Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii kwa Wakati Wetu

Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii kwa Wakati Wetu

Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii kwa Wakati Wetu

“Fahamu, Ee mwanadamu, kwa maana maono haya ni ya wakati wa mwisho.”—DANIELI 8:17.

1. Yehova anataka wanadamu wote wajue nini kuhusu wakati wetu?

YEHOVA hafichi mambo ajuayo juu ya matukio ya wakati ujao. Badala yake, yeye ni Mfunuaji wa siri. Kwa hakika, anataka sote tujue kwamba tunaishi ndani sana katika “wakati wa mwisho.” Hizo ni habari muhimu kama nini kwa watu bilioni sita wanaoishi duniani leo!

2. Kwa nini watu wanahangaikia wakati ujao wa wanadamu?

2 Je, ni ajabu kwamba ulimwengu huu wakaribia mwisho wake? Mwanadamu anaweza kutembea mwezini, lakini katika sehemu nyingi hawezi kutembea kwenye mitaa ya dunia hii bila kuogopa. Anaweza kujaza nyumba vitu vingi vya kisasa, lakini hawezi kuzuia hali inayoongezeka ya kuvunjika kwa familia. Naye anaweza kutokeza njia nyingi za kusambaza habari, lakini hawezi kuwafundisha watu jinsi ya kuishi pamoja kwa amani. Kushindwa huko huunga mkono uthibitisho mwingi wa Kimaandiko wa kwamba twaishi wakati wa mwisho.

3. Maneno “wakati wa mwisho” yalitumiwa lini kwa mara ya kwanza duniani?

3 Maneno hayo yenye kutokeza—“wakati wa mwisho”—yalitumiwa kwa mara ya kwanza duniani na malaika Gabrieli, yapata miaka 2,600 iliyopita. Nabii wa Mungu mwenye hofu alimsikia Gabrieli akisema hivi: “Fahamu, Ee mwanadamu, kwa maana maono haya ni ya wakati wa mwisho.”—Danieli 8:17.

Huu Ndio “Wakati wa Mwisho”!

4. Biblia yarejezea wakati wa mwisho katika njia gani nyinginezo?

4 Semi “wakati wa mwisho” na “wakati wa mwisho ulioamriwa” zapatikana mara sita katika kitabu cha Danieli. (Danieli 8:17, 19; 11:35, 40; 12:4, 9) Semi hizo zahusu “siku za mwisho,” zilizotabiriwa na mtume Paulo. (2 Timotheo 3:1-5) Yesu Kristo alirejezea kipindi hicho kuwa “kuwapo” kwake akiwa Mfalme aliyetawazwa mbinguni.—Mathayo 24:37-39.

5, 6. Ni nani ambao ‘wameenda mbio huko na huko’ katika wakati wa mwisho, na matokeo yamekuwa nini?

5 Andiko la Danieli 12:4 lasema: “Lakini wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa yataongezeka.” Mengi ya mambo ambayo Danieli aliandika yaliwekwa siri na kufungwa ili mwanadamu asipate kuyaelewa kwa karne nyingi. Lakini namna gani leo?

6 Wakati huu wa mwisho, Wakristo wengi waaminifu ‘wameenda mbio huko na huko’ katika Neno la Mungu, Biblia. Matokeo yamekuwa nini? Yehova amebariki jitihada zao, na ujuzi wa kweli umeongezeka. Kwa mfano, Mashahidi watiwa-mafuta wa Yehova wamebarikiwa kupata ufahamu wa ndani unaowawezesha kuelewa kwamba Yesu Kristo alipata kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914. Kulingana na maneno ya mtume yaliyoandikwa katika 2 Petro 1:19-21, watiwa-mafuta hao na waandamani wao waaminifu-washikamanifu ‘wanalikazia uangalifu neno la unabii’ nao wana hakika kabisa kwamba huu ndio wakati wa mwisho.

7. Ni yapi baadhi ya masimulizi ambayo hufanya kitabu cha Danieli kiwe cha pekee?

7 Kitabu cha Danieli ni cha pekee katika njia kadhaa. Humo, mfalme atisha kuwaua watu wake wenye hekima kwa sababu hawawezi kufunua na kufasiri ndoto yake iliyokuwa fumbo, lakini nabii wa Mungu afumbua fumbo hilo. Vijana watatu wanaokataa kuabudu sanamu kubwa sana watupwa kwenye tanuru iliyopashwa moto kupita kiasi, na bado wanaokoka bila kuchomeka. Shamrashamra za sherehe ziendeleapo, mamia ya watu waona mkono ukiandika maneno ya kifumbo kwenye ukuta wa makao ya mfalme. Mahaini waovu wanamfanya mzee fulani atupwe katika tundu la simba, lakini atoka humo salama salimini. Wanyama wanne wanaonekana katika maono, nao wana maana ya kiunabii hadi wakati wa mwisho.

