Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waheshimuni Waliopewa Mamlaka Juu Yenu

Waheshimuni Waliopewa Mamlaka Juu Yenu

Waheshimuni Waliopewa Mamlaka Juu Yenu

“Heshimuni watu wa namna zote, iweni na upendo kwa ushirika mzima wa ndugu, iweni katika kuhofu Mungu, iweni wenye kumheshimu mfalme.”—1 PETRO 2:17.

1, 2. Watu huyaonaje mamlaka leo? Kwa nini?

“WATOTO wanaweza kufanya chochote watakacho. Hawastahi wazazi,” asikitika mama mmoja. “Yapinge Mamlaka” chasema kibandiko kimoja cha gari. Hayo ni mambo mawili yanayoonyesha hali ambayo, kama unavyojua, imeenea sana leo. Kwa ujumla, kutostahi wazazi, walimu, waajiri, na maofisa wa serikali ni mambo ya kawaida ulimwenguni pote.

2 Kwa kutojali huenda wengine wakasema hivi, ‘Sistahi watu wenye mamlaka.’ Mara kwa mara, huenda ukakubaliana na maneno hayo. Tunapata habari nyingi sana juu ya maofisa wa serikali walio wafisadi, waajiri wenye pupa, walimu wasiotekeleza kazi yao ifaavyo, na wazazi wanaowadhulumu watoto wao. Inafurahisha kwamba ni Wakristo wachache tu ambao hawastahi wale wenye mamlaka katika kutaniko.—Mathayo 24:45-47.

3, 4. Kwa nini Wakristo wapaswa kuwastahi watu wenye mamlaka?

3 Tukiwa Wakristo, tuna “sababu yenye kushurutisha” ya kuwastahi wale wenye mamlaka katika ulimwengu. Mtume Paulo aliwashauri Wakristo “[wajitiishe] kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka ila kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.” (Waroma 13:1, 2, 5; 1 Petro 2:13-15) Paulo pia alionyesha sababu ya kuridhisha ya kuwatii wenye mamlaka katika familia: “Nyinyi wake, iweni katika ujitiisho kwa waume zenu, kama inavyofaa katika Bwana. Nyinyi watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo ni lenye kupendeza vema katika Bwana.” (Wakolosai 3:18, 20) Wazee wa kutaniko wanastahili heshima yetu kwa sababu ‘roho takatifu imewaweka rasmi kuwa waangalizi, kulichunga kutaniko la Mungu.’ (Matendo 20:28) Sisi huheshimu mamlaka za kibinadamu kwa sababu tunamstahi Yehova. Bila shaka, kuheshimu mamlaka ya Yehova ndilo jambo muhimu zaidi maishani mwetu.—Matendo 5:29.

4 Tukizingatia mamlaka ya Yehova yaliyo makuu kuliko yote, ebu tuchunguze watu kadhaa ambao hawakuwastahi wenye mamlaka na wengine ambao walifanya hivyo.

Kukosa Staha Hufanya Tukataliwe

5. Ni mtazamo gani usio na staha ambao Mikali alimwonyesha Daudi, na jambo hilo lilisababisha nini?

5 Kutokana na historia ya Mfalme Daudi, tunaweza kuelewa jinsi Yehova awaonavyo wale wanaodharau mamlaka kutoka kwa Mungu. Wakati Daudi alipoagiza sanduku la agano liletwe Yerusalemu, mke wake Mikali ‘alimwona Mfalme Daudi akiruka-ruka na kucheza mbele za BWANA; akamdharau moyoni mwake.’ Mikali alipaswa kumtambua Daudi kuwa kichwa cha familia na pia mfalme wa nchi. Hata hivyo, alitumia kejeli kueleza hisia zake: “Mfalme wa Israeli alikuwa mtukufu leo namna gani, akijifunua mwili wake mbele ya vijakazi vya watumishi wake, mfano wa watu baradhuli mmojawapo, ajifunuavyo mwili mbele ya watu, asipokuwa na haya!” Kwa sababu hiyo Mikali hakuzaa watoto.—2 Samweli 6:14-23.

