Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikia Lile Ambalo Roho Husema

Sikia Lile Ambalo Roho Husema

Sikia Lile Ambalo Roho Husema

“Masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.”—ISAYA 30:21.

1, 2. Yehova amewasilianaje na wanadamu tangu zamani?

ANTENA kubwa zaidi na yenye uwezo mkubwa sana wa kunasa habari ulimwenguni inayotumia mawimbi ya redio yapatikana katika kisiwa cha Puerto Riko. Kwa makumi ya miaka, wanasayansi wamekuwa wakitumainia kutumia chombo hicho kikubwa ili kupokea ujumbe kutoka kwa viumbe katika anga la nje. Lakini hakuna ujumbe wowote wa aina hiyo ambao umewahi kupokewa. Hata hivyo, kuna ujumbe ulio wazi kutoka nje ya makao ya kibinadamu ambao yeyote kati yetu aweza kuupokea wakati wowote—bila hata kutumia chombo chochote cha kisasa. Ujumbe huo watokana na chanzo kikuu zaidi kuliko kiumbe chochote kile cha anga la nje kiwezacho kuwaziwa. Ujumbe huo watoka kwa nani, na ni nani wanaoupokea? Ujumbe huo husemaje?

2 Rekodi ya Biblia ina masimulizi kadhaa juu ya pindi ambazo wanadamu waliweza kusikia ujumbe kutoka kwa Mungu. Nyakati nyingine ujumbe huo uliwasilishwa na viumbe wa roho wakiwa wajumbe wa Mungu. (Mwanzo 22:11, 15; Zekaria 4:4, 5; Luka 1:26-28) Sauti ya Yehova mwenyewe ilisikika pindi tatu. (Mathayo 3:17; 17:5; Yohana 12:28, 29) Mungu alinena pia kupitia manabii wa kibinadamu, ambao wengi wao waliandika aliyowapulizia kusema. Leo, tuna Biblia, ambayo inatia ndani rekodi iliyoandikwa juu ya mengi ya mawasiliano hayo, hali kadhalika mafundisho ya Yesu na wanafunzi wake. (Waebrania 1:1, 2) Kwa kweli Yehova amekuwa akiwasiliana na wanadamu aliowaumba.

3. Kusudi la ujumbe mbalimbali wa Mungu ni nini, nasi twatarajiwa kufanya nini?

3 Ujumbe wote huo uliopuliziwa ambao ulitoka kwa Mungu hausemi mengi juu ya ulimwengu halisi. Wakazia mambo muhimu zaidi, ambayo yanahusu uhai wetu sasa na wakati ujao. (Zaburi 19:7-11; 1 Timotheo 4:8) Yehova hutumia ujumbe huo kutujulisha mapenzi yake na kutuongoza. Hiyo ni mojawapo ya njia ambazo maneno ya nabii Isaya hutimizwa: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.” (Isaya 30:21) Yehova hatulazimishi tusikilize “neno” lake. Ni juu yetu kufuata mwelekezo wa Mungu na kutembea katika njia yake. Kwa sababu hiyo, Maandiko hutuonya kwa upole tusikilize ujumbe kutoka kwa Yehova. Katika kitabu cha Ufunuo, twatiwa moyo mara saba ‘tusikie lile ambalo roho husema.’—Ufunuo 2:7, 11, 17, 29; 3:6, 13, 22.

4. Je, kwa kweli twaweza kutarajia Mungu awasiliane nasi moja kwa moja kutoka mbinguni leo?

4 Leo, Yehova hasemi nasi moja kwa moja kutoka mbinguni. Hata katika nyakati za Biblia, mawasiliano hayo ya pekee yalitukia pindi chache, nyakati nyingine hata karne kadhaa kabla ya kusikiwa tena. Katika historia yote, Yehova amewasiliana mara nyingi na watu wake katika njia zisizo za moja kwa moja. Ndivyo ilivyo leo. Acheni tuchanganue njia tatu ambazo Yehova huwasiliana nasi leo.

