Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mnyanyaso Watokeza Ukuzi Antiokia

Mnyanyaso Watokeza Ukuzi Antiokia

Mnyanyaso Watokeza Ukuzi Antiokia

MNYANYASO ulipoongezeka baada ya Stefano kufia imani, wengi wa wanafunzi wa Yesu waliukimbia Yerusalemu. Mojawapo ya mahali walipokimbilia ni Antiokia ya Siria, iliyoko kilometa 550 hivi kaskazini mwa Yerusalemu. (Matendo 11:19) Mambo yaliyotukia baadaye huko Antiokia yalibadili historia yote ya Ukristo. Ili kufahamu matukio hayo, inafaa kujua mambo machache kuhusu Antiokia.

Katika Milki yote ya Roma, miji ya Roma na Aleksandria tu ndiyo iliyozidi Antiokia kwa ukubwa, ufanisi, na umashuhuri. Jiji hili kubwa la Siria lilitawala bonde lote la kaskazini-mashariki ya Mediterania. Antiokia (ambalo sasa ni Antakya, Uturuki) lilijengwa kando ya Mto mkubwa wa Orontes ambao uliunganisha jiji hilo na bandari ya Seleukia Pieria, iliyoko umbali wa kilometa 32. Lilijengwa mahali palipokuwa na njia kuu za biashara kati ya Roma na Bonde la Eufrati na Tigrisi. Likiwa kituo kikuu cha biashara, shughuli za biashara ziliendeshwa humo na watu kutoka pande zote za milki ya Roma, ambao walileta habari za harakati za kidini kutoka kwao.

Dini na falsafa ya Kigiriki ilikuwa imesitawi katika Antiokia. Hata hivyo, “wakati wa Kristo,” asema mwanahistoria Glanville Downey, “madhehebu ya kale na falsafa zilielekea kuwa mambo ya kibinafsi, watu mmoja-mmoja wakijitafutia wenyewe utatuzi wa kidini wa matatizo na matarajio yao.” (A History of Antioch in Syria) Wengi walivutiwa na ile imani ya Mungu mmoja, sherehe na elimu-maadili ya Kiyahudi.

Wayahudi wengi walikuwa wameishi Antiokia tangu kujengwa kwa jiji hilo mwaka wa 300 K.W.K. Imekadiriwa kuwa idadi yao ilifikia kati ya watu 20,000 na 60,000, wakifanyiza zaidi ya asilimia 10 ya wenyeji. Mwanahistoria Josephus asema kwamba wafalme wa nasaba ya Seleukia waliwatia moyo Wayahudi walifanye Antiokia kuwa makao yao ya kudumu na kuwapa haki kamili za uraia. Wakati huo Maandiko ya Kiebrania yalipatikana katika lugha ya Kigiriki. Hilo lilichochea upendezi wa waliowaunga mkono Wayahudi katika matazamio ya Kimesiya. Kwa sababu hiyo, miongoni mwa Wagiriki kulikuwa na wageuzwa-imani wengi. Hali hizi zote zililifanya jiji la Antiokia kuwa eneo murua la kufanya wanafunzi Wakristo.

Kutoa Ushahidi kwa Wasio Wayahudi

Wengi wa wanafunzi wa Yesu wenye kunyanyaswa, ambao walitawanyika kutoka Yerusalemu, walizungumzia imani yao na Wayahudi pekee. Hata hivyo, huko Antiokia, wanafunzi fulani kutoka Saiprasi na Kirene walizungumza na “watu wenye kusema Kigiriki.” (Matendo 11:20) Ingawa kutolewa ushahidi kwa Wayahudi wenye kusema Kigiriki na wageuzwa-imani kuliendelea tangu mwaka wa 33 W.K., kutolewa kwa ushahidi katika Antiokia kwaonekana kulikuwa jambo jipya. Haukuelekezwa kwa Wayahudi pekee. Ni kweli kwamba mtu asiye Myahudi Kornelio na familia yake tayari walikuwa wanafunzi. Yehova alihitaji kumwonyesha mtume Petro maono ili amsadikishe ubora wa kuwahubiria wasio Wayahudi, au watu wa mataifa.—Matendo 10:1-48.

