Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wachungaji Wakristo, ‘Panueni Mioyo Yenu’!

Wachungaji Wakristo, ‘Panueni Mioyo Yenu’!

Wachungaji Wakristo, ‘Panueni Mioyo Yenu’!

“BWANA ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.” Kwa maneno hayo, Daudi alionyesha uhakika kamili katika Mungu wake. Yehova alimwongoza kiroho kwenye “malisho ya majani mabichi” na “kando ya maji ya utulivu,” na kumwelekeza “katika njia za haki.” Alipozingirwa na wapinzani, Daudi alipokea utegemezo na kitia-moyo, naye akachochewa kumwambia Yehova: “Sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe upo pamoja nami.” Kwa vile alikuwa na Mchungaji Mkubwa Kabisa kama huyo, Daudi aliazimia ‘kukaa nyumbani mwa BWANA milele.’—Zaburi 23:1-6.

Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu pia alipata utunzaji wa Yehova wenye upendo, naye akadhihirisha kikamilifu utunzaji huo kwa jinsi alivyowashughulikia wanafunzi wake alipokuwa duniani. Basi, Maandiko humwita “mchungaji mwema,” “mchungaji mkubwa,” na “mchungaji mkuu.”—Yohana 10:11; Waebrania 13:20; 1 Petro 5:2-4.

Yehova na Yesu Kristo wanaendelea kuwachunga wale wanaowapenda. Kwa sehemu, uchungaji wao huonyeshwa kupitia uandalizi wenye upendo wa wachungaji wa cheo cha chini kutanikoni. Paulo alizungumza na wachungaji hao wa cheo cha chini aliposema: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwalo roho takatifu imewaweka nyinyi rasmi kuwa waangalizi, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.”—Matendo 20:28.

Si rahisi kulichunga kundi kupatana na kiolezo kilichowekwa na Yehova na Kristo Yesu, ingawa ni kazi muhimu leo kuliko wakati uliopita. Hebu wazia juu ya Mashahidi zaidi ya milioni moja ambao wamebatizwa katika miaka mitatu iliyopita! Mashahidi hao wapya hawana uzoefu wa kiroho unaotokana na utendaji wa miaka mingi. Pia, wazia juu ya Mashahidi ambao wangali watoto au matineja. Wanahitaji uangalizi wa wazazi na pia wa wachungaji wa cheo cha chini kutanikoni.

Kwa kweli, kila Mkristo hupatwa na mikazo kutoka nje, kutia ndani mikazo ya marika. Lazima wote wajitahidi kupinga uvutano mkubwa wa kufuata njia ya ulimwengu ya kutimiza tamaa za kibinafsi. Katika nchi fulani, huenda wahubiri wa Ufalme wakavunjika moyo kwa sababu watu hawaitikii ujumbe wao. Wahubiri wengi wana matatizo mabaya ya afya. Huenda matatizo ya fedha yanawanyima wengine kichocheo cha kutafuta Ufalme kwanza. Hapana shaka sisi sote—pamoja na wale wa zamani katika kweli—twahitaji na twastahili msaada wa wachungaji wenye upendo.

Kichocheo Kinachofaa

Wakristo wa karne ya kwanza walishauriwa hivi: ‘Panueni mioyo yenu’! (2 Wakorintho 6:11-13) Yafaa wazee Wakristo wafuate shauri hilo wanapotimiza wajibu wao wa kuchunga. Wanaweza kufanyaje hivyo? Namna gani watumishi wa huduma, ambao wengi wao wanatazamia kuwa wachungaji?

Ikiwa wazee Wakristo wataka kuwa baraka kwa kundi, si lazima wachochewe tu na maoni ya kutimiza wajibu. Wanashauriwa hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo katika utunzaji wenu, si kwa kushurutishwa, bali kwa nia ya kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Petro 5:2) Kwa hiyo, uchungaji wenye mafanikio humaanisha kuwa na nia na hamu ya kuwatumikia wengine. (Yohana 21:15-17) Humaanisha kutambua mahitaji ya kondoo na kutenda haraka. Humaanisha kuonyesha sifa nzuri za Kikristo, zinazoitwa matunda ya roho ya Mungu, wanaposhughulika na wengine.—Wagalatia 5:22, 23.

