Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Gospeli—Je, Ni za Kweli au Ni Hekaya Tu?

Gospeli—Je, Ni za Kweli au Ni Hekaya Tu?

Gospeli—Je, Ni za Kweli au Ni Hekaya Tu?

ULIMWENGUNI kote masimulizi ya maisha ya Yesu wa Nazareti—mwanamume kijana aliyebadili historia ya wanadamu—yamekuwa sehemu ya asili ya jamii. Masimulizi hayo ni sehemu ya mafundisho rasmi na yasiyo rasmi ya watu. Watu wengi huona Gospeli kuwa chanzo cha kweli nyingi na misemo mingi ya kale, kama vile, “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, La yenu, La.” (Mathayo 5:37) Kwa kweli, huenda masimulizi ya Gospeli ndiyo yaliyokuwa msingi wa mambo uliyofundishwa na wazazi wako, iwe walikuwa Wakristo au la.

Gospeli zimewafafanulia mamilioni ya wafuasi wa Kristo wenye mioyo myeupe yule mtu ambaye wao wamekuwa tayari kuteseka na kufa kwa ajili yake. Pia Gospeli zimewaandalia msingi na kichocheo cha kuwa na ujasiri, uvumilivu, imani, na tumaini. Basi, je, hungekubali kwamba ushuhuda usioweza kukanushwa unatakikana ili kuthibitisha kwamba masimulizi hayo ni mambo tu yaliyobuniwa? Ukifikiria jinsi ambavyo masimulizi ya Gospeli yamekuwa na uvutano sana juu ya mawazo na mwenendo wa wanadamu, je, hungedai uthibitisho wenye kusadikisha ikiwa mtu anatilia shaka uasilia wa Gospeli?

Twakuomba uyafikirie maswali fulani yenye kuamsha fikira kuhusu Gospeli. Jionee mwenyewe mambo ambayo wasomi fulani wa Gospeli wanafikiri kuhusu masuala hayo, hata ingawa baadhi yao hawadai kuwa Wakristo. Kisha unaweza kufanya uamuzi wako mwenyewe kutokana na mambo unayoyajua.

MASWALI YA KUFIKIRIA

◆ Je, inawezekana kwamba Gospeli zilibuniwa kwa ustadi sana?

Robert Funk, mwanzilishi wa Semina Juu ya Yesu, asema: “Mathayo, Marko, Luka, na Yohana ‘walimtokeza Mesiya’ ili alingane na mafundisho ya Kikristo yaliyotokea baada ya kifo cha Yesu.” Lakini, wakati Gospeli zilipokuwa zinaandikwa wengi waliosikiliza maneno ya Yesu, wakaona matendo yake, na kumwona baada ya kufufuliwa walikuwa wangali hai. Wao hawakuwashtaki waandikaji wa Gospeli kwa udanganyifu wowote.

Ebu fikiria kifo cha Kristo na ufufuo wake. Si Gospeli tu ambazo zina masimulizi ya kweli kuhusu kifo cha Yesu na kufufuliwa kwake bali pia barua rasmi ya kwanza ya mtume Paulo aliyowaandikia Wakristo katika Korintho la kale. Aliandika: “Niliwapa nyinyi, miongoni mwa mambo ya kwanza, lile nililolipokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba amefufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alionekana kwa Kefa, kisha kwa wale kumi na wawili. Baada ya hilo alionekana kwa zaidi ya ndugu mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wabaki hadi wakati wa sasa, lakini baadhi yao wamelala usingizi katika kifo. Baada ya hilo alionekana kwa Yakobo, kisha kwa mitume wote; lakini mwisho wa wote alionekana pia kwangu kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.” (1 Wakorintho 15:3-8) Watu hao waliojionea mambo hayo walihifadhi mambo ya hakika kuhusu maisha ya Yesu.

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hayaonyeshi kwamba yalibuniwa kama wanavyodai wachambuzi wa siku hizi. Lakini, kubuni huko kwapatikana katika hati za karne ya pili W.K. Basi, masimulizi fulani yasiyo ya Kimaandiko kuhusu Kristo yalitokezwa wakati ambapo uasi kutoka kwa Ukristo wa kweli ulikuwa unaanza katika jumuiya zilizojitenga na kutaniko la mitume.—Matendo 20:28-30.

◆ Je, inawezekana kwamba Gospeli ni hekaya tu?