6. Yehova aliuonaje ukosefu wa staha wa Kora kwa wachaguliwa Wake?

6 Kora ni mtu mmoja mbaya sana ambaye hakuheshimu uongozi wa kitheokrasi uliowekwa rasmi na Mungu. Akiwa Mkohathi, alikuwa na pendeleo lililoje la kumtumikia Yehova kwenye tabenakulo! Hata hivyo, alimkosoa Musa na Aroni, viongozi wa Israeli waliochaguliwa na Mungu. Kora alishirikiana na wakuu wengine wa Israeli na kwa ushupavu akamwambia Musa na Aroni hivi: “Mkutano wote ni mtakatifu, kila mmoja miongoni mwao, BWANA naye yu kati yao; n’nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa BWANA?” Yehova aliuonaje mtazamo wa Kora na waliomwunga mkono? Yehova alikiona kitendo chao kuwa cha kutomheshimu yeye binafsi. Baada ya kuwaona wote waliowaunga mkono wakimezwa na ardhi, Kora na wakuu 250 waliteketezwa kwa moto kutoka kwa Yehova.—Hesabu 16:1-3, 28-35.

7. Je, “mitume walio bora sana” walikuwa na sababu yoyote ya kuyachambua mamlaka ya Paulo?

7 Katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, kulikuwa na watu waliodharau mamlaka ya kitheokrasi. ‘Mitume walio bora sana’ katika kutaniko la Korintho hawakumstahi Paulo. Waliuchambua uwezo wake wa kutoa hotuba, wakisema: “Kuwapo kwake mwenyewe binafsi ni dhaifu na usemi wake wa kudharaulika.” (2 Wakorintho 10:10; 11:5) Iwe Paulo alikuwa msemaji mwenye kutokeza au la, alistahili kupewa staha akiwa mtume. Lakini ni kweli kwamba usemi wa Paulo ulikuwa wenye kudharaulika? Hotuba zake za hadharani ambazo zimeandikwa katika Biblia zathibitisha kwamba alikuwa msemaji mwenye kusadikisha. Kwani, kutokana na mazungumzo mafupi pamoja na Herode Agripa wa Pili, aliyekuwa “mtaalamu katika . . . mabishano miongoni mwa Wayahudi,” Paulo alimfanya mfalme huyo aseme: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo”! (Matendo 13:15-43; 17:22-34; 26:1-28) Hata hivyo, mitume walio bora sana wa Korintho walimshutumu kuwa msemaji mwenye kudharaulika! Yehova aliuonaje mtazamo wao? Katika ujumbe aliowapa waangalizi wa kutaniko la Efeso, Yesu Kristo aliwapongeza wale waliokataa kuvutwa na watu ‘waliosema ni mitume, lakini wao sio.’—Ufunuo 2:2.

Staha Japo Kutokamilika

8. Daudi alionyeshaje kwamba aliheshimu mamlaka ambayo Yehova alikuwa amempa Sauli?

8 Biblia inataja watu wengi waliowaheshimu watu wenye mamlaka, hata walipotumia mamlaka yao vibaya. Daudi alikuwa mmoja wao. Mfalme Sauli, ambaye Daudi alitumikia chini yake, aliyaonea wivu mafanikio ya Daudi, akajaribu kumwua. (1 Samweli 18:8-12; 19:9-11; 23:26) Hata hivyo, ingawa Daudi alipata fursa za kumwua Sauli, yeye alisema: “Hasha! nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi wa BWANA.” (1 Samweli 24:3-6; 26:7-13) Daudi alijua kwamba Sauli alikuwa na makosa, lakini akaacha Yehova amhukumu. (1 Samweli 24:12, 15; 26:22-24) Hakusema kwa maneno yenye kuudhi dhidi ya Sauli.

9. (a) Daudi alihisije alipodhulumiwa na Sauli? (b) Tunajuaje kwamba Daudi alimstahi Sauli kwa kweli?

9 Je, Daudi alihuzunika alipodhulumiwa? “Watu watishao wananitafuta nafsi yangu,” Daudi akamlilia Yehova. (Zaburi 54:3) Alimweleza Yehova hisia zake: “Ee Mungu wangu, uniponye na adui zangu . . . Wenye nguvu wamenikusanyikia; Ee BWANA, si kwa kosa langu, wala si kwa hatia yangu. Bila kosa langu huenda mbio, hujiweka tayari; uamke uonane nami, na kutazama.” (Zaburi 59:1-4) Je, umewahi kuhisi hivyo—kwamba japo hujamkosea mtu fulani mwenye mamlaka, bado anaendelea kukutatiza? Daudi hakukosa kumstahi Sauli. Sauli alipokufa, Daudi hakushangilia bali alitunga wimbo huu wa maombolezo: “Sauli na Yonathani walipendwa na kupendeza maishani . . . Walikuwa wepesi kuliko tai, walikuwa hodari kuliko simba. Enyi binti za Israeli, mlilieni huyo Sauli.” (2 Samweli 1:23, 24) Ni mfano bora kama nini wa staha ya kweli kwa mtiwa-mafuta wa Yehova, hata ingawa Sauli alikuwa amemkosea Daudi!