“Andiko Lote Limepuliziwa”

5. Yehova hutumia nini hasa kuwasiliana nasi leo, nasi twaweza kunufaikaje kutokana nacho?

5 Mungu hutumia Biblia hasa ili kuwasiliana na wanadamu. Imepuliziwa na Mungu, na kila kitu kilichomo chaweza kutunufaisha. (2 Timotheo 3:16) Biblia ina mifano mingi ya watu halisi walioamua kwa hiari kusikiliza au kutosikiliza sauti ya Yehova. Mifano hiyo hutukumbusha umuhimu wa kusikiliza lile ambalo roho ya Mungu husema. (1 Wakorintho 10:11) Pia, Biblia ina hekima yenye kutumika, nayo hutushauri tunapokabili uamuzi fulani maishani. Ni kana kwamba Mungu yu nyuma yetu, akitunong’onezea: “Njia ni hii, ifuateni.”

6. Kwa nini Biblia ni bora zaidi kuliko maandishi mengine yote?

6 Ili kusikia lile ambalo roho husema katika Biblia, lazima tuisome kwa ukawaida. Biblia si mojawapo tu ya vitabu vingi maarufu vipatikanavyo leo ambavyo vimeandikwa vizuri. Biblia imepuliziwa na roho na ina mawazo ya Mungu. Waebrania 4:12 husema hivi: “Kwa maana neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” Tuisomapo Biblia, habari zilizomo hudunga kama upanga hata kufikia mawazo na tamaa zetu zilizo ndani sana, zikifunua ni kwa kadiri gani maisha yetu yanapatana na mapenzi ya Mungu.

7. Kwa nini ni muhimu kusoma Biblia, nasi twatiwa moyo kuisoma mara ngapi?

7 “Fikira na makusudio ya moyo” zaweza kubadilika kadiri wakati upitavyo na kadiri tunavyoathiriwa na mambo tunayojionea maishani—mambo ya kupendeza na magumu. Ikiwa hatujifunzi Neno la Mungu kwa ukawaida, mawazo, mitazamo, na hisia zetu hazitaendelea kupatana na kanuni za Mungu. Kwa hiyo, Biblia hutuonya hivi kwa upole: “Fulizeni kujijaribu kama nyinyi mumo katika imani, fulizeni kujithibitisha wenyewe nyinyi ni nini.” (2 Wakorintho 13:5) Ili tuendelee kusikia lile ambalo roho husema, twapaswa kutii shauri la kusoma Neno la Mungu kila siku.—Zaburi 1:2.

8. Ni maneno gani ya mtume Paulo ambayo hutusaidia kujichunguza kuhusiana na usomaji wa Biblia?

8 Wasomaji wa Biblia wapaswa kukumbuka jambo hili muhimu: Jipe wakati wa kutosha kutafakari mambo unayosoma! Tunapojitahidi kufuata shauri la kusoma Biblia kila siku, haingefaa tusome mbiombio sura kadhaa bila kuelewa tunayosoma. Ingawa ni muhimu kusoma Biblia kwa ukawaida, lengo letu halipaswi kuwa kufuata ratiba fulani tu; twapaswa kutamani kikweli kujifunza juu ya Yehova na makusudi yake. Kwa hiyo, twapaswa kujichunguza wenyewe kwa kutumia maneno ya mtume Paulo. Akiwaandikia Wakristo wenzake, alisema hivi: “Namkunjia Baba magoti yangu, kwa kusudi la kwamba apate kuwaruhusu nyinyi . . . mpate kuwa na Kristo akikaa kupitia imani yenu katika mioyo yenu kwa upendo; ili mpate kutia mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi, ili mpate kwa ukamili kuweza kufahamu kiakili pamoja na watakatifu wote ni nini ulio upana na urefu na kimo na kina, na kuujua upendo wa Kristo uzidio ujuzi, ili mpate kujazwa ujao wote ambao Mungu hutoa.”—Waefeso 3:14, 16-19.

