Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutangaza Habari Njema Katika Mashamba ya Mpunga Taiwan

Kutangaza Habari Njema Katika Mashamba ya Mpunga Taiwan

Sisi Ni Namna ya Watu Walio na Imani

Kutangaza Habari Njema Katika Mashamba ya Mpunga Taiwan

NCHINI Taiwan kwa kawaida kuna mvua nyingi, inayofanya iwezekane kuvuna mpunga mara mbili kwa mwaka. Hata hivyo, mara kwa mara mvua hainyeshi kwa wakati wake, nayo miche inakufa. Jambo hilo linapotukia, je, mkulima anasalimu amri? Hasha. Anajua kwamba ni lazima avumilie. Anakuza miche mipya na kupanda tena. Kisha, hali zikiwa nzuri zaidi, mkulima huvuna vizuri. Wakati mwingine, kupanda na kuvuna kiroho kwafanana na hali hiyo kabisa.

Kuvumilia Katika Mavuno ya Kiroho

Kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova huko Taiwan wamefanya kazi ya kupanda kwa bidii na kuvuna mbegu za kweli za Kimaandiko katika sehemu ambazo hazikuwa na matokeo mazuri. Mojawapo ya sehemu hizi ni Mkoa wa Miao-li. Jitihada za kutoa ushuhuda katika sehemu hiyo hazikuwa na matokeo yoyote. Hivyo, mwaka wa 1973 wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee, walitumwa huko kufanya kazi ya wakati wote ya kutangaza Ufalme. Mwanzoni, baadhi ya watu walipendezwa na habari njema. Lakini, hatimaye upendezi huo ulififia. Kisha mapainia wa pekee hao walitumwa sehemu nyingine.

Mnamo 1991, mapainia wa pekee wengine wawili walitumwa huko. Tena matokeo yalionyesha kwamba hali haikufaa ukuzi wa kiroho. Baada ya miaka michache mapainia hao wa pekee walitumwa kufanya kazi katika mashamba ambayo yalikuwa na tumaini la mavuno. Hivyo, shamba hilo halikufanyiwa kazi kwa kipindi fulani.

Jitihada Mpya Zaleta Matokeo

Mnamo Septemba 1998 iliamuliwa kwamba sehemu zenye matokeo mazuri zaidi nchini Taiwan zihubiriwe. Hilo lingetimizwaje? Mapainia 40 wa pekee wa muda walitumwa wakahubiri sehemu zenye watu wengi zisizo na kutaniko la karibu.

Miji miwili inayopakana katika Mkoa wa Miao-li ilikuwa miongoni mwa ile iliyochaguliwa. Dada waseja wanne wangehubiri huko kwa muda wa miezi mitatu ili kuchunguza uwezekano wa kupata matokeo. Mara baada ya kufika, walitoa ripoti yenye kufurahisha kwamba wamepata watu wengi wanaopendezwa. Baada ya kufanya upainia kwa miezi hiyo mitatu, walikuwa na mafunzo mengi ya Biblia ya nyumbani. Pia walianzisha funzo la kitabu, wakisaidiwa na mzee kutoka kutaniko la karibu.

Dada watatu kati yao walijulisha waziwazi kwamba walitaka kuendelea kutunza “miche” midogo hiyo iliyokuwa ikisitawi vizuri. Basi, wawili kati yao waliwekwa kuwa mapainia wa pekee wa kudumu, na yule wa tatu aliendelea kufanya kazi huko akiwa painia wa kawaida. Mzee kutoka kutaniko la karibu alihamia sehemu hiyo ili kuwasaidia. Zaidi ya watu 60 walihudhuria hotuba ya watu wote ya kwanza iliyotolewa katika sehemu hiyo. Sasa, kutaniko la karibu lasaidia kikundi hicho kipya kuongoza mikutano ya Jumapili kwa ukawaida na mafunzo ya vitabu kadhaa. Karibuni, huenda kutaniko jipya likaanzishwa katika eneo hilo.

Uvumilivu Waleta Baraka Katika Sehemu Nyingine za Taiwan

Sehemu nyingine zilikuwa na matokeo ya aina hiyo. Katika Mkoa wa I-lan katika sehemu ya kaskazini-mashariki ya kisiwa hicho, Funzo la Kitabu la Kutaniko lilianzishwa mahali ambapo mapainia wa pekee walihubiri.

Painia mmoja wa pekee wa muda alipokwenda nyumba kwa nyumba jioni moja alikutana na kijana mmoja, akamwonyesha kikaratasi chenye wakati wa mikutano ya kutaniko. Mara aliuliza hivi: “Nihudhurie mikutano kesho jioni? Ikiwa ndivyo, nivae nini?” Tangu wakati huo, kila juma, painia huyo akawa akiongoza mafunzo ya Biblia manane pamoja na wanaopendezwa. Punde si punde, baadhi ya wanafunzi hao walifanya mipango ili wao wenyewe wawe wahubiri wa habari njema, nao walikuwa na mradi wa kubatizwa.

Mtu mwingine katika mji uo huo alikuwa amekwenda kanisani kwa miaka mingi lakini hakuweza kupata mtu wa kumfundisha Biblia. Alipojulishwa juu ya mpango wa funzo la Biblia, alichukua fursa hiyo ya kujifunza. Alitiwa moyo kutayarisha somo kimbele. Painia wa pekee wa muda aliporudi kwa ajili ya funzo alipata kwamba huyu mwanamke alikuwa amenunua daftari na kuandika maswali yaliyoandikwa katika somo lake. Kisha alikuwa ameandika majibu ya kila swali. Hata alikuwa amenakili maandiko yote yaliyotajwa bila kunukuliwa katika somo lake. Dada alipowasili kuongoza funzo la kwanza, tayari mwanamke huyo alikuwa ametayarisha masomo matatu ya kwanza!

Matokeo kama hayo yalionwa pia katika mji wa Dongshih katikati ya Taiwan. Katika muda wa miezi mitatu waliyohubiri huko mapainia wa pekee wa muda waligawa broshua zaidi ya 2,000. Mwezi wa tatu walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 16. Sehemu kubwa ya mji huo iliharibiwa na tetemeko la ardhi lililokumba Taiwan mnamo Septemba 21, 1999, hata hivyo, wanaopendezwa kadhaa wanafanya maendeleo ya kiroho ingawa wanahitaji kusafiri kwa muda wa saa moja ili wahudhurie mikutano katika Jumba la Ufalme la karibu zaidi. Ndiyo, uvumilivu unahitajika ili kuvuna mazao mazuri ya kimwili na ya kiroho pia.

[Ramani katika ukurasa wa 8]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

CHINA

Mlango-Bahari wa Taiwan

TAIWAN

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.