Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Imani Katika Neno la Mungu la Kiunabii!

Uwe na Imani Katika Neno la Mungu la Kiunabii!

Uwe na Imani Katika Neno la Mungu la Kiunabii!

“Tuna neno la unabii likiwa limefanywa hakika zaidi.”—2 PETRO 1:19.

1, 2. Unabii wa kwanza uliopata kuandikwa ni upi, na swali moja ambalo unabii huo ulizusha ni gani?

YEHOVA ndiye Chanzo cha unabii wa kwanza uliopata kuandikwa. Baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, Mungu alimwambia nyoka hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako [“mbegu yako,” NW] na uzao wake [“mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:1-7, 14, 15) Unabii huo ungeeleweka kikamili karne nyingi baadaye.

2 Unabii huo wa kwanza uliwapa wanadamu wenye dhambi tumaini halisi. Baadaye Maandiko yalimtambulisha Shetani Ibilisi kuwa “nyoka wa awali.” (Ufunuo 12:9) Lakini ni nani angekuwa Mbegu ya Mungu iliyoahidiwa?

Kuitafuta Mbegu

3. Abeli alidhihirishaje imani katika unabii wa kwanza?

3 Tofauti na babake, Abeli aliyemcha Mungu alidhihirisha imani katika unabii huo wa kwanza. Inaonekana Abeli alitambua kuwa damu ingehitaji kumwagwa ili kufunika dhambi. Kwa hiyo, imani ikamchochea kutoa dhabihu ya mnyama ambayo Mungu alikubali. (Mwanzo 4:2-4) Lakini utambulisho wa Mbegu iliyoahidiwa bado haukujulikana.

4. Mungu alimpa Abrahamu ahadi gani, nayo ilionyesha nini kuhusu Mbegu iliyoahidiwa?

4 Miaka ipatayo 2,000 baada ya wakati wa Abeli, Yehova alimpa Abrahamu, aliyekuwa mzee wa ukoo, ahadi hii ya kiunabii: “Katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako [“mbegu yako,” NW] kama nyota za mbinguni . . . katika uzao wako [“mbegu yako,” NW] mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:17, 18) Maneno hayo yalionyesha kwamba Abrahamu alihusika na kutimizwa kwa unabii wa kwanza. Yalionyesha kwamba Mbegu ambayo kupitia kwake kazi za Shetani zingebatilishwa ingetokea katika ukoo wa Abrahamu. (1 Yohana 3:8) “Kwa sababu ya ahadi ya Mungu [Abrahamu] hakusitasita kwa ukosefu wa imani” wala mashahidi wengine wa Yehova wa kabla ya Ukristo ambao “hawakupata utimizo wa ahadi.” (Waroma 4:20, 21; Waebrania 11:39) Badala yake, walidumisha imani katika neno la Mungu la kiunabii.

5. Ahadi ya Mungu ya Mbegu ilitimizwa katika nani, na kwa nini unajibu hivyo?

5 Mtume Paulo alitambulisha Mbegu ya Mungu iliyoahidiwa alipoandika hivi: “Ahadi zilisemwa kwa Abrahamu na kwa mbegu yake. Haisemi: ‘Na kwa hizo mbegu,’ kama katika kisa cha nyingi za namna hiyo, bali kama katika kisa cha moja: ‘Na kwa mbegu yako,’ ambaye ni Kristo.” (Wagalatia 3:16) Mbegu ambayo kupitia kwake mataifa yangejibariki haikutia ndani wazao wote wa Abrahamu. Wazao wa mwana wake Ishmaeli na wazao wa wana aliozaa na Ketura hawakutumiwa kubariki wanadamu. Mbegu ya baraka ilikuja kupitia mwana wake Isaka na mjukuu wake Yakobo. (Mwanzo 21:12; 25:23, 31-34; 27:18-29, 37; 28:14) Yakobo alionyesha kwamba “mataifa” yangemtii Shilo wa kabila la Yuda, lakini baadaye Mbegu hiyo ikawa itoke tu katika ukoo wa Daudi. (Mwanzo 49:10; 2 Samweli 7:12-16) Wayahudi wa karne ya kwanza walitazamia mtu mmoja aje akiwa Mesiya, au Kristo. (Yohana 7:41, 42) Na unabii wa Mungu kuhusu Mbegu ulitimizwa katika Mwana wake, Yesu Kristo.

Mesiya Atokea!