Nyakati nyingine uchungaji huhusisha kuwatembelea ndugu nyumbani kwao. * Lakini wachungaji ‘wanaopanua mioyo yao’ hujitolea. Yaani, wao hufanya mengi zaidi kuliko tu ziara za uchungaji mara kwa mara. Wao hutumia vema kila nafasi kuchunga wengine kundini.

Kuwazoeza Wengine Kuwa Wachungaji

Ndugu yeyote, bila kujali umri, ‘anayejitahidi kufikilia cheo cha mwangalizi ni mwenye kutamani kazi bora.’ (1 Timotheo 3:1) Watumishi wengi wa huduma wameonyesha nia ya kutaka kufikia mapendeleo zaidi. Basi, wazee huwasaidia kwa moyo ndugu hao wenye nia wachukue hatua hiyo muhimu ya “kufikilia cheo cha mwangalizi.” Hilo lamaanisha kuwazoeza wawe wachungaji wenye mafanikio.

Kwa sababu ya kushika sana viwango bora vya Mungu, kutaniko la Kikristo la Yehova halijadhoofishwa na wachungaji wasio wa kweli kama wale wanaotajwa kwenye Ezekieli 34:2-6. Kwa kufaa, Yehova aliwadharau watu hao. Badala ya kulisha kundi, walijilisha wenyewe. Hawakuwatia nguvu wagonjwa, wala kuwaponya wauguao, wala kuwafunga waliovunjika, wala kuwarudisha waliotawanyika au kupotea. Waliwaonea kondoo kwa kutenda kama mbwa-mwitu badala ya wachungaji. Kondoo wasiochungwa walitawanyika, wakatanga-tanga huku na huku bila mtunzaji.—Yeremia 23:1, 2; Nahumu 3:18; Mathayo 9:36.

Kinyume cha wachungaji hao wasio waaminifu, wachungaji Wakristo hufuata mfano wa Yehova. Wao husaidia kuongoza kondoo kwenye “malisho ya majani mabichi” na “kando ya maji ya utulivu” ya kiroho. Hujitahidi kuwaelekeza “katika njia za haki” kwa kuwasaidia waelewe Neno la Yehova vizuri na kulitumia kibinafsi. Wanaweza kufanya hivyo kwa mafanikio kwa sababu wana “sifa ya kustahili kufundisha.”—1 Timotheo 3:2.

Mara nyingi wazee hufundisha kwenye jukwaa wakati wa mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, wazee pia hufundisha mtu mmoja-mmoja. Bila shaka, wengine hufundisha vema zaidi wanapoongea na mtu mmoja-mmoja, ilhali wengine wana kipawa cha kutoa hotuba. Ingawa hivyo, kutoweza kufundisha vizuri katika sehemu fulani hakumaanishi kwamba mtu hastahili kuwa mwalimu. Wazee hufundisha, kwa kutumia nafasi zote wanazopata, kutia ndani uchungaji. Uchungaji fulani hufanywa rasmi, kwa mfano, kwenye ziara zilizopangwa. Lakini uchungaji mwingi waweza kufanywa pia kwa njia isiyo rasmi, nao huleta faida kubwa pia.

