Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dhabihu Zilizompendeza Mungu

Dhabihu Zilizompendeza Mungu

Dhabihu Zilizompendeza Mungu

“Kila kuhani wa cheo cha juu huwekwa rasmi ili kuzitoa zawadi na dhabihu pia.”—WAEBRANIA 8:3.

1. Kwa nini watu huona uhitaji wa kumwendea Mungu?

“KUTOA dhabihu huonekana kuwa jambo la ‘asili’ kwa mwanadamu kama vile kusali; anayetoa dhabihu huonyesha jinsi ahisivyo juu yake mwenyewe, ilhali yule anayesali huonyesha jinsi ahisivyo juu ya Mungu,” aandika mwanahistoria wa Biblia Alfred Edersheim. Tangu wakati ambapo dhambi iliingia ulimwenguni, imesababisha hisia zenye huzuni za hatia, kutenganishwa na Mungu, na kukosa tumaini. Kitulizo kinahitajika kutokana na hisia hizo. Ni rahisi kuelewa kwamba watu wanapojikuta katika hali kama hiyo yenye kukatisha tamaa, wao huona uhitaji wa kumwendea Mungu ili wapate msaada.—Waroma 5:12.

2. Ni habari gani za mapema zilizoandikwa katika Biblia kuhusu matoleo kwa Mungu?

2 Habari za kwanza zilizoandikwa katika Biblia juu ya matoleo kwa Mungu zahusu Kaini na Abeli. Twasoma: “Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama.” (Mwanzo 4:3, 4) Halafu, twaona kwamba Noa, ambaye alihifadhiwa na Mungu katika lile Furiko kubwa ambalo liliharibu kizazi kiovu cha wakati wake, alichochewa ‘kumtolea Yehova sadaka za kuteketezwa [“kuchomwa,” NW] juu ya madhabahu.’ (Mwanzo 8:20) Mara kadhaa, Abrahamu, mtumishi na rafiki mwaminifu wa Mungu, akichochewa na ahadi na baraka za Mungu ‘alijenga madhabahu na kuliitia jina la BWANA.’ (Mwanzo 12:8; 13:3, 4, 18) Baadaye, Abrahamu alikabili jaribu kubwa zaidi la imani yake alipoambiwa na Yehova amtoe mwana wake Isaka akiwa toleo la kuchomwa. (Mwanzo 22:1-14) Masimulizi hayo, yajapokuwa mafupi, yanatoa habari nyingi sana kuhusu dhabihu, kama tutakavyoona.

3. Dhabihu hutimiza fungu gani katika ibada?

3 Kutokana na masimulizi hayo na masimulizi mengine ya Biblia, ni wazi kwamba kutoa aina fulani ya dhabihu kulikuwa sehemu muhimu ya ibada muda mrefu kabla Yehova hajatoa sheria hususa kuhusu dhabihu. Kulingana na hayo, kitabu kimoja chafafanua “dhabihu” kuwa “sherehe ya kidini ambamo kitu fulani hutolewa kwa mungu fulani ili kuanzisha, kudumisha, au kurudisha uhusiano ufaao kati ya mtu na kile akionacho kuwa kitakatifu.” Lakini jambo hilo lazusha maswali fulani muhimu ambayo yafaa tuyachunguze kwa makini, kama vile: Kwa nini dhabihu inahitajiwa katika ibada? Mungu hukubali dhabihu za aina gani? Na dhabihu za kale zamaanisha nini kwetu leo?

Kwa Nini Dhabihu Inahitajiwa?

4. Matokeo yalikuwa nini kwa Adamu na Hawa walipofanya dhambi?

4 Adamu alifanya dhambi kimakusudi. Alikosa kutii kimakusudi kwa kuchukua na kula tunda kutoka kwa mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Adhabu ya tendo hilo la kutotii ilikuwa kifo, kama vile Mungu alivyokuwa amesema wazi: “Siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Hatimaye, Adamu na Hawa wakapata mshahara wa dhambi—wakafa.—Mwanzo 3:19; 5:3-5.

5. Kwa nini Yehova alichukua hatua ya kwanza kwa niaba ya uzao wa Adamu, Naye aliwafanyia nini?

5 Basi, namna gani uzao wa Adamu? Kwa kuwa walirithi dhambi na kutokamilika kutoka kwa Adamu, wao vilevile wametenganishwa na Mungu, hawana tumaini, nao hufa tu kama wanadamu wa kwanza wawili. (Waroma 5:14) Hata hivyo, Yehova si Mungu wa haki na uwezo tu bali pia ni Mungu wa upendo, sifa yake kuu. (1 Yohana 4:8, 16) Kwa hiyo, yeye huchukua hatua ya kwanza kuleta maelewano. Baada ya kusema kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” Biblia yaendelea kusema, “lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23.

