Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini la Ufufuo Ni Hakika!

Tumaini la Ufufuo Ni Hakika!

Tumaini la Ufufuo Ni Hakika!

“Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo.”—MATENDO 24:15.

1. Kwa nini tunaweza kuutumaini ufufuo?

YEHOVA ametupa sababu hakika za kuutumaini ufufuo. Ametuahidi kwamba wafu watafufuliwa, wawe hai tena. Nalo kusudi lake kwa wale wanaolala katika kifo litatimizwa hakika. (Isaya 55:11; Luka 18:27) Kwa kweli, tayari Mungu ameonyesha uwezo wake wa kuwafufua wafu.

2. Tumaini la ufufuo linaweza kutunufaishaje?

2 Imani katika uandalizi wa Mungu wa kuwafufua wafu kupitia Mwana wake, Yesu Kristo, inaweza kututegemeza wakati wa matatizo. Uhakika wa tumaini la ufufuo unaweza pia kutusaidia tudumishe uaminifu-maadili kwa Baba yetu wa mbinguni hata kufikia kifo. Yaelekea, tumaini letu la ufufuo litaimarishwa tunapochunguza ufufuo mbalimbali ulioandikwa katika Biblia. Miujiza hiyo yote ilifanywa kwa nguvu za Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova.

Walipokea Wafu Wao kwa Ufufuo

3. Eliya alipewa uwezo wa kufanya nini wakati mwana wa mjane wa Zarefathi alipokufa?

3 Katika pitio lenye kusisimua la imani iliyoonyeshwa na mashahidi wa Yehova wa kabla ya Ukristo, mtume Paulo aliandika: “Wanawake waliwapokea wafu wao kwa ufufuo.” (Waebrania 11:35; 12:1) Mmojawapo wa wanawake hao ni mjane mmoja maskini katika mji wa Zarefathi uliokuwa Foinike. Kwa kuwa alimkaribisha nabii wa Mungu Eliya, unga wake na mafuta yake yalidumishwa kimuujiza wakati wa njaa kali ambayo ingalimwua yeye na mwanawe. Mtoto huyo alipokufa baadaye, Eliya alimlaza kitandani, akasali, akajinyosha juu ya mvulana huyo mara tatu, na kuomba: “Ee BWANA, Mungu wangu, nakusihi, roho [“nafsi,” NW] ya mtoto huyu imrudie ndani yake tena.” Mungu akasababisha nafsi, au uhai, imrudie mvulana huyo. (1 Wafalme 17:8-24) Hebu wazia jinsi mjane huyo alivyofurahi imani yake ilipothawabishwa kwa ufufuo huo wa kwanza kuwahi kuandikwa—ufufuo wa mwanawe mpendwa!

4. Elisha alifanya muujiza gani huko Shunemu?

4 Mwanamke mwingine aliyepokea mfu wake kwa ufufuo aliishi katika mji wa Shunemu. Alikuwa mke wa mwanamume mmoja mzee na alimwonyesha fadhili nabii Elisha na mtumishi wake. Alithawabishwa kwa kupata mwana. Hata hivyo, miaka kadhaa baadaye, mwanamke huyo alimwita nabii huyo nyumbani kwake, naye akamkuta mvulana huyo akiwa amekufa. Baada ya Elisha kusali na kufanya mambo fulani, “mwili wake yule mtoto ukaanza kupata moto.” “Akapiga chafya mara saba, na mtoto akafumbua macho yake.” Bila shaka, ufufuo huo ulimfurahisha sana mama na mwanawe pia. (2 Wafalme 4:8-37; 8:1-6) Lakini watafurahi kama nini watakapofufuliwa waishi duniani katika “ufufuo ulio bora”—ufufuo utakaofanya iwezekane wasife tena kamwe! Watakuwa na sababu iliyoje ya kumshukuru Mungu wa ufufuo mwenye upendo, Yehova!—Waebrania 11:35.

5. Elisha alihusikaje katika muujiza hata baada ya kifo chake?

5 Hata baada ya Elisha kufa na kuzikwa, Mungu aliipa mifupa yake nguvu kwa roho takatifu. Twasoma hivi: “[Waisraeli fulani] walipokuwa wakimzika mtu, angalia, waliona kikosi [cha Wamoabi]; wakamtupa yule mtu kaburini mwa Elisha; mara yule maiti alipoigusa mifupa ya Elisha, alifufuka, akasimama kwa miguu.” (2 Wafalme 13:20, 21) Ni lazima mtu huyo awe alishangaa na kufurahi kama nini! Hebu wazia furaha tutakayopata wakati wapendwa wetu watakapofufuliwa kwa kupatana na kusudi hakika la Yehova Mungu!

