Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mzeituni Unaostawi Katika Nyumba ya Mungu

Mzeituni Unaostawi Katika Nyumba ya Mungu

Mzeituni Unaostawi Katika Nyumba ya Mungu

KUNA mti unaomea katika nchi ya Israeli ambao ni kama hauwezi kuharibiwa. Hata ukikatwa, mizizi yake hutokeza machipukizi mapya mara moja. Na matunda yake yavunwapo, mti huo huthawabisha mwenyewe kwa mafuta mengi ambayo yanaweza kutumiwa kupikia, kutoa nuru, kudumisha usafi, na kujipaka.

Kulingana na mfano mmoja wa zamani katika kitabu cha Biblia cha Waamuzi, “siku moja miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao.” Miti hiyo ilichagua mti gani kwanza? Ilichagua mzeituni, mti wenye kuzaa sana uwezao kustahimili hali ngumu.—Waamuzi 9:8.

Zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, nabii Musa alitaja Israeli kuwa ‘nchi nzuri, nchi ya mizeituni.’ (Kumbukumbu la Torati 8:7, 8) Hata leo, mashamba ya mizeituni yametapakaa kutoka sehemu za chini ya Mlima Hermoni upande wa kaskazini hadi viunga vya Beersheba upande wa kusini. Mizeituni bado inapatikana kwenye pwani ya Uwanda wa Sharoni, vilima vyenye mawemawe vya Samaria, na mabonde yenye rutuba ya Galilaya.

Mara nyingi waandishi wa Biblia walitumia mzeituni kama mfano. Sehemu mbalimbali za mzeituni zilitumika kufananisha rehema ya Mungu, ahadi ya ufufuo, na maisha ya familia yenye furaha. Kuuchunguza mzeituni kwa makini kutatusaidia kuelewa marejeo hayo ya Kimaandiko na kutafanya tuuthamini sana mti huu wa pekee ambao pamoja na uumbaji mwingine wote, humsifu Mfanyi wake.—Zaburi 148:7, 9.

Mzeituni Usiovutia

Mzeituni hauvutii ukiuona kwa mara ya kwanza. Si mrefu kama mierezi fulani yenye kuvutia ya Lebanoni. Mbao zake hazina thamani kama mbao za mberoshi, na maua yake hayavutii kama maua ya mlozi. (Wimbo Ulio Bora 1:17; Amosi 2:9) Sehemu muhimu zaidi ya mzeituni haionekani—iko chini ya ardhi. Mizizi yake mingi, ambayo hufikia kina cha meta sita chini ya ardhi na kwenda hata mbali zaidi kuelekea upande-upande, ndiyo hasa hufanya mti huo uzae sana na kustahimili hali ngumu.

Mizizi hiyo huiwezesha mizeituni kwenye vilima vyenye mawemawe istahimili ukame wakati ambapo miti iliyo kwenye bonde imekwisha kauka kwa kukosa maji. Mizizi huiwezesha kuendelea kuzaa zeituni kwa karne nyingi, ingawa huenda shina lisilovutia likaonekana kuwa lafaa tu kwa kuni. Mti huo usiovutia huhitaji tu nafasi ya kukua na udongo wenye hewa, bila magugu au mimea mingine inayoweza kuwa na wadudu waharibifu. Mahitaji hayo sahili yakitimizwa, mti mmoja utatoa lita 57 za mafuta kila mwaka.

Bila shaka, zeituni zilipendwa sana na Waisraeli kwa sababu ya mafuta yake yenye thamani. Walitumia katika nyumba zao taa zenye tambi zilizotumia mafuta ya zeituni. (Mambo ya Walawi 24:2) Mafuta ya zeituni yalikuwa muhimu katika upishi. Yalikinga ngozi dhidi ya miali ya jua, na Waisraeli waliyatumia kutengenezea sabuni. Mazao muhimu ya nchi yalikuwa nafaka, divai, na zeituni. Hivyo, ungekuwa msiba mkubwa kwa familia ya Waisraeli mizeituni ikikosa kuzaa.—Kumbukumbu la Torati 7:13; Habakuki 3:17.