6. (a) Tueleweje unabii wa majuma 70? (b) Yesu ‘alikomesha dhambi’ lini na jinsi gani?

6 Nabii Danieli aliandika unabii muhimu kuhusu Mesiya. Katika mwaka wa kwanza wa Dario Mmedi, Danieli alitambua kwamba ukiwa wa Yerusalemu wa miaka 70 ulikaribia kwisha. (Yeremia 29:10; Danieli 9:1-4) Danieli alipokuwa akisali, malaika Gabrieli alikuja na kumfunulia kwamba ‘muda wa majuma sabini umeamriwa ili kukomesha dhambi.’ Mesiya angekatiliwa mbali katikati ya juma la 70. “Majuma sabini ya miaka” yalianza mwaka wa 455 K.W.K., wakati Artashasta wa Kwanza wa Uajemi ‘alipotoa amri ya kuujenga tena Yerusalemu.’ (Danieli 9:20-27; Moffatt; Nehemia 2:1-8) Mesiya angekuja baada ya majuma 7 kuongezea majuma 62. Miaka hii 483 ilianzia mwaka wa 455 K.W.K. hadi mwaka wa 29 W.K., Yesu alipobatizwa na kutiwa mafuta na Mungu kuwa Mesiya, au Kristo. (Luka 3:21, 22) Yesu ‘alikomesha dhambi’ kwa kutoa uhai wake uwe fidia mwaka wa 33 W.K. (Marko 10:45) Ni sababu nzuri kama nini za kuwa na imani katika neno la Mungu la kiunabii! *

7. Ukitumia Maandiko, onyesha jinsi Yesu alivyotimiza unabii wa Kimesiya.

7 Imani katika neno la Mungu la kiunabii hutuwezesha kumtambua Mesiya. Kati ya unabii mwingi wa Kimesiya ambao umetajwa katika Maandiko ya Kiebrania, idadi kubwa ilitumiwa na waandishi wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kumrejezea Yesu moja kwa moja. Kwa mfano: Yesu alizaliwa na bikira huko Bethlehemu. (Isaya 7:14; Mika 5:2; Mathayo 1:18-23; Luka 2:4-11) Aliitwa kutoka Misri, na vitoto vikauawa baada ya kuzaliwa kwake. (Yeremia 31:15; Hosea 11:1; Mathayo 2:13-18) Yesu alichukua magonjwa yetu. (Isaya 53:4; Mathayo 8:16, 17) Kama ilivyotabiriwa, aliingia Yerusalemu akiwa amepanda mwana-punda. (Zekaria 9:9; Yohana 12:12-15) Maneno ya mtunga-zaburi yalitimizwa baada ya Yesu kutundikwa mtini wakati askari walipogawana mavazi yake na kupigia kura vazi lake la ndani. (Zaburi 22:18; Yohana 19:23, 24) Jambo la kwamba mifupa ya Yesu haikuvunjwa na kwamba alidungwa lilitimiza unabii pia. (Zaburi 34:20; Zekaria 12:10; Yohana 19:33-37) Hii ni mifano michache tu kati ya unabii wa Kimesiya unaomrejezea Yesu ambao ulitumiwa na waandishi wa Biblia waliopuliziwa na Mungu. *

Mshangilieni Mfalme wa Kimesiya!

8. Mzee wa Siku ni nani, na unabii ulioandikwa katika Danieli 7:9-14 ulitimizwaje?

8 Katika mwaka wa kwanza wa Mfalme Belshaza wa Babiloni, Yehova alimwotesha Danieli ndoto na kumwonyesha maono ya ajabu. Kwanza, nabii huyo aliona wanyama wanne wakubwa sana. Malaika wa Mungu aliwatambulisha hao wanyama kuwa “wafalme wanne,” hivyo akionyesha kwamba walifananisha serikali za ulimwengu zenye kufuatana. (Danieli 7:1-8, 17) Baadaye Danieli alimwona Yehova, ‘Mzee wa Siku,’ ameketi kwa utukufu kwenye kiti cha ufalme. Alihukumu wanyama hao vikali, akawanyang’anya mamlaka na kumharibu mnyama wa nne. Kisha mamlaka ya milele juu ya “kabila zote, na taifa zote, na lugha zote” yakapewa “mmoja aliye mfano wa mwanadamu.” (Danieli 7:9-14) Ni unabii mzuri kama nini kuhusu kutawazwa kwa “Mwana wa binadamu,” Yesu Kristo, huko mbinguni mwaka wa 1914!—Mathayo 16:13.

