Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha ya Familia Yenye Furaha Huwavuta Wengine kwa Mungu

Maisha ya Familia Yenye Furaha Huwavuta Wengine kwa Mungu

Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti

Maisha ya Familia Yenye Furaha Huwavuta Wengine kwa Mungu

YEHOVA alimbariki Yosefu kwa kumpa hekima nyingi na ufahamu mwingi. (Matendo 7:10) Ikatukia kwamba ufahamu wenye kina wa Yosefu ‘ukawa mwema machoni pa Farao, na machoni pa watumwa wake wote.’—Mwanzo 41:37.

Vivyo hivyo leo, Yehova huwapa watu wake ufahamu wenye kina kupitia funzo lao la Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Hekima hiyo na ufahamu huo hutokeza matunda mazuri mashauri ya Biblia yanapofuatwa. Mara nyingi mwenendo wao mzuri ‘umekuwa mwema machoni pa wote wenye kutazama,’ kama ionyeshwavyo na mambo yafuatayo yaliyotokea Zimbabwe.

• Majirani wa mwanamke mmoja walikuwa Mashahidi wa Yehova. Ingawa mwanamke huyo hakuwapenda Mashahidi, alivutiwa na mwenendo wao, hasa maisha yao ya familia. Aliona uhusiano mzuri sana uliokuwapo baina ya mume na mke na kwamba watoto wao walikuwa watiifu. Hasa aliona jinsi mume huyo alivyompenda sana mke wake.

Katika tamaduni fulani za Afrika wengi huamini kwamba ikiwa mume ampenda sana mke wake, ni lazima yule mke awe ametumia dawa ya uganga ili “amtiishe” mume huyo. Basi yule mwanamke akamwendea yule mke ambaye ni Shahidi akamwuliza: “Naomba ile dawa ya uganga uliyompa mume wako ili mume wangu naye anipende kama mume wako anavyokupenda.” Yule Shahidi akamjibu: “Ah, ni sawa, nitakuletea kesho alasiri.”

Siku iliyofuata, yule dada akampelekea jirani yake ile “dawa ya uganga.” Dawa hiyo ikawa nini? Ikawa ni Biblia pamoja na kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Baada ya kuchunguza habari inayopatikana katika kitabu cha Ujuzi katika sura isemayo “Kujenga Familia Inayomheshimu Mungu,” yule Shahidi akamwambia yule mwanamke: “Hii ndiyo ‘dawa ya uganga’ ambayo mimi na mume wangu hutumia ili ‘kutiishana,’ na ndiyo sababu tunapendana sana.” Wakaanzisha funzo la Biblia, na mwanamke yule akafanya maendeleo haraka kufikia hatua ya kuonyesha wakfu wake kwa Yehova kwa ubatizo wa maji.

• Mapainia wawili wa pekee wanaotumikia katika eneo lililo karibu na mpaka wa kaskazini-mashariki wa Zimbabwe na Msumbiji hawakushiriki utumishi wa nyumba hadi nyumba kwa majuma mawili. Kwa nini? Kwa sababu watu walikuwa wakiwatembelea kusikiliza ujumbe wao. Mmoja wa mapainia hao asimulia jinsi mambo hayo yalivyotukia: “Tulikuwa tukisafiri kilometa 15 kuongoza funzo la Biblia la nyumbani na mtu mmoja aliyekuwa anapendezwa. Haikuwa rahisi kufikia eneo hilo. Ilitubidi tupitie matopeni na kuvuka mito iliyofurika hivi kwamba maji yalikuwa yakitufikia shingoni. Ilitubidi tuvue mavazi yetu na viatu vyetu na kuvibeba kichwani na kuvalia tena baada ya kufika ng’ambo ya pili.

“Bidii yetu ikawavutia sana majirani wa mtu huyo mwenye kupendezwa. Kiongozi wa dini moja katika eneo hilo alikuwa mmojawapo wa wale waliovutiwa na bidii hiyo. Akawaambia wafuasi wake: ‘Je, hamtaki kuwa wenye bidii kama vijana wale wawili ambao ni Mashahidi wa Yehova?’ Siku iliyofuata, wengi wa wafuasi wake wakaja kwetu ili wajue ni kwa nini sisi ni wenye bidii sana. Zaidi ya hayo, majuma mawili yaliyofuata tulipokea wageni wengi sana hivi kwamba hata tulikosa wakati wa kupika chakula chetu!”

Yule kiongozi wa kidini alikuwa mmojawapo wa wale waliowatembelea mapainia hao katika yale majuma mawili. Wazia shangwe ya wale mapainia mtu yule alipokubali funzo la Biblia la nyumbani!