Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hekima I Pamoja na Wenye Kiasi”

“Hekima I Pamoja na Wenye Kiasi”

“Hekima I Pamoja na Wenye Kiasi”

“BWANA anataka nini kwako, ila . . . kwenda kwa unyenyekevu [“kiasi,” “NW”] na Mungu wako!”—MIKA 6:8.

1, 2. Kiasi ni nini, na kinatofautianaje na kimbelembele?

MTUME mashuhuri akataa kujitukuza. Mwamuzi mmoja mjasiri wa Israeli ajiita mdogo katika nyumba ya babake. Mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi akiri kwamba hana mamlaka kamili. Kila mmoja wao anaonyesha kiasi.

2 Kiasi ni kinyume cha kimbelembele. Mtu mwenye kiasi anafahamu vizuri uwezo wake na ustahili wake na hana kiburi wala majisifu. Badala ya kuwa mwenye kiburi, mwenye kujisifu, au mtaka makuu, nyakati zote mtu mwenye kiasi hutambua udhaifu wake. Kwa hiyo, yeye hustahi na kujali hisia za wengine na maoni yao.

3. Ni katika njia gani hekima “i pamoja na wenye kiasi”?

3 Kwa sababu nzuri Biblia inasema hivi: “Hekima i pamoja na wenye kiasi.” (Mithali 11:2, NW) Mtu mwenye kiasi ana hekima kwa sababu yeye hufuata mwendo ambao Mungu anakubali, naye huepuka roho ya kimbelembele ambayo huleta aibu. (Mithali 8:13; 1 Petro 5:5) Hekima ya kuwa mwenye kiasi inathibitishwa na maisha ya watumishi kadhaa wa Mungu. Ebu tufikirie ile mifano mitatu ambayo imetajwa katika fungu la kwanza.

Paulo—Mtu ‘wa Chini’ na ‘Msimamizi-Nyumba’

4. Paulo alipata mapendeleo gani ya kipekee?

4 Paulo alikuwa mashuhuri miongoni mwa Wakristo wa mapema, na kwa sababu nzuri. Katika huduma yake, alisafiri maelfu ya kilometa baharini na barani, na alianzisha makutaniko mengi. Na zaidi, Yehova alimbariki Paulo kwa kumpa maono na uwezo wa kusema lugha za kigeni. (1 Wakorintho 14:18; 2 Wakorintho 12:1-5) Pia Yehova alimpulizia Paulo aandike barua 14 ambazo sasa ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa wazi, inaweza kusemwa kwamba kazi za Paulo zilizidi kazi za wale mitume wengine.—1 Wakorintho 15:10.

5. Paulo alionyeshaje kwamba alikuwa na maoni yenye kiasi juu yake mwenyewe?

5 Kwa kuwa Paulo alikuwa katika mstari wa mbele katika utendaji wa Kikristo, huenda wengine wangetarajia kumwona akifurahia kutukuzwa, hata akiringia mamlaka yake. Lakini, haikuwa hivyo, kwa kuwa Paulo alikuwa mwenye kiasi. Alijiita “mdogo zaidi sana kati ya wale mitume,” akiongezea: “Nami sistahili kuitwa mtume, kwa sababu nililinyanyasa kutaniko la Mungu.” (1 Wakorintho 15:9) Kwa kuwa aliwanyanyasa Wakristo zamani, Paulo hakusahau kamwe kwamba ni kupitia tu fadhili isiyostahiliwa ya Mungu angeweza kuwa na uhusiano na Mungu, sembuse kufurahia mapendeleo ya kipekee ya utumishi. (Yohana 6:44; Waefeso 2:8) Kwa hiyo, Paulo hakuhisi kwamba mafanikio yake ya ajabu katika huduma yalimfanya awe bora kuliko wengine.—1 Wakorintho 9:16.

6. Paulo alionyeshaje kiasi aliposhughulika na Wakorintho?

6 Jinsi Paulo alivyoshughulika na Wakorintho inadhihirisha sana kwamba alikuwa mwenye kiasi. Inaonekana kwamba baadhi yao walivutiwa na wale ambao walifikiri kuwa waangalizi mashuhuri, kutia ndani Apolo, Kefa, na Paulo mwenyewe. (1 Wakorintho 1:11-15) Lakini Paulo hakutafuta sifa kwa Wakorintho wala hakutumia vibaya heshima aliyopewa na wengine. Alipowazuru, yeye hakujitokeza ‘na usemi wenye kupita kiasi wala hekima.’ Badala yake, Paulo alisema hivi juu yake mwenyewe na waandamani wake: “Acheni mtu atukadirie sisi hivyo kama walio chini ya Kristo na wasimamizi-nyumba wa siri takatifu za Mungu.” *1 Wakorintho 2:1-5; 4:1.

