Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tegemeza kwa Uthabiti Fundisho la Mungu

Tegemeza kwa Uthabiti Fundisho la Mungu

Tegemeza kwa Uthabiti Fundisho la Mungu

“Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”—MITHALI 3:5, 6.

1. Kuna uwezekano gani wa kupata ujuzi wa kibinadamu kwa njia isiyo na kifani?

LEO hii, kuna magazeti ya kila siku yapatayo 9,000 ulimwenguni pote. Kila mwaka vitabu vipya vipatavyo 200,000 huchapishwa Marekani peke yake. Kulingana na kadirio moja, kufikia Machi mwaka wa 1998, Internet ilikuwa na vituo vipatavyo milioni 275. Yasemekana kwamba vituo milioni 20 huongezeka kila mwezi. Watu wanaweza kupata habari zozote zile kwa njia isiyo na kifani. Ingawa kuna manufaa, kupatikana kwa habari nyingi hivyo kumesababisha matatizo.

2. Ni matatizo gani yanayoweza kuzuka kwa sababu ya kuwepo kwa habari chungu nzima?

2 Watu fulani wamekuwa waraibu wa habari, nyakati zote wakijaribu kutosheleza tamaa isiyo na kikomo ya kutaka kujua kila kitu kinachoendelea huku wakipuuza mambo muhimu zaidi. Wengine hupata habari nusu-nusu juu ya mambo magumu ya kielimu kisha wanajiona kuwa wataalamu. Wakitegemea ujuzi kidogo walio nao, wao hufanya maamuzi makubwa ambayo yaweza kuwadhuru wao wenyewe au wengine. Pia kuna hatari ya kupata habari zisizo za kweli au zisizo sahihi. Mara nyingi hakuna njia yenye kutegemeka ya kuthibitisha iwapo habari hizo nyingi ni za kweli na zenye kutegemeka.

3. Biblia hutoa maonyo gani dhidi ya kufuatia hekima ya kibinadamu?

3 Kwa muda mrefu, mwanadamu amekuwa na tabia ya kutaka kujua mambo. Hatari ya kupoteza wakati mwingi sana katika kutafuta habari zisizo na faida au hata zenye kudhuru ilionekana katika siku za Mfalme Solomoni. Alisema hivi: “Kubali maonyo; hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.” (Mhubiri 12:12) Karne kadhaa baadaye mtume Paulo alimwandikia Timotheo akimwambia: “Linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu na kutoka kwenye mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli. Kwa kufanya wonyesho wa ujuzi wa namna hiyo wengine wamekengeuka kutoka kwenye imani.” (1 Timotheo 6:20, 21) Naam, Wakristo leo wapaswa kujiepusha na mawazo yenye kudhuru.

4. Ni ipi mojawapo ya njia tunazoweza kudhihirisha kwamba twamtumaini Yehova na mafundisho yake?

4 Watu wa Yehova pia huonyesha hekima kwa kutii maneno ya Mithali 3:5, 6: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Kumtumaini Yehova hutia ndani kukataa wazo lolote ambalo hupingana na Neno la Mungu, liwe latokana na fikira zetu wenyewe au za mwenzetu. Ili kulinda hali yetu ya kiroho, ni muhimu tuzoeze nguvu zetu za ufahamu ili tuweze kutambua habari yenye kudhuru na kuiepuka sikuzote. (Waebrania 5:14) Basi acheni tuzungumzie baadhi ya vyanzo vya habari hiyo.

Ulimwengu Ambao Shetani Ameuzidi Nguvu

5. Mojawapo ya vyanzo vya mawazo yenye kudhuru ni gani, na mwanzilishi ni nani?

5 Ulimwengu hutokeza mawazo tele yenye kudhuru. (1 Wakorintho 3:19) Yesu Kristo alimwomba Mungu juu ya wanafunzi wake akisema: “Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.” (Yohana 17:15) Yesu alipoomba kwamba wanafunzi wake walindwe kwa sababu ya “yule mwovu” alionyesha kwamba Shetani ana uvutano ulimwenguni. Hatulindwi dhidi ya uvutano mbaya wa ulimwengu kwa kuwa tu sisi ni Wakristo. Yohana aliandika hivi: “Sisi twajua twatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Hasa wakati huu, mwishoni mwa siku za mwisho, yatarajiwa kwamba Shetani na roho wake waovu wataufurika ulimwengu kwa habari zenye kudhuru.