6. Mapenzi ya Yehova ni nini kuhusiana na madhara yaliyotokana na dhambi ya Adamu?

6 Hatimaye, ili kutoa uhakikisho kuhusu zawadi hiyo, Yehova Mungu alitoa kitu ambacho kingefunika kile kilichopotea kutokana na dhambi ya Adamu. Katika Kiebrania, yaelekea neno ka·pharʹ mwanzoni lilimaanisha “-funika” au labda “-futa,” nalo pia hutafsiriwa “kufunika.” * Yaani, Yehova aliandaa njia ifaayo ya kufunika dhambi iliyorithiwa kutoka kwa Adamu na kufuta kabisa madhara yaliyotokana nayo ili wale wanaostahili kupata zawadi hiyo waweze kukombolewa kutokana na hatia ya dhambi na kifo.—Waroma 8:21.

7. (a) Hukumu ya Mungu dhidi ya Shetani ilitoa tumaini gani? (b) Ni bei gani ambayo ni lazima ilipwe ili wanadamu wakombolewe kutoka katika dhambi na kifo?

7 Tumaini la kuwekwa huru na utumwa wa dhambi na kifo lilidokezwa mara baada ya wanadamu wa kwanza wawili kufanya dhambi. Akimhukumu Shetani aliyewakilishwa na nyoka, Yehova alisema: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake [“mbegu yako na mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Taarifa hiyo ya unabii iliwatolea tumaini wote ambao wangekuwa na imani katika ahadi hiyo. Hata hivyo, bei fulani yapasa kulipwa ili ukombozi huo upatikane. Mbegu iliyoahidiwa haingekuja tu na kumharibu Shetani; lazima Mbegu hiyo ipondwe kisigino, yaani, ife, japo si milele.

8. (a) Kaini alivunjaje matumaini? (b) Kwa nini dhabihu ya Abeli ilikubalika machoni pa Mungu?

8 Yaelekea Adamu na Hawa walitafakari sana juu ya utambulisho wa Mbegu iliyoahidiwa. Hawa alipomzaa Kaini, mwana wake wa kwanza, alitangaza hivi: “Nimepata mtoto mwanamume kwa BWANA.” (Mwanzo 4:1) Je, alikuwa akifikiri kwamba labda mwana wake angekuwa Mbegu hiyo? Iwapo alifikiri hivyo au la, Kaini alivunja matumaini sana na dhabihu yake. Kwa upande mwingine, Abeli ndugu yake alionyesha imani katika ahadi ya Mungu, akachochewa kuwadhabihu wazao wa kwanza wa wanyama wake kwa Yehova. Twasoma hivi: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu.”—Waebrania 11:4.

9. (a) Abeli aliweka imani katika nini, naye aliionyeshaje? (b) Toleo la Abeli lilitimiza nini?

9 Abeli hakuwa na imani tu kwamba kuna Mungu, imani ambayo huenda Kaini pia alidhihirisha. Abeli alikuwa na imani katika ahadi ya Mungu kuhusu Mbegu fulani ambayo ingewaletea wanadamu waaminifu wokovu. Hakujulishwa jambo hilo lingetimizwaje, lakini ahadi ya Mungu ilimfahamisha Abeli kuwa mtu fulani alipaswa kupondwa kisigino. Naam, yaonekana alifikia mkataa kwamba damu ilipasa kumwagwa—maana hasa ya dhabihu. Abeli alimtolea yule aliye Chanzo cha uhai zawadi iliyohusisha uhai na damu, yaelekea ikiwa wonyesho wa tamaa yake kubwa na matazamio ya kuona kutimizwa kwa ahadi ya Yehova. Wonyesho huo wa imani ndio uliofanya Yehova apendezwe na dhabihu ya Abeli, na kwa kadiri ndogo, ukaonyesha maana halisi ya dhabihu—njia ambayo wanadamu wenye dhambi wanaweza kutumia ili kumkaribia Mungu na kupata kibali chake.—Mwanzo 4:4; Waebrania 11:1, 6.

10. Yehova alidhihirishaje maana ya dhabihu kwa kumwomba Abrahamu amtoe Isaka akiwa dhabihu?

10 Yehova alijulisha wazi, kwa njia yenye kutokeza, maana hasa ya dhabihu alipomwamuru Abrahamu amtoe mwana wake Isaka akiwa toleo la kuchomwa. Ingawa dhabihu hiyo haikutolewa kihalisi, ilifananisha jambo ambalo Yehova angefanya hatimaye—kumtoa Mwana wake mzaliwa-pekee akiwa dhabihu kubwa zaidi iliyopata kutolewa ili kutimiza mapenzi Yake kwa wanadamu. (Yohana 3:16) Kupitia dhabihu na matoleo ya Sheria ya Kimusa, Yehova alitoa vigezo vya unabii ili kuwafundisha wachaguliwa wake yale wapaswayo kufanya ili wasamehewe dhambi zao na kuimarisha tumaini lao la wokovu. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hayo?

