Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Linda Moyo Wako”

“Linda Moyo Wako”

“Linda Moyo Wako”

YEHOVA alimwambia nabii Samweli hivi: “BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Pia akizingatia moyo wa mfano, mtunga-zaburi Daudi aliimba: “[Wewe Yehova] umenijaribu moyo wangu, umenijilia usiku, umenihakikisha usione neno.”—Zaburi 17:3.

Naam, Yehova huutazama moyo apate kujua sisi kwa kweli ni watu wa aina gani. (Mithali 17:3) Basi, ni kwa sababu nzuri Mfalme Solomoni wa Israeli la kale ashauri: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” (Mithali 4:23) Tunawezaje kuulinda moyo wetu wa mfano? Mithali sura ya 4 yajibu swali hilo.

Sikiliza Nidhamu ya Baba

Sura ya 4 ya Mithali yaanza kwa maneno haya: “Wanangu, yasikilizeni mausia [“nidhamu,” “NW”] ya baba yenu, tegeni masikio mpate kujua ufahamu. Kwa kuwa nawapa mafundisho mazuri; msiiache sheria yangu.”Mithali 4:1, 2.

Vijana wanashauriwa wasikilize mafundisho mazuri ya wazazi wao wenye kumcha Mungu, hasa mafundisho ya baba. Yeye ana wajibu wa Kimaandiko wa kuandalia familia yake mahitaji ya kiroho na kimwili. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; 1 Timotheo 5:8) Bila mwongozo wa aina hiyo, ni vigumu kama nini kwa kijana kukomaa! Kwa hiyo, je, haimpasi mtoto akubali kwa heshima nidhamu ya baba yake?

Hata hivyo, namna gani kijana asiye na baba wa kumfundisha? Kwa mfano, Jason mwenye umri wa miaka 11, alifiwa na babake akiwa na umri wa miaka minne. * Mzee mmoja Mkristo alipomwuliza ni jambo gani lililokuwa likimhangaisha sana maishani, Jason alijibu hivi bila kusita: “Sina baba. Nyakati nyingine hilo hufanya nishuke moyo sana.” Hata hivyo, vijana ambao hawana mzazi wa kuwaongoza wanaweza kupata ushauri wenye kufariji. Jason na wengine walio kama yeye wanaweza kutafuta na kupata ushauri kama wa baba kutoka kwa wazee na wengine walio wakomavu katika kutaniko la Kikristo.—Yakobo 1:27.

Akikumbuka malezi yake mwenyewe, Solomoni aendelea kusema hivi: “Nalikuwa mwana [“mwana halisi,” “NW”] kwa baba yangu, mpole, mpenzi wa pekee wa mama yangu.” (Mithali 4:3) Yaonekana kwamba mfalme huyo alikumbuka kwa shauku jinsi alivyolelewa. Akiwa “mwana halisi” aliyezingatia ushauri wa baba yake, haikosi kijana Solomoni alikuwa na uhusiano wa karibu na wenye upendo pamoja na baba yake, Daudi. Isitoshe, Solomoni alikuwa “wa pekee,” au mpendwa sana. Ni muhimu kama nini kwa mtoto kukua katika nyumba yenye uchangamfu na yenye mawasiliano mazuri na wazazi!

Jipatie Hekima na Uelewevu

Akikumbuka ushauri wenye upendo wa baba yake, Solomoni asimulia: “Naye akanifundisha, akaniambia, moyo wako uyahifadhi maneno yangu; shika amri zangu ukaishi. Jipatie hekima, jipatie ufahamu [“uelewevu,” “NW”]; usiusahau; wala usiyakatae maneno ya kinywa changu. Usimwache [hekima], naye atakuhifadhi; umpende, naye atakulinda. Bora hekima, basi jipatie hekima; naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu [“uelewevu,” “NW”].”—Mithali 4:4-7.

Kwa nini hekima ni “bora”? Hekima humaanisha kutumia kwa mafanikio ujuzi na uelewevu. Ujuzi—ambao ni kufahamu mambo kutokana na yaliyoonwa au kutokana na kusoma na kujifunza—ni muhimu ili kuwa na hekima. Lakini ujuzi wetu hautakuwa wenye manufaa ikiwa hatuwezi kuutumia vizuri. Ni lazima tujifunze Biblia kwa ukawaida na vichapo vinavyoitegemea Biblia ambavyo hutolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na pia tujitahidi kutumia mambo tunayojifunza.—Mathayo 24:45.

Kupata uelewevu ni muhimu pia. Bila uelewevu, je, tunaweza kuona jinsi mambo yanavyohusiana na kupata kuelewa kikamili jambo tunalochunguza? Kama hatuna uelewevu, tunawezaje kujua sababu zinazofanya mambo yafanyike kwa njia fulani na kupata ufahamu wenye kina na utambuzi? Naam, tunahitaji uelewevu ili tuweze kusababu kutokana na mambo tujuayo kisha kuamua mambo ifaavyo.—Danieli 9:22, 23.