Ilikuwa vigumu kwa mwandishi aliye pia mchambuzi, C. S. Lewis, kuziona Gospeli kuwa hekaya tu. “Nikiwa mwanahistoria wa mambo ya uandishi nimesadiki kabisa kwamba Gospeli si hekaya kamwe,” akaandika. “Mpangilio wake hauzionyeshi kuwa hekaya. . . . Kuna mambo mengi ambayo hatujui sana kuhusu maisha ya Yesu, na hakuna mtu yeyote anayebuni hekaya ambaye angekosa kutaja mambo hayo.” Pia ni jambo linalopendeza kwamba ingawa mwanahistoria mashuhuri H. G. Wells hakudai kuwa Mkristo, yeye alikiri hivi: “Wote wanne [waandikaji wa Gospeli] wanapatana wanapotufafanulia mtu mwenye utu fulani hususa; wao . . . wanatoa usadikisho wa mambo ya kweli.”

Ebu fikiria pindi moja ambapo Yesu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake kwa mara ya kwanza. Inaelekea kwamba mtu ambaye ni stadi wa kubuni hekaya angemwonyesha Yesu akirudi kwa njia ya kustaajabisha sana, akitoa hotuba ya maana sana, au aking’aa sana akiwa na utukufu mwingi. Badala yake, waandikaji wa Gospeli wanamtaja tu akiwa amesimama mbele ya wanafunzi wake. Kisha akawauliza: “Watoto wachanga, hamna kitu chochote cha kula, je, mnacho?” (Yohana 21:5) Msomi mmoja Gregg Easterbrook akata kauli hivi: “Hayo ndiyo mambo madogo-madogo yanayodokeza kwamba hayo ni masimulizi ya kweli wala si hekaya.”

Madai ya kwamba zile Gospeli ni hekaya tu pia yanaambulia patupu kwa kufikiria mbinu ya kufundisha ambayo marabi walipenda sana wakati wa kuandika Gospeli. Mbinu hiyo ilifanana sana na kujifunza kwa kukariri mambo—mtindo wa kurudia-rudia mambo ili kuyakariri. Jambo hilo lafanya iwe rahisi kuandika maneno ya Yesu na matendo yake kwa usahihi na kwa makini tofauti na kubuni hadithi zilizotiwa chumvi.

◆ Kama Gospeli zingalikuwa hekaya, je, zingaliweza kuandikwa kwa haraka hivyo baada ya kifo cha Yesu?

Kulingana na uthibitisho unaopatikana, Gospeli ziliandikwa kati ya mwaka wa 41 na 98 W.K. Yesu alikufa mwaka wa 33 W.K. Jambo hilo lamaanisha kwamba masimulizi ya maisha yake yaliandikwa kwa muda mfupi sana baada ya huduma yake kwisha. Jambo hilo lapinga kabisa hoja ya kwamba masimulizi ya Gospeli yalikuwa hekaya tu. Hekaya huchukua muda kusitawi. Ebu fikiria mfano wa hekaya ya Iliad na Odyssey ya Homer aliyekuwa mshairi wa kale wa Ugiriki. Wengine husema kwamba hekaya hizo mbili zilizo ndefu zilichukua zaidi ya mamia ya miaka kusitawi na kukamilika. Lakini vipi Gospeli?

Mwanahistoria Will Durant aandika hivi katika kitabu chake Caesar and Christ: “Kwamba wanaume wachache wa kawaida wangeweza . . . kubuni mtu mwenye nguvu na mwenye uvutano mwingi kadiri hiyo, mwenye maadili ya hali ya juu kadiri hiyo na mtu mwenye kuonyesha ubinadamu sana kwa kadiri hiyo, ungekuwa muujiza wenye kustaajabisha mno zaidi ya wowote ulioandikwa katika Gospeli. Baada ya Biblia kuchambuliwa kwa muda wa karne mbili, maelezo yanayohusu maisha, tabia, na mafundisho ya Kristo yanabaki yakiwa wazi vya kutosha, na ndiyo sehemu yenye kusisimua zaidi katika historia ya watu wa Magharibi.”

◆ Je, Gospeli zilirekebishwa baadaye ili zipatane na mahitaji ya Wakristo wa mapema?

Wachambuzi wengine hubisha wakisema kwamba ushindani wa Wakristo wa mapema uliwafanya waandikaji wa Gospeli warekebishe masimulizi yanayomhusu Yesu au kuyaongezea. Lakini, ukichunguza Gospeli kwa makini utaona kwamba hazikurekebishwa hata kidogo. Kama masimulizi ya Gospeli yanayomhusu Yesu yalirekebishwa kwa sababu ya udanganyifu wa Wakristo wa karne ya kwanza, basi kwa nini kungali kuna mambo yanayoshutumu Wayahudi na watu wa Mataifa katika maandishi hayo?