Mwana wa Mungu Aliwafufua Wafu

6. Yesu alifanya muujiza gani karibu na jiji la Naini, na tukio hilo laweza kuwa na matokeo gani juu yetu?

6 Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, ametupa sababu nzuri za kuamini kwamba wafu wanaweza kufufuliwa, wakiwa na matazamio ya kupata uhai udumuo milele. Tukio moja lililotokea karibu na jiji la Naini laweza kutusaidia kuelewa kwamba muujiza wa aina hiyo unawezekana kwa nguvu za Mungu. Wakati mmoja, Yesu alikutana na waombolezaji wakitoka jijini huku wakibeba mwili wa mwanamume mmoja kijana kwenda kuuzika. Alikuwa ndiye mtoto pekee wa mjane. Yesu akamwambia: “Koma kutoa machozi.” Kisha akagusa jeneza na kusema: “Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!” Ndipo akaketi na kuongea. (Luka 7:11-15) Muujiza huo unaimarisha imani yetu kwamba tumaini la ufufuo ni hakika.

7. Kulitukia nini kuhusiana na binti Yairo?

7 Fikiria pia tukio linalohusu Yairo, ofisa-msimamizi wa sinagogi la Kapernaumu. Alimwomba Yesu aje kumsaidia binti yake mpendwa mwenye umri wa miaka 12, aliyekuwa amelala akiwa mgonjwa mahututi. Muda si muda ikaripotiwa kwamba msichana huyo amekufa. Akimsihi Yairo mwenye huzuni nyingi awe na imani, Yesu aliandamana naye hadi nyumbani kwake, ambako watu walikuwa wanalia. Walicheka Yesu alipowaambia hivi: “Mtoto mchanga hakufa, bali analala usingizi.” Kwa kweli alikuwa amekufa, lakini Yesu alitaka kuonyesha kwamba watu wanaweza kufufuliwa kama vile tu wawezavyo kuamshwa kutoka katika usingizi mzito. Alishika mkono wa msichana huyo na kusema: “Msichana, inuka!” Akainuka mara moja, na “wazazi wake wakapigwa na bumbuazi” ya shangwe kubwa. (Marko 5:35-43;Luka 8:49-56) Bilashaka, washiriki wa familia ‘watapigwa na bumbuazi’ wakati wapendwa wao watakapofufuliwa waishi katika dunia paradiso.

8. Yesu alifanya nini kwenye kaburi la Lazaro?

8 Lazaro alikuwa amekufa kwa muda wa siku nne wakati Yesu alipoenda kwenye kaburi lake na kuagiza jiwe lililofunika kaburi hilo liondolewe. Baada ya kusali hadharani ili watu wajue kwamba alitegemea nguvu za Mungu, Yesu alipaaza sauti: “Lazaro, njoo huku nje!” Naye akatoka! Mikono na miguu yake ikiwa bado imefungwa sanda, na uso wake ukiwa umefunikwa kwa kitambaa. “Mfungueni mmwache aende,” Yesu akasema. Walipoona muujiza huo, wengi waliokuwa wamekuja kuwafariji dada za Lazaro, Maria na Martha, wakaweka imani katika Yesu. (Yohana 11:1-45) Je, masimulizi hayo hayakupi tumaini kamili kwamba wapendwa wako waweza kufufuliwa waishi katika ulimwengu mpya wa Mungu?

9. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba sasa Yesu anaweza kuwafufua wafu?

9 Yohana Mbatizaji alipokuwa gerezani, Yesu alimpelekea ujumbe huu wenye kutia moyo: “Vipofu wanaona tena, . . . na wafu wanafufuliwa.” (Mathayo 11:4-6) Kwa kuwa Yesu aliwafufua wafu alipokuwa duniani, kwa hakika anaweza kufanya hivyo akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo ambaye alipewa nguvu na Mungu. Yesu ndiye “ufufuo na uhai,” na inafariji kama nini kujua kwamba hivi karibuni “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka”!—Yohana 5:28, 29; 11:25.

