Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilisaidiwa Kuacha Kuwa Mwenye Haya

Nilisaidiwa Kuacha Kuwa Mwenye Haya

Simulizi la Maisha

Nilisaidiwa Kuacha Kuwa Mwenye Haya

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA RUTH L. ULRICH

Nilishindwa kuvumilia, nikabwaga machozi papo hapo kwenye mlango wa kasisi. Alikuwa ametoka tu kusema mambo mengi yasiyo ya kweli akimshutumu Charles T. Russell, aliyetumikia akiwa msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society. Ebu niwaeleze jinsi mimi, nikiwa msichana mdogo tu, nilivyokuwa nikiwazuru watu.

NILIZALIWA mwaka wa 1910 kwenye shamba moja kule Nebraska, Marekani, katika familia ya kidini sana. Katika familia yetu, tulikuwa tukisoma Biblia pamoja kila asubuhi na jioni baada ya kula. Baba alikuwa msimamizi wa shule ya Jumapili ya kanisa la Methodist katika mji mdogo wa Winside, uliokuwa kilometa sita hivi kutoka kwenye shamba letu. Tulikuwa na gari lenye kukokotwa na farasi lenye madirisha yenye pazia, ili kwamba hata hali ya hewa iweje, tungeenda kanisani Jumapili asubuhi.

Nilipokuwa na umri wa miaka minane hivi, ndugu yangu mdogo alishikwa na ugonjwa wa polio na Mama akampeleka kwenye hospitali moja huko Iowa akatibiwe. Japo mama alimtunza vizuri, ndugu yangu alikufa wakiwa huko. Lakini, akiwa huko Iowa, Mama alikutana na mmoja wa Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Waliongea sana, na Mama hata akahudhuria baadhi ya mikutano ya Wanafunzi wa Biblia pamoja na mwanamke huyo.

Mama aliporudi nyumbani, alileta mabuku kadhaa ya Studies in the Scriptures, ambayo yalichapishwa na Watch Tower Society. Upesi akasadiki kwamba Wanafunzi wa Biblia wanafundisha kweli na kwamba mafundisho ya kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu na waovu kuteswa milele hayakuwa ya kweli.—Mwanzo 2:7; Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4.

Lakini Baba alikasirika sana, hata akapinga jitihada za Mama za kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia. Baba aliendelea kutupeleka mimi na ndugu yangu mkubwa, Clarence, kanisani. Lakini wakati Baba hakuwako nyumbani, Mama alitufundisha Biblia. Basi, sisi watoto tukawa na fursa nzuri ya kulinganisha mafundisho ya Wanafunzi wa Biblia na yale ya kanisa letu.

Mimi na Clarence tulikuwa tukihudhuria kwa ukawaida shule ya Jumapili katika kanisa letu, na Clarence alikuwa akimwuliza mwalimu maswali ambayo hangeweza kujibu. Tulipofika nyumbani, tulikuwa tukimwambia mama na hiyo ilikuwa inatokeza mazungumzo marefu juu ya maswali hayo. Hatimaye, niliacha kanisa na kuanza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia pamoja na Mama, na muda mfupi baadaye hata Clarence akafanya vivyo hivyo.

Kukabiliana na Haya

Mnamo Septemba 1922, tulihudhuria na Mama ule mkusanyiko wenye kukumbukwa wa Wanafunzi wa Biblia huko Cedar Point, Ohio. Bado naweza kuona lile bango kubwa likifumuka wakati Joseph F. Rutherford, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Watch Tower Society, alipohimiza wahudhuriaji zaidi ya 18,000, akitumia maneno ya bango hilo: “Tangazeni Mfalme na Ufalme.” Niliguswa moyo sana na nikaona uharaka wa kuwaeleza wengine habari njema za Ufalme wa Mungu.—Mathayo 6:9, 10; 24:14.

Katika mikusanyiko iliyofanywa tokea mwaka wa 1922 hadi 1928, tulipitisha maazimio kadhaa, na ujumbe wake ukaandikwa katika trakti ambazo Wanafunzi wa Biblia waliwatolea watu kwa makumi ya mamilioni kotekote ulimwenguni. Nilikuwa mrefu na mwembamba na nilikuwa nikienda mbio nyumba hadi nyumba nikitoa trakti hizo. Nilifurahia sana kazi hiyo. Lakini ilikuwa vigumu sana kwangu kuzungumza na wengine kuhusu Ufalme wa Mungu kwenye milango.

