Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtengenezaji wa Silaha Awa Mwokoaji wa Uhai

Mtengenezaji wa Silaha Awa Mwokoaji wa Uhai

Simulizi la Maisha

Mtengenezaji wa Silaha Awa Mwokoaji wa Uhai

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ISIDOROS ISMAILIDIS

Nilikuwa nimepiga magoti huku machozi yakitiririka usoni. “Ee, Mungu, dhamiri yangu hainiruhusu niendelee kufanya kazi ya kutengeneza silaha,” nikasema katika sala. “Nimejitahidi sana kutafuta kazi ya aina nyingine bila mafanikio. Kesho, nitajiuzulu. Tafadhali, Yehova, usiruhusu watoto wetu wanne wakose chakula.” Nilifikiaje hali hii?

MAISHA yalikuwa matulivu na yasiyo na mambo mengi huko Drama kaskazini mwa Ugiriki, nilikozaliwa katika mwaka wa 1932. Baba yangu alikuwa akiniambia alilotaka nifanye maishani. Alinitia moyo niende Marekani ili kupata elimu. Baada ya Ugiriki kuporwa katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, wito ulioenea sana miongoni mwa Wagiriki ulisema hivi: “Unaweza kuiba mali zetu lakini huwezi kuiba kilicho ndani ya akili zetu.” Niliazimia kufuatia elimu ya juu ili nipate kitu ambacho hakuna yeyote angeweza kukiiba.

Tangu ujanani, nilijiunga na vikundi mbalimbali vya vijana vilivyofadhiliwa na Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Huko tulifundishwa kuepuka madhehebu hatari. Nakumbuka kikundi kimoja hususa—Mashahidi wa Yehova—kikitajwa kwa kuwa ilidhaniwa kiliwakilisha mpinga-Kristo.

Baada ya kuhitimu chuo cha ufundi huko Athens mwaka wa 1953, nilisafiri hadi Ujerumani kutafuta kazi na wakati uleule nijiunge na shule. Lakini sikufanikiwa, hivyo nikasafiri hadi nchi nyingine. Baada ya majuma kadhaa nikajikuta katika bandari moja huko Ubelgiji nikiwa sina pesa zozote. Nakumbuka nikiingia ndani ya kanisa na baada ya kuketi chini nikalia sana mpaka pakawa na machozi sakafuni. Nikaomba na kumwahidi Mungu kwamba ikiwa angenisaidia nifike Marekani, nisingejishughulisha na kutafuta vitu vya kimwili mbali ningejipatia elimu na kujitahidi kuwa Mkristo mwema na raia mwema. Hatimaye, nikafika Marekani mwaka wa 1957.

Maisha Mapya Huko Marekani

Maisha huko Marekani yalikuwa magumu kwa mhamiaji asiyejua lugha na asiye na pesa. Usiku nilifanya kazi mbili tofauti na mchana nikajitahidi kwenda shuleni. Nilijiunga na vyuo kadhaa na nikapata digrii. Kisha nikajiunga na Chuo Kikuu cha California huko Los Angeles na kupata digrii ya masomo ya ufundi. Maneno ya baba yangu kuhusu kupata elimu yalinisaidia katika miaka hiyo migumu.

Wakati huo nilifahamiana na msichana Mgiriki mwenye kupendeza aitwaye Ekaterini, tukafunga ndoa mwaka wa 1964. Mwana wetu wa kwanza alizaliwa miaka mitatu baadaye, na katika muda usiozidi miaka minne, tulipata wana wengine wawili na msichana mmoja. Kwa kweli, lilikuwa jambo gumu kumudu familia na wakati uleule kusoma kwenye Chuo Kikuu.

Nilikuwa nikifanya kazi katika Jeshi la Anga la Marekani kwenye kiwanda cha kutengeneza silaha na vyombo vya angani cha Sunnyvale, California. Nilishiriki katika miradi mbalimbali ya kuunda vyombo vya angani kutia ndani ule wa kurusha angani vyombo vya Agena na Apolo. Hata nilitunukiwa medali kwa ajili ya mchango wangu kwa safari za vyombo vya angani, Apolo namba 8 na Apolo namba 11. Baada ya hayo, niliendelea na masomo na kujiingiza sana katika miradi ya kutengeneza vyombo vya kivita vya angani. Kufikia hapo nilijiona kuwa nimepata vitu vyote nilivyotaka maishani—mke mzuri, watoto wanne wazuri, kazi yenye fahari, na nyumba nzuri.