6. Vitumbuizo vyaweza kumfanyaje mtu awe sugu kiadili?

6 Pia yatarajiwa kwamba huenda baadhi ya habari hizo zenye kudhuru zikaonekana kuwa zisizo na madhara yoyote. (2 Wakorintho 11:14) Kwa mfano, fikiria vitumbuizo, vinavyotia ndani vipindi vya televisheni, sinema, muziki, na vichapo. Watu wengi wanakubali kwamba katika visa vingi zaidi na zaidi, baadhi ya vitumbuizo hutokeza mazoea mapotovu, kama vile ukosefu wa maadili, ujeuri, na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. Mwanzoni, huenda vitumbuizo hivyo vilivyopotoka vikawashtua sana watu. Lakini, vikirudiwa-rudiwa, vyaweza kumfanya mtu awe sugu. Hatupaswi kamwe kuviona vitumbuizo vyenye kutokeza mawazo yenye kudhuru kuwa vyenye kukubalika au visivyo na madhara yoyote.—Zaburi 119:37.

7. Ni aina gani ya hekima ya kibinadamu inayoweza kudhoofisha polepole uhakika wetu juu ya Biblia?

7 Fikiria chanzo kingine cha habari zinazoweza kudhuru—zile nadharia chungu nzima zinazochapishwa na wanasayansi na wasomi fulani wanaodai kwamba Biblia haitumainiki. (Linganisha Yakobo 3:15.) Habari hizo zapatikana mara nyingi kwenye magazeti na vitabu maarufu, nazo zaweza kudhoofisha polepole uhakika wetu juu ya Biblia. Watu fulani hujivunia kudhoofisha mamlaka ya Neno la Mungu kwa kukisia-kisia mambo. Hatari kama hiyo ilikuwepo siku za mitume, kama ionekanavyo wazi kutokana na maneno ya mtume Paulo: “Jihadharini: labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.

Adui za Ile Kweli

8, 9. Uasi-imani wajidhihirishaje leo?

8 Waasi-imani pia wanaweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho. Mtume Paulo alitabiri kwamba uasi-imani ungezuka miongoni mwa watu waliodai kuwa Wakristo. (Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3) Maneno yake yalitimia wakati ambapo, baada ya mitume kufa, uasi-imani mkubwa ulitokeza Jumuiya ya Wakristo. Leo, hakuna uasi-imani mkubwa unaozuka miongoni mwa watu wa Mungu. Hata hivyo, watu kadhaa wametuacha, na baadhi yao wameazimia kuwaharibia jina Mashahidi wa Yehova kwa kueneza uwongo na habari zilizopotoka. Baadhi yao hushirikiana na vikundi vingine ili kupinga ibada safi. Wafanyapo hivyo, wao huungana na mwasi-imani wa kwanza kabisa, Shetani.

9 Waasi-imani fulani wanazidi kutumia njia mbalimbali za mawasiliano ya umma, kutia ndani Internet, ili kueneza habari zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, watu wenye mioyo safi wanapochunguza itikadi zetu, huenda wakapata propaganda hizo za waasi-imani. Hata baadhi ya Mashahidi walijiweka katika hatari ya kupata habari hizo bila kujua. Isitoshe, pindi kwa pindi waasi-imani hushiriki katika vipindi vya televisheni au redio. Hilo litukiapo, jambo la hekima kufanya ni nini?

