Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Maisha Yako Yanavyoweza Kuwa na Maana Zaidi

Jinsi Maisha Yako Yanavyoweza Kuwa na Maana Zaidi

Jinsi Maisha Yako Yanavyoweza Kuwa na Maana Zaidi

MITHALI moja ya kale husema hivi: “Usijitaabishe ili kupata utajiri; acha kuzitegemea akili zako mwenyewe. Je! utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, kama tai arukaye mbinguni.” (Mithali 23:4, 5) Yaani, si jambo la hekima kujichosha tukijaribu kuwa matajiri, kwa kuwa utajiri waweza kuruka kana kwamba umebebwa kwenye mabawa ya tai.

Kama ionyeshavyo Biblia, utajiri waweza kutokomea upesi. Unaweza kutoweka kwa usiku mmoja kwa sababu ya misiba ya asili, hali mbaya ya kiuchumi, au matukio mengine yasiyotazamiwa. Zaidi ya hayo, hata wale ambao wamepata ufanisi wa kimwili mara nyingi huwa wametamauka. Fikiria kisa cha John, ambaye kazi yake ilitia ndani kuwatumbuiza wanasiasa, wanamichezo mashuhuri, na watawala.

John ataarifu hivi: “Nilikaza fikira zangu zote katika kazi yangu. Nikawa tajiri sana, nikalala katika hoteli za hali ya juu, na hata wakati mwingine nilisafiri kwenda kazini kwa ndege yangu. Mwanzoni nilifurahia hali hiyo, lakini pole kwa pole nikachoshwa. Watu wale niliowahudumia walionekana wakichukua mambo kijuujuu tu. Maisha yangu hayakuwa na maana.”

Kama John alivyogundua, maisha yenye kukosa mambo ya kiroho hayaridhishi. Katika Mahubiri yake mashuhuri ya Mlimani, Yesu Kristo alionyesha jinsi ya kupata furaha yenye kudumu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.” (Mathayo 5:3) Basi, ni wazi kwamba jambo la hekima ni kutanguliza mambo ya kiroho maishani mwetu. Hata hivyo, kuna mambo mengine yawezayo kuongezea maisha yetu maana.

Familia Yako na Rafiki Zako Ni wa Maana

Je, ungalifurahia maisha ukiwa mbali na familia yako na bila rafiki wa karibu? Kwa hakika la. Muumba wetu ametuumba tukiwa na uhitaji wa kupenda na vilevile wa kupendwa. Hiyo ni mojawapo ya sababu iliyomfanya Yesu akazie umuhimu wa ‘kumpenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mathayo 22:39) Familia ni zawadi ya Mungu ambayo huandaa hali bora ya kuonyesha upendo usio na ubinafsi.—Waefeso 3:14, 15.

Familia yetu yaweza kuyafanyaje maisha yetu yawe na maana zaidi? Familia iliyoungana yaweza kufananishwa na bustani nzuri ambayo huandaa kimbilio lenye kuburudisha kutokana na mkazo wa maisha ya kila siku. Vivyo hivyo, ndani ya familia, tunaweza kupata urafiki wenye kuburudisha na mchangamfu ambao huondolea mbali hisia za upweke. Bila shaka, familia haiandai mahali salama bila jitihada yoyote. Kadiri tunavyoimarisha vifungo vya familia, ndivyo uhusiano katika familia unavyokuwa wa karibu na pia maisha yanakuwa yenye kuridhisha zaidi. Mathalani, wakati tunaotumia kumwonyesha mwenzi wetu wa ndoa upendo na staha ni kama akiba tunayoweka kila siku ambayo hatimaye itatokeza faida kubwa.—Waefeso 5:33.

Ikiwa tuna watoto, tunahitaji kujitahidi kuandaa mazingira mazuri ya kuwalea. Kutumia wakati pamoja nao, na kuwa na mawasiliano mazuri pamoja nao, na kuwafundisha mambo ya kiroho huenda kukawa jambo gumu. Lakini wakati na jitihada kama hizo huleta uradhi mkubwa. Wazazi wenye kufanikiwa huwaona watoto kuwa baraka na vilevile urithi kutoka kwa Mungu unaohitaji kutunzwa vyema.—Zaburi 127:3.