10. Paulo aliweka mfano gani bora katika kuheshimu mamlaka ya baraza linaloongoza yaliyotoka kwa Mungu, na jambo hilo lilisababisha nini?

10 Katika enzi ya Ukristo pia tunapata watu walioheshimu sana mamlaka kutoka kwa Mungu. Kwa mfano, mfikirie Paulo. Alistahi maamuzi ya baraza linaloongoza la karne ya kwanza la kutaniko la Kikristo. Alipotembelea Yerusalemu kwa mara ya mwisho, ndugu wa baraza linaloongoza walimshauri Paulo ajisafishe kisherehe ili adhihirishe kwa wengine kwamba hakuichukia Sheria ya Kimusa. Paulo angaliweza kusababu hivi: ‘Hapo awali ndugu hao waliniagiza niondoke Yerusalemu maisha yangu yalipokuwa hatarini. Sasa wanataka nidhihirishe hadharani kwamba ninastahi Sheria ya Kimusa. Tayari nimewaandikia Wagalatia barua nikiwashauri wajiepushe na kushika Sheria. Nikienda hekaluni, huenda wengine wasielewe ni kwa nini nimefanya hivyo na kufikiri kwamba ninakubaliana na waliotahiriwa.’ Hata hivyo, kwa wazi Paulo hakusababu hivyo. Kwa kuwa hakuna kuridhiana kwokwote kwa kanuni za Kikristo kulikohusika, yeye alistahi na kukubaliana na ushauri wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza. Matokeo yalikuwa kwamba ilibidi Paulo aokolewe kutoka kwa Wayahudi wenye ghasia, na baadaye akafungwa gerezani kwa miaka miwili. Hatimaye, mapenzi ya Mungu yakafanyika. Paulo alitoa ushahidi mbele ya maofisa huko Kaisaria, kisha serikali ikagharimia safari yake ya kwenda Roma kutoa ushahidi mbele ya Kaisari mwenyewe.—Matendo 9:26-30; 21:20-26; 23:11; 24:27; Wagalatia 2:12; 4:9, 10.

Je, Wewe Huonyesha Staha?

11. Tunaweza kuonyeshaje staha kwa mamlaka za ulimwengu?

11 Je, wewe huwastahi ipasavyo wale wenye mamlaka? Wakristo wanaamuriwa ‘wawalipe wote haki zao, . . . kwa yeye atakaye heshima, heshima hiyo.’ Kwa kweli, ujitiisho wetu kwa “mamlaka zilizo kubwa” hutia ndani kulipa kodi na pia kuwaheshimu wenye mamlaka kwa mwenendo na usemi. (Waroma 13:1-7) Tutendeje tukikutana na maofisa wa serikali ambao huenda wakawa wakali? Katika Jimbo la Chiapas, Mexico, wenye mamlaka katika jumuiya moja walinyakua mashamba ya familia 57 za Mashahidi wa Yehova kwa sababu Wakristo hao hawakuwa wakishiriki katika sherehe fulani za kidini. Kwenye mikutano iliyofanywa ili kusuluhisha jambo hilo, sikuzote Mashahidi, wakiwa safi na wamevalia kinadhifu, walizungumza kwa heshima na staha. Zaidi ya mwaka mmoja baadaye, iliamuliwa kwamba warudishiwe mashamba yao. Mtazamo wao ulifanya baadhi ya watazamaji wawastahi kiasi kwamba wao pia walitaka kuwa Mashahidi wa Yehova!