8, 9. Kitabu cha Danieli chaweza kutunufaishaje, hasa sasa, katika wakati wa mwisho?

8 Ni wazi kwamba kitabu cha Danieli kina mambo mawili yaliyo tofauti kabisa. Moja ni masimulizi, jingine ni unabii. Yote mawili yanaweza kujenga imani yetu. Masimulizi yatuonyesha kwamba Yehova Mungu huwabariki wale wanaodumisha uaminifu-maadili kwake. Nazo sehemu za unabii hujenga imani kwa kuonyesha kwamba Yehova hujua wakati ujao mamia ya miaka—hata maelfu ya miaka—mapema.

9 Unabii mbalimbali ulioandikwa na Danieli huzingatia Ufalme wa Mungu. Tuonapo unabii huo ukitimizwa, imani yetu huimarishwa, na ndivyo na usadikisho wetu wa kwamba twaishi wakati wa mwisho. Lakini wachambuzi fulani humshambulia Danieli, wakisema kwamba unabii katika kitabu chake kwa kweli uliandikwa baada ya matukio hayo kutokea. Ikiwa madai hayo ni ya kweli, hilo lingezusha maswali mazito juu ya mambo ambayo kitabu cha Danieli kilitabiri juu ya wakati wa mwisho. Wenye kutilia shaka pia hushuku masimulizi ya kitabu hicho. Kwa hiyo acheni tufanye uchunguzi.

Chashtakiwa!

10. Ni katika maana gani kitabu cha Danieli kinashtakiwa?

10 Jiwazie uko mahakamani, unasikiza kesi. Kiongozi wa mashtaka asisitiza kwamba mshtakiwa ana hatia ya udanganyifu. Vivyo hivyo, kitabu cha Danieli chajionyesha kuwa kitabu asilia kilichoandikwa na nabii Mwebrania aliyeishi katika karne ya saba na ya sita K.W.K. Lakini wachambuzi wanasisitiza kwamba kitabu chake ni udanganyifu. Kwa hiyo basi, acheni kwanza tuone ikiwa ile sehemu ya masimulizi ya kitabu hicho yapatana na mambo hakika ya historia.

11, 12. Ilikuwaje kwa yale mashtaka ya kwamba Belshaza alikuwa mtu wa kuwaziwa tu?

11 Namna gani tukichunguza ile iwezayo kuitwa kesi ya mtawala ambaye hakutajwa. Danieli sura ya 5 yaonyesha kwamba Belshaza alikuwa akitawala akiwa mfalme huko Babiloni wakati jiji hilo lilipopinduliwa mwaka wa 539 K.W.K. Wachambuzi wamebisha jambo hilo kwa sababu jina la Belshaza halikupatikana kwingineko isipokuwa katika Biblia. Badala yake, wanahistoria wa kale walimtaja Nabonido kuwa mfalme wa mwisho wa Babiloni.

12 Hata hivyo, mwaka wa 1854, silinda kadhaa ndogo za udongo zilifukuliwa kwenye magofu ya jiji la Kibabiloni la kale lililoitwa Uru katika Iraki ya leo. Hati hizo za kikabari za Mfalme Nabonido zinatia ndani sala ambayo katika hiyo Mfalme huyo alimtaja “Bel-sar-ussur, mwanangu mkubwa.” Hata wachambuzi walilazimika kukubali: Huyo ndiye Belshaza wa kitabu cha Danieli. Kwa hiyo mtawala ambaye hakutajwa kwa kweli alipata kuishi, ni vile tu mtawala huyo hakuwa ametajwa penginepo ila katika Biblia. Huo ni mojawapo tu wa uthibitisho mwingi kwamba mambo aliyoandika Danieli kwa kweli ni asilia. Uthibitisho huo waonyesha kwamba kwa kweli kitabu cha Danieli ni sehemu ya Neno la Mungu ambalo tunapaswa kulisikiliza sasa hivi, wakati wa mwisho.

13, 14. Nebukadreza alikuwa nani, naye aliabudu hasa mungu gani asiye wa kweli?