Mfano mmoja wapatikana katika Mathayo 6:5-7, ambapo Yesu ananukuliwa akisema: “Wakati msalipo, lazima msiwe kama wanafiki; kwa sababu wao hupendezwa na kusali wakisimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana waonekane na watu. Kwa kweli nawaambia nyinyi, Wanapata thawabu yao kwa ukamili.” Kwa wazi alikuwa akiwashutumu viongozi wa kidini wa Wayahudi. Yesu aliongezea kusema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa hufanya, kwa maana wao huwazia watapata kusikiwa kwa utumizi wao wa maneno mengi.” Kwa kumnukuu Yesu akisema hayo, waandikaji wa Gospeli hawakuwa wakijaribu kugeuza imani ya watu. Wao walikuwa wakiandika tu maneno aliyoyasema Yesu Kristo.

Ebu fikiria pia masimulizi ya Gospeli kuhusu wanawake waliokwenda kwenye kaburi la Yesu na kulipata likiwa tupu. (Marko 16:1-8) Kulingana na Gregg Easterbrook, “katika jamii ya kale ya Mashariki ya Kati, kwa kawaida ushuhuda wa wanawake haukutegemewa: kwa mfano, mashahidi wawili wanaume walitosha kuthibitisha kwamba mwanamke fulani ana hatia ya uzinzi, ilhali hakuna ushuhuda wa wanawake ambao ungeweza kuthibitisha hatia ya mwanamume.” Hata wanafunzi wa Yesu mwenyewe hawakuwaamini wanawake! (Luka 24:11) Basi, haielekei kwamba masimulizi hayo yalibuniwa tu kimakusudi.

Kukosekana kwa mifano katika barua za Maandiko ya Kigiriki na katika kitabu cha Matendo ni hoja yenye nguvu inayothibitisha kwamba mifano inayopatikana katika Gospeli haikuingizwa na Wakristo wa mapema bali ilitajwa na Yesu mwenyewe. Kwa kuongezea, ukilinganisha kwa makini Gospeli na barua hizo utaona kwamba wala maneno ya Paulo wala maneno ya wale waandikaji wengine wa Maandiko ya Kigiriki hayakubadilishwa kwa ujanja na kusemekana ni maneno ya Yesu. Ikiwa Wakristo wa mapema walifanya hivyo, twapaswa kupata angalau habari fulani za barua za Maandiko ya Kigiriki katika masimulizi ya Gospeli. Na kwa kuwa hakuna, kwa hakika twaweza kukata kauli ya kwamba masimulizi ya Gospeli hayajarekebishwa na ni asilia.

◆ Vipi juu ya mambo yaonekanayo kana kwamba yanapingana katika Gospeli?

Kwa muda mrefu, wachambuzi wamedai kwamba Gospeli zinapingana sana. Mwanahistoria Durant alichunguza masimulizi ya Gospeli akiwa na lengo zuri kabisa—yakiwa maandishi ya historia. Japo anasema kwamba kuna mambo yanayoonekana kana kwamba yanapingana, akata kauli hivi: “Ni mambo madogo-madogo yanayopingana, wala si mambo muhimu; katika mambo ya msingi zile gospeli tatu za kwanza zakubaliana sana, na kutokeza Kristo mwenye utu uleule.”

Mambo yanayoonekana kana kwamba yanapingana katika Gospeli hutatuliwa kwa urahisi. Kwa mfano: Andiko la Mathayo 8:5 linasema kwamba “ofisa-jeshi mmoja akamjia [Yesu], akimsihi sana” amponye mtumishi wake mwanamume. Kwenye Luka 7:3, twasoma kwamba huyo ofisa “akatuma kwa [Yesu] wanaume wazee wa Wayahudi kumwomba aje na kumleta mtumwa wake akiwa salama.” Huyo ofisa aliwatuma wazee wamwakilishe. Mathayo asema kwamba huyo ofisa-jeshi mwenyewe alimsihi Yesu kwa sababu alipeleka maombi yake kupitia wazee ambao walikuwa wasemaji wake. Huu ni mfano mmoja tu unaothibitisha kwamba mambo yale yanayoonwa kuwa yanapingana katika Gospeli yanaweza kutatuliwa.

Vipi juu ya madai ya wahakiki wa Biblia kwamba Gospeli hazifikii viwango vya kuthibitishia historia halisi? Durant aendelea kusema: “Kutokana na shauku ya kuvumbua mambo, Uhakiki wa Biblia umetumia kanuni ngumu sana za kuthibitishia uasilia wa Agano Jipya hivi kwamba kanuni hizo zikitumiwa kwingineko basi mamia ya watu mashuhuri wa nyakati za kale—kama Hamurabi, Daudi, na Sokrate—wangeonwa kuwa hekaya tu. Japo upendeleo wa waevanjeli hao na mawazo waliyoshikilia ya kitheolojia, wao wamerekodi matukio mengi ambayo wabuni tu [wa hekaya] wangeficha—kama yale mashindano baina ya mitume ya kutaka ukubwa katika Ufalme, jinsi walivyotoroka baada ya Yesu kukamatwa, na jinsi Petro alivyomkana . . . Hakuna mtu yeyote anayesoma mambo hayo awezaye kutilia shaka ukweli wa mtu anayezungumziwa.”

