Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tangaza Habari Njema kwa Hamu

Tangaza Habari Njema kwa Hamu

Tangaza Habari Njema kwa Hamu

“Iweni wenye kuwaka roho. Tumikieni Yehova kama watumwa.”—WAROMA 12:11.

1, 2. Wakristo hujitahidi kudumisha mtazamo gani wakiwa wahubiri wa habari njema?

MWANAMUME kijana amesisimuka kuhusu kazi mpya. Siku yake ya kwanza kazini, asubiri kwa hamu nyingi maagizo ya mwajiri wake. Atazamia mgawo wake wa kwanza naye autekeleza kwa makini. Ana hamu ya kuufanya vizuri kadiri awezavyo.

2 Hali kadhalika, sisi Wakristo ni kama wafanyakazi wapya. Kwa kuwa twatumaini kuishi milele, ni kana kwamba ndio tu tumeanza kumfanyia Yehova kazi. Kwa hakika Muumba wetu ametuwekea kazi nyingi tutakazozifanya milele. Lakini utume wa kwanza kabisa tuliopokea ni ule wa kutangaza habari njema ya Ufalme wake. (1 Wathesalonike 2:4) Sisi huuonaje mgawo huo kutoka kwa Mungu? Kama vile yule mwanamume kijana, twapaswa kuutekeleza vizuri tuwezavyo, kwa bidii, kwa shangwe—naam, kwa hamu!

3. Ni nini kinachohitajika ili mtu apate kufanikiwa akiwa mhudumu wa habari njema?

3 Si rahisi kudumisha mtazamo huo mzuri. Mbali na huduma yetu, tuna wajibu mwingine mwingi, na baadhi yake waweza kutuchosha kimwili na kihisia-moyo. Kwa jumla, sisi hufaulu kushughulikia mambo hayo huku tukiipa huduma uangalifu wa kutosha. Hata hivyo, laweza kuwa pambano lisilokoma. (Marko 8:34) Yesu alikazia kwamba mafanikio yetu sisi Wakristo yangehitaji jitihada kabambe.—Luka 13:24.

4. Mahangaiko ya kila siku yaweza kuathirije mtazamo wetu wa kiroho?

4 Kwa kuwa tuna mengi ya kufanya, ni rahisi kuhisi tumelemewa au kuchoka nyakati nyingine. “Mahangaiko ya maisha” yaweza kudhoofisha bidii na kuthamini kwetu utendaji wa kitheokrasi. (Luka 21:34, 35; Marko 4:18, 19) Kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, huenda tukaacha ‘upendo tuliokuwa nao hapo kwanza.’ (Ufunuo 2:1-4) Huenda tukafanya mambo fulani ya utumishi wetu kwa Yehova kuwa desturi tu. Biblia huandaaje kitia-moyo kinachohitajika ili tudumishe bidii yetu katika huduma?

Kama “Moto Uwakao” Mioyoni Mwetu

5, 6. Mtume Paulo alilionaje pendeleo lake la kuhubiri?

5 Huduma ambayo Yehova ametukabidhi ni yenye thamani sana kiasi kwamba haipasi kuwa kitu cha kawaida tu. Mtume Paulo aliona kuhubiri habari njema kuwa pendeleo kubwa sana, naye akaona hastahili kukabidhiwa huduma hiyo. Alisema: “Mimi, niliye mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi sana kati ya watakatifu wote, nilipewa fadhili hii isiyostahiliwa, ili niwatangazie mataifa habari njema juu ya kina kisichofikilika cha utajiri wa Kristo na kufanya watu waone jinsi siri takatifu inavyosimamiwa ambayo tangu wakati uliopita usio dhahiri imefichwa katika Mungu, aliyeviumba vitu vyote.”—Waefeso 3:8, 9.

