Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tuwe Wenye Kiasi Kuhusiana na Matarajio Yetu?

Kwa Nini Tuwe Wenye Kiasi Kuhusiana na Matarajio Yetu?

Kwa Nini Tuwe Wenye Kiasi Kuhusiana na Matarajio Yetu?

MATARAJIO na miradi ambayo imetimizwa yatupa uradhi. Hata hivyo, matarajio na matamanio yetu mengi hayatimizwi jinsi tunavyotaka. Hali inayovunja matumaini itokeapo mara kwa mara maishani yaweza kufanya tujiudhi na kuwaudhi wengine pia. Kwa kufaa mwanamume mwenye hekima alitoa wazo hili: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.”—Mithali 13:12.

Ni hali gani zinazoweza kufanya matumaini yetu yavunjwe? Twawezaje kujitahidi kuwa wenye kiasi zaidi kuhusiana na matarajio yetu? Zaidi ya hayo, kwa nini kufanya hivyo kwatunufaisha?

Matarajio na Hali Inayovunja Matumaini

Kwa sababu ya shughuli nyingi za maisha ya leo ni kana kwamba kadiri tunavyong’ang’ana zaidi, ndivyo tunavyorudi nyuma hata zaidi. Yanayotakiwa kutoka kwetu hayana kikomo, nasi tunaposhindwa kutimiza yale ambayo tumeamua kufanya, tunaelekea kujilaumu. Hata tunaweza kuhisi kana kwamba tunavunja matumaini ya wengine. Cynthia aliye mke na mama ambaye anajua matatizo yahusianayo na kulea watoto asema hivi: “Kutokuwa thabiti wakati wa kutia watoto wangu nidhamu na kuhisi kwamba siwafunzi kikamili kwaniudhi.” Stephanie aliye kijana asema hivi kuhusu elimu yake: “Sina wakati wa kutosha kufanya yote nitakayo, nalo hufanya nikose subira.”

Matarajio yenye kupita kiasi yaweza kwa urahisi kugeuka kuwa mwelekeo wa kutaka ukamilifu, nao waweza kuwa wenye kukatisha tamaa kabisa. Kijana ambaye ameoa aitwaye Ben akiri: “Ninapochunguza matendo, mawazo, na hisia zangu, sikuzote naona jinsi ambavyo ningaliweza kufanya vyema zaidi. Daima natafuta ukamilifu, nayo matokeo ni hali ya kuvunja matumaini, kutokuwa na subira, na kukatishwa tamaa.” Gail aliye mke Mkristo asema hivi: “Mwelekeo wa kutaka ukamilifu hauruhusu ushindwe kamwe. Tunataka kuwa mama au wake bora. Lazima tuwe na matokeo, sivyo hatutakuwa wenye furaha; kushindwa kwamaanisha kupoteza wakati na nguvu, nako kwatuudhi.”

Jambo lingine liwezalo kusababisha hali inayovunja matumaini ni afya inayoharibika na uzee. Kupungukiwa kwa nguvu na uwezo wa kutenda kwafanya udhaifu wetu uonekane wazi zaidi, nako kwaongeza hisia za kukatishwa tamaa. “Ninakosa subira kwa sababu siwezi kufanya mambo niliyoweza kufanya kwa urahisi na kwa ukawaida kabla sijawa mgonjwa,” akiri Elizabeth.

Yaliyotangulia ni baadhi ya hali ziwezazo kufanya matumaini ya mtu yavunjwe. Tusipokinza hisia za aina hizo, twaweza hata kukata kauli kwamba watu wengine hawatupendi. Basi, twaweza kuchukua hatua zipi ili tuweze kusitawisha matarajio yenye kiasi na kukabiliana na hali inayovunja matumaini?

Jinsi ya Kusitawisha Matarajio Yenye Kiasi

Kwanza, kumbuka kwamba Yehova ni mwenye kiasi na mwenye kuelewa hisia za wengine. Andiko la Zaburi 103:14 latukumbusha hivi: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” Kwa kuwa Yehova anajua uwezo na udhaifu wetu, anatarajia tufanye kile tu tuwezacho kufanya. Jambo moja analotaka kutoka kwetu ni kwamba ‘twende kwa unyenyekevu na Mungu wetu.’—Mika 6:8.

Pia, Yehova atusihi tumwendee kwa sala. (Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 5:17) Kutoa sala kwaweza kutusaidiaje? Sala hutuliza mawazo yetu na kutusaidia kuwa na usawaziko wa akili. Sala yenye bidii yaonyesha kwamba twakubali kuwa twahitaji msaada—yaonyesha sifa za unyenyekevu na kiasi. Yehova yu tayari kujibu sala zetu kwa kutupa roho yake takatifu, nayo baadhi ya matunda yake ni upendo, fadhili, wema, na kujidhibiti. (Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23) Kutoa sala pia huondoa mahangaiko na hali ya kukatishwa tamaa. Kupitia sala, “mtu hupata faraja isiyopatikana kutokana na chanzo kingine chochote,” asema Elizabeth. Kevin akubali akisema hivi: “Naomba Mungu anipe moyo mtulivu na akili tulivu ili niweze kutatua tatizo fulani. Yehova hakosi kamwe kunisaidia.” Mtume Paulo alielewa thamani ya sala. Hiyo ndiyo sababu alipendekeza hivi: “Acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Naam, kuwasiliana na Yehova kwatusaidia kutotarajia mengi mno kutoka kwa wengine wala kutoka kwetu wenyewe.