9, 10. (a) Sehemu mbalimbali za sanamu iliyoonekana katika ndoto zilionyesha nini? (b) Ungeelezaje utimizo wa Danieli 2:44?

9 Danieli alijua kwamba Mungu “huuzulu wafalme na kuwamilikisha wafalme.” (Danieli 2:21) Akiwa na imani katika Yehova, ‘Mfunuaji wa siri,’ nabii huyo alifunua maana ya sanamu kubwa sana ambayo Mfalme Nebukadreza wa Babiloni aliona katika ndoto. Sehemu zake mbalimbali zaonyesha kusimama na kuanguka kwa serikali za ulimwengu kama Babiloni, Muungano wa Umedi na Uajemi, Ugiriki, na Roma. Mungu pia alimtumia Danieli aeleze matukio ya ulimwengu hadi wakati wetu na baadaye.—Danieli 2:24-30.

10 “Katika siku za wafalme hao,” unabii huo ukasema, “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Wakati “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zilipoisha mwaka wa 1914, Mungu alisimamisha Ufalme wa mbinguni chini ya Kristo. (Luka 21:24; Ufunuo 12:1-5) Kisha kwa nguvu za Mungu “jiwe” la Ufalme wa Kimesiya likachongwa kutoka ‘mlima’ wa enzi kuu ya ulimwengu ya Mungu. Kwenye Har–Magedoni jiwe hilo litapiga sanamu hiyo na kuiponda-ponda kabisa. Kama mlima wa kiserikali unaotawala “dunia yote,” Ufalme wa Kimesiya utasimama milele.—Danieli 2:35, 45; Ufunuo 16:14, 16. *

11. Kugeuzwa umbo kwa Yesu kulionyesha nini kimbele, na maono hayo yalikuwa na matokeo gani juu ya Petro?

11 Akifikiria utawala wake wa Ufalme, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kuna baadhi ya wale ambao wamesimama hapa ambao hawataonja kifo hata kidogo mpaka kwanza wamwone Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.” (Mathayo 16:28) Siku sita baadaye, Yesu alimchukua Petro, Yakobo, na Yohana wakapanda mlima mrefu ambako aligeuzwa umbo mbele yao. Wingu jangavu lilipowafunika mitume, Mungu alitangaza: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye mimi nimemkubali; msikilizeni yeye.” (Mathayo 17:1-9; Marko 9:1-9) Ni wonyesho wa kimbele ulioje wa utukufu wa Ufalme wa Kristo! Si ajabu kwamba Petro aliyarejezea maono hayo yenye kustaajabisha na kusema: “Kwa sababu hiyo tuna neno la unabii likiwa limefanywa hakika zaidi.”—2 Petro 1:16-19. *

12. Kwa nini huu hasa ndio wakati wa kudhihirisha imani yetu katika neno la Mungu la kiunabii?

12 Yaonekana “neno la unabii” latia ndani unabii wa Maandiko ya Kiebrania kumhusu Mesiya na pia maneno ya Yesu kwamba angekuja “na nguvu na utukufu mkubwa.” (Mathayo 24:30) Mgeuko-umbo huo ulithibitisha neno la kiunabii kuhusu kuja kwa Kristo kwa utukufu katika mamlaka ya Ufalme. Hivi karibuni, kufunuliwa kwake katika utukufu kutamaanisha uharibifu kwa wasio na imani na baraka kwa wanaodhihirisha imani. (2 Wathesalonike 1:6-10) Kutimizwa kwa unabii wa Biblia kwathibitisha kwamba hizi ndizo “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5, 16, 17; Mathayo 24:3-14) Akiwa Mfishaji Mkuu wa Yehova, Mikaeli, ambaye ni Yesu Kristo, yuko tayari kumaliza mfumo huu mwovu wa mambo wakati wa “dhiki kubwa.” (Mathayo 24:21; Danieli 12:1) Basi, huu hasa ndio wakati wa kudhihirisha kwamba tuna imani katika neno la Mungu la kiunabii.

