Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kimbelembele Hutokeza Aibu

Kimbelembele Hutokeza Aibu

Kimbelembele Hutokeza Aibu

“Je, kimbelembele kimekuja? Basi aibu itakuja; lakini hekima i pamoja na wenye kiasi.”—MITHALI 11:2, NW.

1, 2. Kimbelembele ni nini, na kimetokeza misiba katika njia zipi?

MLAWI mmoja mwenye husuda aongoza umati wenye kuasi dhidi ya watu waliopewa mamlaka na Yehova. Mwana-mfalme mmoja mwenye tamaa ya makuu atunga hila ya kunyakua utawala wa babake. Mfalme asiye na subira apuuza maagizo ya wazi ya nabii wa Mungu. Waisraeli hao watatu walikuwa na sifa moja: kimbelembele.

2 Kimbelembele ni tabia ya moyoni ambayo ni tisho kubwa kwa wote. (Zaburi 19:13) Mtu mwenye kimbelembele huamua tu kufanya mambo bila kibali. Mara nyingi kufanya hivyo hutokeza msiba. Kimbelembele hata kimewaangamiza wafalme na kuangusha milki nyingi. (Yeremia 50:29, 31, 32; Danieli 5:20) Kimbelembele hata kimewanasa watumishi fulani wa Yehova na kuwaangamiza.

3. Tunaweza kujifunzaje hatari za kuwa wenye kimbelembele?

3 Biblia ina sababu nzuri inaposema: “Je, kimbelembele kimekuja? Basi aibu itakuja; lakini hekima i pamoja na wenye kiasi.” (Mithali 11:2, NW) Biblia inatupa mifano inayothibitisha ukweli wa mithali hiyo. Kuchunguza baadhi ya mifano hiyo kutatusaidia kuona hatari ya kuvuka mipaka iliyowekwa. Basi, ebu tuchunguze jinsi husuda, tamaa ya makuu, na kukosa subira kulivyowafanya wale watu watatu waliotajwa hapo mwanzoni watende kwa kimbelembele, na kuaibika.

Kora—Mwasi Mwenye Husuda

4. (a) Kora alikuwa nani, na yaelekea alishiriki katika matukio gani makuu? (b) Katika miaka yake ya baadaye, Kora alichochea tendo gani baya?

4 Kora alikuwa Mlawi wa Kohathi na pia binamu ya Musa na Aroni. Inaonekana kwamba alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova kwa miaka mingi. Kora alikuwa na pendeleo la kuwa miongoni mwa wale waliookolewa kimuujiza walipovuka Bahari Nyekundu, na yaelekea alishiriki kutekeleza hukumu ya Yehova dhidi ya Waisraeli walioabudu ndama kwenye Mlima Sinai. (Kutoka 32:26) Lakini, hatimaye Kora aliongoza maasi dhidi ya Musa na Aroni, maasi ambayo yaliwahusisha Dathani, Abiramu, na Oni, wa kabila la Reubeni, pamoja na wakuu 250 wa Israeli. * “Ninyi inawatosha,” wakamwambia Musa na Aroni, “kwa kuwa mkutano wote ni mtakatifu, kila mmoja miongoni mwao, BWANA naye yu kati yao; n’nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa BWANA?”—Hesabu 16:1-3.

5, 6. (a) Kwa nini Kora aliasi dhidi ya Musa na Aroni? (b) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba yaelekea Kora hakuthamini mahali pake katika mpango wa Mungu?

5 Kwa nini Kora aliasi baada ya kuwa mwaminifu kwa miaka mingi? Hakika Musa hakuongoza Israeli kwa dhuluma, kwa sababu “alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Hata hivyo, inaonekana Kora aliwahusudu Musa na Aroni na kuchukia umashuhuri wao, na hilo likamfanya aseme—isivyo kweli—kwamba walikuwa wamejitukuza kwa ubinafsi juu ya mkutano.—Zaburi 106:16.