Hata hivyo, mara kwa mara twahitaji kitia-moyo wakati uo huo. Neno linenwalo wakati ufaao ni jema. Mazungumzo pamoja na rafiki mwaminifu aliyekomaa yaweza kutusaidia kuelewa sababu inayofanya tuwe wenye kukatishwa tamaa au wenye wasiwasi. (Mithali 15:23; 17:17; 27:9) Vijana ambao wamekatishwa tamaa hujifunza kwamba kuomba wazazi shauri kwaweza kuwasaidia kuwa na maoni yenye usawaziko. Kwa kushukuru, Kandi akiri hivi: “Mwongozo wenye upendo kutoka kwa wazazi wangu umenisaidia kuwa mwenye kiasi na mwenye usawaziko zaidi, nami nimepata kuwa mtu ambaye wengine wanapenda kuwa pamoja naye.” Naam, kikumbusha katika Mithali 1:8, 9 kinafaa kabisa: “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako, kwa maana hayo yatakuwa kilemba cha neema kichwani pako, na mikufu shingoni mwako.”

Athari za mwelekeo wa kutaka ukamilifu zaelezwa vizuri katika msemo huu: “Kutarajia maisha yawe jinsi tunavyotaka kabisa ni kana kwamba tunataka kukatishwa tamaa.” Ili tuepuke kukatishwa tamaa tunahitaji kurekebisha mawazo yetu. Unyenyekevu na kiasi—yaani kuwa na maoni yanayofaa juu ya udhaifu wetu—hakika zitatusaidia kusitawisha matarajio yenye kiasi na usawaziko. Kwa kufaa, andiko la Waroma 12:3 latuonya kwamba ‘tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ Na kwa kuongezea, andiko la Wafilipi 2:3 latutia moyo tuwe na hali ya akili ya kujishusha chini na kuona wengine kuwa wakuu kuliko sisi.

Elizabeth aliyetajwa mapema, aliona vigumu kuvumilia ugonjwa wake. Kwake, muda ulihitajika ili asitawishe maoni ya Yehova juu ya hali yake na ili aweze kufarijika kwa kujua kwamba Mungu hatasahau utumishi wetu. Colin amelazwa kitandani kwa sababu ya ugonjwa wenye kudhoofisha. Mwanzoni, alihisi kwamba huduma yake haikufaa kitu alipoilinganisha na kile alichoweza kufanya alipokuwa na afya nzuri. Kwa kutafakari maandiko kama vile 2 Wakorintho 8:12, aliweza kuacha kuwa na hisia kama hizo. Mstari huo wasema hivi: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” “Ijapokuwa sina mengi ya kutoa, bado naweza kutoa, nako kwakubalika mbele ya Yehova,” asema Colin. Katika Waebrania 6:10 twakumbushwa: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”

Twawezaje basi, kujua kama matarajio yetu hayapiti kiasi? Jiulize, ‘Je, matarajio yangu yanapatana na matarajio ya Mungu?’ Andiko la Wagalatia 6:4 lasema hivi: “Acheni kila mmoja athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, na ndipo atakuwa na sababu ya mchachawo kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.” Kumbuka kwamba Yesu alisema hivi: “Nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.” Naam, Wakristo wana nira ya kuchukua, hata hivyo nira hiyo ni “ya fadhili,” nayo ni ‘nyepesi,’ naye Yesu aliahidi kwamba itatuburudisha tukijifunza kuibeba kwa njia inayofaa.—Mathayo 11:28-30.

Matarajio Yenye Kiasi Yaleta Thawabu

Tukisikiliza na kufuata ushauri wa Neno la Mungu, huku tukijitahidi kusitawisha matarajio yenye kiasi, tutapata sasa hivi thawabu ya kudumu. Kwanza, kuwa na matarajio ya kiasi kwaleta manufaa ya kiafya. Jennifer, ambaye amepata manufaa kutokana na vikumbusha vya Yehova akiri hivi: “Nina nguvu na shauku nyingi zaidi maishani.” Kwa kufaa, andiko la Mithali 4:21, 22 latusihi kuzingatia kauli za Yehova kwa macho na katika mioyo yetu, “maana ni uhai kwa wale wazipatao, na afya ya mwili wao wote.”

Thawabu nyingine ni ya kuwa na afya njema kiakili na kihisia. “Niruhusupo Neno la Mungu lipenye moyoni na akilini, ninapata kwamba sikuzote mimi ni mwenye furaha,” asema Theresa. Lakini, bado tutapatwa na hali inayovunja matumaini. Hata hivyo, kuvumilia hali hiyo kutakuwa rahisi zaidi. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia,” lasihi andiko la Yakobo 4:8. Yehova aahidi pia kutuimarisha tunapopata shida maishani mwetu na kutubariki kwa amani.—Zaburi 29:11.

Tukiwa na matarajio yenye kiasi tutaweza kudumisha uthabiti wa kiroho. Hilo pia ni baraka. Twaweza kutanguliza mambo muhimu zaidi maishani. (Wafilipi 1:10) Ndipo, miradi yetu ikiwa yenye kiasi na yenye kufikika, tutakuwa na shangwe na uradhi zaidi maishani. Hatutasita kujikabidhi kwa Yehova, tukijua kwamba atatusaidia tufanikiwe. “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wa Mungu wenye uweza, ili apate kuwakweza nyinyi katika wakati upasao,” asema Petro. (1 Petro 5:6) Je, kuna thawabu kubwa zaidi kuliko kuheshimiwa na Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kusitawisha matarajio yenye kiasi kwaweza kutusaidia kukabiliana na kukatishwa tamaa na hali inayovunja matumaini