Ufufuo Mwingine Mbalimbali Huimarisha Tumaini Letu

10. Unaweza kuelezaje ufufuo wa kwanza kuripotiwa kufanywa na mtume?

10 Yesu alipowatuma mitume wake wakiwa wahubiri wa Ufalme, alisema: “Fufueni wafu.” (Mathayo 10:5-8) Bila shaka, walihitaji kutegemea nguvu za Mungu ili kufanya hivyo. Dorkasi (Tabitha), mwanamke mwenye kumcha Mungu, alilala katika kifo huko Yopa mwaka wa 36 W.K. Matendo yake mema yalitia ndani kushona mavazi kwa ajili ya wajane wenye uhitaji, ambao walilia sana alipokufa. Wanafunzi walimtayarisha kwa ajili ya maziko na kumwita mtume Petro aje, labda ili kuwafariji. (Matendo 9:32-38) Aliagiza kila mtu atoke katika chumba cha juu, akasali, na kusema: “Tabitha, inuka!” Akafungua macho yake, akaketi, akachukua mkono wa Petro, naye akamwinua. Ufufuo huo wa kwanza kuripotiwa kufanywa na mtume ulifanya wengi wawe waamini. (Matendo 9:39-42) Ufufuo huo pia unatupa sababu zaidi ya kuutumaini ufufuo.

11. Ni ufufuo gani ulio wa mwisho kuandikwa katika Biblia?

11 Ufufuo wa mwisho katika Biblia ulifanywa huko Troasi. Paulo alipopitia huko akiwa katika safari yake ya mishonari, aliendelea kuhutubu hadi katikati ya usiku. Kwa kulemewa na uchovu na labda joto la taa nyingi na msongamano wa watu mahali pa mkutano, mwanamume kijana aitwaye Eutiko alilala usingizi, akaanguka chini kutoka dirisha la orofa ya tatu. “Akaokotwa akiwa amekufa,” wala si kupoteza fahamu tu. Paulo alijitupa juu ya Eutiko, akamkumbatia, na kuwaambia watazamaji hivi: “Komeni kufanya makelele, kwa maana nafsi yake imo ndani yake.” Paulo alimaanisha kwamba uhai wa mwanamume huyo kijana ulikuwa umerudishwa. Wale waliokuwemo “wakafarijiwa kupita kiasi.” (Matendo 20:7-12) Leo, watumishi wa Mungu hufarijika sana kujua kwamba washiriki wao wa zamani katika utumishi wa Mungu watafufuliwa kwa utimizo wa tumaini la ufufuo.

Ufufuo—Tumaini Ambalo Limekuwako kwa Muda Mrefu

12. Paulo alisema nini kwa usadikisho alipokuwa mbele ya Feliki, Gavana wa Roma?

12 Wakati Paulo alipofanyiwa kesi mbele ya Feliki, Gavana wa Roma, alishuhudia hivi: “Naamini mambo yote yaliyoelezwa katika Sheria na kuandikwa katika Manabii; nami nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:14, 15) Sehemu za Neno la Mungu kama vile “Sheria” zarejezeaje kufufuliwa kwa wafu?

13. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Mungu alidokeza ufufuo alipotoa unabii wa kwanza?

13 Mungu mwenyewe alidokeza ufufuo alipotoa unabii wa kwanza huko Edeni. Akimhukumu “nyoka wa awali,” Shetani Ibilisi, Mungu alisema hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake [“mbegu yako na mbegu yake,” NW] huo utakuponda [“utakuchubua,” NW] kichwa, na wewe utamponda [“utamchubua,” NW] kisigino.” (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:14, 15) Kuchubua kisigino cha mbegu ya mwanamke kulimaanisha kuuawa kwa Yesu Kristo. Ikiwa baadaye Mbegu hiyo ingemchubua nyoka kichwa, basi ingekuwa lazima Kristo afufuliwe kutoka kwa wafu.

14. Inakuwaje kwamba Yehova ni “Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai”?

14 Yesu alisema: “Kwamba wafu wafufuliwa hata Musa alifunua, katika usimulizi juu ya kijiti cha miiba, amwitapo Yehova ‘Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, wao wote wako hai.” (Luka 20:27, 37, 38; Kutoka 3:6) Abrahamu, Isaka, na Yakobo walikuwa wamekufa, lakini kusudi la Mungu la kuwafufua lilikuwa hakika sana hivi kwamba kwake, ni kana kwamba watu hao walikuwa bado hai.