7. Paulo alionyeshaje kiasi hata alipokuwa akitoa ushauri?

7 Paulo hata alionyesha kiasi alipolazimika kutoa ushauri mkali na mwongozo. Badala ya kutumia mamlaka yake akiwa mtume, Paulo aliwasihi Wakristo wenzake “kwa huruma za Mungu” na “Msingi wa upendo.” (Waroma 12:1, 2; Filemoni 8, 9) Kwa nini Paulo alifanya hivyo? Kwa sababu kwa kweli alijiona kuwa ‘mfanyakazi mwenzi’ wa ndugu zake, wala hakujiona kuwa ‘bwana-mkubwa juu ya imani yao.’ (2 Wakorintho 1:24) Inaelekea kwamba sifa ya Paulo ya kiasi ndiyo iliyomfanya apendwe sana na makutaniko ya karne ya kwanza.—Matendo 20:36-38.

Maoni Yenye Kiasi Kuhusu Mapendeleo Yetu

8, 9. (a) Kwa nini tuwe na maoni yenye kiasi juu yetu wenyewe? (b) Wale ambao wana madaraka fulani wanaweza kuonyeshaje kiasi?

8 Paulo aliwawekea Wakristo wa leo mfano mzuri. Hata tuwe tumepewa mapendeleo gani, hatupaswi kuhisi kwamba sisi ni bora kuliko wengine. “Ikiwa yeyote afikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu,” Paulo aliandika, “anadanganya akili yake mwenyewe.” (Wagalatia 6:3) Kwa nini? Kwa sababu “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23; 5:12) Ndiyo, hatupaswi kusahau kwamba sisi sote tumerithi dhambi na kifo kutoka kwa Adamu. Mapendeleo ya pekee hayatuondolei hali yetu ya chini yenye dhambi. (Mhubiri 9:2) Kama Paulo, ni kwa fadhili tu isiyostahiliwa kwamba wanadamu wanaweza kuwa na uhusiano wowote pamoja na Mungu, sembuse kumtumikia katika pendeleo fulani la kipekee.—Waroma 3:12, 24.

9 Akitambua jambo hilo, mtu mwenye kiasi hajivunii mapendeleo yake wala hajisifii mafanikio yake. (1 Wakorintho 4:7) Anapotoa mashauri au mwelekezo, anafanya hivyo kama mfanyakazi mwenzi—wala si kama bwana-mkubwa. Hakika, ingekuwa makosa kwa mtu ambaye hufanya mambo fulani kwa njia bora kutafuta sifa au kutumia vibaya heshima anayopewa na waamini wenzake. (Mithali 25:27; Mathayo 6:2-4) Sifa pekee inayofaa hutoka kwa wengine—na haipaswi kutafutwa. Na tukisifiwa, jambo hilo halipasi kutufanya tujifikirie kuliko ilivyo lazima.—Mithali 27:2; Waroma 12:3.

10. Eleza jinsi wengine wanaoonekana kuwa wa hali ya chini wanavyoweza kuwa “matajiri wa imani” kwelikweli.

10 Tunapokabidhiwa madaraka fulani, kuwa wenye kiasi kutatusaidia kuepuka kujifikiria mno, tukitokeza wazo la kwamba kutaniko linastawi kwa sababu ya jitihada zetu na uwezo wetu. Kwa mfano, huenda tuna kipawa cha kufundisha. (Waefeso 4:11, 12) Lakini, tukiwa wenye kiasi ni lazima tutambue kwamba baadhi ya mambo makubwa zaidi tunayojifunza kwenye mikutano ya kutaniko hayafundishwi kutoka jukwaani. Kwa mfano, je, hutiwi moyo unapoona mzazi ambaye hana mwenzi akija kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme akiambatana na watoto wake? Au mtu ambaye ameshuka moyo anayehudhuria mikutano japo hisia zenye kudumu za kujiona kuwa hafai? Au kijana ambaye anazidi kufanya maendeleo ya kiroho japo mavutano mabaya shuleni na kwingineko? (Zaburi 84:10) Watu hawa huenda wasiwe mashuhuri. Mara nyingi majaribu ya uaminifu-maadili wanayokabili hayaonwi na wengine. Lakini, huenda wao ni “matajiri wa imani” kama tu wale ambao ni mashuhuri. (Yakobo 2:5) Kwani hatimaye, uaminifu ndio humfurahisha Yehova.—Mathayo 10:22; 1 Wakorintho 4:2.