Dumisha Imani Katika Neno la Mungu la Kiunabii

13. Ni nini kiwezacho kutusaidia tudumishe upendo kwa Mungu na kuendeleza imani katika neno lake?

13 Bila shaka tulisisimuka tulipojifunza kwa mara ya kwanza juu ya kutimizwa kwa neno la Mungu la kiunabii. Lakini je, imani yetu imepungua na upendo wetu kupoa tangu wakati huo? Na tusiwe kamwe kama Wakristo katika Efeso ‘walioacha upendo waliokuwa nao hapo kwanza.’ (Ufunuo 2:1-4) Haidhuru tumemtumikia Yehova kwa muda gani, upendo wetu wa kwanza unaweza kupoa ‘tusipofuliza kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake Mungu’ ili kuweka hazina mbinguni. (Mathayo 6:19-21, 31-33) Kujifunza Biblia kwa bidii, kushiriki kwa ukawaida katika mikutano ya Kikristo, na kuhubiri Ufalme kwa bidii kutatusaidia kuendelea kumpenda Yehova, Mwana wake, na Maandiko. (Zaburi 119:105; Marko 13:10; Waebrania 10:24, 25) Kufanya hivyo kutaendeleza imani yetu katika neno la Mungu.—Zaburi 106:12.

14. Wakristo watiwa-mafuta huthawabishwaje kwa imani yao katika neno la Yehova la kiunabii?

14 Kama vile ambavyo neno la Mungu la kiunabii limetimizwa wakati uliopita, basi tunaweza kuwa na imani katika mambo ambayo hilo hutabiri kuhusu wakati ujao. Kwa mfano, kuwapo kwa Kristo katika utukufu wa Ufalme kumetokea, nao Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa waaminifu hadi kifo wamepata utimizo wa ahadi hii ya kiunabii: “Kwake ambaye hushinda hakika nitamruhusu kula kutoka katika mti wa uhai, ambao umo katika paradiso ya Mungu.” (Ufunuo 2:7, 10; 1 Wathesalonike 4:14-17) Yesu huwapa washindi hao pendeleo la “kula kutoka katika mti wa uhai” kwenye ‘paradiso ya mbinguni ya Mungu.’ Wanapofufuliwa na kupitia Yesu Kristo, wao huchukua hali ya kutoweza kufa na kutoharibika inayotolewa na Yehova, “Mfalme wa milele, asiyeweza kuona uharibifu, asiyeonekana, Mungu peke yake.” (1 Timotheo 1:17, UV; 1 Wakorintho 15:50-54; 2 Timotheo 1:10) Ni thawabu iliyoje kwa kumpenda Mungu kwa dhati na kwa imani thabiti katika neno lake la kiunabii!

15. Msingi wa “dunia mpya” uliwekwa kupitia nani, na ni nani wanaoshirikiana nao?

15 Punde baada ya watiwa-mafuta waaminifu waliokufa kufufuliwa katika “paradiso ya Mungu” ya mbinguni, mabaki ya Israeli wa kiroho duniani walikombolewa kutoka “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 14:8; Wagalatia 6:16) Kupitia wao msingi wa “dunia mpya” uliwekwa. (Ufunuo 21:1) Hivyo, “nchi” ikazaliwa, na kufanywa paradiso ya kiroho inayositawi ulimwenguni pote leo. (Isaya 66:8) Sasa umati wenye mfano wa kondoo, ambao unashirikiana na Israeli wa kiroho, unamiminika kwenye paradiso hiyo, “katika siku za mwisho.”—Isaya 2:2-4; Zekaria 8:23; Yohana 10:16; Ufunuo 7:9.

Wakati Ujao wa Wanadamu Watabiriwa Katika Neno la Mungu la Kiunabii

16. Wana matazamio gani wale wanaowaunga mkono watiwa-mafuta kwa uaminifu-mshikamanifu?

16 Wana matazamio gani wale wanaowaunga mkono watiwa-mafuta kwa uaminifu-mshikamanifu? Wao pia wana imani katika neno la Mungu la kiunabii, na tumaini lao ni kuingia katika Paradiso ya kidunia. (Luka 23:39-43) Humo watakunywa kutoka kwenye “mto wa maji ya uhai” wenye kuendeleza uhai na wataponywa na ‘majani ya miti’ iliyopandwa kandokando ya mto huo. (Ufunuo 22:1, 2) Ikiwa una tumaini hilo la ajabu, na uendelee kumpenda sana Yehova na kuwa na imani katika neno lake la kiunabii. Na uwe miongoni mwa wale wanaopata shangwe isiyo na kifani ya uhai udumuo milele katika dunia Paradiso.

