Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nyinyi Nyote Ni Akina Ndugu”

“Nyinyi Nyote Ni Akina Ndugu”

“Nyinyi Nyote Ni Akina Ndugu”

“Lakini nyinyi, msiitwe Rabi, kwa maana mmoja ni mwalimu wenu, lakini nyinyi nyote ni akina ndugu.”—MATHAYO 23:8.

1. Inafaa tuchunguze jambo gani?

“NI NANI anayestahili kuheshimiwa zaidi, mishonari au Mwa-nabetheli?” mwanamke mmoja Mkristo katika nchi ya Mashariki alimwuliza kwa moyo mweupe mishonari mmoja kutoka Australia. Alitaka kujua ni nani anayepaswa kustahiwa zaidi, mishonari wa nchi nyingine au mhudumu mwenyeji anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Watch Tower Society. Swali hilo, lililoulizwa kwa moyo mweupe na ambalo linadhihirisha utamaduni unaozingatia mambo ya kitabaka, lilimshangaza sana mishonari huyo. Hata hivyo, suala la ukubwa hutokana na tamaa ya kutaka kujua kadiri ya mamlaka na uwezo wa mtu.

2. Tuwaoneje waabudu wenzetu?

2 Suala hilo si jipya kamwe. Hata wanafunzi wa Yesu walikuwa na bishano lenye kuendelea juu ya ni nani aliyekuwa mkubwa zaidi. (Mathayo 20:20-24; Marko 9:33-37; Luka 22:24-27) Wao pia walilelewa katika utamaduni wa Dini ya Kiyahudi ya karne ya kwanza, ambao kwa kiasi fulani ulizingatia mambo ya kitabaka. Akifikiria jamii hiyo, Yesu aliwashauri wanafunzi wake hivi: “Lakini nyinyi, msiitwe Rabi, kwa maana mmoja ni mwalimu wenu, lakini nyinyi nyote ni akina ndugu.” (Mathayo 23:8) Jina la cheo cha kidini kama vile “Rabi,” ambalo lamaanisha “Mwalimu,” “laelekea kufanya wale wanaoitwa hivyo wajivune na kuhisi kuwa bora, na wale wasioitwa hivyo waone wivu na kuhisi kuwa duni; na kwa jumla roho hiyo na mwelekeo wake ni kinyume cha ‘usahili wa Kristo,’” akasema Albert Barnes aliye msomi wa Biblia. Kwa kweli, Wakristo huepuka kuwaita waangalizi miongoni mwao “Mzee Fulani,” wakitumia jina “mzee” kama jina la cheo la kurai. (Ayubu 32:21, 22) Kwa upande mwingine, wazee wanaofuata ushauri wa Yesu huwaheshimu washiriki wengine wa kutaniko, kama vile Yehova huwaheshimu waabudu wake waaminifu-washikamanifu na vile Yesu Kristo huwaheshimu wafuasi wake waaminifu-washikamanifu.

Mfano wa Yehova na Yesu

3. Yehova aliwaheshimuje viumbe wake wa kiroho?

3 Ingawa Yehova ndiye “Aliye Juu Zaidi Sana,” aliwaheshimu viumbe wake tangu pale mwanzo kwa kuwashirikisha katika kazi zake. (Zaburi 83:18, NW) Alipomwumba mwanadamu wa kwanza, Yehova alimshirikisha Mwana wake mzaliwa-pekee katika kazi hiyo akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:27-30; Mwanzo 1:26) Yehova hata aliwaalika malaika zake wa mbinguni watoe maoni juu ya jinsi ambavyo Mfalme Ahabu angeharibiwa wakati Alipoamua kumharibu.—1 Wafalme 22:19-23.

4, 5. Yehova huwaheshimuje viumbe wake wa kibinadamu?

4 Yehova hutawala akiwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. (Kumbukumbu la Torati 3:24) Hana haja ya kushauriana na wanadamu. Hata hivyo, yeye hujishusha chini ili kuwatazama. Mtunga-zaburi mmoja aliimba: “Ni nani aliye mfano wa BWANA, Mungu wetu aketiye juu; anyenyekeaye kutazama, mbinguni na duniani? Humwinua mnyonge kutoka mavumbini.”—Zaburi 113:5-8.