Dhabihu Zinazokubalika kwa Yehova

11. Kuhani wa cheo cha juu wa Israeli alitoa aina gani mbili za matoleo, na kwa makusudi gani?

11 “Kila kuhani wa cheo cha juu huwekwa rasmi ili kutoa zawadi na dhabihu pia,” asema mtume Paulo. (Waebrania 8:3) Ona kwamba Paulo anatenganisha matoleo ya kuhani wa cheo cha juu wa Israeli la kale katika sehemu mbili, yaani, “zawadi” na “dhabihu” au “dhabihu kwa ajili ya dhambi.” (Waebrania 5:1) Kwa ujumla, watu hutoa zawadi ili kuonyesha upendo na shukrani, na vilevile kusitawisha urafiki, au kupata kibali. (Mwanzo 32:20; Mithali 18:16) Vivyo hivyo, matoleo mengi ambayo Sheria iliagiza yatolewe yanaweza kuonwa kuwa “zawadi” inayotolewa kwa Mungu ili kupata kibali chake. * Kukiuka Sheria kulihitaji malipo, na ili kutoa malipo hayo, “dhabihu kwa ajili ya dhambi” zilitolewa. Vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, hasa Kutoka, Mambo ya Walawi, na Hesabu, vina habari nyingi sana kuhusu aina mbalimbali za dhabihu na matoleo. Ingawa inaweza kuwa vigumu sana kwetu kufahamu na kukumbuka habari hizo zote, inafaa kuchunguza mambo fulani muhimu kuhusu aina mbalimbali za dhabihu.

12. Ni wapi katika Biblia tuwezapo kupata muhtasari wa dhabihu, au matoleo, katika Sheria?

12 Twaweza kuona kwamba katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 1 hadi ya 7, aina tano kuu za matoleo—toleo la kuchomwa, toleo la nafaka, dhabihu ya ushirika, toleo la dhambi, na toleo la hatia—zimeelezwa kila moja peke yake, ingawa kwa kweli baadhi ya matoleo hayo yalitolewa pamoja. Twaona pia kwamba matoleo hayo yanaelezwa mara mbili katika sura hizo, kwa malengo tofauti: mara ya kwanza katika Mambo ya Walawi 1:2 hadi 6:7, panapoeleza kinaganaga kile kilichopasa kutolewa kwenye madhabahu, na mara ya pili, katika Mambo ya Walawi 6:8 hadi 7:36, panapoonyesha sehemu zilizotengwa kwa ajili ya makuhani na zile zilizohifadhiwa kwa ajili ya mtoaji. Kisha katika Hesabu sura ya 28 na 29, twaona kile kiwezacho kuonwa kuwa ratiba kamili, inayoeleza ni nini ambacho kilihitaji kutolewa kila siku, kila juma, kila mwezi, na kwenye misherehekeo ya kila mwaka.

13. Fafanua matoleo yaliyotolewa kwa hiari yakiwa zawadi kwa Mungu.

13 Matoleo ya kuchomwa, matoleo ya nafaka, na matoleo ya ushirika ni kati ya matoleo yaliyotolewa kwa hiari yakiwa zawadi au njia ya kumkaribia Mungu ili kupata kibali chake. Wasomi fulani wanaonelea kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “toleo la kuchomwa” lamaanisha “toleo la kupaa” au “toleo lenye kupaa.” Hiyo ni tafsiri ifaayo kwa sababu toleo la kuchomwa lilipotolewa, mnyama aliyechinjwa alichomwa kwenye madhabahu na harufu tamu, au ya kuburudisha, ikapaa kuelekea mbinguni kwa Mungu. Jambo lililofanya toleo la kuchomwa liwe tofauti ni kwamba baada ya damu yake kunyunyizwa kuzunguka madhabahu, sehemu zote za mnyama huyu zilitolewa kwa Mungu. Makuhani ‘waliziteketeza zote juu ya madhabahu, ili ziwe sadaka ya kuteketezwa [“toleo la kuchomwa,” NW], dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza [“kuburudisha,” NW] kwa BWANA.’—Mambo ya Walawi 1:3, 4, 9; Mwanzo 8:21.