17. Maisha katika Paradiso ya kidunia yatatia ndani baraka zipi?

17 Wanadamu wasiokamilika hawawezi kueleza kikamili jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso ya kidunia inayokuja, lakini neno la Mungu la kiunabii hutupa ufahamu wenye kina wa baraka ambazo wanadamu watiifu watapata wakati huo. Ufalme wa Mungu utawalapo bila kupingwa na mapenzi yake kufanywa duniani kama yafanywavyo mbinguni, hakuna wanadamu wakatili—wala hata wanyama—‘watakaodhuru wala kuharibu.’ (Isaya 11:9; Mathayo 6:9, 10) Wapole watakaa duniani, na “watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Hakutakuwako watu wenye kufa kwa njaa, kwa kuwa ‘kutakuwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya mlima.’ (Zaburi 72:16) Watu hawatalia tena kwa huzuni. Magonjwa yatatoweka, na hata kifo hakitakuwapo tena. (Isaya 33:24; Ufunuo 21:4) Ebu wazia—hakuna madaktari, hakuna dawa, hakuna hospitali au makao ya watu wasio na akili timamu, na hakuna maziko. Ni matazamio mazuri kama nini!

18. (a) Danieli alihakikishiwa nini? (b) “Tuzo” la Danieli litakuwa nini?

18 Hata kaburi la ujumla la wanadamu litakuwa tupu wafu wafufuliwapo. Yobu mwadilifu alikuwa na tumaini hilo. (Ayubu 14:14, 15) Nabii Danieli pia alikuwa na tumaini hilo, kwa kuwa malaika wa Yehova alimpa uhakikisho huu wenye kufariji: “Lakini wewe ee Danieli, jiendee, ukapumzike kaburini, na wakati huo utakapotimia, utafufuka na kupata tuzo lako.” (Danieli 12:13, Biblia Habari Njema) Danieli alimtumikia Mungu kwa uaminifu hadi kifo. Sasa anapumzika katika kifo, lakini ‘atafufuka’ katika “ufufuo wa walio waadilifu” wakati wa utawala wa Mileani wa Kristo. (Luka 14:14) “Tuzo” la Danieli litakuwa nini? Wakati utakapotimizwa katika Paradiso, unabii wa Ezekieli waonyesha kwamba watu wa Yehova watakuwa na fungu, hata nchi itagawanywa kwa haki na kwa utaratibu. (Ezekieli 47:13–48:35) Kwa hiyo Danieli atakuwa na fungu katika Paradiso, lakini tuzo lake huko litatia ndani mengi zaidi ya kupata nchi tu. Litatia ndani fungu lake katika kusudi la Yehova.

19. Nini kinachohitajiwa ili kuishi katika Paradiso ya kidunia?

19 Namna gani wewe na tuzo lako? Ikiwa una imani katika Neno la Mungu Biblia, yaelekea sana kwamba unatamani kuishi katika Paradiso ya kidunia. Huenda hata ukajiwazia ukiwa humo, ukifurahia baraka zake nyingi, ukitunza dunia, na kuwakaribisha wafu kwa shangwe. Kwani, Paradiso ndiyo makao ya wanadamu. Mungu aliwaumba wanadamu wa kwanza wawili waishi mahali kama hapo. (Mwanzo 2:7-9) Naye ataka wanadamu watiifu waishi milele katika Paradiso. Je, utatenda kulingana na Maandiko ili uwe miongoni mwa mabilioni ya watu ambao hatimaye wataishi kwenye Paradiso duniani? Unaweza kuwepo ikiwa unampenda kikweli Baba yetu wa mbinguni, Yehova, na una imani yenye kudumu katika neno la Mungu la kiunabii.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona sura ya 11 ya Sikiliza Unabii wa Danieli! na habari yenye kichwa “Seventy Weeks” katika Insight on the Scriptures, vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

^ fu. 7 Ona kichapo Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” ukurasa wa 343-344, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

^ fu. 10 Ona sura ya 4 na 9 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

^ fu. 11 Ona makala “Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii,” katika Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 2000.

Ungejibuje?

• Unabii wa kwanza ni upi, na Mbegu iliyoahidiwa ni nani?

• Ni unabii gani mbalimbali wa Kimesiya uliotimizwa katika Yesu?

• Andiko la Danieli 2:44, 45 litatimizwaje?

• Neno la Mungu la kiunabii laonyesha kutakuwa na wakati gani ujao kwa ajili ya wanadamu watiifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unatumaini kuishi katika Paradiso ya kidunia?