5 Kabla ya kuangamiza Sodoma na Gomora, Yehova alisikiliza maswali ya Abrahamu na kutimiza haki kulingana na jinsi Abrahamu alivyoifahamu. (Mwanzo 18:23-33) Ingawa Yehova tayari alijua matokeo ya maombi ya Abrahamu, alimsikiliza Abrahamu kwa subira na kukubali hoja zake.

6. Habakuki alipouliza swali, matokeo yalikuwa nini Yehova alipomwonyesha heshima?

6 Yehova pia alimsikiliza Habakuki, aliyeuliza hivi: “Ee BWANA, nilie hata lini, wewe usitake kusikia?” Je, Yehova aliona kwamba swali hilo lapinga mamlaka yake? La, aliona kwamba Habakuki alikuwa na haki ya kuuliza, kwa hiyo akamfunulia kusudi lake la kuwachochea Wakaldayo watekeleze hukumu. Alimhakikishia nabii huyo kwamba ‘hukumu iliyotabiriwa haikuwa na budi kuja.’ (Habakuki 1:1, 2, 5, 6, 13, 14; 2:2, 3) Yehova alimheshimu Habakuki kwa kuchukua mahangaiko yake kwa uzito na kwa kumjibu. Kwa sababu hiyo, nabii huyo mwenye kuhangaika alichangamka, akawa na shangwe, na kumtumaini kabisa Mungu wa wokovu wake. Jambo hilo limeonyeshwa katika kitabu cha Habakuki kilichopuliziwa ambacho huimarisha tumaini letu katika Yehova leo.—Habakuki 3:18, 19.

7. Kwa nini daraka la Petro katika siku ya Pentekoste 33 W.K. lilikuwa muhimu?

7 Yesu Kristo ni mfano mwingine mzuri wa mtu aliyestahi wengine. Yesu alikuwa amewaambia wanafunzi wake kwamba “yeyote yule anikanaye mimi mbele ya watu, hakika mimi pia nitamkana mbele ya Baba yangu.” (Mathayo 10:32, 33) Hata hivyo, usiku ambao alisalitiwa, wanafunzi wake walimkimbia, na mtume Petro akamkana mara tatu. (Mathayo 26:34, 35, 69-75) Yesu hakutazama sura ya nje tu bali alizingatia hisia za ndani zaidi za Petro, toba yake ya kutoka moyoni. (Luka 22:61, 62) Siku 51 tu baadaye, Kristo alimheshimu mtume huyo mwenye kutubu kwa kumruhusu awakilishe wanafunzi wa Yesu 120 siku ya Pentekoste na kutumia ufunguo wa kwanza kati ya “funguo za ufalme.” (Mathayo 16:19; Matendo 2:14-40) Petro alipewa fursa ya ‘kurudi na kuwatia nguvu ndugu zake.’—Luka 22:31-33.

Kuwaheshimu Washiriki wa Familia

8, 9. Mume anawezaje kumwiga Yehova na Yesu kwa kumheshimu mke wake?

8 Waume na wazazi hufanya vema kumwiga Yehova na Yesu Kristo wanapotumia mamlaka kutoka kwa Mungu. Petro alishauri: ‘Nyinyi waume, endeleeni kukaa pamoja na wake zenu kwa namna kama hiyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, kile cha kike.’ (1 Petro 3:7) Ebu wazia ukitumia chombo cha kauri kinachoweza kuvunjika kwa urahisi zaidi kuliko chombo cha mbao. Je, hungekuwa makini zaidi? Mume anaweza kufanya hivyo kwa kumwiga Yehova, akisikiliza maoni ya mkewe anapoamua mambo ya familia. Kumbuka kwamba Yehova alichukua wakati kusababu na Abrahamu. Kwa kuwa mume si mkamilifu, huenda asielewe mambo yote yanayohusika. Hivyo, halingekuwa jambo la hekima kumheshimu mke wake kwa kufikiria maoni yake kwa moyo mweupe?