6 Yaelekea tatizo moja la Kora ni kwamba hakuthamini mapendeleo yake mwenyewe katika mpango wa Mungu. Ni kweli kwamba Walawi wa Kohathi hawakuwa makuhani, lakini walikuwa walimu wa Sheria ya Mungu. Pia walibeba vyombo vya tabenakulo wakati vyombo hivyo vilipohitaji kusafirishwa. Huo ulikuwa mgawo mkubwa, kwa sababu vyombo hivyo vitakatifu vilipasa kubebwa tu na watu safi kidini na kiadili. (Isaya 52:11) Hivyo, Musa alipomkabili Kora, ni kama alikuwa akimwuliza, Je, unaona mgawo wako kuwa kitu kidogo sana hivi kwamba ni lazima pia uwe kuhani? (Hesabu 16:9, 10) Kora hakutambua kwamba heshima kubwa zaidi ni kumtumikia Yehova kwa uaminifu kulingana na mpango wake—wala si kupata hadhi au cheo fulani cha kipekee.—Zaburi 84:10.

7. (a) Musa alishughulikaje na Kora na wafuasi wake? (b) Maasi ya Kora yalimalizwaje kwa msiba?

7 Musa akawaambia Kora na watu wake wakusanyike kwenye hema la kukutania kesho yake asubuhi wakiwa na chetezo na uvumba. Kora na wafuasi wake hawakuruhusiwa kufukiza uvumba kwa sababu hawakuwa makuhani. Kama wangekuja na chetezo na uvumba, ingekuwa wazi kwamba watu hao bado waliona wana haki ya kuwa makuhani—hata baada ya kuwa na fursa ya kulifikiria jambo hilo usiku kucha. Walipojitokeza asubuhi iliyofuata, kwa haki Yehova alionyesha hasira yake ya kisasi. Kwa habari ya wana wa Reubeni, ‘nchi ilifunua kinywa chake, ikawameza.’ Waliosalia, kutia ndani Kora, waliteketezwa kwa moto kutoka kwa Mungu. (Kumbukumbu la Torati 11:6; Hesabu 16:16-35; 26:10) Kimbelembele cha Kora kilimfanya apate aibu hatimaye—akakataliwa na Mungu!

Kinza “Mwelekeo wa Kuhusudu”

8. “Mwelekeo wa kuhusudu” unaweza kujitokezaje miongoni mwa Wakristo?

8 Simulizi hilo la Kora ni onyo kwetu. Kwa kuwa “mwelekeo wa kuhusudu” umo katika wanadamu wasiokamilika, unaweza kujitokeza hata katika kutaniko la Kikristo. (Yakobo 4:5) Kwa mfano, huenda ikawa tunatamani wadhifa. Kama Kora, huenda tukawahusudu wale ambao wana mapendeleo tunayotamani. Au huenda tukawa kama yule Mkristo wa karne ya kwanza aitwaye Diotrefesi. Alichambua sana mamlaka ya mitume, kwa sababu inaonekana alitaka kuongoza. Yohana akaandika kwamba Diotrefesi “hupenda kuwa na mahali pa kwanza.”—3 Yohana 9.

9. (a) Tunahitaji kuepuka mtazamo gani kuhusu mapendeleo katika kutaniko? (b) Ni maoni gani yanayofaa kuhusu fungu letu katika mpango wa Mungu?

9 Si vibaya kwa mwanamume Mkristo kujitahidi kufikilia mapendeleo katika kutaniko. Paulo hata alipendekeza jambo hilo. (1 Timotheo 3:1) Lakini, hatupaswi kuona mapendeleo ya utumishi kuwa ishara ya kwamba tumestahili heshima fulani, kana kwamba kwa kuyapata, tumepanda kile kiitwacho eti cheo cha ukubwa. Kumbuka kwamba Yesu alisema: “Yeyote yule atakaye kuwa wa kwanza miongoni mwenu lazima awe mtumwa wenu.” (Mathayo 20:26, 27) Ni wazi kwamba si vizuri kuwahusudu wale ambao wana madaraka zaidi, kana kwamba thamani yetu mbele za Mungu hutegemea “cheo” tulicho nacho katika tengenezo lake. Yesu alisema: “Nyinyi nyote ni akina ndugu.” (Mathayo 23:8) Ndiyo, tuwe wahubiri au mapainia, tuwe tumebatizwa majuzi au tuwe washika uaminifu-maadili wa muda mrefu—sote tunaomtumikia Yehova kwa moyo wote tunathaminiwa katika mpango wake. (Luka 10:27; 12:6, 7; Wagalatia 3:28; Waebrania 6:10) Ni baraka kwelikweli kufanya kazi bega kwa bega na mamilioni ya watu ambao wanajaribu kufuata shauri hili la Biblia: “Jifungeni hali ya akili ya kujishusha chini kuelekea mtu na mwenzake.”—1 Petro 5:5.