10. Twaweza kukabilianaje na propaganda za uasi-imani kwa hekima?

10 Mtume Yohana aliwaagiza Wakristo wasiwakaribishe waasi-imani nyumbani kwao. Aliandika hivi: “Ikiwa yeyote aja kwenu na haleti ufundishaji huu, msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kusema salamu kwake. Kwa maana yeye asemaye salamu kwake ni mshiriki katika kazi zake mbovu.” (2 Yohana 10, 11) Kuepuka kushirikiana kwa njia yoyote ile na wapinzani hao kutatulinda dhidi ya fikira zao zenye kufisidi. Kujiweka katika hatari ya kupokea mafundisho ya waasi-imani kupitia vyombo vya habari vya kisasa kungetudhuru kama vile tu kumkaribisha mwasi-imani mwenyewe nyumbani kwetu. Tusiruhusu kamwe hamu ya kutaka kujua mambo itushawishi tufanye mambo yawezayo kutuletea msiba!—Mithali 22:3.

Kutanikoni

11, 12. (a) Habari zenye kudhuru katika kutaniko la karne ya kwanza zilitoka wapi? (b) Wakristo fulani walishindwaje kutegemeza kwa uthabiti mafundisho ya Mungu?

11 Fikiria chanzo kingine tena kiwezacho kutokeza mawazo yenye kudhuru. Ingawa huenda Mkristo aliyejiweka wakfu asinuie kufundisha habari zisizo za kweli, huenda akasitawisha zoea la kunena bila kufikiri. (Mithali 12:18) Kwa sababu ya kutokamilika, sisi sote hukosea kwa ulimi wetu nyakati fulani. (Mithali 10:19; Yakobo 3:8) Yaonekana kwamba, katika siku za Paulo, kulikuwako watu fulani kutanikoni walioshindwa kuongoza ulimi wao, wakahusika katika mashindano ya maneno. (1 Timotheo 2:8) Wengine nao walishikilia mno maoni yao hata wakafikia hatua ya kupinga mamlaka ya Paulo. (2 Wakorintho 10:10-12) Roho hiyo ilitokeza ugomvi wa bure.

12 Nyakati nyingine kutokubaliana huko kulileta “mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo,” na kuharibu amani ya kutaniko. (1 Timotheo 6:5; Wagalatia 5:15) Paulo aliandika hivi juu ya waliosababisha ubishi huo: “Ikiwa mtu yeyote afundisha fundisho jingine na hakubaliani na maneno yenye afya, yale ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala na fundisho ambalo lapatana na ujitoaji-kimungu, yeye ametutumuka kwa kiburi, akiwa asiyeelewa kitu chochote, bali akiwa mwenye maradhi ya kiakili juu ya maswali-maswali na mashindano juu ya maneno. Kutoka katika mambo haya huchipuka husuda, zogo, semi zenye kuudhi, shuku zenye uovu.”—1 Timotheo 6:3, 4.

13. Wengi wa Wakristo katika karne ya kwanza walikuwa na mwenendo wa aina gani?

13 Yapendeza kujua kwamba katika nyakati za mitume, wengi wa Wakristo walikuwa waaminifu na waliendelea kuzingatia kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Walijishughulisha kutazama “mayatima na wajane katika dhiki yao” na kujitunza wenyewe “bila doa kutokana na ulimwengu,” bila kupoteza wakati wao wakibishana bure juu ya maneno. (Yakobo 1:27) Waliepuka “mashirika mabaya” hata ndani ya kutaniko la Kikristo ili walinde hali yao ya kiroho.—1 Wakorintho 15:33; 2 Timotheo 2:20, 21.