6 Mtazamo mzuri wa Paulo kuelekea huduma yake ni mfano bora kwetu. Katika barua yake kwa Waroma, alisema hivi: “Kuna hamu upande wangu kuitangaza habari njema.” Hakuaibikia habari njema. (Waroma 1:15, 16) Alikuwa na mtazamo unaofaa naye alikuwa na hamu ya kutekeleza huduma yake.

7. Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alionya dhidi ya nini?

7 Mtume Paulo alitambua uhitaji wa kudumisha mtazamo wa bidii, basi akawahimiza Wakristo huko Roma hivi: “Msicheze-cheze katika shughuli yenu. Iweni wenye kuwaka roho. Tumikieni Yehova kama watumwa.” (Waroma 12:11) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘cheza-cheza’ lamaanisha kuwa “goigoi, mvivu.” Ingawa labda hatuchezi-chezi kihalisi katika huduma yetu, sote twahitaji kuwa macho ili kutambua dalili zozote za ugoigoi wa kiroho zianzapo na tufanye marekebisho yafaayo katika mtazamo wetu tunapotambua tuna dalili hizo.—Mithali 22:3.

8. (a) Ni nini kilichokuwa kama “moto uwakao” moyoni mwa Yeremia, na kwa nini? (b) Twaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyompata Yeremia?

8 Roho ya Mungu yaweza pia kutusaidia tunapovunjika moyo. Kwa mfano, wakati mmoja nabii Yeremia alivunjika moyo, naye akafikiria kuacha kazi yake ya unabii. Hata alisema hivi kumhusu Yehova: “Sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake.” Je, huo ulikuwa uthibitisho kwamba Yeremia alikuwa na udhaifu mkubwa wa kiroho? La. Kwa hakika, hali ya kiroho yenye nguvu ya Yeremia, upendo wake kwa Yehova, na bidii yake kwa ile kweli zilimpa nguvu ya kuendelea kutoa unabii. Aeleza hivi: “Moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.” (Yeremia 20:9) Ni kawaida kwa watumishi wa Mungu kuvunjika moyo mara kwa mara. Lakini wanaposali Yehova awasaidie, atasoma mioyo yao na kuwapa kwa hiari roho yake takatifu ikiwa, kama Yeremia, wana neno lake mioyoni mwao.—Luka 11:9-13; Matendo 15:8.

“Msiuzime Moto wa Ile Roho”

9. Ni nini kinachoweza kuizuia roho takatifu isitende kwa niaba yetu?

9 Mtume Paulo aliwashauri Wathesalonike hivi: “Msiuzime moto wa ile roho.” (1 Wathesalonike 5:19) Naam, matendo na mitazamo ambayo ni kinyume cha kanuni za Mungu yaweza kuzuia roho takatifu isitende kazi kwa niaba yetu. (Waefeso 4:30) Wakristo leo wana mgawo wa kuhubiri habari njema. Twaliheshimu sana pendeleo hilo. Si ajabu kwamba wale wasiomjua Mungu huidharau kazi yetu. Lakini Mkristo akipuuza huduma yake kwa makusudi, huenda akazima moto wa roho ya Mungu inayochochea.

10. (a) Maoni ya wanadamu wenzetu yaweza kutuathirije? (b) Andiko la 2 Wakorintho 2:17 latoa maoni gani bora kuhusu huduma yetu?

10 Huenda wengine nje ya kutaniko la Kikristo wakaiona huduma yetu kuwa ugawaji tu wa vichapo. Huenda wengine wakawa na maoni yenye makosa kwamba tunaenda nyumba hadi nyumba ili kupokea tu michango. Tukiruhusu maoni hayo yasiyofaa yaathiri mtazamo wetu, huenda yakapunguza mafanikio yetu katika huduma. Badala ya kuruhusu fikira za aina hiyo zituathiri, acheni tudumishe maoni ya Yehova na Yesu kuhusu huduma yetu. Mtume Paulo alitaja maoni hayo bora alipotangaza hivi: “Sisi si wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa weupe wa moyo, ndiyo, tukiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu, mbele ya Mungu, kwa ushirika na Kristo.”—2 Wakorintho 2:17.