Nilikuwa mwenye haya sana hivi kwamba hata niliogopa wakati Mama alipokuwa akiwaalika watu wengi wa jamaa kila mwaka. Nilikuwa nikiingia katika chumba changu cha kulala na kukaa humo. Siku moja, Mama alitaka familia nzima ipigwe picha, akaniita. Kwa kuwa sikutaka kujiunga nao, nilipiga kelele kwelikweli alipokuwa akinivuta nitoke chumbani mwangu.

Lakini, siku ikafika ambapo niliazimia kabisa kuhubiri, nikaweka vichapo vya Biblia katika mfuko wangu. Tena na tena nikasema, “siwezi kuhubiri,” lakini tena nikawa nasema “ni lazima nihubiri.” Hatimaye, nikaenda kuhubiri. Baadaye, nilifurahi sana kwamba nilipata ujasiri wa kuhubiri. Nilifurahia sana kutimiza kazi ya kuhubiri, lakini sikufurahia sana kuhubiri kwenyewe. Ni karibu na wakati huo ambapo nilikutana na kasisi aliyetajwa hapo mwanzoni na kuondoka nikibwaga machozi. Muda ulipozidi kupita, kwa msaada wa Yehova niliweza kuzungumza na watu kwenye milango yao, na shangwe yangu ikaongezeka. Kisha mnamo mwaka wa 1925, nikaonyesha wakfu wangu kwa ubatizo wa maji.

Naanza Huduma ya Wakati Wote

Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilinunua gari kwa pesa nilizorithi kutoka kwa shangazi yangu na kuanza upainia, kama ambavyo huduma ya wakati wote inavyoitwa. Miaka miwili baadaye, mwaka wa 1930, mimi na mwenzangu tukakubali mgawo wa kuhubiri eneo fulani. Kufikia wakati huo Clarence pia alikuwa ameanza upainia. Upesi baadaye alikubali mwaliko wa kutumikia kwenye Betheli, makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, Brooklyn, New York.

Karibu na kipindi hicho wazazi wetu walitengana, basi mimi na Mama tukaagiza tujengewe nyumba ya trela na kuanza kufanya upainia pamoja. Wakati huo ndipo Mshuko Mkuu wa Uchumi ulipotokea Marekani. Ilikuwa vigumu kuendelea kufanya upainia, lakini tukaazimia kwamba hatutaacha. Tulitoa vichapo vya Biblia nasi tukapewa kuku, mayai, na mazao ya shambani, na vitu kama betri zilizokuwa zimetumika kwa muda mrefu na mabati yaliyotupwa. Tuliuza betri na mabati ili kununua petroli na kugharimia mambo mengine. Pia nilijifunza kuweka grisi kwenye gari na kubadilisha oili ili kupunguza gharama. Kama ambavyo Yehova ameahidi, tuliona akitufungulia njia nyingi za kutusaidia kushinda magumu.—Mathayo 6:33.

Naenda Kwenye Migawo ya Mishonari

Mwaka wa 1946, nilialikwa kuhudhuria darasa la saba la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, ambayo ilikuwa karibu na South Lansing, New York. Kufikia wakati huo tulikuwa tumefanya upainia na Mama kwa zaidi ya miaka 15, lakini hakutaka nikose fursa ya kupata mazoezi ya kazi ya mishonari. Basi akanitia moyo nikubali pendeleo hilo la kuhudhuria Shule ya Gileadi. Baada ya kuhitimu, mimi na Martha Hess wa Peoria, Illinois, tukaungana ili tuhubiri pamoja. Sisi, pamoja na wengine wawili, tulipewa mgawo wa kwenda Cleveland, Ohio, kwa mwaka mmoja huku tukingoja mgawo wa kwenda nchi za ng’ambo.

Tulipokea mgawo huo mwaka wa 1947. Mimi na Martha tukapewa mgawo wa kwenda Hawaii. Kwa kuwa ilikuwa rahisi kuhamia visiwa hivyo, Mama alikuja na kuishi karibu na sisi katika jiji la Honolulu. Afya yake ilikuwa inadhoofika, kwa hiyo pamoja na kushughulikia utendaji wa mishonari, nilikuwa pia namsaidia Mama. Niliweza kumtunza mpaka akafa huko Hawaii mwaka wa 1956 akiwa na umri wa miaka 77. Tulipofika Hawaii, kulikuwa na Mashahidi wapatao 130, lakini kufikia wakati Mama alipokufa, Mashahidi walikuwa zaidi ya elfu moja, na ikawa kwamba mishonari hawahitajiki tena huko.

