Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wenye Thamani kwa Yehova Ni Wale Wampendao

Wenye Thamani kwa Yehova Ni Wale Wampendao

Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti

Wenye Thamani kwa Yehova Ni Wale Wampendao

LEBANONI imejulikana sana kwa wingi wa mali ya asili tangu nyakati za Biblia. (Zaburi 72:16; Isaya 60:13) Hasa kilichokuwa chenye thamani kubwa ni mierezi yake mikubwa ambayo ilitumiwa sana kwa ujenzi kwa sababu ya rangi yake, manukato yake, na udumifu wake. Katika karne ya kwanza kitu chenye thamani hata zaidi kilipatikana Lebanoni. Gospeli ya Marko inaripoti kwamba kutoka Tiro na Sidoni, katika eneo la kale la Lebanoni “umati mkubwa, uliposikia ni mambo mengi kadiri gani [Yesu] aliyokuwa akifanya, ukamjia.”—Marko 3:8.

Leo vilevile, Lebanoni huzidi kuzaa matunda yenye thamani kubwa machoni pa Yehova. Mambo yaliyoonwa yafuatayo yanaonyesha jambo hilo.

• Shahidi mchanga aitwaye Wissam, aliombwa atoe hotuba ya dakika 30 darasani kule shuleni. Wissam aliamua kwamba hiyo ingekuwa fursa yenye kufaa ya kutoa ushuhuda. Hivyo, akatumia kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kutayarisha hotuba juu ya uumbaji. Hata hivyo, mwalimu wa Wissam alipoona hotuba ile alisema kwamba kwa kuwa ilikuwa yenye mambo muhimu sana, Wissam angeweza kuongezea muda wake hadi dakika 45.

Wissam alipoanza tu kutoa hotuba mwalimu wake alimkatiza na kuagiza mkuu wa shule aitwe. Punde si punde yule mkuu wa shule akafika, na Wissam akaanza tena. Alipokuwa akiendelea kusikiliza maswali ambayo Wissam alitumia katika utangulizi wake, mkuu huyo wa shule alisisimka na kusema kwamba kila mwanafunzi apaswa kupokea nakala ya hotuba hiyo.

Punde tu mwalimu mwingine aliyekuwa akipita, aliona msisimko katika darasa lile akaulizia lililokuwa likiendelea. Alipofahamishwa, yeye alitaka kujua kama Wissam alikuwa akijaribu kuthibitisha uumbaji au mageuzi. “Uumbaji,” akajibiwa. Alipofahamu kuwa Wissam ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yule mwalimu akaliambia darasa: “Mtaelewa kutokana na hotuba yake kwamba sayansi huunga mkono uumbaji wala si mageuzi.”

Ilitokea kwamba mwalimu huyu alikuwa na nakala ya kitabu Creation na kwamba amekuwa akikitumia katika hotuba zake kwenye chuo kikuu! Kabla ya kuondoka, alitaka kujua kama angeweza kurudi siku iliyofuata pamoja na wanafunzi wa darasa lake ili Wissam awatolee hotuba hiyo. Hilo lilitokeza pindi nyingine ya kutoa ushahidi mzuri juu ya Yehova.

• Nina mwenye umri wa miaka 22 alikuwa mwenye kiu ya maji ya kweli. Siku moja binamu yake alimpa Biblia, akampeleka kwa Kanisa la Pentekoste. Nina aliisoma Biblia kwa furaha akajifunza kutokana na usomaji huo kwamba Wakristo walipaswa kuhubiri na hivyo yeye akaanza kusema na watu aliowafahamu. Kila mtu aliyesema naye alimuuliza hivi: “Je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Hilo lilimtatanisha.

Miaka sita baadaye, Mashahidi wa Yehova walifika kwa akina Nina, wakamwambia juu ya Ufalme wa Mungu. Kwanza alijaribu kukosoa mafundisho yao. Lakini alitambua kwamba majibu yao yote yanapatana na akili na yanategemea Biblia.

Mambo ambayo Nina alijifunza hatimaye, kama vile, jina la Mungu, Yehova; baraka za Ufalme; kutia na mengine yalimsadikisha kwamba alikuwa ameipata kweli. Alijiweka wakfu kwa Mungu akabatizwa. Katika miaka saba ambayo imepita, Nina ametumikia akiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote. Kwa kweli, Yehova huwabariki wale wampendao kwelikweli.—1 Wakorintho 2:9.