Rafiki wema pia huchangia kufanya maisha yawe yenye kuridhisha na yenye maana. (Mithali 27:9) Tunaweza kupata rafiki wengi kwa kuonyesha wengine hisia-mwenzi. (1 Petro 3:8) Rafiki wa kweli husaidia kutuinua tunapoanguka. (Mhubiri 4:9, 10) Na “rafiki . . . [ni] ndugu [aliy]ezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

Jinsi urafiki wa kweli ulivyo wenye kuridhisha! Machweo ni yenye kutazamisha zaidi, mlo ni mtamu zaidi, na muziki ni wenye kupendeza zaidi tunapokuwa pamoja na rafiki. Hata hivyo, familia yenye ukaribu na rafiki wenye kutumainika ni pande mbili tu za maisha yenye maana. Ni maandalizi gani mengine Mungu amefanya ambayo yaweza kufanya maisha yetu yawe na maana zaidi?

Kuridhisha Uhitaji Wetu wa Kiroho

Kama ilivyotajwa hapo awali, Yesu Kristo alihusianisha furaha na kutambua kwetu uhitaji wa kiroho. Tumeumbwa tukiwa na uwezo wa kiroho na wa maadili. Kwa sababu hiyo, Biblia hurejezea “mtu wa kiroho” na “yule mtu wa siri wa moyoni.”—1 Wakorintho 2:15; 1 Petro 3:3, 4.

Kulingana na kitabu kiitwacho An Expository Dictionary of New Testament Words, cha W. E. Vine, moyo wetu wa kitamathali unawakilisha “utendaji wote wa mtu wa kiakili na wa kiadili, kutia ndani fikira na hisia za moyoni.” Akitoa ufafanuzi, Vine aongezea hivi: “Yaani, moyo unatumiwa kitamathali kuwakilisha hisia za ndani za mtu.” Kitabu hicho pia hutaarifu kwamba “moyo, ukiwa ndani sana, una ‘yule mtu asiyeonekana’ . . . yule mtu halisi.”

Tunaweza kuridhishaje mahitaji ya yule “mtu wa kiroho,” au ya “yule mtu asiyeonekana,” yaani, “yule mtu wa siri wa moyoni”? Tunachukua hatua muhimu katika kutimiza hilo na kuridhisha tamaa yetu ya kiroho tunapotambua umaana wa maneno ya mtunga-zaburi mwenye kupuliziwa aliyeimba hivi: “Jueni kwamba BWANA ndiye Mungu; ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake; tu watu wake, na kondoo wa malisho yake.” (Zaburi 100:3) Bila shaka, kutambua jambo hilo hutufanya tukate kauli ya kwamba tunatoa hesabu mbele za Mungu. Ikiwa tunataka kuwa miongoni mwa ‘watu wake na kondoo wa malisho yake,’ basi, ni lazima tutende kwa kupatana na Neno lake, Biblia.

Je, hilo ni jambo baya? La, kwa kuwa kutambua kwamba mwenendo wetu wamhusu Mungu hufanya maisha yetu yawe na maana zaidi. Hilo latutia moyo kuwa na mradi wenye kufaa wa kuwa watu bora. “Heri mtu yule amchaye BWANA, apendezwaye sana na maagizo yake,” yasema Zaburi 112:1. Kumhofu Mungu kwa staha na kutii sheria zake kutoka moyoni kunaweza kufanya maisha yetu yawe na maana zaidi.

Kwa nini kumtii Mungu kunaturidhisha? Kwa sababu tuna dhamiri, zawadi ambayo Mungu amewapa wanadamu wote. Dhamiri ni kama mchunguzi mwadilifu anayekubali au kukataa yale ambayo tumefanya au yale tunayonuia kufanya. Sisi sote tumepatwa na dhiki ya kusumbuliwa na dhamiri. (Waroma 2:15) Hata hivyo, dhamiri yetu pia yaweza kututhawabisha. Tunapowatendea Mungu na wanadamu wenzetu bila ubinafsi, tunahisi vizuri na kuridhika. Tunapata kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Kuna sababu muhimu inayofanya hali iwe hivyo.

Muumba wetu alituumba kwa njia ya kwamba tunaathiriwa na tamaa na mahitaji ya wengine. Kuwasaidia wengine hutufurahisha moyo. Kwa kuongezea, Biblia hutuhakikishia kwamba tukimsaidia mtu mwenye uhitaji, Mungu huona hilo kuwa fadhili aliyofanyiwa yeye.—Mithali 19:17.