Wachungaji na Walimu Nyakati Zote

Daktari huhitaji ujuzi na uzoefu ili afanye kazi yake. Ingawa hivyo, watu anaotibu huthamini anapoonyesha fadhili, huruma, hangaiko, na upendezi wa kweli. Anapaswa kuwa na sifa hizo. Vivyo hivyo, mwalimu na mchungaji mwema apaswa kuwa na sifa kama hizo, zikiwa sehemu ya utu wake wa kila siku. Mwalimu wa kweli huwa tayari kuwafundisha wale walio karibu naye ikihitajika. “Neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!” yasema Mithali 15:23. Huenda “wakati wa kufaa” ni pale anapoongea kwenye jukwaa, anapohubiri nyumba hadi nyumba, au anapoongea na mtu kwenye Jumba la Ufalme au kwenye simu. Hali kadhalika, mchungaji mwema hujitahidi kuonyesha sifa njema, zenye kujali nyakati zote, sio tu anapofanya ziara za uchungaji. Huku akiwa ‘amepanua moyo wake,’ atatumia kila nafasi kuwachunga kondoo, awatunze ifaavyo kwa wakati ufaao. Hilo ndilo hufanya kondoo wampende.—Marko 10:43.

Wolfgang, sasa ni mzee, akumbuka ziara ya kirafiki ambayo mtumishi mmoja wa huduma na mke wake waliifanyia familia yake. Asema hivi: “Watoto wetu walifurahia sana jinsi walivyosikilizwa na burudisho tulilopokea. Wangali wanaikumbuka ziara hiyo.” Naam, mtumishi huyo wa huduma alionyesha kwamba anajali; alikuwa ‘anaupanua moyo wake.’

Nafasi nyingine ya ‘kupanua moyo wako’ ni kuwatembelea wagonjwa, kuwatumia barua fupi ya kitia-moyo, au kuwapigia simu—kufanya chochote kinachowaonyesha kuwa unawajali! Wasaidie inapohitajika. Wakitaka kuongea, sikiliza kwa makini. Zungumza kuhusu mambo mazuri na yenye kupendeza kuhusu utendaji wa kitheokrasi katika kutaniko lenu na kwingineko. Wasaidie wautafakari wakati ujao mtukufu ambao wale wanaompenda Yehova wanatarajia.—2 Wakorintho 4:16-18.

Mbali na Ziara za Uchungaji

Tunapozingatia kusudi la uchungaji, ni wazi kwamba kufanya ziara rasmi za uchungaji nyumbani kwa akina ndugu, ingawa ni muhimu, ni sehemu tu ya mambo yanayohusika. Mchungaji mwenye upendo ‘hupanua moyo wake’ kwa kuwa mwenye kufikiwa kwa urahisi katika hali mbalimbali na nyakati zote. Uhusiano mzuri anaositawisha kati yake na ndugu zake huwahakikishia kwamba nyakati za magumu, hawatahitaji kuogopa jambo lolote baya kwa kuwa wanajua kwamba ndugu yao mwenye upendo, mchungaji Mkristo, anawajali.—Zaburi 23:4.

Naam, nyinyi nyote wachungaji Wakristo ‘panueni mioyo yenu.’ Onyesheni upendo wa kweli kwa ndugu zenu—watieni moyo, waburudisheni, wajengeni kiroho kadiri mnavyoweza. Wasaidieni wawe thabiti katika imani. (Wakolosai 1:23) Kondoo ambao wana wachungaji ‘wanaopanua mioyo yao’ hawatapungukiwa kitu. Wataazimia, kama Daudi, kukaa katika nyumba ya Yehova milele. (Zaburi 23:1, 6) Je, mchungaji mwenye upendo angehitaji nini zaidi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Madokezo ya kufanya ziara za uchungaji yamo katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1993, ukurasa wa 20-23, na la Machi 15, 1996, ukurasa wa 24-27.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Wachungaji Wakristo

• Hutumikia kwa hamu na kwa hiari

• Hulisha na kulijali kundi

• Huwasaidia wengine wajitahidi kufikia cheo cha kuwa wachungaji

• Huwatembelea wagonjwa na kuwajali

• Wako macho kuwasaidia ndugu zao nyakati zote

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wazee ni wachungaji sikuzote, iwe katika utumishi wa shambani, kwenye mikutano, au kwenye vikusanyiko vya kirafiki