Absalomu—Laghai Mwenye Tamaa ya Makuu

10. Absalomu alikuwa nani, na alijaribuje kujipendekeza kwa wale waliokuwa wakimwendea mfalme ili wapate hukumu?

10 Maisha ya mwana wa tatu wa Mfalme Daudi, Absalomu, yanatupa somo kuhusu tamaa ya makuu. Mwana huyo laghai na mwenye hila alijaribu kujipendekeza kwa watu ambao walikuwa wakimwendea mfalme ili wapate hukumu. Kwanza alidokeza kwamba Daudi hakujali mahitaji yao. Kisha akaacha ujanja na kutaja waziwazi kusudi lake. “Laiti mimi ningewekwa kuwa mwamuzi katika nchi hii,” Absalomu akasema, “ili kila mtu mwenye neno au dawa aje kwangu, nimpatie haki yake!” Absalomu alitumia ujanja mwingi sana. “Alipokaribia mtu ye yote kumsujudia,” Biblia inasema, “hunyosha mkono wake, na kumshika, na kumbusu. Hivyo ndivyo Absalomu alivyowatendea Israeli wote, waliomwendea mfalme ili wapate hukumu.” Matokeo yakawa nini? “Absalomu akawadanganya watu wa Israeli.”—2 Samweli 15:1-6.

11. Absalomu alijaribuje kunyakua ufalme wa Daudi?

11 Absalomu aliazimia kunyakua utawala wa babake. Miaka mitano awali, aliagiza mwana mkubwa wa Daudi, Amnoni, auawe eti alipize kisasi kwa sababu ya kubakwa kwa dadake, Tamari. (2 Samweli 13:28, 29) Lakini, huenda hata wakati huo Absalomu alikuwa akitamani kiti cha ufalme, akiona kumwua Amnoni kuwa njia nzuri ya kuondoa mpinzani. * Kwa vyovyote vile, wakati ulipowadia, Absalomu alichukua hatua. Akaagiza itangazwe kotekote nchini kwamba amekuwa mfalme.—2 Samweli 15:10.

12. Eleza jinsi kimbelembele cha Absalomu kilivyomwaibisha.

12 Kwa muda fulani, Absalomu alifanikiwa, kwa kuwa “fitina yao ikawa na nguvu; maana watu waliokuwa pamoja na Absalomu wakazidi kuwa wengi.” Baada ya muda, Mfalme Daudi alilazimika kutoroka ili kuokoa uhai wake. (2 Samweli 15:12-17) Lakini punde tu baadaye, maasi ya Absalomu yakakatizwa alipouawa na Yoabu, akatupwa shimoni, na kufunikwa kwa mawe. Ebu wazia—mtu huyo mwenye tamaa ya makuu aliyetaka kuwa mfalme hata hakuzikwa kwa heshima alipokufa! * Kwa kweli kimbelembele kilimfanya Absalomu apate aibu.—2 Samweli 18:9-17.

Epuka Tamaa ya Makuu Yenye Ubinafsi

13. Roho ya kutamani makuu inaweza kukuaje katika moyo wa Mkristo?

13 Kuinuka kwa Absalomu kunyakua ufalme na kuanguka kwake kunatufundisha somo fulani. Katika ulimwengu wa leo wenye ushindani mkali, ni kawaida kwa watu kuwarairai wakubwa wao, wakijipendekeza kwao ili tu waonekane au labda wapate pendeleo fulani au kupandishwa cheo. Wakati uo huo, wanaweza kujisifu kwa wale walio chini yao, wakitumaini kupata upendeleo wao na kuungwa mkono. Tusipojihadhari, roho hiyo ya kutamani makuu inaweza kukua katika mioyo yetu. Inaonekana jambo hilo lilitokea miongoni mwa wengine katika karne ya kwanza, ikiwalazimu mitume wawaonye vikali.—Wagalatia 4:17; 3 Yohana 9, 10.