Ndipo mimi na Martha tukapokea barua kutoka kwa Watch Tower Society ambayo ilitupa mgawo wa kwenda Japani. Kwanza tulikuwa na wasiwasi kama katika umri wetu tungeweza kujifunza Kijapani. Nilikuwa na umri wa miaka 48 wakati huo, na Martha alikuwa mdogo wangu kwa miaka minne. Lakini tuliacha mambo hayo mikononi mwa Yehova na kukubali mgawo huo.

Punde tu baada ya mkusanyiko wa kimataifa wa 1958 uliofanyiwa Yankee Stadium na Uwanja wa Polo huko New York City, tulifunga safari ya kwenda Tokyo kwa meli. Tulikumbwa na kimbunga tulipokaribia bandari ya Yokohama, ambako tulilakiwa na Don na Mabel Haslett, Lloyd na Melba Barry, na mishonari wengine. Wakati huo, kulikuwa na Mashahidi 1,124 pekee nchini Japani.

Tulianza mara moja kujifunza Kijapani na kushiriki katika huduma ya mlango hadi mlango. Tukitumia alfabeti ya Kiingereza, tuliandika maneno yetu ya kuhubiri kwa Kijapani, ambayo tulikuwa tukisoma. Wenye nyumba walijibu kwa kusema, “Yoroshii desu” au, “Kekko desu,” ambayo tulijifunza kuwa yanamaanisha, “Ni sawa” au, “Ni nzuri.” Lakini nyakati nyingine hatukujua kama mwenye nyumba anapendezwa au hapendezwi, kwa kuwa maneno ayo hayo pia yalikuwa yakitumiwa kukataa jambo. Namna ya sauti au uso wa mwenye nyumba ndio ungeonyesha kama amekubali au amekataa. Ilituchukua muda kutambua jambo wanalomaanisha.

Mambo Yaliyonichangamsha Moyo

Nikiwa ningali nang’ang’ana na lugha, siku moja nilizuru bweni la Kampuni ya Mitsubishi, nikakutana na mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 20. Alifanya maendeleo mazuri ya kuijua Biblia, akabatizwa mwaka wa 1966. Mwaka mmoja baadaye, akaanza kufanya upainia na punde tu baadaye akawekwa rasmi kuwa painia wa pekee. Ametumikia akiwa painia wa pekee tangu wakati huo. Nyakati zote nimetiwa moyo sana kuona jinsi ambavyo ametumia wakati wake na nguvu zake tokea ujanani katika huduma ya wakati wote.

Kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli ya Biblia ni jambo gumu hasa kwa watu wanaoishi katika jumuiya ambayo si ya Kikristo. Lakini, maelfu ya watu wamekabili ugumu huo, kutia ndani watu kadhaa kati ya wale ambao nimejifunza nao Biblia. Wameondoa madhabahu ghali za Kibuddha na Shinto ambazo mara nyingi hupatikana katika nyumba za Wajapani. Kwa kuwa wakati mwingine watu wa ukoo huona matendo hayo kuwa kutoheshimu wafu, inahitaji ujasiri kwa wapya kuondoa madhabahu hizo. Matendo yao yenye ujasiri yatukumbusha matendo ya wale Wakristo wa mapema walioondolea mbali vitu vilivyohusika na ibada isiyo ya kweli.—Matendo 19:18-20.

Namkumbuka mwanafunzi mmoja wa Biblia, mke wa nyumbani, aliyekuwa akipanga kuhama jiji la Tokyo pamoja na familia yake. Alitaka kuhamia nyumba mpya isiyo na vitu vinavyohusika na ibada ya kipagani. Basi akamweleza mume wake vile anavyotaka, naye akakubali. Alinijulisha jambo hilo kwa furaha nyingi lakini ghafula akakumbuka kwamba alibeba chombo kikubwa cha marumaru kilicho ghali sana ambacho alikuwa amenunua kwa sababu ilisemekana chombo hicho huleta furaha nyumbani. Kwa kuwa alikuwa na shaka kama kilihusika na ibada isiyo ya kweli, alikiponda-ponda chombo hicho kwa nyundo na kukitupa.

Kumwona mwanamke huyo na wengine wakitupilia mbali kwa hiari vitu vilivyotumiwa katika ibada isiyo ya kweli na kwa ujasiri kuanza maisha mapya ya utumishi kwa Yehova kumenithawabisha na kuniridhisha sana. Mimi humshukuru Yehova kwa ukawaida kwamba nimeweza kufurahia utumishi wa mishonari kwa zaidi ya miaka 40 nchini Japani.