Jamaa Mwenye Udumifu

Nikiwa kazini mapema mwaka wa 1967, nilifahamiana na Jim, mtu mpole sana na mwenye fadhili. Jim alionekana mwenye furaha daima na hakukataa kamwe nilipomwalika tunywe kahawa pamoja wakati wa mapumziko. Yeye alitumia pindi hizo kusema nami habari za Biblia. Jim aliniambia kwamba alikuwa akijifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova.

Nilishtuka kusikia kwamba Jim alikuwa akishirikiana na kikundi hicho cha kidini. Ilikuwaje mtu mwenye sifa nzuri kama yeye anaswe na madhehebu ya mpinga-Kristo? Hata hivyo, nilivutiwa sana na fadhili ya Jim na jinsi alivyopendezwa nami. Aliniletea kitu fulani tofauti cha kusoma kila siku. Kwa mfano, siku moja alifika ofisini mwangu na kuniambia: “Isidoros, makala hii ya Mnara wa Mlinzi inaeleza jinsi ya kuimarisha maisha ya familia. Nenda nayo nyumbani na uisome pamoja na mke wako.” Nilimwahidi kuwa ningeisoma, lakini baadaye nilienda chooni na kurarua gazeti hilo vipande vipande na kulitupa ndani ya pipa la takataka.

Kwa miaka mitatu niliharibu kila kitabu na gazeti ambazo Jim alinipa. Nikiwa na ubaguzi dhidi ya Mashahidi wa Yehova, na bado nikitaka kudumisha urafiki wangu na Jim, niliamua niwe nikimsikiliza kisha kuyapuuza mara moja yale aliyosema.

Hata hivyo, kutokana na mazungumzo hayo, nilifahamu kuwa mengi ya mambo niliyoamini na kufanya yalikuwa kinyume cha mafundisho ya Biblia. Nilitambua kwamba mafundisho kama Utatu, moto wa helo, na kutokufa kwa nafsi hayakuwa ya Kimaandiko. (Mhubiri 9:10; Ezekieli 18:4; Yohana 20:17) Nikiwa mfuasi mwenye kiburi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki, sikutaka kukiri waziwazi kwamba Jim alikuwa akisema kweli. Lakini kwa kuwa sikuzote alitumia Biblia wala si maoni yake mwenyewe, hatimaye nilitambua kwamba mtu huyo alikuwa na ujumbe wa maana wa kunipa kutoka kwa Biblia.

Mke wangu alitambua kwamba jambo fulani linaendelea, kisha akataka kujua kama nilikuwa nikizungumza na yule rafiki yangu aliyeshirikiana na Mashahidi. Nilipojibu ndiyo, yeye akasema: “Ni afadhali tujiunge na dini iwayo yote lakini si ya Mashahidi wa Yehova.” Hata hivyo, muda si muda, mimi, mke wangu na watoto wetu tulikuwa tukihudhuria mikutano ya Mashahidi kwa ukawaida.

Uamuzi Mgumu

Nilipokuwa nikijifunza Biblia, nilisoma maneno haya ya nabii Isaya: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Nikajiuliza, ‘Inawezekanaje mtumishi wa Mungu mpenda-amani awe ameajiriwa kubuni na kutengeneza silaha zenye kuharibu?’ (Zaburi 46:9) Ilinichukua muda mfupi kuamua kutafuta kazi nyingine.

Inaeleweka kwamba huu ulikuwa uamuzi mgumu. Nilikuwa na kazi yenye fahari. Nilikuwa nimejikakamua kwa miaka mingi kufanya kazi ngumu, kusoma, na kujidhabihu ili kufikia mahali nilipo. Nimepanda cheo kazini na sasa nakabili uwezekano wa kuiacha kazi-maisha yangu. Hata hivyo, upendo wangu mwingi kwa Yehova na tamaa nyingi ya kufanya mapenzi yake, mwishowe ilinisaidia kufikia uamuzi.—Mathayo 7:21.

Niliamua kufanya kazi katika kampuni moja huko Seattle, Washington. Hata hivyo, punde si punde, nikakata tamaa nilipogundua kwamba kazi hii haikupatana hata kidogo na andiko la Isaya 2:4. Jitihada zangu za kutohusika moja kwa moja hazikufaulu na dhamiri yangu ikawa inanisumbua. Ikawa wazi kwamba siwezi kuendelea kufanya kazi hiyo na wakati uleule kudumisha dhamiri safi.—1 Petro 3:21.

Ilibainika kwamba ni lazima tufanye mabadiliko muhimu. Katika muda usiozidi miezi sita, tulibadilisha maisha yetu na kupunguza gharama ya familia kwa nusu. Kisha tukauza nyumba yetu kubwa na kununua nyingine ndogo huko Denver, Colorado. Sasa nilikuwa tayari kufanya lile badiliko kubwa la mwisho—kuacha kazi yangu ya kuajiriwa. Niliandika barua ya kujiuzulu, nikaeleza msimamo wangu wa kutokuwamo. Usiku huo, baada ya watoto kulala, nilipiga magoti pamoja na mke wangu na kusali kwa Yehova, kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa makala haya.