13 Katika kitabu cha Danieli kuna unabii unaohusu mfuatano wa serikali za ulimwengu na matendo ya baadhi ya watawala wake. Mmoja wa watawala hao aweza kuitwa mpiganaji aliyejenga milki. Akiwa mwana-mrithi wa mfalme wa Babiloni, yeye na jeshi lake waliyavunjavunja majeshi ya Farao Neko wa Misri huko Karkemishi. Lakini ujumbe fulani ulimlazimu mwana-mfalme huyo wa Babiloni mwenye ushindi awaache majenerali wake wamalizie vita hiyo. Alipopata kujua kwamba baba yake, Nabopolasa, amekufa, kijana huyo aitwaye Nebukadreza alianza kutawala mwaka wa 624 K.W.K. Wakati wa utawala wake wa miaka 43, alijenga milki iliyotia ndani maeneo ambayo pindi moja yalikaliwa na Ashuru, akapanua milki yake hadi Siria na Palestina kuelekea kusini kufikia mpaka wa Misri.

14 Nebukadreza hasa alimwabudu Marduki, mungu mkuu wa Babiloni. Mfalme alimsifia Marduki ushindi wake wote. Huko Babiloni, Nebukadreza alijenga na kurembesha mahekalu ya Marduki na ya miungu mingine mingi ya Babiloni. Ile sanamu ya dhahabu ambayo mfalme huyo wa Babiloni alijenga katika uwanda wa Dura huenda iliwekwa wakfu kwa Marduki. (Danieli 3:1, 2) Na yaonekana Nebukadreza alitegemea sana uaguzi alipokuwa akipanga mbinu zake za vita.

15, 16. Nebukadreza alifanyia Babiloni nini, na nini kilichotukia alipojisifu kuhusu ukuu wake?

15 Kwa kumalizia kujenga zile kuta mbili kubwa za Babiloni ambazo baba yake alikuwa ameanza kujenga, Nebukadreza alifanya jiji hilo kuu lionekane kama haliwezi kushindwa. Ili kumridhisha mke wake Mmedi, aliyetamani vilima na misitu ya nyumbani kwao, yasemekana kwamba Nebukadreza alijenga zile bustani zenye kuning’inia—mojawapo ya maajabu saba ya ulimwengu wa kale. Alifanya Babiloni kuwa jiji kuu zaidi lenye kuta wakati huo. Alijivunia kama nini kituo hicho cha ibada isiyo ya kweli!

16 Nebukadreza alijisifu siku moja akisema, “Mji huu sio Babeli mkubwa nilioujenga mimi?” Hata hivyo, kulingana na Danieli 4:30-36, “neno lile lilipokuwa katika kinywa cha mfalme,” akapatwa na kichaa. Akiwa hastahili kutawala kwa miaka saba, alikula majani kama vile tu Danieli alivyotabiri. Kisha akarudishiwa ufalme. Je, unajua maana ya unabii ya mambo hayo yote? Je, unaweza kueleza jinsi utimizo wake mkubwa zaidi hutuleta hadi wakati wa mwisho?

Kuchunguza Unabii Mbalimbali

17. Unaweza kufafanuaje ndoto ya kiunabii ambayo Mungu alimwotesha Nebukadreza katika mwaka wa pili wa utawala wake akiwa mtawala wa ulimwengu?

17 Sasa acheni tuchunguze unabii fulani wa kitabu cha Danieli. Mwaka wa pili wa utawala wa Nebukadreza akiwa mtawala wa ulimwengu wa unabii wa Biblia (606/605 K.W.K.), Mungu alimwotesha ndoto yenye kuogofya. Kulingana na Danieli sura ya 2, ndoto hiyo ilikuwa juu ya sanamu kubwa yenye kichwa cha dhahabu, kifua na mikono ya fedha, tumbo na viuno vya shaba, miguu ya chuma, na nyayo za miguu za chuma kilichochanganyika na udongo. Ni nini kinachowakilishwa na sehemu hizo mbalimbali za sanamu hiyo?

18. Ni nini kinachowakilishwa na kichwa cha dhahabu, kifua na mikono ya fedha, na viuno vya shaba vya sanamu iliyoonekana katika ndoto?

18 Nabii wa Mungu alimwambia Nebukadreza hivi: “Wewe, Ee mfalme . . . u kichwa kile cha dhahabu.” (Danieli 2:37, 38) Nebukadreza aliongoza nasaba iliyotawala Milki ya Babiloni. Nasaba hiyo ilipinduliwa na Umedi na Uajemi, zinazowakilishwa na kifua na mikono ya fedha ya ile sanamu. Kisha ikaja Milki ya Ugiriki, inayowakilishwa na tumbo na viuno vya shaba. Serikali hiyo ya ulimwengu ilianzaje?

19, 20. Aleksanda Mkuu alikuwa nani, naye alitekeleza fungu gani katika kufanya Ugiriki kuwa serikali ya ulimwengu?