◆ Je, Ukristo wa kisasa wamwakilisha Yesu anayetajwa katika Gospeli?

Semina Juu ya Yesu imetangaza kwamba utafiti wake juu ya Gospeli “hautegemei matakwa ya mabaraza ya kanisa.” Lakini mwanahistoria Wells alitambua kwamba kuna tofauti kubwa sana kati ya mafundisho ya Yesu kama yanavyoonyeshwa katika Gospeli na mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo. Aliandika hivi: “Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba mitume wa Yesu walijua Utatu—hata kutokana na Yesu. . . . Wala [Yesu] hakusema neno lolote kuhusu kuabudiwa kwa mamake Maria, akiwa Isis, Malkia wa mbinguni. Mafundisho yote ambayo kwa kawaida hutumiwa katika Jumuiya ya Wakristo, aliyapuuza.” Basi, mtu hawezi kupima ubora wa Gospeli kwa msingi wa mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo.

UMEFIKIA MKATAA GANI?

Baada ya kuyafikiria mambo ambayo yametajwa, wewe unaonaje? Je, kuna uthibitisho mzuri na wenye kusadikisha kwamba Gospeli ni hekaya tu? Watu wengi wanaona kwamba maswali na shaka zinazozushwa kuhusu uasilia wa Gospeli hazina msingi na hazisadikishi. Ili ufikie uamuzi wako binafsi unahitaji kusoma zile Gospeli bila kuwa na upendeleo. (Matendo 17:11) Unapofikiria upatano, unyofu, na usahihi wa jinsi Gospeli zinavyomwonyesha Yesu, bila shaka utaona kwamba masimulizi hayo si mkusanyo tu wa hekaya. *

Ukichunguza Biblia kwa makini na kutumia shauri lake, utaona jinsi inavyoweza kubadili maisha yako yawe bora. (Yohana 6:68) Na ndivyo ilivyo na maneno ya Yesu yaliyorekodiwa katika Gospeli. Isitoshe, humo ndani unaweza kujifunza kuhusu wakati ujao mzuri ajabu unaowangoja wanadamu watiifu.—Yohana 3:16; 17:3, 17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 29 Ona sura ya 5 hadi 7 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? na broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote. Vichapo hivyo vyote vimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Uthibitisho wa Kuripoti kwa Usahihi

MIAKA kadhaa iliyopita mwandikaji mmoja wa Australia ambaye zamani alikuwa mchambuzi wa Biblia alikiri hivi: “Kwa mara ya kwanza maishani mwangu nilifanya jambo ambalo kwa kawaida mwandishi wa habari hufanya kwanza: nilichunguza ukweli wa mambo. . . . Na nilishangaa, kwa sababu mambo niliyokuwa nikisoma [katika masimulizi ya Gospeli] hayakuwa hekaya wala hayakuwa hadithi ya kubuni iliyofanywa isikike kama ni kweli. Mambo hayo yaliripotiwa. Mambo yaliyoripotiwa moja kwa moja na masimulizi ya matukio ya ajabu . . . Kuna jambo fulani ambalo huonekana katika mambo yaliyoripotiwa, na zile Gospeli zina jambo hilo.”

Vivyo hivyo, E. M. Blaiklock, ambaye ni profesa wa maandishi ya kale ya Kigiriki katika Chuo Kikuu cha Auckland, alitoa hoja hii: “Nadai kuwa mwanahistoria. Na mimi huchunguza kihistoria maandishi ya zamani. Na nakuhakikishia kwamba uthibitisho wa kwamba Kristo aliishi, akafa, na kufufuliwa ni mkubwa kuliko uthibitisho wa mambo mengi yaliyotendeka katika historia.”

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

 

FOINIKE

GALILAYA

Mto Yordani

YUDEA

[Picha]

“Uthibitisho wa kwamba Kristo aliishi, kuliko uthibitisho wa mambo mengi akafa, na kufufuliwa ni mkubwa yaliyotendeka katika historia ya kale.”—PROFESA E. M. BLAIKLOCK

[Hisani]

Ramani zilizo kwenye mandhari ya nyuma: Based on a map copyrighted by Pictorial Archive (Near Eastern History) Est. and Survey of Israel.