Baada ya muda usiozidi mwezi mmoja, tulihamia Denver, na baada ya majuma mawili, mnamo Julai mwaka wa 1975, mimi na mke wangu tukabatizwa. Kwa muda wa miezi sita sikuweza kupata kazi, na pole kwa pole tulikuwa tukimaliza akiba yetu. Kufikia mwezi wa saba, pesa zilizobaki kwenye akiba hazikutosha hata kulipia amana ya nyumba ya mwezi mmoja. Niliamua kutafuta hata kazi ndogondogo, lakini mara baada ya hapo nikapata kazi ya uhandisi. Mshahara ulikuwa nusu tu ya ule niliokuwa nikipata; hata hivyo, ulikuwa ni zaidi ya niliokuwa nimemwomba Yehova. Nilifurahi kama nini kwamba nilikuwa nimeweka masilahi ya kiroho kwanza!—Mathayo 6:33.

Kulea Watoto Wetu Wampende Yehova

Wakati huohuo mimi na Ekaterini tulikuwa wenye shughuli nyingi za kufanya ile kazi ngumu ya kuwalea watoto wetu wanne kupatana na kanuni za Mungu. Tumefurahi kuwaona wote wakifikia ukomavu wa Kikristo kwa msaada wa Yehova, na kutumia maisha yao kikamili katika kazi muhimu ya kuhubiri Ufalme. Wana wetu watatu Christos, Lakes na Gregory wamehitimu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na sasa wanatumikia katika migawo mbalimbali, wakitembelea makutaniko na kuyatia nguvu. Toula binti yetu, anatumikia akiwa mjitoleaji kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko New York. Tuliguswa moyo tulipoona wote wakiacha kazi-maisha na kazi zenye mishahara mikubwa ili kumtumikia Yehova.

Wengi wametaka kujua siri ya kuwalea watoto kwa mafanikio. Bila shaka, hakuna njia fulani hususa ya kuwalea watoto, lakini kwa bidii nyendelevu sisi tulijitahidi kutia ndani ya mioyo yao upendo kwa Yehova na jirani. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Mathayo 22:37-39) Watoto walijifunza kwamba hatuwezi kusema tunampenda Yehova ikiwa tunatenda kinyume cha tunayosema.

Siku moja katika juma, kwa kawaida Jumamosi, tulishiriki huduma ya shambani tukiwa familia. Tulikuwa na funzo la Biblia la familia kwa ukawaida kila Jumatatu jioni baada ya chakula, na pia tulikuwa na funzo la Biblia na kila mtoto. Walipokuwa wachanga, tulijifunza na kila mtoto kwa vipindi vifupi katika juma, na umri wao ulipoongezeka, tukawa tunajifunza kwa muda mrefu zaidi mara moja kwa juma. Wakati wa funzo, watoto walieleza hisia zao na kuzungumza kwa uhuru juu ya matatizo yao.

Tulifurahia pia tafrija zenye kujenga tukiwa familia. Tulifurahia kupiga ala za muziki pamoja, na kila mtoto alipiga muziki alioupenda. Katika miisho-juma fulani tulikaribisha familia nyingine kwa ushirika wenye kujenga. Tulipanga pia safari za likizo tukiwa familia. Kwenye moja ya safari hizo, tulitumia majuma mawili kutalii milima ya Colorado, tukashiriki utumishi wa shambani pamoja na makutaniko ya huko. Watoto wetu hufurahia kukumbuka walivyofanya kazi katika idara mbalimbali kwenye mikusanyiko ya wilaya na kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika sehemu mbalimbali. Tulipowapeleka watoto Ugiriki kuwaona watu wa ukoo, walikutana pia na Mashahidi wengi waaminifu ambao waliwahi kufungwa gerezani kwa ajili ya imani yao. Hilo liliwavutia sana na kuwasaidia waazimie kubaki imara na jasiri kwa ajili ya kweli.

Bila shaka, mara kwa mara, baadhi ya watoto walikosa adabu au wakachagua mashirika yasiyofaa. Nyakati nyingine, sisi wazazi tuliwatatiza watoto, labda kwa kuweka vizuizi vilivyopita kiasi katika mambo fulani. Lakini kwa kutumia “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova,” linalopatikana katika Biblia, sisi sote tulisaidiwa kunyoosha mambo.—Waefeso 6:4; 2 Timotheo 3:16, 17.