12. Kwa nini ni muhimu kumwonyesha mume wako asiyeamini “staha yenye kina kirefu”?

12 Unawezaje kustahi mamlaka ya familia yanayotoka kwa Mungu? Baada ya kuzungumzia mfano wa Yesu katika kuvumilia uovu, mtume Petro alisema: “Kwa namna kama hiyo, nyinyi wake, iweni katika ujitiisho kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa neno, wapate kuvutwa bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kuwa mashahidi wa kujionea mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:1, 2; Waefeso 5:22-24) Petro alikazia umuhimu wa mke kuwa mwenye kujitiisha kwa mume wake kwa “staha yenye kina kirefu,” ingawa huenda waume wengine wasifanye lolote kustahili staha hiyo. Huenda mtazamo wenye staha wa mke ukamvutia mume asiyeamini.

13. Wake wanaweza kuwaheshimuje waume zao?

13 Katika muktadha wa maandiko haya, Petro ataka tuzingatie mfano wa Sara, ambaye mume wake Abrahamu, alikuwa mfano wenye kutokeza wa imani. (Waroma 4:16, 17; Wagalatia 3:6-9; 1 Petro 3:6) Je, wake wa waume waamini wawastahi kidogo kuliko wake wa waume wasioamini wafanyavyo? Namna gani ikiwa hukubaliani na mume wako juu ya jambo fulani? Yesu alitoa ushauri fulani ambao unaweza kutumiwa katika hali hiyo: “Ikiwa mtu fulani aliye chini ya mamlaka akushurutisha ufanye utumishi kwa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Je, unamstahi mume wako kwa kukubaliana na mapendezi yake? Ikiwa waona jambo hilo kuwa ngumu, zungumza naye kulihusu. Usidhani kwamba anajua jinsi unavyohisi. Lakini unapomjulisha mapendezi yako, fanya hivyo kwa staha. Biblia yatushauri hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.”—Wakolosai 4:6.

14. Kuwaheshimu wazazi kwatia ndani nini?

14 Namna gani watoto wako? Neno la Mungu laamuru: “Watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hili ni lenye uadilifu: ‘Heshimu baba yako na mama yako’; ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi.” (Waefeso 6:1-3) Ona kwamba kuwatii wazazi wako huonwa kuwa na maana moja na ‘kumheshimu baba yako na mama yako.’ Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “heshima” lamaanisha “kukadiria thamani” au “kutathmini.” Hivyo, kutii kwahitaji mengi zaidi ya kufuata sheria za wazazi shingo upande, sheria ambazo huenda ukaona hazifai. Mungu anataka uwaheshimu sana wazazi wako na kuthamini mwongozo wao.—Mithali 15:5.

15. Watoto wanaweza kudumishaje staha hata ikiwa wanaona kwamba wazazi wao walikosea?

15 Wazazi wako wakifanya jambo linaloelekea kupunguza staha yako kwao, utafanya nini? Jaribu kuwa na maoni kama yao. Je, si wao ‘waliokuzaa’ na kukuandalia mahitaji yako? (Mithali 23:22) Je, hawachochewi na upendo walio nao kwako? (Waebrania 12:7-11) Zungumza na wazazi wako kwa staha na kuwaeleza kwa upole jinsi unavyohisi. Hata ikiwa wanajibu kwa njia isiyokupendeza, usizungumze nao kwa kukosa staha. (Mithali 24:29) Kumbuka jinsi Daudi alivyodumisha staha yake kwa Sauli hata wakati mfalme alipoacha kufuata ushauri wa Mungu. Mwombe Yehova akusaidie kukabiliana na hisia zako. “Ifunueni mioyo yenu mbele zake,” Daudi akasema. “Mungu ndiye kimbilio letu.”—Zaburi 62:8; Maombolezo 3:25-27.

Waheshimu Wale Wanaoongoza

16. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya walimu wasio wa kweli na malaika?