14. Kwa nini tuepuke roho ya kutamani makuu na ya kujitukuza?

14 Yehova hataki katika tengenezo lake watu wenye kujitutumua na wenye hila wanaojaribu ‘kutafuta utukufu wao wenyewe.’ (Mithali 25:27) Hata Biblia inaonya hivi: “BWANA ataikata midomo yote ya kujipendekeza, nao ulimi unenao maneno ya kiburi [“makuu,” NW].” (Zaburi 12:3) Absalomu alikuwa na midomo ya kujipendekeza. Aliwarairai wale aliotaka kujipendekeza kwao—ili tu apate mamlaka aliyotamani sana. Kinyume cha hali hiyo, sisi tumebarikiwa kama nini kuwa miongoni mwa udugu ambao hufuata shauri hili la Paulo: “[Msifanye] jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini mkifikiria kwamba wengine ni wakubwa kuliko nyinyi.”—Wafilipi 2:3.

Sauli—Mfalme Asiye na Subira

15. Pindi moja Sauli alijionyeshaje kuwa mwenye kiasi?

15 Pindi moja Sauli, ambaye baadaye alipata kuwa mfalme wa Israeli, alikuwa mtu mwenye kiasi. Kwa mfano, ebu fikiria jambo lililotendeka alipokuwa angali kijana. Samweli, nabii wa Mungu, aliposema maneno mazuri kumhusu, Sauli alijibu hivi kwa unyenyekevu: “Je! mimi si Mbenyamini, mtu wa kabila iliyo ndogo kuliko kabila zote za Israeli? na jamaa yangu nayo si ndogo kuliko jamaa zote za kabila la Benyamini? Kwa nini basi, kuniambia hivyo?”—1 Samweli 9:21.

16. Ni katika njia gani Sauli alikosa subira?

16 Lakini, baadaye Sauli akakosa kuwa mwenye kiasi. Alipokuwa akipigana na Wafilisti, alirudi Gilgali, ambako alitazamiwa amngojee Samweli aje amsihi Mungu kwa dhabihu. Samweli alipochelewa kufika kwa wakati uliopangwa, kwa kimbelembele Sauli mwenyewe akatoa dhabihu ya kuteketezwa. Alipomaliza tu, Samweli akafika. “Umefanya nini?” Samweli akamwuliza. Sauli akajibu: “Ni kwa sababu naliona ya kuwa watu wanatawanyika mbali nami, na wewe hukuja siku zile zilizonenwa . . . Kwa hiyo nalijishurutisha, nikatoa sadaka ya kuteketezwa.”—1 Samweli 13:8-12.

17. (a) Ukitazama kijuujuu tu, kwa nini matendo ya Sauli huenda yakaonekana kuwa yalifaa? (b) Kwa nini Yehova alimkemea Sauli kwa kukosa subira?

17 Ukitazama kijuujuu tu, huenda matendo ya Sauli yakaonekana kuwa yalifaa. Kwani, watu wa Mungu walikuwa “katika dhiki,” na ‘kufadhaishwa,’ wakitetemeka kwa sababu ya hali mbaya waliyokabili. (1 Samweli 13:6, 7) Si vibaya kuchukua hatua ikihitajika. * Lakini, kumbuka kwamba Yehova anaweza kusoma mioyo na kutambua nia zetu za ndani kabisa. (1 Samweli 16:7) Kwa hiyo, huenda aliona mambo fulani kuhusu Sauli ambayo hayatajwi moja kwa moja katika masimulizi hayo ya Biblia. Kwa mfano, huenda Yehova aliona kwamba Sauli alikosa subira kwa sababu ya kiburi. Labda Sauli alikasirika sana kwamba yeye—mfalme wa Israeli yote—ati amngoje mtu ambaye alimwona kuwa nabii aliyezeeka, mwenye kuchelewa-chelewa! Kwa vyovyote vile, Sauli alihisi kwamba kuchelewa kwa Samweli kulimpa haki ya kujifanyia mambo mwenyewe na kupuuza maagizo ya wazi ambayo alikuwa amepewa. Matokeo yakawaje? Samweli hakumsifu Sauli kwa hatua aliyochukua. Badala yake, alimkemea akisema: “Ufalme wako hautadumu . . . kwa sababu wewe hukulishika neno lile BWANA alilokuamuru.” (1 Samweli 13:13, 14) Kwa mara nyingine tena, kimbelembele kilitokeza aibu.

Jihadhari Usije Ukakosa Subira

18, 19. (a) Eleza jinsi kukosa subira kunavyoweza kumfanya mtumishi wa Mungu wa wakati huu atende kwa kimbelembele. (b) Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu utendaji wa kutaniko la Kikristo?

