Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ushinde Mwelekeo wa Kutarajia Ukamilifu?

Kwa Nini Ushinde Mwelekeo wa Kutarajia Ukamilifu?

Kwa Nini Ushinde Mwelekeo wa Kutarajia Ukamilifu?

Je, wajitahidi sikuzote kufanya mambo kwa kadiri uwezavyo? Ni dhahiri, ukifanya hivyo waweza kujinufaisha mwenyewe na wengine kwa njia nyingi. Kwa upande mwingine, baadhi ya watu wamepita kiasi nao wamekuwa wenye kutarajia ukamilifu. Maana yake ni nini?

MAANA moja ya ‘kutarajia ukamilifu’ ni “mwelekeo wa kuona chochote kile kisicho kikamilifu kuwa hakikubaliki.” Yaelekea unafahamu watu wenye mwelekeo huo. Waweza kuona kwamba matarajio yao ya kupita kiasi yaweza kusababisha matatizo mengi na kuleta hali ya kutoridhika na kuvunjika moyo. Watu wengi wenye usawaziko hutambua kwamba matarajio ya juu na ya kupita kiasi katika mambo yote ya maisha si jambo zuri. Mwelekeo wa aina hiyo wapaswa kushindwa. Hata hivyo, ikiwa sisi wenyewe tuna mwelekeo huo wa kutarajia ukamilifu, si rahisi kuuona, hivyo ni vigumu kuushinda.

Nelson ana madaraka makubwa kazini na matatizo mengi ya kutatua. Kwa kawaida anachanganua takwimu, na matokeo mazuri kazini ndilo jambo kuu kwake. Mwelekeo wa kutarajia ukamilifu mara nyingi huonwa kuwa wa lazima ili kufanikiwa leo. Huenda baadhi ya watu wakathamini ufanisi wa Nelson, lakini mwelekeo wake unamwathiri kimwili, kwa kuwa anapatwa na maumivu ya kichwa na mikazo ya kiakili. Je, mwelekeo wako ni kama wa Nelson?

Vijana pia wanaathiriwa na mwelekeo wa kutarajia ukamilifu. Rita, kutoka Rio de Janeiro, alipokuwa mtoto aliipenda shule sana. Alijaribu sana kutoonekana kuwa mwenye kutarajia makuu, hata hivyo alihuzunika sana ikiwa hakushinda katika mtihani. Rita asema: “Tangu utotoni nimejilinganisha na wengine waliokuwa na wakati mwingi, ilhali nilikuwa mwenye mikazo ya akili na mwenye haraka ya kushughulikia mambo. Sikuwa na wakati wa kupumzika kwa kuwa shughuli zilikuwa nyingi sikuzote.”

Maria alipokuwa msichana mchanga alilia machozi kwa kukatishwa tamaa kwa sababu hakuweza kuchora vizuri kama wengine. Zaidi ya hayo, alipojitahidi kujifunza kucheza muziki na kuimba kwa ukamilifu, mara nyingi alipatwa na mikazo ya akili na wasiwasi badala ya kufurahia kucheza au kuimba. Msichana mwingine kutoka Brazili aitwaye Tânia, aliyejaribu kuwa mwenye busara na kuepuka ushindani, alikiri kwamba bado alijiwekea viwango vilivyokuwa vya juu mno shuleni na nyumbani. Alihisi kwamba ikiwa kazi yake haingekuwa kamilifu watu hawangempenda. Isitoshe, mara kwa mara Tânia alitarajia mengi mno kutoka kwa wengine, naye akakatishwa tamaa na kuvunjika moyo.

Ijapokuwa ustadi, bidii, na kuridhika na lile lililotimizwa ni muhimu, ukijiwekea miradi usiyoweza kufikia huenda ukaathiriwa na hisi zisizofaa kama woga wa kushindwa. Wazazi ama wengine waweza kuweka viwango vya juu sana vya michezo au kazi ya shuleni, vijana wasiweze kuvifikia. Kwa mfano, mama ya Ricardo alikuwa na matarajio ya juu kuhusu mwana wake, alitaka awe daktari, ajue kucheza piano, na ajue lugha kadhaa. Je, waweza kuona kwamba mwelekeo huo ukipita kiasi waweza kuleta matatizo na kuvunja moyo?

Kwa Nini Uepuke Kuwa Mwenye Kutarajia Ukamilifu?

Kazi inayofikia viwango bora kabisa, inatafutwa sana. Kwa hivyo, lazima watu wajitahidi ili kazi yao iwe bora. Sababu nyingine inayofanya wengi wajitahidi zaidi na zaidi ni hofu ya kupoteza riziki. Baadhi ya wafanyakazi wamekuwa kama mwanariadha anayejikaza sana kuvunja rekodi. Kisha, akabilipo mashindano makali huenda akajilazimisha kufanya mazoezi zaidi, labda hata atatumia dawa isiyo halali ili afanye maendeleo zaidi na—aamini—kushinda. Badala ya kumsaidia mtu kufanya maendeleo kwa njia ifaayo, mwelekeo wa kutarajia ukamilifu wafanya watu wasukumwe na “hofu ya kushindwa” au “kutaka kuwa wa kwanza.”—The Feeling Good Handbook.

Hakika, baadhi ya watu waona kwamba matokeo yao ya michezo na sanaa yaweza sikuzote kufanyiwa maendeleo. Hata hivyo, kulingana na Dakt. Robert S. Eliot, “matarajio ya yule aliyetarajia ukamilifu hayatimizwi kamwe.” Akaongeza hivi: “Matarajio hayo hutokana na hisi za hatia, kutaka kujitetea, na kuogopa dhihaka.” Kwa hiyo, maneno ya Mfalme Solomoni mwenye hekima ni ya kweli kabisa: “Tena nikafikiri amali zote, na kila kazi ya ustadi, ya kwamba inatoka katika mtu kupingana na mwenzake. Hayo nayo ni ubatili na kujilisha upepo.”—Mhubiri 4:4.

Unaweza kufanya nini ukiwa na mwelekeo wa kutarajia ukamilifu? Je, unapojitahidi zaidi, ndipo unapokatishwa tamaa hata zaidi? Je, ungependa kuacha kuwa mwenye kutarajia mengi mno na kupumzika zaidi? Ukamilifu una maana gani? Je, unataka sana kufanya mambo kwa kadiri uwezavyo huku ukiepuka mwelekeo wa kutarajia ukamilifu? Ikiwa watu wasiokamilika wanaweza kutumia uwezo waliopewa na Mungu kuvumbua mambo kwa faida ya wengine, wazia kile watakachoweza kutimiza katika hali ya ukamilifu na wakiongozwa na Mungu!

[Picha katika ukurasa wa 4]

Huenda wazazi na wengine wakatarajia ukamilifu, vijana wasiweze kuufikia