14. Tusipojihadhari, majadiliano ya kawaida yaweza kubadilikaje na kuwa ubishi wenye kudhuru?

14 Leo pia, hali zilizotajwa kwenye fungu la 11 hazipatikani sana katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, twaonyesha hekima tukitambua kwamba mabishano hayo ya bure yaweza kuzuka. Bila shaka, ni sawa kujadiliana masimulizi ya Biblia au kutaka kujua juu ya hali mbalimbali za ulimwengu mpya uliotabiriwa ambazo kufikia sasa hazijulikani bado. Wala hakuna ubaya wowote wa kujadiliana mambo ya kibinafsi, kama vile mavazi na mapambo au aina za vitumbuizo. Hata hivyo, tukiwa wenye kushikilia maoni yetu sana na kukasirika wengine wasipokubaliana nasi, huenda kutaniko likagawanyika kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Mazungumzo ambayo mwanzoni hayana madhara yoyote yaweza kutokeza madhara kwelikweli.

Kuilinda Amana Yetu

15. “Mafundisho ya roho waovu” yaweza kutudhuru kiroho kwa kadiri gani, na Maandiko yanatushaurije?

15 Mtume Paulo aonya hivi: “Tamko lililopuliziwa lasema wazi kwamba katika vipindi vya wakati vya baadaye wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakikazia uangalifu matamko yaliyopuliziwa yenye kuongoza vibaya na mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:1) Naam, mawazo yenye kudhuru ni hatari kwelikweli. Yaeleweka ni kwa nini Paulo alimsihi hivi rafiki yake mpendwa Timotheo: “Ewe Timotheo, linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu na kutoka kwenye mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli. Kwa kufanya wonyesho wa ujuzi wa namna hiyo wengine wamekengeuka kutoka kwenye imani.”—1 Timotheo 6:20, 21.

16, 17. Mungu ametukabidhi nini, nasi twapaswa kuilindaje?

16 Sisi leo twaweza kunufaishwaje na onyo hilo lenye upendo? Timotheo alipewa amana—kitu chenye thamani, akitunze na kukilinda. Ilikuwa nini? Paulo aeleza: “Fuliza kushika kiolezo cha maneno yenye afya ulichosikia kutoka kwangu pamoja na imani na upendo vinavyohusiana na Kristo Yesu. Amana hii bora ilinde kupitia roho takatifu inayokaa katika sisi.” (2 Timotheo 1:13, 14) Naam, amana ya Timotheo ilitia ndani “maneno yenye afya,” “fundisho ambalo lapatana na ujitoaji-kimungu.” (1 Timotheo 6:3) Kwa kupatana na maneno hayo, Wakristo leo wameazimia kulinda imani yao na kweli zote ambazo wamekabidhiwa.

17 Kulinda amana hiyo hutia ndani kusitawisha mambo kama vile mazoea mazuri ya kujifunza Biblia na kudumu katika sala, huku ‘tukifanya lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.’ (Wagalatia 6:10; Waroma 12:11-17) Paulo azidi kuonya hivi kwa upole: “Fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole. Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele ambao uliitiwa nawe ukatoa tangazo bora la hadharani mbele ya mashahidi wengi.” (1 Timotheo 6:11, 12) Paulo anaposema “Pigana pigano bora” na “pata mshiko imara” anaonyesha wazi kwamba lazima tuchukue hatua na kuazimia kupinga uvutano mbalimbali wenye kudhuru kiroho.

Ufahamu Wahitajiwa

18. Twaweza kuonyeshaje usawaziko wa Kikristo katika jinsi tunavyoziona habari za kilimwengu?

18 Bila shaka, katika kupigana pigano bora la imani, ufahamu wahitajiwa. (Mithali 2:11; Wafilipi 1:9) Kwa mfano, ungekuwa upumbavu kutotumaini habari zote za kilimwengu. (Wafilipi 4:5; Yakobo 3:17) Baadhi ya mawazo ya kibinadamu hayapingani na Neno la Mungu. Yesu alidokeza kwamba wagonjwa wahitaji kumwendea tabibu anayestahili—mtaalamu wa kilimwengu. (Luka 5:31) Licha ya kwamba matibabu yaliyokuwapo wakati wa Yesu yalikuwa duni, alikiri kwamba manufaa fulani yangeweza kupatikana kutokana na msaada wa tabibu. Wakristo leo huonyesha usawaziko kuhusiana na habari za kilimwengu, lakini wao hukataa kujiweka katika hatari ya kupata habari zinazoweza kuwadhuru kiroho.