16 Wazee wa kutaniko huwekwa rasmi na roho takatifu, hata hivyo bado hawajakamilika, nao hukosea. (Zaburi 130:3; Mhubiri 7:20; Matendo 20:28; Yakobo 3:2) Kwa sababu hiyo, huenda wengine katika kutaniko wasifurahishwe na wazee. Tutendeje tukihisi kwamba jambo fulani kutanikoni halishughulikiwi ifaavyo, au ikiwa angalau inaonekana hivyo? Ona tofauti kati ya walimu wa uwongo wa karne ya kwanza na malaika: “Wenye kuthubutu, washupavu, hawatetemekei watukufu bali husema kwa maneno yenye kuudhi, lakini malaika, ijapokuwa wao ni wakubwa zaidi kwa nguvu na uwezo, hawaleti dhidi yao shtaka katika maneno yenye kuudhi, wakiwa hawafanyi hivyo kwa sababu ya kumstahi Yehova.” (2 Petro 2:10-13) Ingawa walimu wasio wa kweli walisema kwa maneno yenye kuudhi dhidi ya “watukufu”—wazee waliopewa mamlaka katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza—malaika hawakusema kwa maneno yenye kuudhi dhidi ya walimu hao wasio wa kweli ambao walileta mgawanyiko kati ya akina ndugu. Malaika walijua yaliyokuwa yakiendelea katika makutaniko kwa kuwa wana cheo kikubwa zaidi na wanaifahamu haki vema kuliko wanadamu. Hata hivyo, “kwa sababu ya kumstahi Yehova,” waliacha yeye awahukumu walimu hao.—Waebrania 2:6, 7; Yuda 9.

17. Imani yako inahusikaje unapokabiliana na matatizo ambayo wewe wahisi kwamba wazee ndio wamekosea?

17 Hata ikiwa jambo halishughulikiwi ipasavyo, je, haitupasi kuwa na imani katika Yesu Kristo akiwa Kichwa anayeishi wa kutaniko la Kikristo? Je, hajui kinachotendeka katika kutaniko lake mwenyewe la ulimwenguni pote? Je, haitupasi kustahi jinsi anavyoshughulika na hali hiyo na kutambua uwezo wake wa kuongoza mambo? Kwa kweli, ‘sisi ni nani tuwe tukihukumu jirani yetu?’ (Yakobo 4:12; 1 Wakorintho 11:3; Wakolosai 1:18) Kwa nini usimweleze Yehova mahangaiko yako katika sala zako?

18, 19. Unaweza kufanya nini ukihisi kwamba mzee fulani amekosea?

18 Kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, matatizo yanaweza kutokea. Mara kwa mara hata mzee anaweza kukosea, jambo hilo likivuruga wengine. Kuchukua hatua ya harakaharaka katika hali kama hiyo hakutaibadili. Huenda kufanya hivyo kukafanya tatizo hilo liwe baya hata zaidi. Wale wenye ufahamu wa kiroho watamngojea Yehova ili arekebishe mambo na kutoa, kwa wakati wake na kwa njia yake, nidhamu yoyote ile ambayo huenda ikahitajiwa.—2 Timotheo 3:16; Waebrania 12:7-11.

19 Namna gani ikiwa jambo fulani linakutia wasiwasi? Badala ya kuzungumza na wengine katika kutaniko, kwa nini usiwaendee wazee kwa staha ili kupata msaada? Bila kuchambua, eleza jinsi ambavyo jambo hilo limekuathiri. Waonyeshe “hisia-mwenzi” sikuzote, na kudumisha staha unapowaeleza jambo hilo. (1 Petro 3:8) Usitumie kejeli, lakini tumaini ukomavu wao wa Kikristo. Thamini kitia-moyo chochote cha Kimaandiko ambacho huenda wakatoa kwa fadhili. Na ikionekana kwamba hatua nyingine za marekebisho zinahitajiwa, uwe na hakika kwamba Yehova atawaongoza wazee wafanye yaliyo sawa na yafaayo.—Wagalatia 6:10; 2 Wathesalonike 3:13.

20. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Hata hivyo, kuna habari nyingine ya kuchunguza kuhusiana na kuwaheshimu na kuwastahi wale wenye mamlaka. Je, haiwapasi watu waliopewa mamlaka kuwastahi watu walio chini ya usimamizi wao? Ebu tuchunguze jambo hilo katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Tuna sababu gani nzuri ya kuwaheshimu wale wenye mamlaka?

• Yehova na Yesu huwaonaje wale wasiostahi mamlaka kutoka kwa Mungu?

• Tuna mifano gani mizuri ya watu ambao waliwaheshimu wale waliopewa mamlaka?

• Tunaweza kufanya nini ikiwa yaonekana kwamba mtu aliye na mamlaka juu yetu amekosea?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Sara alistahi sana mamlaka ya Abrahamu na alikuwa mwenye furaha

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mikali alikosa kustahi mamlaka ya Daudi akiwa kichwa cha familia na mfalme

[Picha katika ukurasa wa 15]

“Hasha! nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi wa BWANA”

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kwa nini usimweleze Yehova mahangaiko yako katika sala zako?