11. Ni nini kilichowawezesha Wakristo wa kwanza kudumisha bidii licha ya mnyanyaso, na mfano wao utuathirije?

11 Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu, wanafunzi wake huko Yerusalemu walikabili kipindi cha mnyanyaso. Walitishwa na kuamuriwa waache kuhubiri. Ingawa hivyo, Biblia yasema kuwa ‘walijazwa roho takatifu, wakasema neno la Mungu kwa ujasiri.’ (Matendo 4:17, 21, 31) Maneno ya Paulo kwa Timotheo miaka kadhaa baadaye yaonyesha mtazamo mzuri ambao Wakristo wapaswa kudumisha. Paulo alisema hivi: “Mungu alitupa sisi si roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili. Kwa hiyo usiwe mwenye kuaibikia ushahidi juu ya Bwana wetu, wala juu yangu mimi mfungwa kwa ajili yake, bali chukua sehemu yako katika kupatwa na uovu kwa ajili ya habari njema kulingana na nguvu ya Mungu.”—2 Timotheo 1:7, 8.

Tuna Wajibu Gani kwa Jirani Yetu?

12. Sababu kuu inayofanya tuhubiri habari njema ni gani?

12 Ili tuwe na mtazamo unaofaa kwa huduma yetu, lazima tuwe na nia inayofaa. Kwa nini sisi huhubiri? Sababu kuu ipo kwenye maneno ya mtunga-zaburi: “Wacha Mungu wako watakuhimidi [Yehova]. Wataunena utukufu wa ufalme wako, na kuuhadithia uweza wako. Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu, na utukufu wa fahari ya ufalme wake.” (Zaburi 145:10-12) Naam, sisi huhubiri ili kumsifu Yehova hadharani na kulitakasa jina lake mbele ya wanadamu wote. Hata ikiwa wachache watusikiliza, sisi humletea Yehova sifa tunapotangaza kwa uaminifu ujumbe wa wokovu.

13. Ni nini hutuchochea kuwatangazia wengine tumaini la wokovu?

13 Pia, sisi huhubiri kwa sababu twawapenda watu na tunataka kuepuka hatia ya damu. (Ezekieli 33:8; Marko 6:34) Maneno ya Paulo kuelekea wale walio nje ya kutaniko la Kikristo yanahusu jambo hilo: “Kwa Wagiriki na kwa Wabaribari pia, kwa wenye hekima na kwa wasio na akili pia mimi ni mdeni.” (Waroma 1:14) Paulo alitambua kuwa ana deni la kuwatangazia watu habari njema, kwa kuwa ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Leo, twatambua upendo na wajibu huohuo kwa jirani yetu. Upendo wa Yehova kwa wanadamu ulimchochea kumtuma Mwana wake duniani awafie. (Yohana 3:16) Hiyo ilikuwa dhabihu kubwa. Twaiga upendo wa Yehova tunapotumia wakati na jitihada kutangazia wengine habari njema ya wokovu unaotegemea dhabihu ya Yesu.

14. Biblia hufafanuaje ulimwengu ulio nje ya kutaniko la Kikristo?

14 Mashahidi wa Yehova huwaona wanadamu wenzao kuwa watu wanaoweza kujiunga na udugu wa Kikristo. Lazima tuhubiri kwa ujasiri, ingawa ujasiri wetu si mabishano. Ni kweli kuwa Biblia hutumia maneno makali inaposema kuhusu ulimwengu kwa jumla. Paulo atumia neno “ulimwengu” kuonyesha kitu kisichofaa asemapo kuhusu “hekima ya ulimwengu huu” na “tamaa za kilimwengu.” (1 Wakorintho 3:19; Tito 2:12) Paulo pia aliwakumbusha Wakristo Waefeso kwamba wanapotembea “kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu,” basi ni “wafu” kiroho. (Waefeso 2:1-3) Maneno hayo na mengineyo yapatana na haya ya mtume Yohana: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.”—1 Yohana 5:19.

