Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Inakosekana?

Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Inakosekana?

Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Inakosekana?

“Huenda siku moja kukaidi mamlaka iliyosimamishwa, iwe ya kidini au ya kilimwengu, ya kijamii au ya kisiasa, ambako kunatukia ulimwenguni pote, kukaonekana kuwa tukio lenye kutokeza la mwongo uliopita.”

MIAKA imepita tangu miaka ya 1960, mwongo ambao umetajwa hapo juu na mwanahistoria na mwanafalsafa, Hannah Arendt. Leo mwelekeo wa kutoheshimu mamlaka waendelea kuimarika hata zaidi.

Kwa mfano, ripoti moja ya karibuni katika gazeti la The Times la London ilisema hivi: “Wazazi fulani hawamruhusu mwalimu awe na mamlaka juu ya mtoto wao na anapojaribu kumtia nidhamu wazazi hao hulalamika.” Mara nyingi, watoto wao wanapotiwa nidhamu shuleni, wazazi huenda huko si kuwatisha walimu tu bali pia kuwashambulia.

Msemaji wa Shirika la Taifa la Walimu Wakuu nchini Uingereza amenukuliwa akisema: “Watu wanasema ‘Nina haki,’ badala ya kusema ‘Nina wajibu.’” Wazazi wengine hawafundishi watoto wao kuwa na heshima ifaayo kwa mamlaka wala hawawatii nidhamu—nao hawataki watu wengine wafanye hivyo. Watoto wanaodai “haki” zao huachwa wapuuze mamlaka ya wazazi na ya walimu pia, na matokeo yanaweza kutabirika—“kizazi kipya kisichoheshimu mamlaka na kisichojua lililo jema na lililo baya,” aandika mwandishi wa magazeti Margarette Driscoll.

Gazeti la Time katika makala yake ya “Kizazi Kilichopotoka” lilibainisha jinsi ambavyo vijana wengi Warusi wamekata tamaa lilipomnukuu mwimbaji wa rapu anayependwa sana ambaye alisema: “Mtu aliyezaliwa katika ulimwengu huu, ambamo hakuna chochote kinachodumu wala haki yoyote, anawezaje kuitumaini jamii?” Mwanasoshiolojia Mikhail Topalov alikubaliana na maoni hayo kwa kusema: “Vijana hawa si wapumbavu. Wameona wazazi wao wakidanganywa na serikali, wamewaona wakipoteza akiba zao na kazi zao. Je, tunaweza kuwatazamia waheshimu mamlaka?”

Hata hivyo, ingekuwa makosa kukata kauli kwamba vijana tu ndio wasiotumaini mamlaka. Leo, watu wa umri wote hawatumaini wala hawaheshimu mamlaka yoyote ile. Je, hilo lamaanisha kwamba hatuwezi kutumaini mamlaka yoyote? Yakitumiwa ifaavyo, mamlaka ambayo hufafanuliwa kuwa “uwezo au haki ya kudhibiti, kuhukumu, au kukataza vitendo vya wengine,” yanaweza kunufaisha. Yanaweza kumnufaisha mtu mmoja-mmoja na jumuiya pia. Makala ifuatayo itazungumzia jinsi ambavyo mamlaka hunufaisha.