufuata haki kumefanya nichume fedha kidogo sana. Lakini sasa naona kuwa nina wakati ujao mwema, na maisha yangu yana kusudi la kweli. Nafahamu kwamba maisha yangu ya awali pamoja na faida yake yote ni kama nyumba hafifu ambayo ingeanguka wakati wowote. Dhamiri yangu haikuhisi lolote hapo awali. Lakini sasa, kutokana na funzo langu la Biblia, dhamiri hunichoma kila mara ninaposhawishiwa kutofuata haki—hata katika mambo madogo. Najitahidi kuishi kupatana na Zaburi 37:3, inayosema: ‘Umtumaini BWANA ukatende mema, ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu.’”

“Achukiaye Hongo Ataishi”

Kama vile Alexander alivyogundua, kweli ya Biblia yaweza kumchochea mtu aushinde ufisadi. Alifanya mabadiliko kama yale ambayo mtume Paulo ataja katika barua yake kwa Waefeso: “Mweke mbali utu wa hapo zamani unaofuatana na njia yenu ya kwanza ya mwenendo na ambao unafisidiwa kulingana na tamaa zake za udanganyifu; . . . mfanywe upya katika kani inayotendesha akili yenu, na mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu. Kwa sababu hii, sasa kwa kuwa mmeweka mbali ukosefu wa lililo kweli, semeni kweli kila mmoja wenu pamoja na jirani yake, kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake. Mwibaji na asiibe tena, bali acheni afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili apate kuwa na kitu fulani cha kugawa kwa mtu aliye katika uhitaji.” (Waefeso 4:22-25, 28) Wakati ujao hasa wa mwanadamu hutegemea mabadiliko kama hayo.

Pupa na ufisadi zisipozuiwa, zaweza kuiangamiza dunia, kama zilivyohusika katika kuangamia kwa Milki ya Roma. Hata hivyo, yafurahisha kwamba Muumba wa mwanadamu hakusudii kuacha mambo yafanyike bila utaratibu. Ameazimia “kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.” (Ufunuo 11:18) Na Yehova awaahidi wale wanaotamani ulimwengu usio na ufisadi kwamba karibuni kutakuwako “mbingu mpya na dunia mpya . . . na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kufuata haki leo. Ijapokuwa hivyo, Yehova atuhakikishia kuwa hatimaye, “anayetamani faida ya ulanguzi anaitaabisha jamaa yake, lakini achukiaye hongo ataishi.” * (Mithali 15:27, BHN) Tunapoukataa ufisadi sasa, twaonyesha unyofu wetu tusalipo kwa Mungu: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:10.

Tunapongojea Ufalme huo uchukue hatua, kila mmoja wetu aweza ‘kupanda katika haki’ kwa kukataa kuunga mkono au kujiingiza katika rushwa. (Hosea 10:12) Tukifanya hivyo, maisha yetu pia yatadhihirisha nguvu za Neno la Mungu lililopuliziwa. Upanga wa roho waweza kushinda ufisadi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Jina lake limebadilishwa.

^ fu. 28 Pasipo shaka kuna tofauti kati ya rushwa na bahashishi. Rushwa hutolewa ili kupotoa haki au kwa makusudi mengine mapotovu, lakini bahashishi ni shukrani kwa utumishi uliotolewa. Hayo yameelezwa kwenye “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Oktoba 1, 1986, la Mnara wa Mlinzi.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Biblia yaweza kutusaidia kusitawisha “utu mpya” na kuepuka ufisadi