Mbali na kutokeza uradhi wa ndani, je, kuzingatia uhitaji wetu wa kiroho kwaweza pia kutusaidia kwa njia yenye kutumika? Naam, Raymond, ambaye ni mfanyabiashara katika Mashariki ya Kati aamini hilo lawezekana. “Mradi wangu ulikuwa ni kuchuma tu fedha,” anasema. “Lakini tangu nilipokiri moyoni mwangu kwamba kuna Mungu na kwamba Biblia huonyesha mapenzi yake, nikawa mtu tofauti. Kutafuta riziki sasa si jambo kuu katika maisha yangu. Kujitahidi kumpendeza Mungu kumeniepusha na hisia mbaya ya chuki. Ingawa baba yangu aliuawa katika ghasia, mimi sina tamaa yoyote ya kulipiza kisasi.”

Kama Raymond alivyogundua, kutimiza vyema mahitaji ya “mtu wa kiroho” kwaweza kuponya majeraha makubwa ya kihisia-moyo. Hata hivyo, tukishindwa kukabiliana na matatizo ya kila siku, basi maisha hayatakuwa yenye kuridhisha kabisa.

Tunaweza Kuwa na “Amani ya Mungu”

Katika ulimwengu huu wenye shughuli nyingi, ni siku chache tu zinazopita bila kuwa na balaa fulani. Aksidenti hutokea, mipango huharibika, na watu hututamausha. Mambo hayo yanaweza kutuhuzunisha. Ingawaje, kwa wale wanaomtumikia Yehova Mungu, Biblia huwaahidi uradhi wa ndani—“amani ya Mungu.” Twapataje amani hii?

Mtume Paulo aliandika hivi: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Badala ya kujaribu kung’ang’ana na matatizo peke yetu, tunahitaji kusali kwa bidii huku tukimtwika Mungu mahangaiko yetu ya kila siku. (Zaburi 55:22) Imani ya kwamba yeye hujibu aina hiyo ya sala kupitia Mwanaye,Yesu Kristo, itazidi kuongezeka tukuavyo kiroho na kutambua jinsi ambavyo Mungu hutusaidia.—Yohana 14:6, 14; 2 Wathesalonike 1:3.

Baada ya kuwa tumeimarisha uhakika wetu katika Yehova Mungu, yule ‘asikiaye kuomba,’ ndipo tutakapoweza kukabiliana vyema na majaribu, kama vile magonjwa yenye kudumu muda mrefu, uzee, au kufiwa. (Zaburi 65:2) Hata hivyo, ili kufurahia kikweli maisha yenye maana ni lazima tufikirie wakati ujao pia.

Shangilia Tumaini Lililo Mbele Yetu

Biblia yaahidi “mbingu mpya na dunia mpya,” serikali adilifu na yenye kujali ikitawala wanadamu watiifu. (2 Petro 3:13) Katika ulimwengu huo mpya ulioahidiwa na Mungu, amani na haki itachukua mahali pa vita na ukosefu wa haki. Hiyo si ndoto tu mbali ni usadikisho unaoweza kuzidi kupata nguvu siku kwa siku. Hizo ni habari njema kwelikweli na hapana shaka zinaandaa sababu ya kushangilia.—Waroma 12:12; Tito 1:2.

John, aliyetajwa mwanzoni, anahisi kuwa sasa maisha yake ni yenye maana zaidi. “Ingawa mimi sikuwa mtu mwenye kupendelea sana mambo ya kidini, sikuzote nilikuwa na imani katika Mungu,” yeye anasema. “Hata hivyo, sikufanya lolote kuhusu imani hiyo mpaka nilipotembelewa na Mashahidi wawili wa Yehova. Niliwauliza maswali mengi, kama vile, ‘Tupo hapa kwa kusudi gani? Tunaelekea wapi?’ Majibu yao ya Kimaandiko yenye kuridhisha yalinifanya nihisi nikiwa mwenye kusudi kwa mara ya kwanza katika maisha yangu. Huo ukawa mwanzo tu. Tamaa ya kujua kweli niliyositawisha ilinifanya nibadili mtazamo wangu wote. Hata ingawa sasa sina vitu vingi vya kimwili, najihisi nikiwa tajiri mkubwa kiroho.”

Kama John, labda hujaamsha uwezo wako wa kiroho kwa miaka mingi. Ukisitawisha “moyo wa hekima” unaweza kuuamsha. (Zaburi 90:12) Ukiazimia na ukitia bidii, unaweza kuwa mwenye shangwe, amani, na tumaini la kweli. (Waroma 15:13) Naam, na maisha yako yaweza kuwa na maana zaidi.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Sala inaweza kutupa “amani ya Mungu”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, unafahamu kile kinachoweza kufanya maisha ya familia yawe yenye kuridhisha zaidi?