Hata hivyo, kwa kawaida mafuta ya zeituni yalikuwa mengi. Yaelekea kwamba Musa aliliita Bara Lililoahidiwa ‘nchi ya zeituni’ kwa sababu mizeituni ilipandwa kwa wingi sana katika eneo hilo. Mtaalamu wa mambo ya asili, H. B. Tristram, wa karne ya 19 aliutaja mzeituni kuwa “mti wa kawaida wa nchi hiyo.” Kwa sababu ya thamani yake na wingi wake, mafuta ya zeituni yalitumika katika eneo lote la Mediterania yakiwa kama fedha ya kimataifa. Yesu Kristo mwenyewe alitaja deni ambalo lilikadiriwa kuwa “vipimo mia vya bathi vya mafuta ya mzeituni.”—Luka 16:5, 6

“Kama Miche ya Mizeituni”

Mzeituni wenye mafaa ni mfano ufaao wa baraka za Mungu. Mtu anayemcha Mungu angethawabishwaje? “Mkeo atakuwa kama mzabibu uzaao, vyumbani mwa nyumba yako,” mtunga-zaburi akaimba. “Wanao kama miche ya mizeituni wakiizunguka meza yako.” (Zaburi 128:3) “Miche ya mizeituni” ni nini, na kwa nini mtunga-zaburi anailinganisha na wana?

Mzeituni ni wa pekee kwa kuwa machipukizi mapya huchipuka daima kutoka kwenye shina lake. * Wakati shina kuu liachapo kuzaa kama zamani kwa sababu ya uzee, wakulima wanaweza kuacha miche au machipukizi mapya yakue na kuwa sehemu muhimu ya mti huo. Baada ya muda, mti wa awali utazungukwa na mashina machanga matatu au manne yenye nguvu, kama wana wanaoizunguka meza. Miche hiyo inatumia mzizi uleule, nayo hutoa mazao mazuri ya zeituni.

Hali hiyo ya mzeituni ni mfano ufaao wa jinsi imani ya wana na binti iwezavyo kuwa thabiti kwa sababu ya mizizi ya kiroho yenye nguvu ya wazazi wao. Watoto wakuapo, wao vilevile huzaa matunda na kuwategemeza wazazi wao, ambao hufurahi kuona watoto wao wakimtumikia Yehova pamoja nao.—Mithali 15:20.

“Yako Matumaini ya Mti”

Baba mzee-mzee anayemtumikia Yehova hupendezwa na watoto wake wenye kumcha Mungu. Lakini watoto haohao huomboleza wakati hatimaye baba yao ‘anapoenda njia ya ulimwengu wote.’ (1 Wafalme 2:2) Ili kutusaidia kuvumilia msiba kama huo wa familia, Biblia hutuhakikishia kwamba kutakuwa na ufufuo.—Yohana 5:28, 29; 11:25.

Yobu, aliyekuwa baba ya watoto wengi, alifahamu vizuri kwamba maisha ya mwanadamu ni mafupi. Aliyalinganisha na maua ambayo hunyauka upesi. (Ayubu 1:2; 14:1, 2) Yobu alitamani sana kufa ili aepuke maumivu, akiliona kaburi kuwa mahali pa kujificha ambapo angeweza kutoka. “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?” Yobu akauliza. Kisha kwa uhakika akajibu: “Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, hata kufunguliwa kwangu kunifikilie. Wewe [Yehova] ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:13-15.

Yobu alionyeshaje imani kwamba Mungu angemwita kutoka kaburini? Kwa kutumia mti ambao kutokana na jinsi anavyoufafanua, yaelekea ni mzeituni. “Yako matumaini ya mti,” Yobu akasema. “Ya kuwa ukikatwa utachipuka tena.” (Ayubu 14:7) Mzeituni unaweza kukatwa, lakini kufanya hivyo hakutauharibu. Utakufa tu uking’olewa. Mizizi isipong’olewa, huo mti utachipuka tena ukiwa na nguvu mpya.

Hata ikiwa ukame wa muda mrefu unanyaukisha mzeituni wa zamani, shina lililonyauka laweza kuchipuka tena. “Ijapokuwa mizizi yake huchakaa mchangani, na shina lake kufa katika udongo; lakini kwa harufu ya maji utachipuka, na kutoa matawi kama mche.” (Ayubu 14:8, 9) Yobu aliishi katika nchi kavu na yenye vumbi ambako yaelekea aliona mashina mengi ya mizeituni iliyozeeka ambayo yalionekana yamenyauka na bila uhai. Hata hivyo, mvua iliponyesha mti huo “mfu” ulichipuka tena na mizizi yake kutoa shina jipya kana kwamba ni “mche.” Uwezo huo wa kipekee wa kuchipuka tena ulifanya mkulima mmoja wa bustani wa Tunisia aseme: “Kwa kweli mizeituni haiwezi kufa.”

Kama vile mkulima anavyotamani kuona mizeituni yake iliyonyauka ikichipuka tena, ndivyo Yehova hutamani kufufua watumishi wake waaminifu. Anangojea kwa hamu wakati ambapo watu waaminifu kama Abrahamu na Sara, Isaka na Rebeka, na wengine wengi watafufuliwa. (Mathayo 22:31, 32) Itakuwa ajabu kama nini kuwakaribisha wafu na kuwaona wakiishi tena maisha kamili yenye manufaa!

Mzeituni wa Mfano

Sifa ya Mungu ya kutobagua na pia uandalizi wake wa ufufuo hudhihirisha rehema yake. Mtume Paulo alitumia mzeituni kuonyesha jinsi ambavyo Yehova huwarehemu watu bila kujali rangi au malezi yao. Kwa karne nyingi Wayahudi walijivunia kuwa wachaguliwa wa Mungu, “uzao wa Abrahamu.”—Yohana 8:33 Luka 3:8.

Haikuwa lazima uwe mzaliwa wa taifa la Kiyahudi ili kupata kibali cha Mungu. Hata hivyo, wanafunzi wote wa kwanza wa Yesu walikuwa Wayahudi, na walikuwa na pendeleo la kuwa wanadamu wa kwanza kuteuliwa na Mungu kufanyiza mbegu ya Abrahamu iliyoahidiwa. (Mwanzo 22:18; Wagalatia 3:29) Paulo aliwalinganisha wanafunzi hao Wayahudi na matawi ya mzeituni wa mfano.

Wengi wa Wayahudi wa asili walimkataa Yesu, wakijinyima pendeleo la kuwa washiriki wa “kundi dogo,” au “Israeli wa Mungu.” (Luka 12:32; Wagalatia 6:16) Hivyo wakawa kama matawi ya mzeituni wa mfano yaliyokatwa. Ni nani wangechukua mahali pao? Mwaka wa 36 W.K., wasio Wayahudi walichaguliwa kuwa sehemu ya mbegu ya Abrahamu. Ilikuwa kana kwamba Yehova alipandikiza matawi ya mzeituni-mwitu kwenye mzeituni wa bustani. Wale ambao wangefanyiza mbegu ya Abrahamu iliyoahidiwa wangetia ndani watu wa mataifa. Wakristo wasio Wayahudi sasa wangeweza kuwa ‘washiriki wa mzizi wa unono wa mzeituni.’—Waroma 11:17.

Lingekuwa jambo lisilowazika na lililo “kinyume cha asili” kwa mkulima kupandikiza tawi la mzeituni-mwitu kwenye mzeituni wa bustani. (Waroma 11:24) “Pandikiza mti mzuri kwenye mti wa mwituni, na, kama vile Waarabu wasemavyo, ule mzuri utashinda ule wa mwituni,” chaeleza kitabu The Land and the Book, “lakini huwezi kupandikiza mti wa mwituni kwa mti mzuri ukafanikiwe.” Wakristo Wayahudi hali kadhalika walishangaa wakati ambapo Yehova ‘kwa mara ya kwanza alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwayo watu kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 10:44-48; 15:14) Hata hivyo, hiyo ilikuwa ishara ya wazi kwamba kutimizwa kwa kusudi la Mungu hakukutegemea taifa moja tu. La, kwa kuwa “katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—Matendo 10:35.

Paulo alionyesha kwamba kwa kuwa “matawi” ya mzeituni ya Wayahudi wasio waaminifu yalikatwa, mtu yeyote aweza kukatwa vivyo hivyo akikosa upendeleo wa Yehova kwa sababu ya kiburi na kutotii. (Waroma 11:19, 20) Kwa kweli jambo hilo laonyesha kwamba hatupaswi kupuuza fadhili isiyostahiliwa ya Mungu.—2 Wakorintho 6:1.

Kupaka Mafuta

Maandiko yanarejezea kihalisi na kwa mfano matumizi ya mafuta ya zeituni. Zamani, majeraha na machubuko ‘yalilainishwa kwa mafuta’ ili yapone haraka. (Isaya 1:6) Kulingana na mojawapo ya mifano ya Yesu, Msamaria aliyekuwa jirani mwema alipaka mafuta ya zeituni na divai kwenye majeraha ya mtu aliyemkuta kwenye barabara ya kwenda Yeriko.—Luka 10:34.

Mtu huburudika na kupata kitulizo apakapo mafuta ya zeituni kichwani. (Zaburi 141:5) Wazee Wakristo wanaweza ‘kumpaka mafuta mshiriki wa kutaniko katika jina la Yehova’ wanaposhughulika na ugonjwa wa kiroho. (Yakobo 5:14) Ushauri wenye upendo wa wazee unaotokana na Maandiko na sala zao za kutoka moyoni kwa niaba ya mwamini mwenzao aliye mgonjwa kiroho zinalinganishwa na mafuta ya zeituni yenye kutuliza. Yapendeza kwamba kuna usemi wa Kiebrania ambao wakati mwingine humwita mtu mzuri “mafuta safi ya zeituni.”

‘Mzeituni Unaostawi Katika Nyumba ya Mungu’

Kwa kuzingatia mambo ambayo yametajwa, si ajabu kwamba watumishi wa Mungu wanaweza kulinganishwa na mizeituni. Daudi alitamani kuwa kama “mzeituni mbichi, unaostawi katika nyumba ya Mungu.” (Zaburi 52:8, BHN) Kama vile mara nyingi familia za Waisraeli zilivyokuwa na mizeituni iliyozingira nyumba zao, vivyo hivyo Daudi alitaka kuwa karibu na Yehova na kuzaa matunda kwa sifa ya Mungu.— Zaburi 52:9.

Ufalme wa Yuda wa makabila mawili ulikuwa kama “mzeituni wenye majani mabichi, mzuri, wenye matunda mema” wakati ulipokuwa mwaminifu kwa Yehova. (Yeremia 11:15, 16) Lakini watu wa Yuda walipoteza hali hiyo ya kupendelewa ‘walipokataa kusikia maneno ya Yehova; wakafuata miungu mingine.’—Yeremia 11:10.

Ili kuwa mzeituni unaostawi katika nyumba ya Mungu, ni lazima tumtii Yehova na kuwa tayari kukubali nidhamu ambayo yeye hutumia “kutupogoa” ili tuweze kuzaa matunda zaidi ya Kikristo. (Waebrania 12:5, 6) Isitoshe, kama vile mzeituni wa kawaida huhitaji mizizi mingi ili kustahimili ukame, twahitaji kuimarisha mizizi yetu ya kiroho kusudi tuvumilie majaribu na mnyanyaso.—Mathayo 13:21; Wakolosai 2:6, 7.

Mzeituni wafananisha vizuri Mkristo mwaminifu, ambaye huenda asijulikane katika ulimwengu bali anatambuliwa na Mungu. Mtu kama huyo akifa katika mfumo huu, ataishi tena katika ulimwengu mpya unaokuja.—2 Wakorintho 6:9; 2 Petro 3:13.

Mzeituni ambao ni kama hauwezi kuharibiwa, ambao huendelea kuzaa matunda mwaka baada ya mwaka watukumbusha ahadi hii ya Mungu: “Kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.” (Isaya 65:22) Ahadi hiyo ya kiunabii itatimizwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.—2 Petro 3:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Kwa kawaida machipukizi hayo mapya hupogolewa kila mwaka ili yasidhoofishe mti wenyewe.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Shina la zamani lisilovutia ambalo liko huko Jávea, Mkoa wa Alicante, Hispania

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashamba ya mizeituni katika Mkoa wa Granada, Hispania

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mzeituni wa zamani nje ya kuta za Jerusalem

[Picha katika ukurasa wa 26]

Biblia hutaja kupandikizwa kwa matawi kwenye mzeituni

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mzeituni huu wa zamani umezungukwa na miche ya matawi machanga