Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?

Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?

Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?

NI NANI asiyeshukuru kwamba polisi wana mamlaka ya kukamata wahalifu ambao huiba mali yetu au kutisha familia yetu? Na je, hatuthamini kwamba mahakama zina mamlaka ya kuadhibu wahalifu ili kuilinda jumuiya?

Tunaweza pia kukumbuka huduma nyinginezo zinazonufaisha umma, kama vile kutengeneza barabara, usafi, na elimu, ambazo hugharimiwa kwa kodi zinazotozwa na serikali. Wakristo wa kweli wanakubali kabisa kwamba ni muhimu kuheshimu mamlaka iliyowekwa rasmi. Lakini wanaheshimu mamlaka kwa kadiri gani? Na mamlaka yapasa kuheshimiwa katika sehemu gani za maisha?

Mamlaka Katika Jumuiya

Biblia huwaambia watu wote, wawe waamini au wasiwe waamini, waheshimu mamlaka ya serikali, ambayo huinufaisha jumuiya. Mtume Mkristo Paulo aliwaandikia waamini wenzake huko Roma kuhusu jambo hilo, na inafaa kufikiria anayosema, kama ilivyoandikwa kwenye Waroma 13:1-7.

Paulo alikuwa raia wa Roma ambayo ilikuwa serikali ya ulimwengu wakati huo. Barua ya Paulo iliyoandikwa wapata mwaka wa 56 W.K., iliwashauri Wakristo wawe raia wenye mfano mzuri. Aliandika: “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka ila kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.”

Paulo hapa anaeleza kwamba hakungekuwako mamlaka yoyote ya kibinadamu kama Mungu hangeiruhusu iweko. Kulingana na maoni hayo mamlaka zilizo kubwa zina cheo chenye kuhusu katika kusudi la Mungu. Basi “yeye aipingaye mamlaka amechukua msimamo dhidi ya mpango wa Mungu.”

Ingawa huenda raia wanaofanya mema wakasifiwa na mamlaka zilizo kubwa, mamlaka hizo pia zimeidhinishwa kuadhibu wakosaji. Wanaotenda mabaya wana sababu nzuri ya kuhofu haki ya mamlaka hizo ya kuchukua hatua zikiwa “mlipiza-kisasi,” kwa kuwa serikali hufanya hivyo zikiwa “mhudumu wa Mungu.”

Paulo amalizia kutoa hoja zake kwa kusema: “Kuna sababu yenye kushurutisha nyinyi watu kuwa katika ujitiisho, si kwa sababu ya hasira hiyo ya kisasi tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu. Kwa maana hiyo ndiyo sababu mnalipa kodi pia; kwa maana wao ni watumishi wa Mungu wa watu wote wakitumikia daima kwa kusudi hilihili.”

Mamlaka zilizo kubwa ndizo zilizo na wajibu wa kujua kodi itatumiwaje, wala si mlipa-kodi. Akiwa raia mnyofu, Mkristo anadumisha dhamiri safi. Anajua kwamba akijitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa na kulipa kodi anazodaiwa, anazingatia viwango vya jumuiya anakoishi na pia anaishi kulingana na matakwa ya Mungu.

Familia na Mamlaka

Namna gani mamlaka katika familia? Mtoto mchanga anapotaka kuangaliwa, mara nyingi hulia au hata kupiga yowe. Lakini mzazi mwenye hekima atatambua mahitaji ya kweli ya mtoto na hataruhusu hasira za ghafula za mtoto zitawale. Baadhi ya watoto, wanapokuwa na umri mkubwa kidogo, huachiliwa wafanye watakavyo na kuruhusiwa wajiwekee viwango vyao wenyewe. Kwa kuwa wanakosa maarifa, wanaweza kufanya uhalifu au makosa mengine na kuvuruga familia na jumuiya kwa ujumla, mambo ambayo wenye mamlaka mitaani wanajua vizuri.

“Wazazi huwatia watoto wao nidhamu wakiwa wamechelewa mno,” asema Rosalind Miles, mtungaji wa kichapo Children We Deserve. “Unaanza wakati mtoto anapozaliwa.” Ikiwa tangu pale mwanzo wazazi wanaongea kwa mamlaka yenye fadhili na yenye kujali na wanakuwa thabiti katika yale wafanyayo, muda si muda watoto wao watajifunza kukubali mamlaka yao na nidhamu yenye upendo wanayotoa.

Biblia ina habari nyingi sana kuhusu mamlaka ya familia. Katika kitabu cha Mithali, Solomoni mwenye hekima akazia muungano wa wazazi wanaomhofu Mungu mbele ya watoto wao, akisema: “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Mithali 1:8) Wazazi wadumishapo muungano wa aina hiyo, ulio wa kiasi mbele ya watoto wao, watoto hujua msimamo wa wazazi wao. Huenda wakajaribu kuwagonganisha wazazi katika jitihada za kufanya wanavyotaka, lakini muungano wa wazazi katika mamlaka ni ulinzi kwa vijana.

Biblia yasema kwamba mume ndiye mwenye wajibu mkubwa zaidi kuhusiana na hali njema ya kiroho ya watoto wake na mke wake pia. Wajibu huo huitwa ukichwa. Ukichwa huo wapaswa kutumiwaje? Paulo aonyesha kwamba kama vile Yesu alivyo Kichwa cha kutaniko ndivyo mwanamume alivyo kichwa cha mke wake. Kisha Paulo aendelea kusema: “Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujikabidhi mwenyewe kwa ajili yalo.” (Waefeso 5:25) Mwanamume anapofuata kielelezo cha Yesu na kutumia ukichwa kwa njia ya upendo, atapata “staha yenye kina kirefu” ya mke wake. (Waefeso 5:33) Watoto katika jamaa kama hiyo wataona pia manufaa ya mamlaka kutoka kwa Mungu na watatiwa moyo kuyakubali.—Waefeso 6:1-3.