Gideoni—“Mdogo” Katika Nyumba ya Baba Yake

11. Gideoni alionyeshaje kiasi alipokuwa akizungumza na malaika wa Mungu?

11 Gideoni, kijana hodari wa kabila la Manase, aliishi wakati wa mvurugo katika historia ya Israeli. Kwa miaka saba, watu wa Mungu walikuwa wameumia kwa kudhulumiwa na Wamidiani. Lakini, sasa wakati ulikuwa umewadia wa Yehova kuwakomboa watu wake. Basi, malaika akamtokea Gideoni, akasema: “BWANA yu pamoja nawe, Ee shujaa.” Gideoni alikuwa mwenye kiasi, kwa hiyo hakujitutumua kwa sababu ya kusifiwa huko ambako hakutarajia. Badala yake, akamwambia malaika huyo kwa staha: “Ee Bwana wangu, ikiwa BWANA yu pamoja nasi, mbona mambo haya yote yametupata?” Malaika huyo akamweleza Gideoni mambo kwa wazi: ‘Utawaokoa Israeli na mkono wa Midiani.’ Gideoni alijibuje? Badala ya kuchukua mgawo huo kwa hamu nyingi akiuona kuwa fursa ya kuwa shujaa katika taifa lote, Gideoni alijibu: “Ee Bwana, nitawaokoa Israeli kwa jinsi gani? Tazama, jamaa zangu ndio walio maskini sana katika Manase, na mimi ndimi niliye mdogo katika nyumba ya baba yangu.” Alionyesha sifa ya kiasi iliyoje!—Waamuzi 6:11-15.

12. Gideoni alionyeshaje busara alipotekeleza mgawo wake?

12 Kabla ya kumtuma Gideoni aende vitani, Yehova alimjaribu. Kwa njia gani? Gideoni aliambiwa aharibu madhabahu ya babake ya kuabudia Baali na aikatekate Ashera iliyokuwa kando yake. Mgawo huo ulihitaji ujasiri, lakini Gideoni pia alionyesha kiasi na busara katika njia aliyoutimiza. Badala ya kufanya mambo aliyoagizwa hadharani, Gideoni alifanya kazi hiyo usiku ambapo yaelekea hangeonekana. Isitoshe, Gideoni alitimiza mgawo wake kwa tahadhari iliyohitajika. Alichukua watumishi kumi—labda ili baadhi yao wawe walinzi na waliobaki wamsaidie kuharibu madhabahu na Ashera. * Kwa vyovyote vile, kwa baraka za Yehova, Gideoni alitekeleza mgawo wake, na baadaye akatumiwa na Mungu kukomboa Israeli kutoka kwa Wamidiani.—Waamuzi 6:25-27.

Kuonyesha Kiasi na Busara

13, 14. (a) Tunaweza kuonyeshaje kiasi tunapopata pendeleo fulani la utumishi? (b) Ndugu A. H. Macmillan aliwekaje mfano mzuri wa kuwa mwenye kiasi?

13 Tunaweza kujifunza mengi kutokana na jinsi Gideoni alivyoonyesha kiasi. Kwa mfano, inakuwaje tunapopokea pendeleo fulani la utumishi? Je, kwanza tunafikiria umashuhuri au sifa zitakazotokezwa na pendeleo hilo? Au kwa kiasi na kwa sala tunafikiria kama tunaweza kutimiza matakwa ya mgawo huo? Ndugu A. H. Macmillan, aliyemaliza mwendo wake wa duniani mwaka wa 1966 aliweka mfano mzuri kwa habari hiyo. Pindi moja C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, alimwomba Ndugu Macmillan atoe maoni yake kuhusu mtu ambaye angesimamia kazi Ndugu Russell asipokuwapo. Katika mazungumzo yaliyofuata, Ndugu Macmillan hakujipendekeza hata kidogo, ijapokuwa ingekuwa rahisi sana kwake kufanya hivyo. Mwishowe, Ndugu Russell alimwomba Ndugu Macmillan afikirie kukubali mgawo huo. “Niliduwaa pale nilipokuwa nimesimama,” Ndugu Macmillan akaandika miaka mingi baadaye. “Nilifikiria jambo hilo kwa uzito sana, na kusali juu yake kwa muda fulani kabla ya kumwambia hatimaye kwamba ningefurahi kufanya yote niwezayo ili kumsaidia.”