Solomoni aendelea kusimulia maneno ya babake akisema: “Umtukuze [hekima], naye atakukuza; atakupatia heshima, ukimkumbatia. Atakupa neema kuwa kilemba kichwani; na kukukirimia taji ya uzuri.” (Mithali 4:8, 9) Hekima ya Mungu humlinda yule anayeikumbatia. Isitoshe, hiyo humletea heshima na kumpamba. Basi, kwa vyovyote vile, na tujipatie hekima.

‘Mkamate Sana Nidhamu’

Akirudia mafundisho ya babake, mfalme wa Israeli afuatia kusema: “Mwanangu, sikiliza, na kuzipokea kauli zangu; na miaka ya maisha yako itakuwa mingi. Nimekufundisha katika njia ya hekima; nimekuongoza katika mapito ya unyofu. Uendapo, hatua zako hazitadhiikika, wala ukipiga mbio hutajikwaa. Mkamate sana elimu [“nidhamu,” “NW”], usimwache aende zake; mshike, maana yeye ni uzima wako.”Mithali 4:10-13.

Akiwa mwana halisi wa babake, haikosi Solomoni alifahamu manufaa ya nidhamu yenye upendo, ambayo hufundisha na kurekebisha. Tunawezaje kutarajia kufanya maendeleo kufikia ukomavu wa kiroho au kutumaini kuboresha maisha yetu pasipo nidhamu yenye usawaziko? Tusipojifunza kutokana na makosa yetu au tusiporekebisha maoni yasiyofaa, kwa kweli hatutafanya maendeleo ya kiroho. Nidhamu ifaayo hufanya tuwe wenye kumcha Mungu na hivyo kutusaidia tutembee “katika mapito ya unyofu.”

Aina nyingine ya nidhamu pia hufanya ‘miaka ya maisha yetu iwe mingi.’ Jinsi gani? Yesu Kristo alisema: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni asiye mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Je, kujitia nidhamu katika mambo madogo-madogo hakutafanya iwe rahisi zaidi kwetu kujitia nidhamu katika mambo makubwa, ambayo huenda maisha yetu wenyewe yakategemea? Kwa mfano, kulizoeza jicho ‘lisifulize kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake’ kungefanya isiwe rahisi kutumbukia katika ukosefu wa adili. (Mathayo 5:28) Kwa kawaida, kanuni hiyo inawahusu wanaume na wanawake pia. Tukitia akili zetu nidhamu ili ‘kuingiza kila fikira katika utekwa,’ inakuwa vigumu kufanya dhambi nzito katika usemi au katika kutenda.—2 Wakorintho 10:5.

Ni kweli kwamba kwa kawaida inakuwa vigumu kukubali nidhamu na huenda ikaonekana kuwa yenye kukuzuia. (Waebrania 12:11) Lakini, mfalme mwenye hekima atuhakikishia kwamba tukiikamata nidhamu, itakuwa rahisi kufanya maendeleo. Kama vile mazoezi yafaayo humwezesha mkimbiaji kukimbia kwa kasi sana bila kuanguka wala kujiumiza, kuikamata nidhamu hutuwezesha kuendelea katika njia ya uhai kwa mwendo thabiti bila kujikwaa. Bila shaka, ni lazima tuwe waangalifu kuhusu njia tunayochagua.

Jiepushe na “Njia ya Waovu”

Solomoni aonya hivi kwa hima: “Usiingie katika njia ya waovu, wala usitembee katika njia ya wabaya. Jiepushe nayo, usipite karibu nayo, igeukie mbali, ukaende zako. Maana hawalali isipokuwa wametenda madhara; huondolewa usingizi, ikiwa hawakumwangusha mtu. Maana wao hula mkate wa uovu, nao hunywa divai ya jeuri.”—Mithali 4:14-17.

Waovu ambao njia zao Solomoni ataka tujiepushe nazo, hujiruzuku kwa matendo yao maovu. Kutenda maovu ni kama kula na kunywa. Hawawezi kulala wasipotenda jeuri. Utu wao wenyewe umepotoka! Je, kweli tunaweza kulinda mioyo yetu ilhali tunashirikiana nao? Ni jambo la upumbavu kama nini ‘kutembea katika njia ya wabaya’ kwa kutazama jeuri ambayo huonyeshwa katika vitumbuizo vingi vya ulimwengu wa leo! Kujaribu kuwa wenye huruma nyororo hakupatani kabisa na hali ya kuendelea kutazama vipindi vibaya katika televisheni au sinema ambavyo hutufanya tusiwe na hisia.

Kaa Katika Nuru

Akiwa bado anatumia mfano wa njia, Solomoni atangaza: “Bali njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” (Mithali 4:18) Kujifunza Biblia na kujitahidi kutumia maishani yale isemayo kwaweza kulinganishwa na kuanza safari wakati wa giza la alfajiri. Anga jeusi la usiku ligeukapo na kuwa rangi ya buluu nzito, bado hatuwezi kuona vizuri. Lakini kadiri siku inavyopambazuka, polepole tunaanza kupambanua vitu tunavyoona. Hatimaye, jua linang’aa kwa uangavu, na tunaona kila kitu vizuri kabisa. Naam, hatua kwa hatua tunapata kuielewa kweli vizuri tunapodumu katika kusoma Maandiko kwa subira na kwa bidii. Kulisha moyo wetu chakula cha kiroho ni muhimu ili kuulinda dhidi ya mawazo yasiyo ya kweli.