9. Twawezaje kusitawisha na kukuza tamaa ya kujifunza kutokana na Yehova?

9 Ni kweli kwamba baadhi yetu hatupendi kusoma, ilhali wengine ni wasomaji sana. Lakini, hata tuwe watu wa aina gani, twaweza kusitawisha na kukuza tamaa ya kufundishwa na Yehova. Mtume Petro alieleza kwamba twapaswa kuwa na hamu ya kuijua Biblia, naye alitambua kwamba tamaa hiyo huenda ikahitaji kusitawishwa. Aliandika hivi: “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni, fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno, ili kupitia hilo mpate kukua kufikia wokovu.” (1 Petro 2:2) Ili ‘tufanyize hamu sana’ ya kujifunza Biblia, ni lazima tujitie nidhamu. Kama vile tu tunavyoweza kupenda chakula zaidi na zaidi baada ya kukionja mara kadhaa, maoni yetu juu ya kusoma na kujifunza yaweza kubadilika na kuwa mazuri tukijitia nidhamu na kufuata utaratibu fulani kwa kawaida.

‘Chakula kwa Wakati Ufaao’

10. Ni nani walio “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na Yehova anawatumiaje leo?

10 Njia nyingine ambayo Yehova hutumia kusema nasi leo yatambulishwa na Yesu kwenye Mathayo 24:45-47. Alisema juu ya kutaniko la Kikristo lililotiwa mafuta kwa roho—“mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye amewekwa aandae ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ Kila mmoja wa washiriki wa jamii hiyo ni ‘mtumishi wa Yesu wa nyumbani.’ Hao, pamoja na “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” hutiwa moyo na kuongozwa. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Vichapo kama vile Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na vinginevyo ni sehemu kubwa ya chakula kwa wakati ufaao. Chakula zaidi cha kiroho huandaliwa kupitia hotuba na maonyesho kwenye mikusanyiko, makusanyiko na mikutano ya kutaniko.

11. Sisi huonyeshaje kwamba twakubali lile ambalo roho husema kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”?

11 Habari inayoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hukusudiwa kuimarisha imani yetu na kuzoeza nguvu zetu za ufahamu. (Waebrania 5:14) Huenda shauri hilo likawa la ujumla ili kila mmoja alitumie kibinafsi. Mara kwa mara, sisi hupokea pia shauri linalohusu mambo hususa juu ya mwenendo wetu. Twapaswa kuwa na mtazamo gani iwapo kwa kweli twasikiliza lile ambalo roho husema kupitia jamii ya mtumwa? Mtume Paulo ajibu hivi: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea.” (Waebrania 13:17) Ni kweli kwamba wote wanaotumiwa ni wanadamu wasio wakamilifu. Hata hivyo, Yehova hupenda kuwatumia watumishi wake wa kibinadamu, ingawa si wakamilifu, watuongoze wakati huu wa mwisho.

Kuongozwa na Dhamiri Yetu

12, 13. (a) Yehova ametupa mwongozo gani mwingine? (b) Dhamiri yaweza kuwa na uvutano gani unaofaa hata kwa watu wasio na ujuzi sahihi juu ya Neno la Mungu?

12 Yehova ametupa mwongozo mwingine—dhamiri yetu. Alimwumba mwanadamu akiwa na uwezo fulani ndani yake wa kutambua mema na mabaya. Ndivyo tulivyo. Katika barua aliyowaandikia Waroma, mtume Paulo alieleza hivi: “Wakati wowote ule watu wa mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ijapokuwa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. Wao ndio walewale waonyeshao kiini cha sheria kuwa imeandikwa katika mioyo yao, huku dhamiri yao ikitoa ushahidi pamoja nao na, kati ya fikira zao wenyewe, wanashtakiwa au hata wanatetewa.”—Waroma 2:14, 15.