Wakati Wenye Furaha Zaidi Maishani Mwangu

Baada ya watoto wetu kujiunga na utumishi wa wakati wote, mimi na Ekaterini tulifikiria mambo kwa uzito kuona namna tungepanua utumishi wetu katika kazi hii muhimu ya kuokoa uhai. Hivyo, katika mwaka wa 1994, nilistaafu mapema na sisi wawili tukaanza kutumikia tukiwa mapainia wa kawaida. Huduma yetu inatia ndani kutembelea vyuo na vyuo vikuu vya mahali tunakoishi, ambako tunatolea wanafunzi ushahidi na kujifunza Biblia na baadhi yao. Kwa sababu niliyafahamu matatizo yao—kwa kuwa miaka michache iliyopita nilikuwa katika hali kama hiyo—nilifanikiwa sana kuwasaidia wajifunze juu ya Yehova. Ni shangwe kama nini kwangu kuweza kujifunza na wanafunzi kutoka Bolivia, Brazili, Chile, China, Ethiopia, Mexico, Misri, Thailand, na Uturuki! Mimi pia hufurahia kushiriki kutoa ushuhuda kupitia simu, hasa kwa wenye kusema Kigiriki.

Ijapokuwa nina matatizo mengi kwa sababu ya matamshi mazito ya Kigiriki pamoja na kuzeeka, nimejitahidi daima kuwa na nia ya kutumika, sawa na ile iliyokuwa na Isaya aliyetangaza hivi: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Tumekuwa na shangwe ya kusaidia watu zaidi ya sita kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova. Kwa hakika huu umekuwa wakati wenye furaha zaidi maishani mwetu.

Wakati mmoja nilitumia maisha yangu yote kutengeneza silaha za kuangamiza wanadamu wenzangu. Hata hivyo, kwa fadhili yake isiyostahiliwa, Yehova aliniwezesha mimi na familia yangu kuwa watumishi wake walio wakfu na kutumia maisha yetu kuwapelekea watu habari njema za uhai udumuo milele katika dunia iliyo paradiso. Ninapofikiria uamuzi mgumu niliofanya, mimi hukumbuka maneno haya ya Malaki 3:10: ‘Nijaribuni kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.’ Kwa kweli ametumwagia baraka—mpaka tukatosheka!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

Lakes: Baba yangu alichukia unafiki. Alijitahidi sana asiwe mnafiki hasa katika kuwekea familia yake kielelezo kizuri. Mara nyingi, baba alituambia hivi: “Ikiwa umeweka maisha yako wakfu kwa Yehova hiyo ni hatua muhimu. Unapaswa kuwa tayari kujidhabihu kwa ajili ya Yehova. Hiyo ndiyo maana ya kuwa Mkristo.” Maneno hayo yamedumu akilini mwangu na yameniwezesha kufuata kielelezo chake katika kujidhabihu kwa ajili ya Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

Christos: Nimethamini sana uaminifu-mshikamanifu wa moyo wote wa wazazi wangu kwa Yehova na uwajibikaji wao wa dhati wakiwa wazazi. Tulifanya mambo yote tukiwa familia—iwe ni utumishi wa shambani au kwenda likizo. Ingawa wazazi wangu wangeweza kujiingiza katika mambo mengi, wao walichagua kuishi maisha sahili na kuzingatia utumishi. Leo, mimi huhisi mwenye furaha kwelikweli ninapojishughulisha sana na utumishi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

Gregory: Mbali na maneno yao ya kunitia moyo kupanua huduma yangu, kielelezo chao na shangwe yao katika utumishi wa Yehova zilinichochea kuchanganua upya hali zangu na kuondolea mbali wasiwasi na mahangaiko kuhusu kuanza utumishi wa wakati wote, na kujitoa kikamili zaidi katika kazi ya Yehova. Nawashukuru wazazi wangu kwa kunisaidia kupata shangwe ambayo hutokana na kujikakamua.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

Toula: Sikuzote wazazi wetu walisisitiza kwamba uhusiano wetu na Yehova ndicho kitu chenye thamani zaidi tuwezacho kuwa nacho na kwamba njia pekee ya kupata furaha ya kweli ni kumpa Yehova kilicho bora. Walimfanya Yehova awe halisi kwetu. Mara nyingi, baba yetu alitueleza kwamba kuna furaha isiyo na kifani kumaliza siku ukiwa na dhamiri safi, ukijua kwamba umefanya yote uwezayo kumfurahisha Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nilipokuwa askari huko Ugiriki, mwaka wa 1951

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na Ekaterini mwaka wa 1966

[Picha katika ukurasa wa 26]

Familia yangu mwaka wa 1996: (kushoto kuelekea kulia, nyuma) Gregory, Christos, Toula; (mbele) Lakes, Ekaterini, na mimi