14 Baadaye kidogo, Ndugu Russell akafa, na ikawa kwamba Watch Tower Society haina msimamizi. Kwa kuwa Ndugu Macmillan ndiye aliyekuwa msimamizi wakati Ndugu Russell alipokuwa katika safari ya mwisho ya kuhubiri, ndugu fulani alimwambia hivi: “Mac, kuna uwezekano mkubwa kwamba ni wewe utakuwa msimamizi. Ulikuwa mwakilishi wa pekee wa Ndugu Russell wakati alipokuwa ameenda, na alituambia sisi sote tufanye yale unayotuambia. Sasa, alienda na hakurudi. Inaonekana ni wewe utaendeleza kazi hii.” Ndugu Macmillan akajibu: “Ndugu, hupaswi kufikiria mambo hayo hivyo. Hii ni kazi ya Bwana na wadhifa pekee unaopokea katika tengenezo la Bwana ni ule ambao Bwana anaona unafaa akupe; na nina hakika mimi sistahili kufanya kazi hiyo.” Kisha Ndugu Macmillan akapendekeza mtu mwingine achukue wadhifa huo. Kama Gideoni, yeye alikuwa na maoni yenye kiasi juu yake mwenyewe—na ni vizuri tusitawishe maoni kama hayo.

15. Tunaweza kutumia ufahamu katika njia zipi zinazofaa tunapowahubiria wengine?

15 Sisi pia tunapaswa kuwa wenye kiasi katika njia ambayo tunatekeleza mgawo wetu. Gideoni alikuwa mwenye busara, na alijaribu kutowakasirisha wapinzani wake bila sababu. Vivyo hivyo, katika kazi yetu ya kuhubiri, tunapaswa kuwa wenye kiasi na wenye busara kuhusu jinsi tunavyozungumza na wengine. Ni kweli kwamba tunapigana vita ya kiroho ya kupindua “mambo yaliyotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki” na “mawazowazo.” (2 Wakorintho 10:4, 5) Lakini hatupaswi kuzungumza kwa kuwadharau wengine au kuwafanya wawe na sababu yoyote halali ya kuudhika na ujumbe wetu. Badala yake, ni lazima tustahi maoni yao, tukazie mambo tunayokubaliana nao, kisha tuzingatie mambo yafaayo ya ujumbe wetu.—Matendo 22:1-3; 1 Wakorintho 9:22; Ufunuo 21:4.

Yesu—Mfano Bora wa Kuonyesha Kiasi

16. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa na maoni ya kiasi juu yake mwenyewe?

16 Yesu Kristo ni mfano bora wa mtu mwenye kiasi. * Licha ya uhusiano wa karibu sana na Baba yake, Yesu hakusita kukiri kwamba hakuwa na mamlaka juu ya mambo mengine. (Yohana 1:14) Kwa mfano, mama ya Yakobo na Yohana alipoomba kwamba wana wake wawili waketi kando ya Yesu katika ufalme wake, Yesu alisema: “Huku kuketi kwenye mkono wangu wa kuume na kwenye mkono wangu wa kushoto si kwangu mimi kutoa.” (Mathayo 20:20-23) Pindi nyingine, Yesu alikiri waziwazi hivi: “Mimi siwezi kufanya kitu chochote kwa uanzisho wangu . . . natafuta sana, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi yake aliyenituma mimi.”—Yohana 5:30; 14:28; Wafilipi 2:5, 6.

17. Yesu alionyeshaje kiasi aliposhughulika na wengine?

17 Kwa kila njia, Yesu alikuwa mkuu kuliko wanadamu wasiokamilika, na Yehova Baba yake alimpa mamlaka kubwa kuliko mwanadamu yeyote yule. Lakini, Yesu alishughulika na wafuasi wake kwa kiasi. Yeye hakuwalemea kwa wonyesho mkubwa wa ujuzi mwingi. Aliwajali wengine na kuwaonea huruma naye aliyafikiria mahitaji yao ya kibinadamu. (Mathayo 15:32; 26:40, 41; Marko 6:31) Kwa hiyo, ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, yeye hakuwa mwenye kudai ukamilifu kwa wengine. Yeye hakuwataka wanafunzi wake wafanye mengi zaidi ya uwezo wao, wala hakuwapa mambo ambayo wasingeweza kuyahimili. (Yohana 16:12) Si ajabu kwamba aliwaburudisha wengi!—Mathayo 11:29.