19, 20. (a) Wazee hutendaje kwa ufahamu wanapowasaidia wale wanaosema bila hekima? (b) Kutaniko hushughulikaje na wale ambao huendeleza kwa kichwa kigumu mafundisho yasiyo ya kweli?

19 Wazee pia wanapaswa kutumia ufahamu wanapowasaidia wasemao bila hekima. (2 Timotheo 2:7) Nyakati nyingine, washiriki wa kutaniko waweza kujikuta wakibishana juu ya mambo madogo-madogo na ya kukisia-kisia. Ili kudumisha muungano wa kutaniko, wazee wapaswa kushughulikia matatizo hayo upesi. Wakati huohuo, wanaepuka kuwashuku ndugu zao kuwa wenye nia mbaya au kuwaona mara moja kuwa waasi-imani.

20 Paulo alieleza mtazamo ambao wazee wapaswa kuwa nao watoapo msaada. Alisema hivi: “Akina ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua, nyinyi mlio na sifa za ustahili wa kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole.” (Wagalatia 6:1) Akisema hasa juu ya Wakristo wenye shaka nyingi, Yuda aliandika hivi: “Endeleeni kuwaonyesha rehema baadhi ya walio na shaka; waokoeni kwa kuwanyakua kutoka katika moto.” (Yuda 22, 23) Bila shaka, iwapo baada ya kumwonya mtu fulani tena na tena bado anaendeleza kwa kichwa kigumu mafundisho yasiyo ya kweli, wazee wahitaji kuchukua hatua thabiti ili kulinda kutaniko.—1 Timotheo 1:20; Tito 3:10, 11.

Kujaza Akilini Mwetu Mambo Yanayostahili Sifa

21, 22. Twapaswa kuteua nini, na twapaswa kujaza nini akilini mwetu?

21 Kutaniko la Kikristo huepuka maneno yenye kudhuru ambayo ‘husambaa kama kioza cha kidonda.’ (2 Timotheo 2:16, 17; Tito 3:9) Huepuka maneno hayo yenye kudhuru iwe yadhihirisha “hekima” ya kilimwengu yenye kupotosha, propaganda za waasi-imani, au maneno yanayosemwa kutanikoni bila kufikiriwa. Ingawa tamaa inayofaa ya kujifunza mambo mapya hunufaisha, hamu isiyo na mipaka ya kutaka kujua mambo yaweza kumweka mtu katika hatari ya kupata mawazo yenye kudhuru. Twazijua mbinu za Shetani. (2 Wakorintho 2:11) Twajua kwamba anajitahidi sana kutukengeusha ili atufanye tupunguze mwendo wetu katika utumishi wa Mungu.

22 Tukiwa wahudumu bora, na tutegemeze kwa uthabiti fundisho la Mungu. (1 Timotheo 4:6) Na tutumie wakati wetu kwa hekima kwa kuteua habari tunayochagua kupokea. Tukifanya hivyo, hatutatikiswa kwa urahisi na propaganda zinazotokana na Shetani. Naam, na tuendelee kufikiria “mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaikio zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa likiwako.” Tukijaza mambo hayo akilini na mioyoni mwetu, Mungu wa amani atakuwa nasi.—Wafilipi 4:8, 9.

Tumejifunza Nini?

• Hekima ya kilimwengu yaweza kuhatarishaje hali yetu ya kiroho?

• Twaweza kujilindaje dhidi ya habari za uasi-imani zenye kudhuru?

• Ni usemi wa aina gani unaopasa kuepukwa kutanikoni?

• Usawaziko wa Kikristo huonyeshwaje wakati wa kushughulika na habari chungu nzima zilizopo leo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Magazeti mengi na vitabu vingi maarufu hupingana na kanuni zetu za Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo waweza kujadiliana bila kushikilia maoni yao sana