Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Makamilifu Si Ndoto Tu!

Maisha Makamilifu Si Ndoto Tu!

Maisha Makamilifu Si Ndoto Tu!

Ulimwengu mkamilifu—wamaanisha nini kwako? Ebu wazia jamii ya wanadamu isiyo na uhalifu, dawa za kulevya, njaa, umaskini, wala ukosefu wa haki. Watu wote ni wazima kihisia-moyo na kimwili. Hakuna huzuni wala kukosa furaha kwa kuwa hata kifo kimeondolewa. Je, ulimwengu kama huo utawezekana?

IJAPOKUWA kuna maendeleo ya sayansi na tekinolojia, walio wengi hawaamini kwamba akili na ujuzi wa wanadamu waweza kutokeza ulimwengu wenye amani na furaha. Kwa upande mwingine, mwelekeo wa wanadamu ni wa kufanya maendeleo na kurekebisha mambo yasiyo makamilifu. Bila shaka, kutamani tu mambo mazuri hakutasaidia wasio na makao na watu maskini, wala kuponya wagonjwa na wasiojiweza watamanio kuondolewa mateso yao. Ulimwengu mkamilifu hautakuja kupitia jitihada za wanadamu. Hata hivyo, ijapokuwa kuna taabu na uonevu leo, kuna sababu nzuri za kuamini kwamba ulimwengu mkamilifu uko karibu.

Ufikiriapo maisha makamilifu, huenda ukakumbuka maisha ya Yesu Kristo. Yesu hakuwa mtu mkamilifu pekee aliyepata kuishi duniani. Adamu na Hawa, walioumbwa kwa mfano wa Mungu walikuwa na maisha makamilifu katika paradiso. Hata hivyo, walipoteza hali hiyo bora kwa kumwasi Baba yao wa mbinguni. (Mwanzo 3:1-6) Muumba aliingiza katika wanadamu tamaa ya kuishi milele. Andiko la Mhubiri 3:11 lathibitisha jambo hilo likisema hivi: “Kila kitu [Mungu] amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.”

Hata ingawa kutokamilika na dhambi zilisababisha maisha ya “ubatili” na “utumwa wa uharibifu,” ona maneno yenye kutia moyo ya mtume Paulo: “Kwa maana taraja lenye hamu la viumbe linangoja kufunuliwa kwa wana wa Mungu. Kwa maana viumbe vilitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yavyo vyenyewe bali kupitia yeye aliyevitiisha hivyo, juu ya msingi wa tumaini kwamba viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:19-21) Biblia inaonyesha waziwazi kwamba maandalizi ya Mungu ya kurudisha maisha makamilifu yanapatikana kupitia Yesu Kristo.—Yohana 3:16; 17:3.

Zaidi ya kuwa na tumaini hilo zuri ajabu la wakati ujao, sisi sote twaweza kudhihirisha maendeleo yetu ya kiroho, huku tukisonga mbele hata sasa.

Jitahidi Kuwa Mwenye Kiasi

Yesu Kristo aliiona habari ya ukamilifu kuwa muhimu hivi kwamba aliwaambia wasikilizaji wengi hivi: “Lazima nyinyi basi mwe wakamilifu, kama Baba yenu wa kimbingu alivyo mkamilifu.” (Mathayo 5:48) Je, Yesu alitaka tusiwe na kasoro katika mfumo huu mwovu wa mambo? La. Twapaswa kujitahidi kusitawisha sifa za ukarimu, fadhili, na upendo kwa wanadamu wenzetu, hata hivyo tunakosea mara nyingi. Mmojawapo wa mitume wa Yesu aliandika hivi: “Ikiwa twaungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu hata kutusamehe dhambi zetu na kutusafisha ukosefu wote wa uadilifu. Ikiwa twatoa taarifa: ‘Sisi hatujafanya dhambi,’ tunamfanya yeye mwongo, na neno lake halimo ndani yetu.”—1 Yohana 1:9, 10.

Hata hivyo, twaweza kufanyia maendeleo jinsi tunavyojiona na jinsi tunavyowatendea wengine huku tukijaribu kuwa wenye kiasi. Unaweza kupata wapi maagizo mazuri zaidi ya kusitawisha utu wenye usawaziko na kiasi kuliko yale yapatikanayo katika Neno la Mungu, Biblia? Kusitawisha sifa kama shangwe na kiasi kutatusaidia kuelewana na wazazi wetu au watoto wetu, watu kazini, na mwenzi wetu wa ndoa. Mtume Paulo aliwasihi Wakristo hivi: “Sikuzote shangilieni katika Bwana. Mara moja tena hakika nitasema, Shangilieni! Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.”—Wafilipi 4:4, 5.