“Miujiza” ya Wakati Wetu

Ninapoikumbuka miaka zaidi ya 70 ambayo nimetumia katika huduma ya wakati wote, mimi hustaajabia mambo ambayo naona kama ni miujiza ya wakati wetu. Nikiwa msichana mwenye haya sana, sikupata kuwazia kwamba ningeweza kutumia maisha yangu yote nikizungumza na watu kuhusu Ufalme ambao wengi hata hawataki kuusikia. Na si mimi tu ambaye nimeweza kufanya hivyo, lakini nimeona mamia, hata maelfu, ya wengine pia wakifanya hivyo. Na wamefanya hivyo kwa matokeo mazuri sana hivi kwamba wale Mashahidi waliokuwa zaidi tu ya elfu moja nchini Japani nilipofika huko mwaka wa 1958, wamepita 222,000 leo!

Tulipofika na Martha Japani kwa mara ya kwanza, tulipewa mgawo wa kuishi kwenye ofisi ya tawi jijini Tokyo. Mwaka wa 1963, ofisi mpya yenye orofa sita ilijengwa mahali hapo, na tumeishi hapo tangu wakati huo hadi sasa. Mnamo Novemba 1963 tulikuwa miongoni mwa wale 163 waliosikiliza hotuba ya kuweka wakfu iliyotolewa na msimamizi wa tawi, Lloyd Barry. Kufikia wakati huo tulikuwa Mashahidi 3,000 nchini Japani.

Imependeza sana kuona kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme ikikua haraka sana, tukifikia zaidi ya Mashahidi 14,000 mwaka wa 1972 wakati ambapo ofisi mpya ya tawi iliyoongezwa ilimalizika katika jiji la Numazu. Lakini, kufikia mwaka wa 1982 kulikuwa na watangazaji wa Ufalme zaidi ya 68,000 nchini Japani, na ofisi kubwa zaidi ilijengwa katika jiji la Ebina, kilometa 80 hivi kutoka Tokyo.

Wakati uo huo, ofisi ya zamani ya tawi iliyokuwa katikati ya Tokyo ilirekebishwa. Baadaye, ikawa makao ya mishonari kwa zaidi ya mishonari 20 ambao wametumikia nchini Japani kwa miaka 40 au 50 au zaidi, kutia ndani mimi na mwenzangu wa muda mrefu, Martha Hess. Daktari mmoja na mke wake, ambaye ni mwuguzi, pia wanaishi katika makao yetu. Wao hututunza, wakishughulikia kwa upendo mahitaji yetu ya kiafya. Hivi karibuni, mwuguzi mwingine amejiunga nasi na dada Wakristo huja kuwasaidia wauguzi hao wakati wa mchana. Washiriki wawili wa familia ya Betheli ya Ebina huja kwa zamu kututayarishia mlo na kusafisha makao yetu. Kwa kweli Yehova amekuwa mwema kwetu.—Zaburi 34:8, 10.

Jambo kuu katika maisha yangu ya mishonari lilitukia mwezi wa Novemba uliopita, miaka 36 baada ya kuwekwa wakfu kwa jengo ambamo wengi wetu sisi mishonari twaishi sasa. Novemba 13, 1999, nilikuwa miongoni mwa watu 4,486, kutia ndani mamia ya Mashahidi wa zamani kutoka nchi 37, waliohudhuria kuwekwa wakfu kwa majengo yaliyoongezwa ya ofisi ya tawi ya Japani ya Watch Tower Bible and Tract Society katika Ebina. Kwa wakati huu, kuna watu wapatao 650 katika ofisi hiyo ya tawi.

Katika miaka 80 hivi tangu nilipoanza kuhubiri nyumba hadi nyumba na kuwapa watu ujumbe wa Biblia nikiwa mwenye haya, Yehova amekuwa akiniimarisha. Amenisaidia kuacha kuwa mwenye haya. Naamini kabisa kwamba Yehova anaweza kutumia mtu yeyote yule anayemtumaini, hata wale ambao wana haya sana kama mimi. Nimekuwa na maisha yenye uradhi kama nini kuongea na watu nisiowafahamu kuhusu Mungu wetu, Yehova!

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na Mama na Clarence, aliyekuwa ametuzuru kutoka Betheli

[Picha katika ukurasa wa 23]

Washiriki wa darasa letu wakijifunza kwenye uwanja wa Shule ya Gileadi karibu na South Lansing, New York

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kushoto: Mimi, Martha Hess, na mama, tukiwa Hawaii

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kulia: Washiriki wa makao yetu ya mishonari ya Tokyo

[Picha katika ukurasa wa 24]

Chini: Nikiwa na mwenzangu wa muda mrefu, Martha Hess

[Picha katika ukurasa wa 25]

Majengo ya ofisi ya tawi yaliyoongezwa katika Ebina yaliwekwa wakfu mwezi wa Novemba uliopita