18 Masimulizi ya tendo la kimbelembele la Sauli limeandikwa katika Neno la Mungu kwa manufaa yetu. (1 Wakorintho 10:11) Ni rahisi sana tukasirikie kutokamilika kwa ndugu zetu. Kama Sauli, huenda tukakosa subira, tukihisi kwamba tukitaka mambo yafanywe vizuri, ni lazima tuyafanye sisi wenyewe. Kwa mfano, tuseme ndugu fulani ana ustadi mkubwa wa kufanya mambo fulani kwa utaratibu. Hachelewi kufanya mambo, anajua vizuri jinsi mambo yanavyopasa kufanywa kutanikoni, na ana kipawa cha kusema na kufundisha. Vilevile anatambua kwamba wengine si waangalifu kama yeye, na kamwe hawafanyi mambo kwa njia bora kama ambavyo angependa. Je, hiyo imfanye akose subira? Je, awachambue ndugu zake, labda akidokeza kwamba kama si kwa sababu ya jitihada zake mambo hayangefanywa nalo kutaniko lingeathirika? Hicho kingekuwa kimbelembele!

19 Kwa kweli, ni nini kinachofanya kutaniko la Wakristo liwe na muungano? Je, ni ustadi katika usimamizi? uwezo wa kufanya mambo kwa njia bora? ujuzi mwingi? Ni kweli kwamba mambo hayo yanafaa ili kutaniko liendeshwe vizuri. (1 Wakorintho 14:40; Wafilipi 3:16; 2 Petro 3:18) Lakini, Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangetambuliwa hasa kwa upendo wao. (Yohana 13:35) Hiyo ndiyo sababu wazee wenye kujali, ingawa wana utaratibu, wanatambua kwamba kutaniko si kampuni inayohitaji usimamizi mkali; badala yake, ni kundi linalohitaji kutunzwa kwa wororo. (Isaya 32:1, 2; 40:11) Kupuuza kwa kimbelembele kanuni kama hizo mara nyingi hutokeza ugomvi. Tofauti na hiyo, utaratibu wa kimungu hutokeza amani.—1 Wakorintho 14:33; Wagalatia 6:16.

20. Tutazungumzia nini katika makala ifuatayo?

20 Masimulizi ya Biblia kuhusu Kora, Absalomu, na Sauli yanaonyesha wazi kwamba kimbelembele hutokeza aibu, kama inavyotajwa kwenye Mithali 11:2. Lakini, mstari uo huo waongezea kusema: “Hekima i pamoja na wenye kiasi.” Kiasi ni nini? Kuna mifano gani katika Biblia ambayo inaweza kutusaidia kuelewa sifa hii, na tunawezaje kuonyesha kiasi leo? Maswali haya yatazungumziwa katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa kuwa Reubeni ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, huenda wazao wake waliochochewa na Kora kuasi walichukia mamlaka ya Musa juu yao kwa sababu Musa alikuwa wa uzao wa Lawi.

^ fu. 11 Kileabu, mwana wa pili wa Daudi, hatajwi baada ya kuzaliwa. Huenda alikufa wakati fulani kabla ya maasi ya Absalomu.

^ fu. 12 Katika nyakati za Biblia kuzika maiti kulikuwa jambo muhimu sana. Kwa hiyo, kutozikwa kulikuwa jambo la msiba na mara nyingi kulionyesha kukataliwa na Mungu.—Yeremia 25:32, 33.

^ fu. 17 Kwa mfano, Finehasi alichukua hatua ya haraka ili kukomesha pigo ambalo lilikuwa limeua makumi ya maelfu ya Waisraeli, naye Daudi aliwatia moyo watu wake wenye njaa sana wale pamoja naye mikate ya wonyesho katika “nyumba ya Mungu.” Mungu hakuyashutumu matendo hayo mawili kuwa kimbelembele.—Mathayo 12:2-4; Hesabu 25:7-9; 1 Samweli 21:1-6.

Je, Wakumbuka?

• Kimbelembele ni nini?

• Husuda ilimfanyaje Kora atende kwa kimbelembele?

• Tunajifunza nini kutokana na simulizi la Absalomu mwenye tamaa ya makuu?

• Tunaweza kuepukaje roho isiyo na subira iliyoonyeshwa na Sauli?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Sauli alikosa subira akatenda kwa kimbelembele