15. Kwa nini Abrahamu alikuwa na sababu ya kuuamini ufufuo?

15 Abrahamu alikuwa na sababu za kuutumaini ufufuo, kwa kuwa wakati yeye na mke wake, Sara, walipokuwa wazee sana wasiweze kuzaa watoto, Mungu alirudisha kimuujiza nguvu zao za kuzaa. Huo ulikuwa kama ufufuo. (Mwanzo 18:9-11; 21:1-3; Waebrania 11:11, 12) Mwana wao, Isaka, alipokuwa na umri wa miaka 25 hivi, Mungu alimwambia Abrahamu amtoe dhabihu. Hata hivyo, Abrahamu alipokuwa karibu kumwua Isaka, malaika wa Yehova alizuia mkono wake. Abrahamu “alihesabu kwamba Mungu alikuwa aweza kumfufua [Isaka] hata kutoka kwa wafu; na kutoka huko alimpokea pia katika njia ya kielezi.”—Waebrania 11:17-19; Mwanzo 22:1-18.

16. Sasa Abrahamu amelala katika kifo, akingojea nini?

16 Abrahamu alitumainia kufufuliwa chini ya utawala wa Mesiya, Mbegu iliyoahidiwa. Kabla ya kuwa mwanadamu, Mwana wa Mungu alitazama kutoka juu na kuona imani ya Abrahamu. Hivyo, akiwa mwanadamu, Yesu Kristo aliwaambia Wayahudi hivi: “Baba yenu Abrahamu alishangilia sana katika tazamio la kuona siku yangu.” (Yohana 8:56-58; Mithali 8:30, 31) Abrahamu sasa amelala katika kifo, akingojea kufufuliwa aishi duniani chini ya Ufalme wa Mungu wa Kimesiya.—Waebrania 11:8-10, 13.

Ushuhuda wa Sheria na Zaburi

17. ‘Mambo yaliyoelezwa katika Sheria’ yalirejezeaje kufufuliwa kwa Yesu Kristo?

17 Tumaini la Paulo la ufufuo lapatana na ‘mambo yaliyoelezwa katika Sheria.’ Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: ‘Mleteeni kuhani mganda wa malimbuko ya mavuno yenu; naye atautikisa mganda mbele za BWANA [katika Nisani 16] ili kwamba ukubaliwe kwa ajili yenu.’ (Mambo ya Walawi 23:9-14) Labda Paulo alikumbuka sheria hiyo alipoandika: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza kati ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” Akiwa “matunda ya kwanza,” Yesu alifufuliwa siku ya Nisani 16, 33 W.K. Baadaye, wakati wa kuwapo kwake, kungekuwa na ufufuo wa ‘matunda ya baadaye’—wafuasi wake watiwa-mafuta kwa roho.—1 Wakorintho 15:20-23; 2 Wakorintho 1:21; 1 Yohana 2:20, 27.

18. Petro alionyeshaje kwamba ufufuo wa Yesu ulitabiriwa katika Zaburi?

18 Zaburi pia zinaunga mkono ufufuo. Siku ya Pentekoste 33 W.K. mtume Petro alinukuu Zaburi 16:8-11, akisema: “Daudi asema kwa habari [ya Kristo], ‘Nilikuwa na Yehova mbele ya macho yangu daima; kwa sababu yeye yuko kwenye mkono wangu wa kuume ili nisipate kutikiswa kamwe. Kwa ajili ya hilo moyo wangu ulipata kuwa mchangamfu na ulimi wangu ukashangilia sana. Zaidi ya hayo, hata mwili wangu utakaa katika tumaini; kwa sababu hutaacha nafsi yangu katika Hadesi, wala hutaruhusu mwaminifu-mshikamanifu wako aone uharibifu.’” Petro aliendelea kusema: “[Daudi] aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachiliwa mbali katika Hadesi wala mwili wake haukuona uharibifu. Yesu huyu Mungu alimfufua.”—Matendo 2:25-32.

19, 20. Petro alinukuu Zaburi 118:22 wakati gani, na jambo hilo lilihusianaje na kifo na ufufuo wa Yesu?