15. Kuhusu watu mmoja-mmoja walio nje ya kutaniko la Kikristo, sisi huepuka kufanya nini, na kwa nini?

15 Hata hivyo, kumbuka kwamba maneno hayo huurejezea ulimwengu kwa jumla ambao umejitenga na Mungu, wala si kwa watu mmoja-mmoja. Wakristo hawajitwalii daraka la kuamua kimbele jinsi mtu yeyote yule atakavyoitikia kazi ya kuhubiri. Hawana sababu ya kusema kwamba mtu yeyote yule ni mbuzi. Si juu yetu kuamua yatakayotokea wakati Yesu atakapokuja kutenganisha “kondoo” na “mbuzi.” (Mathayo 25:31-46) Yesu ndiye hakimu aliyewekwa rasmi; wala si sisi. Isitoshe, mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba watu fulani waliokuwa na mwenendo mbaya sana wameukubali ujumbe wa Biblia, wakabadilika, na kuwa Wakristo wanaoishi maisha safi. Basi, ingawa huenda tusishirikiane na watu fulani-fulani, hatusiti kuwatangazia tumaini la Ufalme nafasi itokeapo. Maandiko yataja watu fulani ambao, ingawa si waamini, ‘walikuwa na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.’ Baadaye wakawa waamini. (Matendo 13:48) Hatuwezi kamwe kujua yule aliye na mwelekeo ufaao hadi baada ya kumtolea ushahidi—labda mara kadhaa. Kwa kuzingatia hilo, twawatendea kwa “upole” na kwa “staha yenye kina kirefu” wale ambao hawajaukubali ujumbe wa wokovu, tukitumaini kwamba huenda baadhi yao wakaukubali ujumbe wa uhai.—2 Timotheo 2:25; 1 Petro 3:15.

16. Sababu moja inayofanya tutake kusitawisha “usanifu wa kufundisha” ni gani?

16 Kusitawisha ustadi tukiwa walimu kutaboresha hamu yetu ya kutangaza habari njema. Kwa mfano: Huenda mchezo wenye kuvutia usimpendeze mtu asiyejua kuucheza. Lakini humfurahisha yule anayejua kuucheza. Vivyo hivyo, Wakristo wanaositawisha “usanifu wa kufundisha” huongeza furaha yao katika huduma. (2 Timotheo 4:2; Tito 1:9) Paulo alimshauri Timotheo hivi: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.” (2 Timotheo 2:15) Twaweza kusitawishaje ustadi wetu wa kufundisha?

17. Twaweza ‘kufanyizaje hamu sana’ ya ujuzi wa Biblia, na ujuzi huo utainufaishaje huduma yetu?

17 Njia moja ni kuongeza ujuzi sahihi. Mtume Petro atutia moyo hivi: “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni, fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno, ili kupitia hilo mpate kukua kufikia wokovu.” (1 Petro 2:2) Kwa kawaida, mtoto mwenye afya huwa na hamu ya maziwa. Hata hivyo, huenda Mkristo akahitaji ‘kufanyiza hamu sana’ ya ujuzi wa Biblia. Hilo laweza kufanywa kwa kusitawisha mazoea mazuri ya kujifunza na kusoma. (Mithali 2:1-6) Tukitaka kuwa walimu stadi wa Neno la Mungu, lazima tujitahidi na tujitie nidhamu, lakini jitihada hizo huthawabisha. Furaha inayotokana na kulichunguza Neno la Mungu itafanya tuwake roho ya Mungu, huku tukiwa na hamu ya kuwaeleza wengine mambo tunayojifunza.