Katika jiji lenye jumuiya kubwa ya Wayahudi iliyokuwa imekaa humo kwa muda mrefu pasipo uhasama kati yao na wasio Wayahudi, watu hao wasio Wayahudi waliweza kutolewa ushahidi na kukubali habari njema. Yaonekana huko Antiokia hali ilifaa kwa mambo hayo na ‘idadi kubwa walipata kuwa waamini.’ (Matendo 11:21) Na wakati wageuzwa-imani, ambao hapo awali waliabudu miungu ya wapagani, walipogeuka wakawa Wakristo walikuwa wametayarishwa kipekee ili kuwatolea ushahidi watu hao wasio Wayahudi ambao walikuwa wangali wanaabudu miungu ya wapagani.

Kutaniko la Yerusalemu, liliposikia habari juu ya maendeleo huko Antiokia, lilimtuma Barnaba akaichunguze habari hiyo. Lilikuwa jambo la hekima na upendo kumchagua Barnaba. Mwanamume huyo alikuwa mwenyeji wa Saiprasi, sawa na baadhi ya wale waliokuwa wameanza kutoa ushahidi kwa wasio Wayahudi. Barnaba angejihisi salama miongoni mwa watu wa Antiokia wasio Wayahudi. Hao nao wangemwona kama mtu wa jumuiya jirani. * Angeunga mkono kazi iliyokuwa ikifanywa. Kwa hivyo “alipowasili na kuiona fadhili isiyostahiliwa ya Mungu, akashangilia na kuanza kuwatia wote moyo waendelee katika Bwana wakiwa na kusudi la moyo,” na “umati mkubwa ukaongezwa kwa Bwana.”—Matendo 11:22-24.

Mwanahistoria Downey aonelea hivi, “sababu ya kufanikiwa kwa Wakristo hao wa mapema katika Antiokia, yaelekea ilikuwa kwamba tofauti na ilivyokuwa Yerusalemu, wamishonari hao hawakuwa na haja ya kuwahofu Wayahudi wenye ushupavu; pia jiji hilo, likiwa jiji kuu la Siria, lilitawalwa na kamanda wa kijeshi na hivyo likawa lenye utulivu nao wafanya-ghasia wakawa hawawezi kutenda jeuri kama ilivyokuwa imefanyika Yerusalemu, ambapo watawala wa Yudea walionekana (angalau kwa wakati huo) kushindwa kuwazuia Wayahudi wenye kufanya ghasia.”

Kukiwa na hali hizo zenye kufaa na pia mengi ya kufanya, yaelekea Barnaba aliona uhitaji wa msaada, akamkumbuka rafiki yake Sauli. Kwa nini alimkumbuka Sauli, au Paulo? Inavyoonekana, ingawa Paulo hakuwa mmoja wa wale mitume 12, yeye alikuwa amepokea utume kwa mataifa. (Matendo 9:15, 27; Waroma 1:5; Ufunuo 21:14) Kwa sababu hiyo, Paulo alikuwa mwenzi aliyefaa kutangaza habari njema katika jiji hilo la Antiokia la watu wasio Wayahudi. (Wagalatia 1:16) Kwa hiyo Barnaba, akaenda huko Tarso, akampata Paulo, akamleta Antiokia.—Matendo 11:25, 26; ona sanduku kwenye ukurasa wa 26-27.

Waitwa Wakristo kwa Uongozi wa Kimungu

Kwa mwaka mzima Barnaba na Sauli “[wa]lifundisha umati mkubwa, na ilikuwa kwanza katika Antiokia kwamba wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.” Haielekei Wayahudi wangekuwa watu wa kwanza kuwaita wafuasi wa Yesu, Wakristo (Kigiriki) au Wamesiya (Kiebrania), kwa kuwa walimkataa Yesu kama Mesiya au Kristo, kwa hiyo hawangekubali kimya kimya kumpa cheo hicho kwa kuwaita wafuasi wake Wakristo. Wengine hufikiri kuwa huenda wenyeji wapagani ndio waliowabandika jina Wakristo ama kwa mzaha au kwa kuwadharau. Hata hivyo, Biblia huonyesha jina Wakristo lilitoka kwa Mungu.—Matendo 11:26.

Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kitenzi kinachotumiwa kuhusiana na jina hilo jipya na ambacho kwa kawaida hutafsiriwa “waliitwa,” siku zote hutumiwa kuhusiana na mambo yapitayo akili ya kibinadamu, mambo ya uaguzi, au ya kimungu. Hivyo wasomi hutafsiri neno hilo kuwa “kutoa tamko la uaguzi,” “kujua mambo ya kimungu,” au “kutoa amri ya kimungu au onyo la upole, kufundisha kutoka mbinguni.” Kwa kuwa wafuasi wa Yesu waliitwa Wakristo “kwa uongozi wa kimungu,” inawezekana kuwa Yehova aliwaelekeza Sauli na Barnaba kutoa jina hilo.

Jina hilo jipya likaendelea kutumiwa. Hivyo wanafunzi wa Yesu hawangeweza tena kufikiriwa kimakosa kuwa farakano la Dini ya Kiyahudi kwa kuwa tofauti kati ya hizi dini mbili ilikuwa wazi kabisa. Kufikia mwaka wa 58 W.K., maofisa wa Kiroma walikuwa wameitambua barabara jamii ya Wakristo. (Matendo 26:28) Kulingana na mwanahistoria Tacitus, kufikia mwaka 64 W.K., jina hilo lilikuwa pia linatumiwa na wenyeji wa mji wa Roma.

Yehova Huwatumia Waaminifu Wake

Maendeleo makubwa yalifanywa kuhusiana na habari njema huko Antiokia. Kwa baraka za Yehova na azimio la wanafunzi wa Yesu la kutoacha kuhubiri, Antiokia likawa kituo cha Ukristo katika karne ya kwanza. Mungu alitumia kutaniko hilo kama kituo cha kupeleka habari njema kwenye nchi za mbali. Kwa mfano, mtume Paulo alifunga safari zake zote za kimishonari huko Antiokia.

Siku hizi, bidii na kuazimia kujapokuwa upinzani kumesaidia pia katika kuenezwa kwa Ukristo wa kweli na kuwawezesha wengi kusikia na kuonyesha uthamini wao kwa habari njema. * Hivyo ikiwa unakabiliwa na upinzani kwa sababu unaunga mkono ibada safi, kumbuka kuwa Yehova anazo sababu za kuruhusu hali hiyo. Sawa na ilivyokuwa katika karne ya kwanza, ni lazima watu leo wapewe fursa ya kusikia habari za Ufalme wa Mungu na kuunga mkono. Azimio lako la kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu huenda ndilo jambo pekee lenye kuhitajiwa kumsaidia mtu fulani kuupokea ujuzi sahihi wa neno la Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwenye siku nyangavu, kisiwa cha Saiprasi chaweza kuonekana kutoka Mlima Casius ulio kusini magharibi mwa Antiokia.

^ fu. 18 Ona Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1999, ukurasa wa 9; Amkeni! la Aprili 22, 1999, ukurasa wa 21-22; 1999 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 250-252.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26, 27]

“Miaka ya Ukimya” wa Sauli

MARA ya mwisho kwa Sauli kutajwa katika kitabu cha Matendo kabla ya kusafiri kwenda Antiokia wapata mwaka wa 45 W.K., ni wakati ambapo njama ya kumuua ilizimwa huko Yerusalemu na waamini wenzake wakampeleka hadi Tarso. (Matendo 9:28-30; 11:25) Hilo lilikuwa limetukia miaka tisa mapema wapata mwaka wa 36 W.K. Alikuwa anafanya nini wakati huo wote—ambao umeitwa miaka ya ukimya wa Sauli?