9 Katika nchi ambako mamlaka ya wanaume yameimarika sana, yampasa mume akumbuke kwamba huenda ikambidi mke wake kushinda kizuizi kikubwa ili kuweza kueleza hisia zake za ndani zaidi. Iga jinsi ambavyo Yesu Kristo, wakati alipokuwa duniani, alishughulika na wanafunzi wake ambao ni sehemu ya jamii ya bibi arusi wake wa wakati ujao. Aliwapenda sana, akizingatia udhaifu wao wa kimwili na wa kiroho hata kabla hawajaeleza mahitaji yao. (Marko 6:31; Yohana 16:12, 13; Waefeso 5:28-30) Kwa kuongezea, chukua wakati kuchunguza yale ambayo mke wako anafanya kwa ajili yako na familia yenu, na kuonyesha uthamini kwa maneno na matendo. Yehova na Yesu waliwathamini, wakawapongeza, na kuwabariki watu waliostahili. (1 Wafalme 3:10-14; Ayubu 42:12-15; Marko 12:41-44; Yohana 12:3-8) Baada ya mume wake kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mwanamke mmoja Mkristo katika nchi ya Mashariki alisema: “Mume wangu alikuwa akitembea hatua tatu au nne mbele yangu, na kuacha nibebe kila kitu. Sasa yeye hubeba mifuko yote na huonyesha uthamini kwa yale ninayofanya nyumbani!” Neno la uthamini wa moyo mweupe humsaidia sana mke wako ahisi anathaminiwa.—Mithali 31:28.

10, 11. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano mzuri wa Yehova katika kushughulika na taifa la Israeli lenye kuasi?

10 Inawapasa wazazi waige mfano wa Mungu katika kushughulika na watoto wao, hasa karipio linapohitajika. “BWANA aliwashuhudia [“alifuliza kuwaonya,” NW] Israeli, na Yuda,” waache njia zao mbaya, lakini ‘wakafanya shingo zao kuwa ngumu.’ (2 Wafalme 17:13-15) Waisraeli hata “walimdanganya kwa vinywa vyao, wakamwambia uongo kwa ndimi zao.” Huenda wazazi wengi wakahisi kwamba watoto wao hufanya hivyo mara kwa mara. Waisraeli ‘walimjaribu Mungu,’ wakamtia uchungu, wakimfanya aumie. Lakini Yehova “anayo rehema, husamehe uovu wala haangamizi.”—Zaburi 78:36-41.

11 Yehova hata aliwasihi Waisraeli: “Haya, njoni, tusemezane, . . . Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isaya 1:18) Ingawa Yehova hakuwa mwenye makosa, alialika taifa hilo lije wasemezane. Ni mtazamo mzuri kama nini wa kuigwa na wazazi wanaposhughulika na watoto wao! Inapohitajika, waonyesheni heshima kwa kusikiliza wanapotoa maoni yao, na kusababu nao mkiwaonyesha ni kwa nini inawabidi wabadilike.

12. (a) Kwa nini yatupasa kuepuka kuwaheshimu watoto wetu zaidi kuliko Yehova? (b) Ni nini kinachohitajiwa ikiwa tutaheshimu hadhi ya watoto wetu tunapowakaripia?

12 Ni kweli kwamba wakati mwingine watoto wanahitaji kushauriwa kwa uzito. Wazazi hawangetaka kuwa kama Eli ‘aliyewaheshimu wana wake kuliko Yehova.’ (1 Samweli 2:29) Hata hivyo, watoto wanahitaji kujua sababu yenye upendo ya marekebisho. Wanapaswa kufahamu kwamba wazazi wao wanawapenda. Paulo anashauri akina baba hivi: “Msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Ingawa ni kweli baba ana mamlaka, jambo linalozungumziwa hapa ni uhitaji wa baba wa kuheshimu hadhi ya watoto kwa kutowakasirisha kwa sababu ya kuwa mkali mno. Naam, kufikiria hadhi ya watoto huhitaji wakati na jitihada kwa upande wa wazazi, lakini matokeo ya kufanya hivyo yanastahili jitihada zozote zile.

13. Biblia ina maoni gani kuhusu walio wazeewazee katika familia?

13 Kuwaheshimu washiriki wa familia kunatia ndani mengi zaidi ya kumheshimu mke wako na watoto wako. “Unapokuwa mzee, tii watoto wako,” yasema mithali moja ya Kijapani. Maana ya mithali hiyo ni kwamba wazazi walio wazeewazee wanapaswa kutumia mamlaka yao kwa kiasi na wanapaswa kusikiliza yale wasemayo watoto wao, ambao ni watu wazima. Ingawa ni jambo linalopatana na Maandiko kwa wazazi kuwaheshimu watoto wao kwa kuwasikiliza, watoto wanapaswa kuwastahi washiriki wa familia wenye umri mkubwa. “Usimdharau mama yako akiwa mzee,” lasema andiko la Mithali 23:22. Mfalme Solomoni alitimiza mithali hiyo na kumheshimu mama yake alipomwendea kumwomba jambo fulani. Solomoni aliagiza kiti cha enzi kiwekwe upande wa kuume wa kiti chake mwenyewe na kusikiliza kile Bath-sheba, mama yake mzee, alichotaka kumwambia.—1 Wafalme 2:19, 20.