13 Watu wengi wasiomjua Yehova wanaweza, kwa kiasi fulani, kuwaza na kutenda kupatana na kanuni za Mungu za mema na mabaya. Ni kana kwamba wanasikia sauti ndogo ndani yao ikiwaelekeza upande ufaao. Ikiwa watu wasio na ujuzi sahihi juu ya Neno la Mungu waweza kuisikia sauti hiyo, basi, Wakristo wa kweli wapaswa kuisikia hata zaidi! Bila shaka, dhamiri ya Mkristo ambayo imesafishwa na ujuzi sahihi juu ya Neno la Mungu na ambayo hutenda kulingana na roho takatifu ya Yehova yaweza kuandaa mwongozo wenye kutegemeka.—Waroma 9:1.

14. Dhamiri iliyozoezwa na Biblia yaweza kutusaidiaje kufuata mwongozo wa roho ya Yehova?

14 Dhamiri nzuri, ambayo imezoezwa na Biblia, yaweza kutukumbusha njia ambayo roho yataka tufuate. Huenda nyakati fulani Maandiko au vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia visitaje moja kwa moja hali fulani hususa ambamo huenda tukajikuta. Hata hivyo, huenda dhamiri yetu ikatuonya, ikitutahadharisha dhidi ya mwenendo uwezao kutudhuru. Iwapo hivyo, kupuuza maonyo ya dhamiri yetu, kwa kweli kwaweza kuwa kupuuza lile ambalo roho ya Yehova husema. Hali kadhalika, kwa kujifunza kutegemea dhamiri yetu ya Kikristo iliyozoezwa, twaweza kufanya maamuzi mazuri hata wakati ambapo hakuna mwelekezo wowote hususa ulioandikwa. Hata hivyo, ni muhimu kukumbuka kwamba wakati ambapo hakuna kanuni, amri, wala sheria ya Mungu inayohusika, haingefaa kuwasisitizia Wakristo wenzetu maoni ya dhamiri yetu wenyewe katika mambo ambayo ni ya kibinafsi kabisa.—Waroma 14:1-4; Wagalatia 6:5.

15, 16. Ni nini kinachoweza kuifanya dhamiri yetu ikosee, nasi twaweza kuzuiaje hilo lisitokee?

15 Dhamiri safi, iliyozoezwa na Biblia ni zawadi nzuri kutoka kwa Mungu. (Yakobo 1:17) Lakini ili zawadi hiyo iweze kutenda ifaavyo na kutulinda kiadili, lazima tuilinde isije ikaharibiwa na uvutano mbalimbali. Desturi, mapokeo, na mazoea ya kwetu yanayopingana na kanuni za Mungu, yakifuatwa, yaweza kufanya dhamiri yetu ikosee na kushindwa kutuhimiza kuelekea upande ufaao. Huenda tukashindwa kuchanganua mambo ifaavyo na hata kujidanganya na kuamini kwamba tendo fulani baya kwa kweli ni zuri.—Linganisha Yohana 16:2.

16 Tukiendelea kupuuza maonyo ya dhamiri yetu, sauti yake itazidi kufifia hadi tuwe sugu kiadili. Mtunga-zaburi alisema juu ya watu hao aliposema hivi: “Mioyo yao imenenepa [“haina hisia,” NW] kama shahamu.” (Zaburi 119:70) Watu fulani ambao hupuuza maonyo ya dhamiri yao hupoteza uwezo wao wa kufikiri sawasawa. Hawaongozwi tena na kanuni za Mungu na hawawezi kufanya maamuzi yafaayo. Ili kuepuka hali hiyo, twapaswa kukubali mwongozo wa dhamiri ya Kikristo hata jambo lionekanapo kuwa dogo.—Luka 16:10.