Alipotoka Yerusalemu, Sauli alienda katika mikoa ya Siria na ya Kilikia, nayo makutaniko yaliyokuwa Yudea yakapata habari hii: “Yule mtu ambaye hapo zamani alitunyanyasa sasa anaitangaza habari njema juu ya imani ambayo hapo zamani aliangamiza kabisa.” (Wagalatia 1:21-23) Huenda ripoti hiyo yarejezea utendaji wake na Barnaba huko Antiokia, lakini hapana shaka kwamba hata kabla ya hapo, Sauli hakukaa bila kufanya lolote. Kufikia mwaka wa 49 W.K., kulikuwa na idadi fulani ya makutaniko huko Siria na Kilikia. Moja lilikuwa Antiokia, lakini inadhaniwa kwamba mengine yalifanyizwa kutokana na utendaji wa Sauli wa miaka hiyo inayoitwa eti ukimya.—Matendo 11:26; 15:23, 41.

Baadhi ya wasomi wanaamini kwamba matukio yenye kutazamisha katika maisha ya Sauli yapasa kuonwa kuwa yalitukia wakati huo. Mengi ya magumu aliyoyapata akiwa ‘mhudumu wa Kristo’ yangekuwa vigumu kujua yalitukia lini katika maisha yake ya umishonari. (2 Wakorintho 11:23-27) Ni wakati gani ambapo Wayahudi walimpiga Sauli mapigo 39 mara tano? Ni wapi alipopigiwa mara tatu kwa ufito? Ni wapi alipopata kuwa gerezani kwa ‘utele’? Kuwekwa kwake kizuizini huko Roma kulitukia baadaye. Tunalo simulizi kuhusu wakati mmoja ambapo alipigwa na kufungwa—huko Filipi. Vipi juu ya hayo mengine? (Matendo 16:22, 23) Mwandikaji mmoja adokeza kwamba, wakati huo, Sauli “alikuwa akitoa ushahidi juu ya Kristo katika masinagogi ya Wayahudi waliotawanyika na kwa sababu hiyo akanyanyaswa na mamlaka za kidini na zile za umma.”

Sauli alivunjikiwa na meli mara nne, lakini Maandiko hutoa maelezo kuhusu kisa kimoja tu, ambacho kilitukia baada ya yeye kuorodhesha magumu yake alipowaandikia Wakorintho. (Matendo 27:27-44) Basi, yaelekea visa hivyo vingine vitatu vilitokea alipokuwa katika safari za baharini ambazo hatujui chochote kuzihusu. Tukio lolote kati ya hayo au matukio hayo yote huenda yalitokea wakati wa ile “miaka ya ukimya.”

Tukio jingine ambalo yaonekana lilitokea wakati huo lafafanuliwa kwenye 2 Wakorintho 12:2-5. Sauli alisema: “Najua mtu mmoja katika muungano na Kristo ambaye, miaka kumi na minne iliyopita alinyakuliwa hadi kwenye mbingu ya tatu, katika paradiso, na kusikia maneno yasiyotamkika ambayo hairuhusiki kisheria mtu kuyasema.” Yaonekana Sauli alikuwa akisema juu yake mwenyewe. Kwa kuwa, aliandika maneno hayo wapata mwaka wa 55 W.K., miaka 14 mapema ya hapo yaturudisha nyuma kwenye mwaka wa 41 W.K., katikati ya ile “miaka ya ukimya.”

Bila shaka, maono hayo yalimpa Sauli ufahamu wa pekee. Je, yalimtayarisha afae zaidi akiwa “mtume kwa mataifa”? (Waroma 11:13) Je, baadaye yaliathiri namna yake ya kufikiri, kuandika, na kusema? Je, Sauli alipata mazoezi na ukomavu kwa ajili ya madaraka ya wakati ujao katika ile miaka ya tangu ageuzwe imani hadi wakati alipoitwa kwenda Antiokia? Hata maswali hayo yajibiweje, tunaweza kuwa na hakika kwamba alipoombwa kumsaidia Barnaba kuongoza kazi ya kuhubiri huko Antiokia, Sauli mwenye bidii, alikuwa amestahili kikamili kutimiza mgawo huo.—Matendo 11:19-26.

[Ramani katika ukurasa wa 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

SIRIA

Orontes

Antiokia

Seleukia

SAIPRASI

BAHARI YA MEDITERANIA

Yerusalemu

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Juu: Jiji la kisasa la Antiokia

Katikati: Mandhari ya kusini ya Seleukia

Chini: Ukuta wa Bandari ya Seleukia