14. Tunaweza kuwaheshimuje washiriki wazeewazee wa kutaniko?

14 Katika familia yetu kubwa ya kiroho, tuna fursa nzuri ya “kuongoza” katika kuwaonyesha heshima washiriki wazeewazee wa kutaniko. (Waroma 12:10) Huenda wasiweze kufanya mengi kama walivyofanya hapo zamani, na huenda jambo hilo likawavunja moyo. (Mhubiri 12:1-7) Shahidi mmoja mtiwa-mafuta aliye mzeemzee, ambaye alikuwa amelazwa katika chumba cha wagonjwa, alisema hivi kwa kuvunjika moyo: “Ninataka sana kufa ili niweze kuendelea na kazi huko mbinguni.” Inaweza kusaidia kuwatambua na kuwaheshimu wazeewazee kama hao. Waisraeli waliamriwa: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee.” (Mambo ya Walawi 19:32) Onyesha ufikirio kwa kuwafanya watu wenye umri mkubwa zaidi wahisi wanahitajika na kuthaminiwa. ‘Kuondokea’ kwaweza kutia ndani kuketi chini na kusikiliza wakisimulia mambo waliyotimiza miaka mingi iliyopita. Kwa kufanya hivyo tutawaheshimu wazeewazee na kuboresha maisha yetu ya kiroho.

‘Katika Kuonyesha Heshima Iweni Wenye Kuongoza’

15. Wazee wanaweza kufanya nini ili kuwaonyesha heshima washiriki wa kutaniko?

15 Washiriki wa kutaniko husitawi wanapowekewa mfano mzuri na wazee. (1 Petro 5:2, 3) Japo wana shughuli nyingi sana, wazee wenye kujali huchukua hatua ya kwanza kuongea na wachanga, vichwa vya familia, mama wasio na wenzi wa ndoa, wake wa nyumbani, na walio wazeewazee, haidhuru watu hao wana matatizo au la. Wazee husikiliza maoni ya washiriki wa kutaniko na kuwapongeza kwa yale wawezayo kufanya. Mzee mwenye uangalifu anayempongeza ndugu au dada kwa yale afanyayo anamwiga Yehova, ambaye huwathamini viumbe wake wa duniani.

16 Kwa nini tuwe na maoni kwamba wazee pamoja na wengineo katika kutaniko wanastahili heshima?

16 Kwa kumwiga Yehova, wazee huweka mfano mzuri katika kutumia shauri la Paulo: “Katika upendo wa kidugu iweni na shauku nyororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wenye kuongoza.” (Waroma 12:10) Huenda jambo hilo likawa gumu kwa wazee katika nchi ambamo ni jambo la kawaida kuzingatia mambo ya kitabaka. Kwa mfano, katika nchi moja ya Mashariki, kuna maneno mawili kwa neno “ndugu,” moja linarejezea mtu mwenye cheo cha juu na lile lingine linarejezea mtu mwenye cheo cha kawaida tu. Hadi hivi karibuni, washiriki wa kutaniko walitumia neno linalorejezea mtu mwenye cheo cha juu kwa wazee na wale wenye umri mkubwa, na kutumia neno linalorejezea mtu mwenye cheo cha kawaida kwa watu wale wengine. Hata hivyo, walitiwa moyo watumie neno linalorejezea mtu mwenye cheo cha kawaida kila wakati kwa sababu, kama Yesu alivyowaambia wafuasi wake, “nyinyi nyote ni akina ndugu.” (Mathayo 23:8) Ingawa huenda tofauti hiyo isiwe wazi katika nchi nyingine, yatupasa sote tujihadhari na mwelekeo wa kibinadamu wa kuwa na ubaguzi wa kitabaka.—Yakobo 2:4.

17. (a) Kwa nini wazee wapaswa kuwa wenye kufikika? (b) Ni katika njia zipi wazee wanaweza kumwiga Yehova katika kushughulika na washiriki wa kutaniko?