Iga Mfano wa Yesu wa Kiasi

18, 19. Tunaweza kuigaje kiasi cha Yesu kwa (a) jinsi tunavyojiona, na (b) jinsi tunavyowatendea wengine?

18 Ikiwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi alionyesha kiasi, namna gani sisi. Mara nyingi wanadamu wasiokamilika hawakubali kwa urahisi kwamba hawana mamlaka kamili. Lakini, kwa kumwiga Yesu, Wakristo hujitahidi kuwa wenye kiasi. Wao si wenye kiburi mno wasiwape madaraka wale ambao wamestahili kuyapokea; wala wao si wenye kujivuna na wasiotaka kukubali mwelekezo kutoka kwa wale ambao wamepewa mamlaka. Wakionyesha roho ya kushirikiana, wao huacha mambo yote kutanikoni yatendeke kwa “adabu na kwa mpango.”—1 Wakorintho 14:40.

19 Pia sifa ya kiasi itatufanya tuyafikirie mahitaji ya wengine na kutokuwa wenye kudai mno katika mambo tunayowatarajia wafanye. (Wafilipi 4:5) Huenda tukawa na uwezo fulani na nguvu fulani ambazo huenda wengine hawana. Lakini, tukiwa wenye kiasi, hatutawatarajia wengine sikuzote wafanye mambo kama ambavyo tungependa wafanye. Tukijua kwamba kila mtu ana udhaifu wake, tutaonyesha sifa ya kiasi kwa kutozingatia kasoro za wengine. Petro aliandika: “Juu ya mambo yote, iweni na upendo wenye juhudi nyingi nyinyi kwa nyinyi, kwa sababu upendo hufunika wingi wa dhambi.”—1 Petro 4:8.

20. Tunaweza kufanya nini ili kushinda mwelekeo wowote wa kukosa kiasi?

20 Kama ambavyo tumejifunza, kwa kweli hekima i pamoja na wenye kiasi. Lakini, namna gani ukitambua kwamba una mielekeo ya kukosa kiasi au ya kuwa na kimbelembele? Usivunjike moyo. Badala yake, fuata mfano wa Daudi, aliyesali hivi: “Umzuie mtumishi wako asitende mambo ya kiburi [“kimbelembele,” NW], yasinitawale mimi.” (Zaburi 19:13) Kwa kuiga imani ya watu kama Paulo, Gideoni, na—zaidi ya wote—Yesu Kristo, sisi binafsi tutaona ukweli wa maneno haya: “Hekima i pamoja na wenye kiasi.”—Mithali 11:2, NW.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “walio chini” linaweza kurejezea mtumwa ambaye alipiga makasia katika sehemu ya chini ya meli kubwa. Kwa kutofautisha, huenda “wasimamizi-nyumba” wakakabidhiwa mapendeleo zaidi, labda ya kutunza nyumba nyingi. Hata hivyo, machoni pa wakubwa wengi, msimamizi-nyumba alipaswa kuwa mtiifu kama tu mtumwa mwenye kupiga makasia katika sehemu ya chini ya meli.

^ fu. 12 Busara na tahadhari za Gideoni hazipasi kuonwa kuwa woga. Badala yake, ujasiri wake unathibitishwa na andiko la Waebrania 11:32-38, ambapo Gideoni ameorodheshwa miongoni mwa watu ‘waliofanywa kuwa wenye nguvu’ na ‘kuwa mashujaa katika vita.’

^ fu. 16 Kwa kuwa sifa ya kiasi hutia ndani kutambua udhaifu wako, Yehova hawezi kusemwa kwa haki kuwa mwenye kiasi. Lakini yeye ni mnyenyekevu.—Zaburi 18:35.

Je, Wakumbuka?

• Kiasi ni nini?

• Tunaweza kuigaje sifa ya Paulo ya kiasi?

• Tunaweza kujifunza nini kuhusu kiasi kutokana na mfano wa Gideoni?

• Yesu aliwekaje mfano bora wa kiasi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sifa ya Paulo ya kiasi ilimfanya apendwe na Wakristo wenzake

[Picha katika ukurasa wa 17]

Gideoni alitumia busara kutekeleza mapenzi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu, Mwana wa Mungu, huonyesha kiasi katika mambo yote ayafanyayo