19 Katika karne ya nne K.W.K., mwanamume mmoja kijana alitekeleza fungu muhimu katika kutimiza unabii wa Danieli. Alizaliwa mwaka wa 356 K.W.K., na watu wamemwita Aleksanda Mkuu. Baba yake, Filipo, alipouawa mwaka wa 336 K.W.K., Aleksanda mwenye umri wa miaka 20 akaanza kutawala Makedonia.

20 Mapema mwezi wa Mei mwaka wa 334 K.W.K., Aleksanda alianza vita vyake vya ushindi. Alikuwa na jeshi dogo lakini lenye nguvu la askari-jeshi 30,000 wa miguu na askari wapanda-farasi 5,000. Kwenye Mto Granicus kaskazini-magharibi mwa Asia Ndogo (sasa Uturuki), Aleksanda alishinda vita yake ya kwanza dhidi ya Waajemi mwaka wa 334 K.W.K. Kufikia mwaka wa 326 K.W.K., mshindi huyo asiyechoka alikuwa ameshinda Waajemi na alikuwa amefika upande wa mashariki wa Mto Indus, katika Pakistan ya leo. Lakini Aleksanda alishindwa vita yake ya mwisho akiwa Babiloni. Juni 13, 323 K.W.K., baada ya kuishi miaka 32 na miezi 8 tu, Aleksanda alishindwa na adui mwenye kutisha zaidi, kifo. (1 Wakorintho 15:55) Lakini kupitia ushindi wake mbalimbali, Ugiriki ilikuwa imepata kuwa serikali ya ulimwengu, kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Danieli.

21. Mbali na Milki ya Roma, ni serikali gani nyingine ya ulimwengu ambayo inawakilishwa na miguu ya chuma ya sanamu hiyo iliyoonekana katika ndoto?

21 Ni nini kinachowakilishwa na miguu ya chuma ya sanamu hiyo kubwa? Ilifananisha Roma iliyo kama chuma ambayo iliponda na kuvunjavunja Milki ya Ugiriki. Waroma walimwua Yesu kwenye mti wa mateso mwaka wa 33 W.K., wakikosa kustahi Ufalme wa Mungu uliotangazwa na Yesu Kristo. Roma iliwanyanyasa wanafunzi wa Yesu ikijaribu kuvunjavunja Ukristo wa kweli. Hata hivyo, ile miguu ya chuma katika sanamu ambayo Nebukadreza aliona kwenye ndoto yafananisha Milki ya Roma pamoja na serikali za kisiasa zilizotokana na milki hiyo—Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani.

22. Sanamu hiyo iliyoonekana katika ndoto inatusaidiaje kutambua kwamba tunaishi ndani sana katika wakati wa mwisho?

22 Uchunguzi wa makini wathibitisha kwamba tunaishi ndani sana katika wakati wa mwisho, kwa kuwa tumefikia nyayo ya miguu ya chuma na udongo ya sanamu hiyo iliyoonekana katika ndoto. Leo, baadhi ya serikali ni kama chuma au ni za kimabavu, ilhali nyingine ni kama udongo. Licha ya kwamba udongo, ambao “mbegu za [“uzao wa,” NW] wanadamu” zimefanyizwa kutokana nao, waweza kuvunjika kwa urahisi, tawala zilizo kama chuma zimelazimika kuacha watu wa kawaida watoe maoni katika serikali zinazowatawala. (Danieli 2:43; Ayubu 10:9) Bila shaka, utawala wa kimabavu hauwezi kushikamana na watu wa kawaida kama vile chuma isivyoweza kuungana na udongo. Lakini karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha ulimwengu huu uliogawanyika kisiasa.—Danieli 2:44.

23. Unaweza kufafanuaje ndoto na maono ambayo Danieli alipata katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Belshaza?

23 Sura ya 7 ya unabii wa Danieli wenye kuvutia pia hutuleta katika wakati wa mwisho. Sura hiyo yasimulia tukio fulani katika mwaka wa kwanza wa Mfalme Belshaza wa Babiloni. Wakati huo akiwa na umri wa miaka 70 na kitu, Danieli anaota “ndoto, na [kuona] maono ya kichwa chake, kitandani mwake.” Maono hayo yanamwogofya kama nini! “Tazama”! asema kwa mshangao. “Pepo nne za mbinguni zilivuma kwa nguvu juu ya bahari kubwa. Ndipo wanyama wakubwa wanne wakatoka baharini, wote wa namna mbalimbali.” (Danieli 7:1-8, 15) Ni wanyama wa ajabu kama nini! Wa kwanza ni simba mwenye mabawa, naye wa pili ni kama dubu. Kisha chui mwenye mabawa manne na vichwa vinne! Mnyama wa nne mwenye nguvu zisizo za kawaida ana meno makubwa ya chuma na pembe kumi. Miongoni mwa pembe zake kumi yazuka ‘pembe ndogo’ yenye “macho kama macho ya mwanadamu” na “kinywa kilichokuwa kikinena maneno makuu.” Ni wanyama wa ajabu kama nini!