Faida za Kuwa Mwenye Kiasi

Usipotarajia mengi mno na kuepuka mwelekeo wa kutarajia ukamilifu ambao unakudhuru na kukuumiza, wewe mwenyewe na wengine pia mwanufaika. Kujijua vizuri kwatia ndani kuwa mwenye kiasi kuhusu yale unayotaka kufanya na pia kujua uwezayo kutimiza. Kumbuka, Mungu alituumba tuishi duniani na kufurahia kazi ya maana yenye kutunufaisha na kuwanufaisha wengine pia.—Mwanzo 2:7-9.

Ikiwa wewe umekuwa mwenye kutarajia kutimiza mengi mno, kwa nini usimwendee Yehova kwa sala? Kupata pendeleo la Mungu kutakupa kitulizo kikubwa. Yehova anajua maumbile yetu na kutokamilika kwetu, kwa hiyo si vigumu kumpendeza. Mtunga-zaburi atuhakikishia: “Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:13, 14) Twashukuru kama nini kwamba Mungu anatendea wanadamu kwa huruma! Anajua udhaifu wetu, hata hivyo tunaweza kuwa kama watoto wapendwa kwake.

Badala ya kufuatia ukamilifu, ni hekima kama nini kusitawisha utambuzi wa kiroho na mtazamo wenye usawaziko! Isitoshe, twajua kwamba hakuna awezaye kumzuia Yehova asitimize kusudi lake la kuwapa wanadamu hali ya ukamilifu chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Lakini ukamilifu wa wanadamu wamaanisha nini?

Maisha Makamilifu Ni Bora Kuliko Kutarajia Ukamilifu

Ukamilifu si sawa na kuwa na mwelekeo wa kutarajia ukamilifu. Watakaopata pendeleo la kuishi katika Paradiso duniani chini ya Ufalme wa Mungu hakika hawatakuwa watu wenye kutarajia mengi wala wanaojifanya kuwa waadilifu. Takwa moja la kuokoka dhiki kuu ni kuthamini kwa moyo dhabihu ya fidia, kama vile umati mkubwa wa kimataifa ulioelezwa na mtume Yohana ulivyosema: “Sisi tunawiwa wokovu na Mungu wetu, aketiye juu ya hicho kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:9, 10, 14) Wote watakaookoka dhiki kubwa iliyo karibu watashukuru kwamba Kristo alitoa uhai wake kwa hiari kwa ajili yao na kwa wote wanaoonyesha imani katika yeye. Dhabihu aliyotoa kwa upendo ni msingi wa kuondoa kutokamilika na udhaifu wao.—Yohana 3:16; Waroma 8:21, 22.

Maisha makamilifu yatakuwaje? Badala ya mashindano na kujitakia makuu, upendo na fadhili zitafanya maisha yawe yenye kufurahisha, nazo wasiwasi na kutojistahi zitaondolewa kabisa. Hata hivyo, maisha makamilifu hayatakuwa yenye kuchosha. Neno la Mungu halielezi mambo yote juu ya Paradiso lakini linafafanua aina ya maisha tuwezayo kutazamia: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu.”—Isaya 65:21-23.

Badala ya kuwaza kuhusu tafrija, maduka, tekinolojia, au usafiri, mambo ambayo Ufalme utaandaa, wazia jinsi utakavyofurahia kuuona utimizo wa maneno haya: “Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema BWANA.” (Isaya 65:25) Maisha makamilifu yatakuwa tofauti sana na maisha ya leo! Ikiwa utapata kuwa mmojawapo wa wale watakaostahili kuishi wakati huo, utakuwa na sababu ya kuamini kwamba Baba yako wa mbinguni mwenye upendo atapendezwa nawe na familia yako. “Nawe utajifurahisha kwa Bwana, naye atakupa haja za moyo wako.”—Zaburi 37:4.

Maisha makamilifu si ndoto tu. Yehova atatimiza kikamili kusudi lake lenye upendo kwa wanadamu.Wewe na familia yako mwaweza kuwa miongoni mwa wale watakaopata kuwa watu wakamilifu na kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Biblia inatabiri hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Tunaweza kufanyia maendeleo jinsi tunavyojiona na kuona wengine, tukiepuka mwelekeo wa kutarajia ukamilifu au kuhangaikia mno mambo madogo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, unaweza kuwazia ukiwa katika hali ya amani na uadilifu katika Paradiso?