Wenye Furaha Ni Wale Wasikilizao na Kutii

17. Tusikilizapo ‘neno nyuma yetu’ na kutii dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia, tutabarikiwaje?

17 Tujizoezapo kusikiliza ‘neno nyuma yetu’—linapoandaliwa kupitia Maandiko na mtumwa mwaminifu na mwenye busara—na tutiipo makumbusho ya dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia, Yehova atatubariki kwa roho yake. Roho takatifu nayo itaboresha uwezo wetu wa kupokea na kuelewa mambo ambayo Yehova anatuambia.

18, 19. Mwongozo wa Yehova waweza kutunufaishaje katika huduma yetu, na maishani mwetu?

18 Pia, roho ya Yehova itatupa ujasiri wa kukabili hali ngumu kwa hekima na moyo mkuu. Kama roho ya Mungu ilivyochochea mitume, yaweza kuchochea nguvu zetu za kiakili na kutusaidia sikuzote tutende na kunena kulingana na kanuni za Biblia. (Mathayo 10:18-20; Yohana 14:26; Matendo 4:5-8, 13, 31; 15:28) Roho ya Yehova pamoja na jitihada zetu wenyewe zitatufanikisha kufanya maamuzi muhimu maishani, zikitupa moyo mkuu wa kutekeleza maamuzi hayo. Kwa mfano, huenda ukawa unafikiria kubadili maisha yako na kutumia wakati mwingi zaidi kwa mambo ya kiroho. Au huenda ukakabili maamuzi muhimu ambayo yatabadili maisha yako, kama vile kuchagua mwenzi wa ndoa, kuchunguza kwa uangalifu kazi ambayo tumeahidiwa, au kununua nyumba. Badala ya kujiachilia tuongozwe na hisia zetu peke yake tunapoamua, twapaswa kusikiliza lile ambalo roho ya Mungu husema na kutenda kulingana na mwongozo wake.

19 Sisi huthamini kwelikweli makumbusho na mashauri tunayopokea kutoka kwa Wakristo wenzetu, kutia ndani na wazee. Hata hivyo, hatuhitaji kungojea wengine waturekebishe. Ikiwa twajua njia tunayopaswa kufuata na marekebisho ambayo twahitaji kufanya katika mtazamo na mwenendo wetu ili tumpendeze Mungu, basi tufanye hivyo. Yesu alisema hivi: “Ikiwa mwajua mambo haya, wenye furaha ni nyinyi ikiwa mwayafanya.”—Yohana 13:17.

20. Wale ambao husikiliza ‘neno nyuma yao’ hupata baraka gani?

20 Yaonekana kwamba ili kujua jinsi ya kumpendeza Mungu, Wakristo hawahitaji kusikia sauti halisi kutoka mbinguni, wala hawahitaji kutembelewa na malaika. Wamebarikiwa kuwa na Neno la Mungu lililoandikwa na mwongozo wenye upendo kupitia jamii yake ya watiwa-mafuta walio duniani. Wakisikiliza kwa makini ‘neno hilo nyuma yao’ na kufuata mwongozo wa dhamiri zilizozoezwa na Biblia, watafanikiwa kufanya mapenzi ya Mungu. Kisha bila shaka wataona utimizo wa ahadi ya mtume Yohana: “Yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17.

Pitio Fupi

• Kwa nini Yehova huwasiliana na wanadamu aliowaumba?

• Kusoma Biblia kwa ukawaida kwaweza kutunufaishaje?

• Twapaswa kuitikiaje mwelekezo wa jamii ya mtumwa?

• Kwa nini hatupaswi kupuuza mwongozo wa dhamiri iliyozoezwa na Biblia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mwanadamu hahitaji chombo cha kisasa ili kupokea ujumbe kutoka kwa Mungu

[Hisani]

Courtesy Arecibo Observatory/David Parker/Science Photo Library

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova husema nasi kupitia Biblia na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”