24. Kulingana na Danieli 7:9-14, ni nini ambacho Danieli anaona mbinguni, na maono hayo yarejezea nini?

24 Maono ya Danieli yageukia mbingu sasa. (Danieli 7:9-14) ‘Mzee wa Siku,’ Yehova Mungu, aonekana ameketi kwa utukufu akiwa Hakimu. ‘Maelfu elfu wamtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi wasimama mbele zake.’ Akiwahukumu wanyama hao vikali, Mungu awanyang’anya utawala na kumharibu mnyama wa nne. Utawala wenye kudumu juu ya “watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote” wapewa “mmoja aliye mfano wa mwanadamu.” Hilo larejezea wakati wa mwisho na kutawazwa kwa Mwana wa binadamu, Yesu Kristo, mwaka wa 1914.

25, 26. Ni maswali gani yawezayo kuzuka tusomapo kitabu cha Danieli, na ni kichapo gani kiwezacho kutusaidia kuyajibu?

25 Wasomao kitabu cha Danieli bila shaka watakuwa na maswali. Kwa mfano, wale wanyama wanne katika Danieli sura ya 7 wanawakilisha nini? Unabii wa “majuma sabini” katika Danieli 9:24-27 wamaanisha nini? Namna gani Danieli sura ya 11 na pambano la kiunabii kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini”? Twaweza kutarajia nini kutokana na wafalme hao katika wakati wa mwisho?

26 Yehova amewapa watumishi wake watiwa-matufa walio duniani, waitwao “watakatifu wake Aliye juu” katika Danieli 7:18, ufahamu wenye kina juu ya mambo hayo. Isitoshe, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amefanya uandalizi ili sisi sote tupate ufahamu wenye kina zaidi wa maandiko yaliyopuliziwa ya nabii Danieli. (Mathayo 24:45) Uandalizi huo sasa wapatikana kupitia kutolewa hivi majuzi kwa kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! Kichapo hicho chenye kurasa 320 chenye picha nzuri chazungumzia sehemu zote za kitabu cha Danieli. Chazungumzia unabii wote wenye kujenga imani na masimulizi yote yaliyoandikwa na nabii mpendwa, Danieli.

Maana Hasa Katika Wakati Wetu

27, 28. (a) Kuna ukweli gani kuhusu kutimizwa kwa unabii wa kitabu cha Danieli? (b) Tunaishi katika wakati gani, na twapaswa kufanya nini?

27 Sasa fikiria jambo hili la maana: Isipokuwa mambo machache tu, unabii wote wa kitabu cha Danieli tayari umetimizwa. Kwa mfano, tayari twaona hali ya ulimwengu iliyofananishwa na nyayo za miguu ya sanamu ambayo ilionekana kwenye ndoto ya Danieli sura ya 2. Kile kisiki cha shina cha Danieli sura ya 4 kilifunguliwa wakati Mfalme wa Kimesiya, Yesu Kristo, alipotawazwa mwaka wa 1914. Naam, kama ilivyotabiriwa katika Danieli sura ya 7, Mzee wa Siku akampa utawala Mwana wa binadamu.—Danieli 7:13, 14; Mathayo 16:27–17:9.

28 Zile siku 2,300 za Danieli sura ya 8 na pia zile siku 1,290 na zile siku 1,335 za Danieli sura ya 12—zote hizo zimepita. Uchunguzi wa Danieli sura ya 11 waonyesha kwamba pambano kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” limefikia hatua zake za mwisho-mwisho. Yote hayo yaongezea uthibitisho wa Kimaandiko wa kwamba tunaishi ndani sana katika wakati wa mwisho. Kwa kufikiria wakati wa pekee tunamoishi, yatupasa tuazimie kufanya nini? Bila shaka, yatupasa kusikiliza neno la kiunabii la Yehova Mungu.

Ungejibuje?

• Mungu anataka wanadamu wote wajue nini kuhusu wakati wetu?

• Kitabu cha Danieli kinawezaje kujenga imani yetu?

• Sanamu ambayo Nebukadreza aliona katika ndoto ilikuwa na sehemu gani, nazo zilifananisha nini?

• Kuna jambo gani kuu kuhusu kutimizwa kwa unabii katika kitabu cha Danieli?

[Maswali ya Funzo]