19 Siku kadhaa baadaye, Petro alisimama mbele ya Sanhedrini na kutaja Zaburi tena. Alipoulizwa jinsi alivyomponya mwombaji mlemavu, mtume huyo alisema: “Acheni ijulikane kwenu nyote na kwa watu wote wa Israeli, kwamba katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, ambaye nyinyi mlimtundika mtini lakini ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, kwa yeye mtu huyu asimama hapa akiwa timamu mbele yenu. [Yesu huyo ndiye] ‘jiwe lililotendwa na nyinyi wajenzi kama lisilo la maana ambalo limekuwa ndicho kichwa cha pembe.’ Zaidi ya hilo, hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina jingine chini ya mbingu ambalo limepewa miongoni mwa watu ambalo kwalo lazima sisi tupate kuokolewa.”—Matendo 4:10-12.

20 Hapa Petro alinukuu Zaburi 118:22, akiitumia kueleza kifo na ufufuo wa Yesu. Kwa kuchochewa na viongozi wao wa kidini, Wayahudi walimkataa Yesu. (Yohana 19:14-18; Matendo 3:14, 15) ‘Kukataliwa kwa jiwe na wajenzi’ kulisababisha kifo cha Kristo, lakini ‘jiwe hilo kuwa kichwa cha pembe’ kulimaanisha kufufuliwa kwake kwenye utukufu wa roho mbinguni. Kama mtunga-zaburi alivyotabiri, ‘neno hilo lilitoka kwa BWANA.’ (Zaburi 118:23) Kulifanya “jiwe” kuwa Kichwa cha pembe kulimaanisha kumkweza akiwa Mfalme-Mteule.—Waefeso 1:19, 20.

Wategemezwa na Tumaini la Ufufuo

21, 22. Yobu alikuwa na tumaini gani, kama ilivyoandikwa kwenye Ayubu 14:13-15, na hilo laweza kuwafarijije waliofiwa leo?

21 Ingawa sisi wenyewe hatujaona yeyote akifufuliwa kutoka kwa wafu, tumeona masimulizi fulani ya Maandiko yanayotuhakikishia kwamba kutakuwa na ufufuo. Hivyo, tunaweza kuwa na tumaini alilokuwa nalo mwanamume mnyofu, Yobu. Alipokuwa akiteseka, aliomba: “Laiti [Yehova] ungenificha kuzimuni, . . . na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka! Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:13-15) Mungu ‘atakuwa na tamaa ya kazi ya mikono yake,’ akitamani sana kumfufua Yobu. Hilo linatupa tumaini lililoje!

22 Huenda mshiriki wa familia mwenye kumhofu Mungu akawa mgonjwa sana kama Yobu, na huenda hata akafa. Huenda waliofiwa wakalia kwa huzuni, kama Yesu alivyolia Lazaro alipokufa. (Yohana 11:35) Lakini inafariji kama nini kujua kwamba Mungu ataita, na wale walio katika kumbukumbu yake wataitika! Itakuwa kana kwamba wamerudi kutoka safarini—wakiwa na afya njema, bila ugonjwa wala udhaifu wowote.

23. Watu wengine wameonyeshaje uhakika wao katika tumaini la ufufuo?

23 Kifo cha Mkristo mmoja mwaminifu aliyekuwa amezeeka, kiliwachochea waamini wenzake waandike: “Tafadhali pokea rambirambi zetu kuhusu kifo cha mama yako. Baada ya muda mfupi tu tutamkaribisha—akiwa mzuri na mwenye nguvu!” Wazazi waliofiwa na mwana wao walisema: “Tunatazamia kwa hamu iliyoje wakati Jason atakapoamka! Atatazama huku na huku na kuona Paradiso aliyoitamani sana. . . . Sisi tuliompenda tunachochewa sana kuwepo pia.” Naam, twaweza kushukuru kama nini kwamba tumaini la ufufuo ni hakika!

Ungejibuje

• Imani katika uandalizi wa Mungu wa kuwafufua wafu inaweza kutunufaishaje?

• Ni matukio gani yaliyoandikwa katika Maandiko ambayo hufanya tuutumaini ufufuo?

• Kwa nini inaweza kusemwa kwamba ufufuo ni tumaini ambalo limekuwako kwa muda mrefu?

• Tunaweza kuwa na tumaini gani lenye kututegemeza kuhusu wafu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa nguvu za Yehova, Eliya alimfufua mvulana wa mjane

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yesu alipomfufua binti Yairo, wazazi wake walipigwa na bumbuazi ya shangwe kubwa

[Picha katika ukurasa wa 15]

Siku ya Pentekoste 33 W.K., mtume Petro alishuhudia kwa ujasiri kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu