Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini la Ufufuo Lina Nguvu

Tumaini la Ufufuo Lina Nguvu

Tumaini la Ufufuo Lina Nguvu

“Nimekubali hasara ya vitu vyote . . . ili kumjua [Yesu Kristo] na nguvu ya ufufuo wake.”—WAFILIPI 3:8-10.

1, 2. (a) Kasisi mmoja aliufafanuaje ufufuo miaka mingi iliyopita? (b) Ufufuo utatukiaje?

MWANZONI mwa miaka ya 1890, vyombo vya habari vya umma viliripoti juu ya mahubiri ya ajabu ya kasisi mmoja wa Brooklyn, New York, Marekani. Alisema kwamba ufufuo utahusisha kukusanywa tena na kuhuishwa kwa mifupa yote na nyama zilizokuwa zimefanyiza mwili wa mwanadamu, uwe uliharibiwa na moto au aksidenti, uwe uliliwa na mnyama au ukawa mbolea. Mhubiri huyo aliamini kwamba siku fulani yenye urefu wa saa 24, hewa ingekuwa nyeusi kutokana na mikono, miguu, vidole, mifupa, misuli, na ngozi za mabilioni ya watu waliokufa. Viungo hivyo vingekuwa vikitafuta viungo vingine vya mwili uleule. Kisha nafsi zingetoka mbinguni na helo na kuingia ndani ya miili hiyo iliyofufuliwa.

2 Ufufuo kupitia kuunganishwa tena kwa chembe za awali ni jambo lisilopatana na akili, na wanadamu hawana nafsi isiyoweza kufa. (Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Si lazima Yehova, aliye Mungu wa ufufuo, akusanye tena chembe zilizofanyiza mwili wa mtu hapo awali. Anaweza kuwaumbia miili mipya wale wanaofufuliwa. Yehova amempa Mwana wake, Yesu Kristo, nguvu za kuwafufua wafu, kukiwa na uwezekano wa kupata uhai udumuo milele. (Yohana 5:26) Hivyo Yesu alisema: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.” (Yohana 11:25, 26) Ni ahadi yenye kutia moyo kama nini! Hiyo hututia moyo tuvumilie majaribu na hata kukabili kifo tukiwa Mashahidi waaminifu wa Yehova.

3. Kwa nini Paulo alihitaji kuutetea ufufuo?

3 Ufufuo haupatani na fundisho la kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa—jambo ambalo Plato, mwanafalsafa Mgiriki, aliamini. Hivyo, kulitukia nini wakati mtume Paulo alipowatolea ushahidi Wagiriki mashuhuri kwenye Areopago huko Athene, akataja Yesu, na kusema kwamba Mungu alimfufua? “Basi,” yasema masimulizi hayo, “waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine wao wakaanza kudhihaki.” (Matendo 17:29-34) Wengi waliomwona Yesu Kristo aliyefufuliwa walikuwa bado hai na, licha ya kudhihakiwa, walishuhudia kwamba alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu. Lakini walimu wa uwongo walioshirikiana na kutaniko la Korintho waliukataa ufufuo. Hivyo, Paulo akatetea vikali fundisho hilo la Kikristo kwenye 1 Wakorintho sura ya 15. Uchunguzi wa makini wa hoja zake wathibitisha kabisa uhakika na nguvu za tumaini la ufufuo.

Uthibitisho Hakika wa Ufufuo wa Yesu

4. Paulo alitoa uthibitisho gani wa mashahidi waliojionea ufufuo wa Yesu?

4 Ona jinsi Paulo alivyoanza utetezi wake. (1 Wakorintho 15:1-11) Wakorintho wataamini kabisa habari njema za wokovu isipokuwa tu wawe walipata kuwa waamini bila kusudi lolote. Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, akazikwa, na kufufuliwa. Hata Yesu aliyefufuliwa alimtokea Kefa (Petro), ‘kisha wale kumi na wawili.’ (Yohana 20:19-23) Alionekana na watu wapatao 500, labda wakati alipoamuru: “Nendeni mkafanye wanafunzi.” (Mathayo 28:19, 20) Yakobo na pia mitume wote waaminifu walimwona. (Matendo 1:6-11) Yesu alimtokea Sauli karibu na Damasko “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake”—kana kwamba alikuwa tayari amefufuliwa kwenye uhai wa roho. (Matendo 9:1-9) Wakorintho walipata kuwa waamini kwa sababu Paulo aliwahubiria, nao wakakubali habari njema.

5. Paulo alisababu jinsi gani kama ilivyoandikwa kwenye 1 Wakorintho 15:12-19?

5 Ona jinsi Paulo anavyosababu. (1 Wakorintho 15:12-19) Kwa kuwa mashahidi waliojionea wanahubiri kwamba Kristo alifufuliwa, inawezaje kusemwa kwamba hakuna ufufuo? Ikiwa Yesu hakufufuliwa kutoka kwa wafu, kuhubiri kwetu na imani yetu ni bure, nasi ni waongo wanaotoa ushahidi dhidi ya Mungu kwa kusema kwamba alimfufua Kristo. Ikiwa wafu hawafufuliwi, ‘sisi bado tumo katika dhambi zetu,’ na wale waliokufa katika mwungano na Kristo wameangamia. Isitoshe, “ikiwa ni katika maisha haya tu tumetumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi sana kati ya watu wote.”

6. (a) Paulo alisema nini kuthibitisha ufufuo wa Yesu? (b) “Adui wa mwisho” ni nini, naye atafanywaje kuwa si kitu?

6 Paulo anathibitisha ufufuo wa Yesu. (1 Wakorintho 15:20-28) Kwa kuwa Kristo ndiye “matunda ya kwanza” ya wale ambao wamelala katika kifo, wengine pia wangefufuliwa. Kwa kuwa kifo kilitokana na kutotii kwa mwanadamu Adamu, ufufuo ni kupitia mwanadamu—Yesu. Walio wake wangefufuliwa wakati wa kuwapo kwake. Kristo atafanya ‘kuwa si kitu serikali yote na mamlaka yote na nguvu’ zinazopinga enzi kuu ya Mungu naye atatawala akiwa Mfalme hadi Yehova awekapo maadui wake wote chini ya miguu yake. Hata “adui wa mwisho”—kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu—atafanywa kuwa si kitu kupitia ustahili wa dhabihu ya Yesu. Kisha Kristo atamkabidhi Mungu wake na Baba yake Ufalme na kujitiisha kwa “Yule aliyetiisha vitu vyote kwake, ili Mungu apate kuwa vitu vyote kwa kila mtu.”

Je, Wanabatizwa Kuwa Wafu?

7. Ni nani “wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu” na jambo hilo lamaanisha nini kwao?

7 Wanaopinga ufufuo wanaulizwa: “Watafanya nini wao wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu?” (1 Wakorintho 15:29) Paulo hakumaanisha kwamba walio hai wanabatizwa kwa niaba ya wafu, kwa kuwa ni lazima wanafunzi wa Yesu wajifunze, waamini, na kubatizwa wakiwa mtu mmoja-mmoja. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 2:41) Wakristo watiwa-mafuta ‘wanabatizwa kwa kusudi la kuwa wafu’ kwa kufuatia sana maisha ambayo huongoza kwenye kifo na ufufuo. Ubatizo wa aina hiyo huanza roho ya Mungu inapotokeza ndani yao tumaini la kimbingu na huisha wanapofufuliwa kutoka kwa wafu na kupata uhai wa roho usioweza kufa mbinguni.—Waroma 6:3-5; 8:16, 17; 1 Wakorintho 6:14.

8. Wakristo wana uhakika gani hata wakiuawa na Shetani na watumishi wake?

8 Kama maneno ya Paulo yaonyeshavyo, tumaini la ufufuo huwawezesha Wakristo wakabili daima hatari na kifo kwa sababu ya kuhubiri Ufalme. (1 Wakorintho 15:30, 31) Wanajua ya kwamba Yehova anaweza kuwafufua akimruhusu Shetani na watumishi wake wawaue. Mungu tu ndiye awezaye kuangamiza nafsi zao, au uhai wao, katika Gehena, inayofananisha uharibifu wa milele.—Luka 12:5.

Uhitaji wa Kuwa Macho

9. Twapaswa kuepuka nini ikiwa tumaini la ufufuo litakuwa na nguvu zenye kututegemeza?

9 Tumaini la ufufuo lilimtegemeza Paulo. Alipokuwa Efeso, huenda maadui wake walimtupa katika uwanja wa michezo apigane na wanyama-mwitu. (1 Wakorintho 15:32) Ikiwa walifanya hivyo, aliokolewa kama vile Danieli alivyookolewa kutoka kwa simba. (Danieli 6:16-22; Waebrania 11:32, 33) Kwa kuwa aliutumaini ufufuo, Paulo hakuwa na mtazamo wa waasi-imani wa Yuda wakati wa Isaya. Walisema: “Tule, tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (Isaya 22:13) Ikiwa tumaini la ufufuo litakuwa na nguvu za kutegemeza maisha yetu kama lilivyotegemeza maisha ya Paulo, basi twapaswa kuepuka wale wenye mtazamo kama huo usiofaa. “Msiongozwe vibaya,” akaonya Paulo. “Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Bila shaka, kanuni hiyo inafaa katika sehemu mbalimbali za maisha.

10. Tunaweza kudumishaje tumaini letu la ufufuo?

10 Paulo aliwaambia hivi wale waliotilia shaka ufufuo: “Amkeni mwe na utimamu wa akili katika njia ya uadilifu na msizoee dhambi, kwa maana wengine hawana ujuzi juu ya Mungu. Ninasema ili kuwasukuma mwone aibu.” (1 Wakorintho 15:34) Katika ‘wakati huu wa mwisho,’ twahitaji kutenda kupatana na ujuzi sahihi wa Mungu na Kristo. (Danieli 12:4; Yohana 17:3) Tukifanya hivyo tutadumisha tumaini la ufufuo.

Wanafufuliwa na Mwili Gani?

11. Paulo alitoa mfano gani wa kuonyesha jinsi Wakristo watiwa-mafuta watakavyofufuliwa?

11 Kisha Paulo ajibu maswali fulani. (1 Wakorintho 15:35-41) Huenda mdadisi akauliza hivi labda akitaka kutilia shaka ufufuo: “Wafu watafufuliwaje? Ndiyo, wanafufuliwa wakiwa na mwili wa aina gani?” Kama Paulo alivyoonyesha, mbegu inayopandwa katika udongo kwa kweli hufa inapobadilika kuwa mche. Vivyo hivyo, ni lazima mtu aliyezaliwa kwa roho afe. Kama vile mmea huchipuka kutoka kwa mbegu ukiwa mwili mpya, ndivyo mwili wa Mkristo mtiwa-mafuta unavyokuwa tofauti na mwili wa kibinadamu. Ingawa maisha yake yanabaki kama yalivyokuwa kabla ya kufa, yeye hufufuliwa akiwa kiumbe kipya mwenye mwili wa roho, awezaye kuishi mbinguni. Yaelekea, watakaofufuliwa duniani watafufuliwa wakiwa na miili ya kibinadamu.

12. Maneno “miili ya kimbingu” na “miili ya kidunia” yamaanisha nini?

12 Kama Paulo alivyosema, mwili wa mwanadamu ni tofauti na wa wanyama. Hata miili ya wanyama hutofautiana. (Mwanzo 1:20-25) “Miili ya kimbingu” ya viumbe wa roho hutofautiana kwa utukufu na “miili ya kidunia” ya nyama. Pia, kuna tofauti katika utukufu wa jua, mwezi, na nyota. Lakini watiwa-mafuta wanaofufuliwa wana utukufu mkubwa zaidi.

13. Kulingana na 1 Wakorintho 15:42-44, ni nini hupandwa na ni nini hufufuliwa?

13 Baada ya kutaja tofauti zilizopo, Paulo aliendelea kusema: “Ndivyo pia ulivyo ufufuo wa wafu.” (1 Wakorintho 15:42-44) Alisema: “Hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika.” Huenda hapa Paulo akawa anamaanisha watiwa-mafuta wakiwa kikundi. Hupandwa katika uharibifu kwenye kifo, hufufuliwa katika kutoharibika, bila dhambi. Ingawa hawaheshimiwi na ulimwengu, hufufuliwa waishi mbinguni na kufanywa dhahiri pamoja na Kristo katika utukufu. (Matendo 5:41; Wakolosai 3:4) Wakati wa kufa hupandwa “ukiwa mwili wa nyama” na hufufuliwa “ukiwa mwili wa kiroho.” Kwa kuwa jambo hilo linawezekana kwa Wakristo watiwa-mafuta, tunaweza kuwa na hakika kwamba wanadamu wengine watafufuliwa waishi duniani.

14. Paulo aliwatofautishaje Kristo na Adamu?

14 Halafu Paulo awatofautisha Kristo na Adamu. (1 Wakorintho 15:45-49) Mtu wa kwanza, Adamu, “akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) “Adamu wa mwisho”—Yesu—“akawa roho ipayo uhai.” Alitoa uhai wake uwe dhabihu ya fidia, kwanza kwa niaba ya wafuasi wake watiwa-mafuta. (Marko 10:45) Wakiwa wanadamu, ‘wanachukua mfano wa yeye aliyefanywa kwa mavumbi,’ na wanapofufuliwa wanakuwa kama Adamu wa mwisho. Hapana shaka kwamba dhabihu ya Yesu itawanufaisha wanadamu wote watiifu, kutia ndani wale watakaofufuliwa duniani.—1 Yohana 2:1, 2.

15. Kwa nini Wakristo watiwa-mafuta hawafufuliwi katika mwili wa nyama, nao hufufuliwaje wakati wa kuwapo kwa Yesu?

15 Wakristo watiwa-mafuta hawafufuliwi katika mwili wa nyama wanapokufa. (1 Wakorintho 15:50-53) Mwili wa nyama na damu uwezao kuharibika hauwezi kurithi kutoharibika wala Ufalme wa mbinguni. Baadhi ya watiwa-mafuta hawangelazimika kulala kwa muda mrefu katika kifo. Wakimaliza kwa uaminifu mwendo wao wa dunia wakati wa kuwapo kwa Yesu, ‘wangebadilishwa, kwa dakika, katika kupepeseka kwa jicho.’ Wangefufuliwa mara moja kwenye uhai wa roho katika kutoharibika na utukufu. Hatimaye, idadi ya “bibi-arusi” wa mbinguni wa Kristo itakuwa 144,000.—Ufunuo 14:1; 19:7-9; 21:9; 1 Wathesalonike 4:15-17.

Kushinda Kifo!

16. Kulingana na Paulo na manabii wa zamani, kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu mwenye dhambi kitafanywaje?

16 Paulo alitangaza kwa ushindi kwamba kifo kingemezwa milele. (1 Wakorintho 15:54-57) Wakati mwili huu wenye kuharibika na uwezao kufa uvaapo kutoharibika na hali ya kutokufa, maneno haya yatatimizwa: “Kifo kimemezwa milele.” “Kifo, ushindi wako uko wapi? Kifo, kichomeo chako kiko wapi?” (Isaya 25:8; Hosea 13:14) Kichomeo kiletacho kifo ni dhambi, na nguvu ya dhambi ilikuwa ni Sheria, iliyohukumia watenda-dhambi kifo. Lakini kwa sababu ya dhabihu ya Yesu na ufufuo, kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu mwenye dhambi hakitashinda.—Waroma 5:12; 6:23.

17. Maneno ya 1 Wakorintho 15:58 yanatumikaje leo?

17 “Kwa sababu hiyo, ndugu zangu wapendwa,” akasema Paulo, “iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Maneno hayo yanawahusu mabaki watiwa-mafuta wa leo na “kondoo wengine” wa Yesu hata wakifa katika siku hizi za mwisho. (Yohana 10:16) Kazi zao wakiwa watangazaji wa Ufalme si bure, kwa kuwa watafufuliwa. Basi, tukiwa watumishi wa Yehova, na tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana tunapongoja siku ambapo kwa furaha tunaweza kupaaza sauti: “Kifo, kichomeo chako kiko wapi?”

Tumaini la Ufufuo Latimizwa!

18. Tumaini la Paulo katika ufufuo lilikuwa na nguvu kadiri gani?

18 Maneno ya Paulo yaliyoandikwa katika 1 Wakorintho sura ya 15 yadhihirisha kwamba tumaini la ufufuo lilikuwa na nguvu maishani mwake. Alikuwa na hakika kabisa kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu na kwamba wengine pia wangefufuliwa kutoka kwa kaburi la kawaida la wanadamu. Je, una imani yenye nguvu kama hiyo? Paulo aliona manufaa za kibinafsi kuwa “takataka nyingi,” ‘akakubali hasara ya vitu vyote’ ili ‘kumjua Kristo na nguvu ya ufufuo wake.’ Mtume huyo alikuwa tayari kufa kama Kristo akiwa na tumaini la kupata “ufufuo wa mapema zaidi.” Wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta 144,000 wanafufuliwa katika ufufuo huo ambao pia unaitwa “ufufuo wa kwanza.” Naam, wanafufuliwa kwenye uhai wa roho mbinguni, ilhali “wale wafu waliosalia” watafufuliwa kwenye dunia.—Wafilipi 3:8-11; Ufunuo 7:4; 20:5, 6.

19, 20. (a) Ni watu gani wanaotajwa katika Biblia ambao watafufuliwa waishi duniani? (b) Wewe unatazamia kwa hamu kufufuliwa kwa nani?

19 Tumaini la ufufuo limekuwa jambo halisi na tukufu kwa watiwa-mafuta ambao wamekuwa waaminifu hadi kifo. (Waroma 8:18; 1 Wathesalonike 4:15-18; Ufunuo 2:10) Waokokaji wa “dhiki kubwa” wataona tumaini la ufufuo likitimizwa duniani ‘bahari itoapo wafu walio ndani yake, na kifo na Hadesi viwatoapo wafu ndani yake.’ (Ufunuo 7:9, 13, 14; 20:13) Miongoni mwa wale watakaofufuliwa waishi duniani ni Ayubu, aliyefiwa na wana saba na binti watatu. Hebu wazia jinsi atakavyofurahi kuwakaribisha—na jinsi watakavyofurahi kuona kwamba wana ndugu saba zaidi na dada wengine watatu warembo!—Ayubu 1:1, 2, 18, 19; 42:12-15.

20 Itakuwa baraka iliyoje wakati Abrahamu na Sara, Isaka na Rebeka—naam na wengine wengi, kutia ndani “manabii wote”—watakapofufuliwa waishi duniani! (Luka 13:28) Danieli alikuwa mmojawapo wa manabii hao ambao waliahidiwa kufufuliwa chini ya utawala wa Mesiya. Kwa miaka 2,500 hivi, Danieli amepumzika kaburini, lakini kwa nguvu za ufufuo, karibuni ‘atafufuka na kupata tuzo lake’ akiwa mmoja wa “wakuu katika nchi zote.” (Danieli 12:13, Biblia Habari Njema; Zaburi 45:16) Itasisimua kama nini kuwakaribisha waaminifu wa zamani na pia baba yako, mama yako, mwana wako, binti yako, au wapendwa wengine uliopokonywa na adui kifo!

21. Kwa nini haitupasi kukawia kuwatendea wengine mema?

21 Huenda baadhi ya rafiki na wapendwa wetu wakawa wametumikia Mungu kwa miaka mingi na wamezeeka. Uzee unaweza kufanya iwe vigumu kwao kupambana na magumu ya maisha. Ni jambo lenye upendo kama nini kuwasaidia kadiri tuwezavyo hivi sasa! Hivyo, wakifa hatutajuta kwamba kwa njia fulani hatukutimiza wajibu wetu kwao. (Mhubiri 9:11; 12:1-7; 1 Timotheo 5:3, 8) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatasahau mambo mazuri tunayofanyia wengine, haidhuru umri wao au hali zao. “Maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo,” akaandika Paulo, “acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Wagalatia 6:10; Waebrania 6:10.

22. Twapaswa kuazimia kufanya nini hadi tumaini la ufufuo litimizwe?

22 Yehova ndiye “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Neno lake hutufariji na hutusaidia kuwafariji wengine kwa tumaini lenye nguvu la ufufuo. Hadi tutakaposhuhudia kutimizwa kwa tumaini hilo kwa kufufuliwa kwa wafu waishi duniani, na tuwe kama Paulo, aliyekuwa na imani katika ufufuo. Na tumwige hasa Yesu, ambaye tumaini lake katika nguvu za Mungu za kumfufua lilitimizwa. Karibuni wale waliomo katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti ya Kristo na kutoka. Jambo hilo na litufariji na kutuletea shangwe. Lakini zaidi ya yote, na tumshukuru Yehova, aliyefanya iwezekane kushinda kifo kupitia Bwana wetu Yesu Kristo!

Ungejibuje?

• Paulo alitoa uthibitisho gani wa mashahidi waliojionea ufufuo wa Yesu?

• “Adui wa mwisho” ni nini, nacho kitafanywaje kuwa si kitu?

• Kuhusu Wakristo watiwa-mafuta, ni nini kinachopandwa na nini kinachofufuliwa?

• Ni watu gani waliotajwa katika Biblia ambao ungependa kufahamiana nao wanapofufuliwa waishi duniani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mtume Paulo aliutetea ufufuo vikali

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ufufuo wa Ayubu, familia yake, na wengine wengi utaleta furaha isiyo na kifani!