17 Ni kweli kwamba Paulo alitutia moyo kuwaona wazee fulani kuwa wanastahili “heshima maradufu,” lakini wao bado ni ndugu tu. (1 Timotheo 5:17) Ikiwa tunaweza ‘kukaribia kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa’ cha Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, je, haitupasi kuwa na uhuru uo huo tunapowakaribia wazee, ambao wanapaswa kumwiga Yehova? (Waebrania 4:16; Waefeso 5:1) Waangalizi wanaweza kukadiria kama wao ni wenye kufikika kwa kuzingatia ni mara nyingi kadiri gani watu huwaendea kuomba msaada au kutoa madokezo. Jifunze somo kutokana na jinsi ambavyo Yehova huhusisha wengine katika miradi yake. Yeye huwaheshimu wengine kwa kuwapa madaraka mbalimbali. Hata ikiwa madokezo fulani yaliyotolewa na Shahidi mwingine huenda yasifae, wazee wanapaswa kuthamini kwamba alijali jambo hilo. Kumbuka jinsi Yehova alivyoshughulikia maswali yenye kupenya ya Abrahamu na kilio cha huzuni cha Habakuki.

18. Wazee wanaweza kumwigaje Yehova katika kuwarekebisha wale wanaohitaji msaada?

18 Baadhi ya Wakristo wenzetu wanahitaji marekebisho. (Wagalatia 6:1) Hata hivyo, wana thamani machoni pa Yehova na wanastahili kutendewa kwa heshima. “Mwenye kutoa ushauri anaponitendea kwa staha, ninamwendea bila woga,” akasema Shahidi mmoja. Watu wengi huitikia ushauri vizuri wakitendewa kwa heshima. Huenda ikachukua muda, lakini kuwasikiliza wale ambao wamekosea hufanya iwe rahisi zaidi kwao kukubali ushauri wowote unaohitajika. Kumbuka jinsi Yehova alivyosababu na Waisraeli tena na tena kwa kuwa aliwahurumia. (2 Mambo ya Nyakati 36:15; Tito 3:2) Ushauri unaotolewa kwa hisia-mwenzi na kwa huruma utawachochea wale wanaohitaji msaada.—Mithali 17:17; Wafilipi 2:2, 3; 1 Petro 3:8.

19. Yatupasa kuwaonaje watu ambao wana imani tofauti na ya Wakristo?

19 Kuwaheshimu wengine hutia ndani pia kuwaheshimu wale ambao huenda wakawa ndugu zetu wa kiroho wakati ujao. Huenda sasa watu hao wasiukubali kwa haraka ujumbe wetu, lakini bado tunahitaji kuwaonyesha subira na kutambua hadhi yao wakiwa wanadamu. Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Je, hatupaswi kuwa na maoni kama ya Yehova? Tukijitahidi sikuzote kuwa majirani wema kwa kufikiria watu wote, huenda tukapata fursa ya kuwatolea ushahidi. Bila shaka, sisi huepuka ushirika ambao waweza kutuhatarisha kiroho. (1 Wakorintho 15:33) Hata hivyo, sisi huonyesha “fadhili ya kibinadamu,” bila kuwadharau watu wenye imani tofauti na yetu.—Matendo 27:3.

20. Mfano wa Yehova na Yesu Kristo wapaswa kutuchochea tufanye nini?

20 Naam, Yehova na Yesu Kristo wanastahi kila mmoja wetu. Na tukumbuke sikuzote jinsi watendavyo na kama wao tuwe wenye kuongoza katika kuonyeshana heshima. Na tukumbuke sikuzote maneno haya ya Bwana wetu Yesu Kristo: “Nyinyi nyote ni akina ndugu.”—Mathayo 23:8.

Ungejibuje?

• Unapaswa kuwaonaje waabudu wenzako?

• Mfano wa Yehova na Yesu hukuchocheaje kuwaheshimu wengine?

• Waume na wazazi wanaweza kuwaheshimuje wengine?

• Kuwaona Wakristo wenzao kama ndugu zao huwachochea wazee kutenda katika njia zipi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mheshimu mke wako kwa maneno ya uthamini

[Picha katika ukurasa wa 18]

Waheshimu watoto wako kwa kuwasikiliza

[Picha katika ukurasa wa 18]

Watendee washiriki wa kutaniko kwa heshima