Wazazi wasio na wenzi, kutia ndani wale ambao wamefiwa na wenzi, wanaweza kukabilianaje na suala hilo? Mzazi, awe mama au baba, anaweza kutegemea moja kwa moja mamlaka ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. Sikuzote Yesu alisema kwa mamlaka ya Baba yake na ya Maandiko yaliyopuliziwa.—Mathayo 4:1-10; 7:29; Yohana 5:19, 30; 8:28.

Biblia ina kanuni nyingi nzuri zinazohusu matatizo ambayo watoto hukabili. Kwa kuzijua kanuni hizo na kuzifuata, mzazi ataweza kutoa ushauri wenye upendo unaowafaa watoto wake. (Mwanzo 6:22; Mithali 13:20; Mathayo 6:33; 1 Wakorintho 15:33; Wafilipi 4:8, 9) Wazazi wanaweza pia kurejezea habari zinazotegemea Biblia ambazo zimekusudiwa hasa kuwasaidia wawazoeze watoto wao waelewe manufaa ya kuheshimu mamlaka ya Maandiko. *

Kutaniko la Kikristo na Mamlaka

“Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye mimi nimemkubali; msikilizeni yeye.” (Mathayo 17:5) Maneno hayo, yaliyosemwa na Yehova Mungu mwenyewe, yalithibitisha kwamba Yesu husema kwa mamlaka ya Mungu. Aliyosema yameandikwa katika masimulizi ya Gospeli nne ambazo tunaweza kuzirejezea kwa urahisi.

Kabla ya kupaa mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Akiwa Kichwa cha kutaniko lake, Yesu amewalinda watiwa-mafuta wake ambao hufuata hatua zake duniani na, tangu kumwagwa kwa roho takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K., amewatumia pia kujulisha kweli, wakiwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47; Matendo 2:1-36) Amefanya nini kutimiza hayo yote ili kuliimarisha kutaniko la Kikristo? “Alipopaa juu . . . , alitoa zawadi [zikiwa] wanadamu.” (Waefeso 4:8) ‘Zawadi hizo za wanadamu’ ni wazee Wakristo wanaowekwa rasmi na roho takatifu na wanaopewa mamlaka ya kushughulikia masilahi ya kiroho ya waamini wenzao.—Matendo 20:28.

Kwa sababu hiyo Paulo ashauri: “Kumbukeni wale ambao wanaongoza miongoni mwenu, ambao wamelisema neno la Mungu kwenu, nanyi mfikiriapo jinsi mwisho wa mwenendo wao upatavyo kuwa, igeni imani yao.” Kwa kuwa wanaume hawa waaminifu hufuata hatua za Yesu kwa makini, bila shaka ni jambo la hekima kuiga imani yao. Paulo aendelea kusema: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea, [“mkitambua daima mamlaka yao juu yenu,” The Amplified Bible] kwa maana wao wanafuliza kulinda juu ya nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wapate kufanya hili kwa shangwe na si kwa kutweta, kwa maana hili lingekuwa lenye hasara kwenu.”—Waebrania 13:7, 17.

Inakuwaje mwongozo huo unapopuuzwa? Baadhi ya washiriki wa kutaniko la Kikristo la mapema walifanya hivyo, wakawa waasi-imani. Himenayo na Fileto wanatajwa kuwa watu waliopindua imani ya wengine na ambao semi zao tupu ‘zilihalifu lililo takatifu.’ Walisisitiza kwamba ufufuo tayari ulikuwa umetokea, yaonekana ufufuo wa kiroho au wa mfano, kwa hiyo hakungekuwa na ufufuo mwingine wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu.—2 Timotheo 2:16-18.

Mamlaka iliyowekwa rasmi ilitoa msaada. Wazee Wakristo waliweza kukanusha hoja hizo kwa kuwa wakiwa wawakilishi wa Yesu Kristo, walitumia mamlaka ya Maandiko. (2 Timotheo 3:16, 17) Ndivyo hali ilivyo leo katika kutaniko la Kikristo ambalo hufafanuliwa kuwa “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Mafundisho ya uwongo hayataruhusiwa tena kuharibu “kiolezo cha maneno yenye afya,” ambayo yamehifadhiwa kwa ajili yetu yakiwa amana nzuri katika Biblia.—2 Timotheo 1:13, 14.

Ingawa kuheshimu mamlaka kunaendelea kudidimia kwa haraka ulimwenguni, sisi tukiwa Wakristo tunatambua kwamba mamlaka zifaazo katika jumuiya, katika familia, na katika kutaniko la Kikristo zimewekwa kwa manufaa yetu. Kuheshimu mamlaka ni muhimu ili hali yetu ya kimwili, kihisia-moyo, na kiroho iwe njema. Kwa kukubali na kuheshimu mamlaka hiyo itokayo kwa Mungu, tutalindwa na mamlaka zilizo kubwa zaidi—Yehova Mungu na Yesu Kristo—na kunufaika milele.—Zaburi 119:165; Waebrania 12:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Ona vitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na Siri ya Kupata Furaha ya Familia, vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Biblia ina habari nyingi sana kuhusu mamlaka ya familia

[Picha katika ukurasa wa 6]

Wazazi wasio na wenzi wanaweza kutegemea moja kwa moja mamlaka ya Yehova Mungu na Yesu Kristo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wakristo hutambua kwamba mamlaka zifaazo katika familia, katika kutaniko la Kikristo, na katika jumuiya zimewekwa kwa manufaa yao

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Photo by Josh Mathes, Collection of the Supreme Court of the United States