Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mkubwa Zaidi Kuliko Mioyo Yetu

Yehova Ni Mkubwa Zaidi Kuliko Mioyo Yetu

Yehova Ni Mkubwa Zaidi Kuliko Mioyo Yetu

“YEHOVA hufurahishwa na wale wanaomhofu,” akaandika mtunga-zaburi. Kwa kweli, Muumba hufurahi anapoona kila mmoja wa watumishi wake wanadamu akijitahidi kushika kanuni zake zenye uadilifu. Mungu huwabariki waaminifu-washikamanifu wake, huwatia moyo, na kuwafariji wanapokata tamaa. Yeye anajua kuwa waabudu wake si wakamilifu, kwa hiyo yeye ni mwenye kiasi kuhusiana na anayotarajia watimize.—Zaburi 147:11, NW.

Huenda isiwe vigumu kwetu kuamini kwamba Yehova anawapenda sana watumishi wake kwa ujumla. Hata hivyo, inaonekana wengi hujishughulisha mno na kasoro zao hivi kwamba wanaamini kuwa Yehova hawezi kamwe kuwapenda. Huenda wakakata kauli, “Nimekosa ukamilifu sana hivi kwamba Yehova hawezi kunipenda.” Bila shaka, sote huwa na hisia zisizofaa mara kwa mara. Lakini inaonekana wengine hupambana daima na hisia zinazowafanya wahisi hawafai kitu.

Hisia za Kuvunjika Moyo

Katika nyakati za Biblia waaminifu kadhaa walivunjika moyo sana. Yobu alichukia maisha na kuhisi kwamba Mungu alikuwa amemwacha. Hana, aliyemzaa Samweli, alisononeka sana kwa kukosa mtoto, akalia kwa uchungu. Daudi ‘alipindika na kuinama sana,’ naye Epafrodito alishuka moyo kwa sababu habari za ugonjwa wake ziliwahuzunisha akina ndugu.—Zaburi 38:6; 1 Samweli 1:7, 10; Ayubu 29:2, 4, 5; Wafilipi 2:25, 26.

Namna gani Wakristo leo? Labda ugonjwa, kuzeeka, au hali nyinginezo za kibinafsi huzuia wengine wasifanye mengi katika utumishi mtakatifu kama vile ambavyo wangetaka. Huenda jambo hilo likawafanya wakate kauli kwamba wanamkosea Yehova na waamini wenzao. Au huenda wengine wakajilaumu daima kwa makosa ya wakati uliopita, wakitilia shaka kwamba Yehova amewasamehe. Labda wengine waliokulia katika hali ngumu za kifamilia wanaamini kwamba hawastahili kabisa kupendwa. Hilo lawezekanaje?

Watu wengine hukulia katika familia ambako roho ya ubinafsi, kejeli, na hofu ndiyo hudhihirishwa zaidi kuliko roho ya upendo. Huenda wasipate kamwe kujua kama inawezekana kuwa na baba anayewapenda, anayetafuta fursa za kuwapongeza na kuwatia moyo, asiyetilia maanani makosa madogo-madogo na aliye tayari kuwasamehe hata makosa mazito, na ambaye uchangamfu wake hufanya familia nzima ihisi salama. Kwa kuwa hawakupendwa na baba zao, huenda ikawa vigumu kwao kuelewa kinachomaanishwa na kuwa na Baba wa mbinguni anayewapenda.

Kwa mfano, Fritz aandika: “Maisha yangu nikiwa mtoto na nikiwa kijana yaliathiriwa sana na tabia ya baba ya kutoonyesha upendo. * Hakuwa akitoa pongezi hata kidogo, nami sikuwa na ukaribu naye. Hata nyakati nyingi nilimwogopa.” Kwa sababu hiyo, Fritz, ambaye sasa ana umri wa miaka 50, angali anahisi hafai. Naye Margarette aeleza: “Wazazi wangu hawakunionyesha urafiki wala upendo. Nilipoanza kujifunza Biblia, ilikuwa vigumu kwangu kuelewa jinsi baba mwenye upendo alivyo.”

Hisia kama hizo, hata ziwe zimesababishwa na nini, zinaweza kumaanisha kwamba nyakati nyingine utumishi wetu kwa Mungu hauchochewi hasa na upendo, bali huchochewa kwa kadiri kubwa na hali ya kujihisi wenye hatia au wenye hofu. Hatuoni kama tunajitahidi vya kutosha. Tamaa ya kumpendeza Yehova na waamini wenzetu huenda ikatufanya tuhisi kwamba hatuwezi kufanya yote tutakayo kufanya. Kwa sababu hiyo huenda tukashindwa kutimiza miradi yetu, tukajilaumu, na kushuka moyo.

Tunaweza kufanya nini? Labda tunahitaji kujikumbusha kadiri ya wema wa Yehova. Mtume Yohana alielewa sifa hiyo yenye upendo ya utu wa Mungu.

“Mungu Ni Mkubwa Zaidi Kuliko Mioyo Yetu”

Mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Yohana aliwaandikia waamini wenzake hivi: “Kwa hili tutajua kwamba twatokana na kweli, na tutahakikishia mioyo yetu mbele yake kwa habari ya chochote kile ambacho mioyo yetu huenda ikatulaumu katika hicho, kwa sababu Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.” Kwa nini Yohana aliandika maneno hayo?—1 Yohana 3:19, 20.

Yohana alijua vizuri kwamba inawezekana kwa mtumishi wa Yehova kujihisi mwenye hatia. Labda Yohana mwenyewe alipatwa na hisia kama hizo. Akiwa mwanamume kijana mwenye hasira kali, Yohana alisahihishwa mara kwa mara na Yesu Kristo kwa kuwa mkali mno aliposhughulika na wengine. Hata Yesu alimpa Yohana na ndugu yake Yakobo “jina la ziada Boanerge, ambalo lamaanisha Wana wa Ngurumo.”—Marko 3:17; Luka 9:49-56.

Katika miaka 60 iliyofuata, Yohana akawa mpole, akawa Mkristo mwenye usawaziko, mwenye upendo, na mwenye rehema. Kufikia wakati ambapo yeye, akiwa mtume wa mwisho aliye hai, aliandika barua yake ya kwanza iliyopuliziwa, alijua kwamba Yehova hashutumu kila mmoja wa watumishi wake kwa kila kosa dogo afanyalo. Bali, yeye ni Baba mchangamfu, mwema, mkarimu, na mwenye huruma, anayewapenda sana wanaompenda na kumwabudu katika kweli. Yohana aliandika: “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.

Yehova Hufurahia Utumishi Wetu Kwake

Mungu anajua udhaifu na kasoro tulizozaliwa nazo, naye huzifikiria. “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi,” akaandika Daudi. Yehova anajua jinsi ambavyo malezi yetu yameathiri utu wetu. Hata anatujua vema zaidi ya vile tujijuavyo.—Zaburi 103:14.

Anajua kwamba wengi wetu tungetaka kuwa tofauti na vile tulivyo, lakini hatuwezi kushinda hali yetu ya kutokamilika. Hali yetu inaweza kulinganishwa na ile ya mtume Paulo aliyeandika: “Jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” Sote tunapambana na hali hiyohiyo. Nyakati nyingine huenda jambo hilo likafanya tujihisi wenye hatia.—Waroma 7:19.

Kumbuka jambo hili sikuzote: Jambo muhimu zaidi ni vile Yehova atuonavyo, si vile tujionavyo. Anapoona tukijitahidi kumfurahisha, yeye huitikia si kwa kuonyesha kuridhika kidogo tu bali kwa furaha. (Mithali 27:11) Ingawa huenda yale tunayotimiza yakaonekana kuwa madogo kwa kulinganisha, utayari wetu na nia yetu nzuri humfurahisha. Yeye hatazami tu yale tunayotimiza; anatambua yale tunayotaka kufanya; anajua mapendezi yetu. Yehova anaweza kujua yaliyo moyoni mwetu.—Yeremia 12:3; 17:10.

Kwa mfano, wengi wa Mashahidi wa Yehova ni wenye haya na wanyamavu kiasili, watu wasiopenda kujitokeza sana. Kwa watu kama hao, kuhubiri habari njema nyumba hadi nyumba kwaweza kuwa jambo gumu lenye kuogofya. Hata hivyo, kwa kusukumwa na tamaa ya kumtumikia Mungu na kusaidia jirani, hata Mashahidi walio na haya hujifunza kuwafikia majirani wao na kuzungumza juu ya Biblia. Huenda wakahisi kwamba wanatimiza machache sana, na huenda jambo hilo likawafanya wakose furaha. Huenda moyo wao ukawaonyesha kwamba utumishi wao haufai. Lakini kwa kweli Yehova hufurahia jitihada kubwa wafanyayo katika utumishi wao. Isitoshe, hawawezi kuwa na hakika ni lini na ni wapi mbegu za kweli zilizopandwa zitaota, zikue, na kuzaa matunda.—Mhubiri 11:6; Marko 12:41-44; 2 Wakorintho 8:12.

Mashahidi wengine wamekuwa wagonjwa kwa muda mrefu au wanazeeka. Kwao, kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme kwaweza kuwa jambo lenye maumivu mengi na wasiwasi mwingi. Kusikiliza hotuba juu ya kazi ya kuhubiri huenda kukawakumbusha mambo waliyokuwa wakifanya na yale wangali wanataka kufanya, japo udhaifu unawazuia. Huenda wakajihisi wenye hatia sana kwa kuwa hawawezi kutii ushauri unaotolewa kwa kadiri ambavyo wangetaka. Lakini, Yehova huthamini uaminifu-mshikaminifu wao na uvumilivu wao. Maadamu wanadumisha uaminifu-mshikamanifu wao, yeye hasahau kamwe sifa yao ya uaminifu.— Zaburi 18:25; 37:28.

‘Tuihakikishie Mioyo Yetu’

Kufikia wakati Yohana alipozeeka, ni lazima awe alielewa mengi kuhusu wema wa Mungu. Kumbuka kwamba aliandika: “Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.” Isitoshe, alitutia moyo ‘tuihakikishie mioyo yetu.’ Yohana alimaanisha nini kwa maneno hayo?

Kwa mujibu wa Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words, kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa ‘hakikisha’ chamaanisha “kutumia ushawishi, kushawishi.” Yaani, ili kuihakikishia mioyo yetu, twahitaji kuishawishi iamini kwamba Yehova anatupenda. Jinsi gani?

Fritz, aliyetajwa hapo awali, ametumikia akiwa mzee katika mojawapo ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka zaidi ya 25 na ameona kwamba funzo la kibinafsi linaweza kuuhakikishia moyo wake upendo wa Yehova. “Ninajifunza Biblia na vichapo vyetu kwa ukawaida na kwa umakini. Jambo hilo hunisaidia nisizingatie mambo yaliyopita bali nizingatie tumaini letu zuri la wakati ujao. Mara kwa mara, mambo niliyofanya wakati uliopita hunisumbua akili sana, na huhisi kwamba Mungu hawezi kunipenda. Lakini kwa ujumla, ninaona kwamba funzo la kawaida huimarisha moyo wangu, huzidisha imani yangu, na hunisaidia kuwa mwenye furaha na usawaziko.”

Ni kweli kwamba huenda kujifunza Biblia na kutafakari kusibadili hali yetu halisi. Hata hivyo, funzo laweza kubadili maoni yetu kuhusu hali yetu. Kuyaweka mawazo ya Neno la Mungu mioyoni mwetu hutusaidia tuwaze jinsi awazavyo. Isitoshe, funzo hutuwezesha kupata uelewevu zaidi juu ya wema wa Mungu. Hatua kwa hatua tunaweza kuelewa kwamba Yehova hatulaumu kwa sababu ya malezi yetu wala kwa sababu ya magonjwa yetu. Yeye anajua hatulaumiki kwa mizigo ambayo wengine wetu hubeba—iwe ya kihisia-moyo au ya kimwili—naye huzingatia jambo hilo.

Namna gani Margarette aliyetajwa hapo awali? Alipomjua Yehova, kujifunza Biblia kulimnufaisha sana pia. Yeye, kama Fritz, ilimbidi abadili maoni kuhusu baba. Sala ilimsaidia Margarette kuunganisha mambo aliyojifunza. “Kwanza, nilimwona Yehova kuwa rafiki yangu wa karibu, kwa kuwa nilijua zaidi upendo wa rafiki kuliko upendo wa baba. Nilijifunza hatua kwa hatua kumweleza Yehova hisia zangu, shaka zangu, wasiwasi wangu, na shida zangu zote. Nilizungumza naye tena na tena katika sala, na wakati huohuo kuunganisha mambo yote mapya niliyokuwa nikijifunza kumhusu, kama vile picha inayounganishwa kwa vipande mbalimbali. Baada ya muda, hisia zangu kwa Yehova zikakua kiasi cha kwamba sasa si vigumu kumwona kama Baba mwenye upendo,” Margarette asema.

Kuondolewa Wasiwasi Wote

Maadamu mfumo huu mwovu wa zamani unaendelea, hakuna awezaye kutumaini kuishi bila wasiwasi. Kwa Wakristo fulani, jambo hilo lamaanisha kwamba wasiwasi na hali ya kutojiamini huenda zikawapata tena na kuwashusha moyo. Lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anajua nia yetu nzuri na jitihada tunazofanya katika utumishi wake. Hatasahau kamwe upendo tunaoonyesha kwa jina lake.—Waebrania 6:10.

Katika dunia mpya inayokuja chini ya Ufalme wa Kimesiya, wanadamu wote waaminifu wanaweza kutarajia kuondolewa mizigo ya mfumo wa Shetani. Kitakuwa kitulizo kilichoje! Kisha tutaona uthibitisho zaidi wa wema wa Yehova. Hadi wakati huo, na tuwe na hakika kwamba “Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.”—1 Yohana 3:20.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

Yehova si mtawala mkali bali ni Baba mchangamfu, mwema na mwenye huruma

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kujifunza Neno la Mungu hutusaidia kufikiri kama afikirivyo