Maana au umuhimu wa unabii wa Biblia pia hueleweka hatua kwa hatua. Unabii hueleweka vizuri roho ya Yehova inapoufafanua na unapotimizwa kwa matukio ya ulimwengu au mambo yanayowapata watu wa Mungu. Twahitaji kungojea ‘nuru ing’ae na izidi kung’aa’ badala ya kuanza kukisia-kisia kutimizwa kwa unabii.

Namna gani wale wanaokataa mwongozo wa Mungu kwa kukataa kutembea katika nuru? “Njia ya waovu ni kama giza,” asema Solomoni. “Hawajui ni kitu gani kiwakwazacho.” (Mithali 4:19) Waovu ni kama mtu ajikwaaye gizani asijue kilichomfanya ajikwae. Hata wakati inapoonekana kwamba wasiomcha Mungu wanafanikiwa kwa sababu ya kukosa uadilifu, mafanikio yao ni ya muda tu. Kuhusu watu hao, mtunga-zaburi aliimba: “Hakika Wewe huwaweka penye utelezi, [Wewe Yehova] huwaangusha mpaka palipoharibika.”—Zaburi 73:18.

Uwe Mwangalifu

Mfalme wa Israeli aendelea kusema: “Mwanangu, sikiliza maneno yangu; tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako; uzihifadhi ndani ya moyo wako. Maana ni uhai kwa wale wazipatao, na afya ya mwili wao wote. Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.Mithali 4:20-23.

Mfano wa Solomoni mwenyewe wadhihirisha kwamba ushauri unafaa ili kuulinda moyo. Ni kweli kwamba yeye ‘alikuwa mwana halisi’ kwa babake ujanani na aliendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova hata alipokuwa mtu mzima. Lakini Biblia yasimulia hivi: “Ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake [wa kigeni] wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa BWANA, Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake.” (1 Wafalme 11:4) Hata mioyo mizuri kabisa yaweza kushawishiwa kufanya mabaya tusipokuwa waangalifu wakati wote. (Yeremia 17:9) Twapaswa kuweka vikumbusha vya Neno la Mungu moyoni—“ndani ya moyo.” Vikumbusha hivyo vyatia ndani mwongozo unaotolewa katika sura ya 4 ya Mithali.

Chunguza Hali ya Moyo Wako

Je, tunaulinda moyo wetu wa mfano kwa mafanikio? Tunawezaje kujua hali ya utu wa ndani? “Kutoka katika wingi wa moyo kinywa husema,” akasema Yesu Kristo. (Mathayo 12:34) Pia alisema: “Kutoka moyoni huja mawazowazo maovu, mauaji-kimakusudi, uzinzi, uasherati, wizi, shuhuda zisizo za kweli, makufuru.” (Mathayo 15:19, 20) Naam, maneno na matendo yetu hudhihirisha kwa kiasi kikubwa jinsi tulivyo moyoni.

Kwa kufaa, Solomoni atushauri: “Kinywa cha ukaidi ukitenge nawe, na midomo ya upotovu uiweke mbali nawe. Macho yako yatazame mbele, na kope zako zitazame mbele yako sawasawa. Ulisawazishe pito la mguu wako, na njia zako zote zithibitike; usigeuke kwa kuume wala kwa kushoto; ondoa mguu wako maovuni.”—Mithali 4:24-27.

Kwa kuzingatia ushauri wa Solomoni, twahitaji kuchunguza usemi wetu na matendo yetu. Ni lazima tuepuke usemi uliopotoka na wa ujanja ili kulinda moyo wetu na kumfurahisha Mungu. (Mithali 3:32) Hivyo, twapaswa kutafakari kwa sala kuhusu yale yanayodhihirishwa na usemi wetu na matendo yetu. Basi na tutafute msaada wa Yehova ili kurekebisha udhaifu wowote tunaoona.—Zaburi 139:23, 24.

Zaidi ya yote, ‘macho yetu na yatazame mbele.’ Na tuyakaze kwenye mradi wa kumtumikia Baba yetu wa mbinguni kwa nafsi yote. (Wakolosai 3:23) Ufuatapo mwenendo huo mnyofu, Yehova na akufanikishe ‘katika njia zako zote,’ na akubariki sana kwa kutii ushauri wake uliopuliziwa ili ‘kuulinda moyo wako.’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Si jina lake halisi.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Je, wewe huepuka vitumbuizo vinavyoonyesha jeuri?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nufaika na ushauri wa watu wenye ujuzi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nidhamu haipunguzi maendeleo yako

[Picha katika ukurasa wa 24]

Jifunze Biblia daima