Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Waamini Usichoweza Kukiona?

Je, Waamini Usichoweza Kukiona?

Je, Waamini Usichoweza Kukiona?

MTU anaposema, ‘Naamini tu niwezacho kukiona,’ haimaanishi kuwa haamini chochote kile kisichoonekana kwa macho. Kwa kweli, sisi sote twaamini vitu tusivyoweza kuviona kwa macho.

Ulipokuwa shuleni, huenda ikawa ulifanya jaribio la kuthibitisha kuwapo kwa uga-sumaku. Huenda jaribio hilo likafanywa hivi: Nyunyiza vipande vya chuma juu ya karatasi. Kisha weka karatasi juu ya sumaku. Karatasi inapotikiswa, vipande vya chuma hukusanyika karibu na ncha za sumaku, kulingana na jinsi uga-sumaku unavyozivuta. Ikiwa umefanya jaribio hilo, je, uliweza kuuona uga-sumaku kwa macho? La, lakini, ni rahisi kuona athari ya uga-sumaku kwenye vipande vya chuma, ikikutolea uthibitisho wenye kusadikisha kwamba kuna uga-sumaku.

Bila kushuku twakubali vitu vingine tusivyoweza kuviona. Tutazamapo mchoro mzuri na kustaajabia sanaa ya kuchongwa, hatutilii shaka kuwapo kwa mchoraji wala mchongaji. Vilevile, tutazamapo poromoko la maji au machweo, je, hatupaswi kusukumwa kukubali ya kwamba, huenda ikawa vitu hivi vimetengenezwa na Msanii Mkuu?

Kizuiacho Wengine Wasiamini

Baadhi ya watu wameacha kuamini kwamba kuna Mungu kwa sababu ya yale waliyofundishwa kanisani. Mmojawapo wa watu hao ni mwanamume kutoka Norway aliyefundishwa kwamba Mungu anachoma watu katika moto wa mateso. Kwa sababu mwanamume huyo hakuweza kuelewa jinsi Mungu awezavyo kutesa watu kwa njia hiyo, hatimaye akaacha kuamini kwamba kuna Mungu.

Hata hivyo, baadaye, mwanamume huyo alikubali kuchunguza Biblia pamoja na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alishangazwa kujua ya kuwa, kulingana na Biblia, hakuna moto wa mateso wateswapo waovu. Biblia yafananisha kifo na usingizi. Kaburini hatuumii hata kidogo; hatujui neno lo lote. (Mhubiri 9:5, 10) Mwanamume huyo alijifunza pia kwamba kupatana na hukumu ya Mungu, wanadamu waovu wasiorekebishika watabaki kaburini milele. (Mathayo 12:31, 32) Wafu wengine wote watafufuliwa katika wakati uliowekwa na Mungu, wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso. (Yohana 5:28, 29; 17:3) Alikubali ufafanuzi huo. Ulipatana na maelezo ya Biblia kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Mwanamume huyo mwenye moyo mweupe aliendelea kujifunza Neno la Mungu, hatimaye akaja kumpenda Mungu wa Biblia.

Wengine wamepoteza imani katika Muumba mwenye upendo kwa sababu ya taabu na ukosefu wa haki ambazo zimeenea kila mahali. Wanakubaliana na mwanamume mmoja kutoka Sweden aliyeelekeza kidole mbinguni na kuuliza: “Twawezaje kuamini kwamba kuna Mungu mwenye nguvu zote, mkarimu sana kule juu huku tukiwa na uovu na ufisadi mwingi hapa chini?” Kwa kuwa hakuna aliyeweza kujibu swali lake, hata yeye akaja kuacha kuamini kwamba kuna Mungu. Baadaye, akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Akajua kwamba Neno la Mungu hutoa jibu linaloridhisha kwa lile swali ambalo limeulizwa kwa miaka mingi, Kwa nini Mungu ameruhusu uovu uwepo? *

Mwanamume huyo mwenye moyo mweupe alipata kujua kwamba kuwapo kwa uovu hakuthibitishi kwamba hakuna Mungu. Kwa mfano: Mtu aweza kuunda kisu cha kukata nyama. Huenda mteja akanunua kisu hicho na kukitumia, si kukata nyama, lakini kuua mtu. Kutumiwa vibaya kwa kisu hicho hakukanushi kwa vyo vyote kwamba kuna mtu aliyekiunda. Vivyo hivyo, ingawa dunia haijatumiwa kupatana na kusudi la Muumba, jambo hilo halikanushi kwamba kuna Muumba.

Biblia husema kwamba kazi ya Mungu ni kamilifu. Kwake hakuna “uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Mungu huwapa wanadamu zawadi nyingi nzuri, lakini baadhi ya zawadi hizo zimetumiwa vibaya na matokeo yamekuwa kuteseka kwingi. (Yakobo 1:17) Hata hivyo, Mungu atakomesha kuteseka. Hatimaye, “wenye upole watairithi nchi, . . . nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:11, 29.

Yule mwanamume kutoka Sweden aliyetajwa awali alihuzunika alipoona kuteseka kwa wanadamu wenzake. Kwa kweli, hangaiko lake la upendo kwa wengine huthibitisha kwamba kuna Mungu. Jinsi gani?

Watu wengi wasiomwamini Mungu wanaamini nadharia ya mageuzi. Wanaoamini nadharia ya mageuzi wafundisha kwamba ‘viumbe bora ndio wasalimikao’—kwamba wanadamu na wanyama hushindana wenyewe kwa wenyewe na walio bora zaidi tu ndio wasalimikao. Yaani, viumbe bora husalimika; wanyonge hufa. Hiyo ndiyo hali ya kawaida ya mambo, watu hao wasema. Lakini, ikiwa “hali ya kawaida” ni kwamba, wanyonge wafe ili wenye nguvu wasalimike, inakuwaje kwamba baadhi ya wenye nguvu, kama yule mwanamume kutoka Sweden, wahuzunika wanapoona kuteseka kwa wanadamu wenzao?

Kupata Kumjua Mungu

Hatuwezi kumwona Mungu kwa sababu hana umbo la kibinadamu. Hata hivyo, Mungu anataka tumjue. Njia moja ya kumjua Mungu ni kwa kutazama kazi zake za ajabu—“michoro” na “sanaa za kuchongwa” za uumbaji. Katika Waroma 1:20, Biblia husema: ‘Kwa maana sifa za Mungu zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.’ Ndiyo, kutafakari kuhusu kazi za ajabu za Mungu kwaweza kukusaidia kuujua utu wa Mungu kindani zaidi, sawa na vile kutazama mchoro au sanaa ya kuchongwa kuwezavyo kukusaidia kuujua utu wa msanii.

Bila shaka, haiwezekani kujibu maswali yote yenye kusumbua kwa kuangalia tu kazi za uumbaji za Mungu. Lakini kwa kuchunguza Neno la Mungu, Biblia, twaweza kupata majibu ya maswali kama hayo. Wale wanaume wawili waliotajwa mapema walikuja kuamini kuna Mungu anayetujali kupitia kusoma Biblia na kuwa tayari kukubali mawazo mapya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ukitaka kujua zaidi ni kwa nini Mungu ameruhusu uovu uwepo, tafadhali soma kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, sura ya 10, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]

J. Hester and P. Scowen (AZ State Univ.), NASA ▸