18. Mikutano ya Kikristo yaweza kutusaidiaje kulitumia sawasawa neno la ile kweli?

18 Mikutano ya Kikristo pia hutimiza fungu muhimu katika kutumia Neno la Mungu kwa ustadi. Maandiko ya Biblia yanaposomwa katika hotuba za watu wote na kwenye mazungumzo mengine ya Biblia, ni vema tufuatane na msemaji kwa kusoma Biblia zetu wenyewe. Ni busara tusikilize kwa makini sehemu za mikutano, kutia ndani zile zinazozungumzia hasa kazi yetu ya kuhubiri. Hatupaswi kamwe kupuuza faida ya maonyesho, labda kwa kuruhusu akili zetu kutanga-tanga. Kujitia nidhamu na kusikiliza kwa makini kwahitajika pia. (1 Timotheo 4:16) Mikutano ya Kikristo hujenga imani yetu, hutusaidia kufanyiza hamu sana ya Neno la Mungu, na hutuzoeza kuwa na hamu ya kutangaza habari njema.

Twaweza Kuutumaini Utegemezo wa Yehova

19. Kwa nini ni muhimu kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri?

19 Wakristo ‘wanaowaka roho’ na ambao wana hamu ya kutangaza habari njema hujitahidi kushiriki katika huduma kwa ukawaida. (Waefeso 5:15, 16) Ni kweli kwamba hali hutofautiana, na haiwezekani kwa watu wote kutumia wakati uleule katika kazi hii inayookoa uhai. (Wagalatia 6:4, 5) Ingawa hivyo, labda ukawaida wa kuwaambia wengine tumaini letu ndilo jambo muhimu zaidi kuliko jumla ya wakati tunaotumia katika kazi ya kuhubiri. (2 Timotheo 4:1, 2) Kadiri tuhubirivyo, ndivyo tutambuavyo umuhimu wa kazi hii. (Waroma 10:14, 15) Huruma na hisia-mwenzi zetu zitaongezeka tunapokutana kwa ukawaida na watu wenye mioyo myeupe wanaougua na kulia na ambao hawana tumaini.—Ezekieli 9:4; Waroma 8:22.

20, 21. (a) Kungali kuna kazi gani mbele yetu? (b) Yehova anategemezaje jitihada zetu?

20 Yehova ametukabidhi habari njema. Huo ndio utume wa kwanza tunaopokea kutoka kwake kama ‘wafanyakazi wenzake.’ (1 Wakorintho 3:6-9) Tuna hamu ya kutimiza wajibu huo kutoka kwa Mungu kwa nafsi yetu yote na kwa uwezo wetu wote. (Marko 12:30; Waroma 12:1) Kungali kuna watu wengi wenye mwelekeo ufaao katika ulimwengu ambao wana hamu ya kuijua kweli. Kuna kazi nyingi ya kufanya, lakini twaweza kuutumaini utegemezo wa Yehova tuendeleapo kuitimiza huduma yetu kikamili.—2 Timotheo 4:5.

21 Yehova hutupa roho yake takatifu naye hutuandalia “upanga wa roho,” Neno la Mungu. Kupitia msaada wake, twaweza kufungua vinywa vyetu “kwa uhuru wa usemi kujulisha siri takatifu ya habari njema.” (Waefeso 6:17-20) Maneno ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Thesalonike yanatuhusu: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu.” (1 Wathesalonike 1:5) Naam, na tutangaze habari njema kwa hamu!

[Mambo ya Kupitia]

• Kwa sababu ya mahangaiko ya maisha, huenda bidii yetu katika huduma ikapatwa na nini?

• Ni kwa njia gani tamaa yetu ya kutangaza habari njema yapasa kuwa kama “moto uwakao” mioyoni mwetu?

• Tunapaswa kuepuka mitazamo gani isiyofaa kuelekea huduma?

• Kwa jumla, twapaswa kuwaonaje wale walio na imani tofauti na yetu?

• Yehova hutusaidiaje kudumisha bidii yetu katika kazi ya kuhubiri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wakristo huiga bidii ya Yeremia na Paulo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Upendo kwa Mungu na jirani ndio huchochea hamu yetu katika huduma