14. Toleo la nafaka lilitolewaje?

14 Toleo la nafaka linafafanuliwa kwenye kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 2. Lilikuwa toleo la hiari la unga mwembamba, ambao kwa kawaida ulitiwa mafuta yenye ubani. “[Kuhani] atatwaa konzi moja katika huo unga mwembamba, na katika mafuta yake, na huo ubani wote; kisha kuhani atauteketeza kuwa ndio ukumbusho wake juu ya madhabahu, ni kafara ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza [“kuburudisha,” NW] kwa BWANA.” (Mambo ya Walawi 2:2) Ubani ulikuwa sehemu mojawapo ya uvumba mtakatifu uliochomwa kwenye madhabahu ya uvumba katika tabenakulo na hekalu. (Kutoka 30:34-36) Mfalme Daudi alifikiria hilo aliposema: “Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba, kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni.”—Zaburi 141:2.

15. Dhabihu ya ushirika ilitolewa kwa kusudi gani?

15 Toleo jingine la hiari lilikuwa dhabihu ya ushirika, ambayo yafafanuliwa katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 3. Dhabihu ya ushirika yaweza pia kutafsiriwa kuwa “dhabihu ya matoleo ya amani.” Katika Kiebrania, neno “amani” lamaanisha mengi zaidi ya kutokuwa na vita au machafuko. “Katika Biblia, lamaanisha hivyo, na pia lamaanisha hali au uhusiano wenye amani pamoja na Mungu, ufanisi, shangwe, na furaha,” chasema kitabu Studies in the Mosaic Institutions. Hivyo, dhabihu za ushirika zilitolewa si kwa ajili ya kupata amani pamoja na Mungu, kana kwamba kumtuliza, bali ili kushukuru au kusherehekea kwa sababu ya hali nzuri ya amani pamoja na Mungu ambayo hufurahiwa na wale wanaokubaliwa naye. Makuhani na mtoaji walikula dhabihu baada ya kumtolea Yehova damu na mafuta. (Mambo ya Walawi 3:17; 7:16-21; 19:5-8) Katika njia ya mfano na yenye kupendeza, mtoaji, makuhani, na Yehova Mungu walikuwa kana kwamba wanakula pamoja, hilo likionyesha uhusiano wenye amani uliokuwepo miongoni mwao.

16. (a) Kusudi la toleo la dhambi na toleo la hatia lilikuwa nini? (b) Matoleo hayo yalitofautianaje na toleo la kuchomwa?

16 Dhabihu zilizotolewa ili kutafuta msamaha wa dhambi au kufunika ukiukaji wa Sheria zilitia ndani toleo la dhambi na toleo la hatia. Ingawa dhabihu hizi zilichomwa kwenye madhabahu, zilikuwa tofauti na toleo la kuchomwa kwa kuwa mafuta na sehemu fulani za mnyama ndizo zilizotolewa kwa Mungu, bali si mnyama mzima. Mabaki ya mnyama huyo yalitupwa nje ya kambi au wakati mwingine yaliliwa na makuhani. Tofauti hiyo ni muhimu. Toleo la kuchomwa lilikuwa zawadi kwa Mungu ili kufanya iwezekane kumkaribia, hivyo toleo lote lilitolewa kwa Mungu peke yake. Jambo la kutokeza ni kwamba toleo la dhambi au toleo la hatia lilitangulia toleo la kuchomwa, ikidokeza kwamba msamaha wa dhambi ulihitajika ili zawadi ya mtenda-dhambi ikubalike kwa Mungu.—Mambo ya Walawi 8:14, 18; 9:2, 3; 16:3, 5.

17, 18. Toleo la dhambi liliandaliwa kwa sababu gani, na ni kwa kusudi gani matoleo ya hatia yalitolewa?

17 Toleo la dhambi lilikubalika tu kwa ajili ya dhambi isiyo ya kukusudia dhidi ya Sheria, dhambi iliyofanywa kwa sababu ya udhaifu wa mwili. “Kama mtu ye yote akifanya dhambi pasipo kukusudia, katika neno lolote ambalo BWANA amelizuilia lisifanywe,” ndipo mtenda-dhambi angetoa toleo la dhambi kulingana na hadhi, au cheo chake katika jumuiya. (Mambo ya Walawi 4:2, 3, 22, 27) Kwa upande mwingine, watenda-dhambi wasiotubu walikatiliwa mbali; hakukuwa na dhabihu zozote kwa ajili yao.—Kutoka 21:12-15; Mambo ya Walawi 17:10; 20:2, 6, 10; Hesabu 15:30; Waebrania 2:2.

18 Maana na kusudi la toleo la hatia zafafanuliwa katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 5 na 6. Huenda mtu akawa alifanya dhambi bila kukusudia. Hata hivyo, huenda ikawa dhambi yake ilimfanya awe na hatia ya kuvunja haki za wanadamu wenzake au za Yehova Mungu, kosa lililopasa kulipizwa au kusahihishwa. Aina kadhaa za dhambi zinatajwa. Baadhi ya dhambi hizo zilikuwa za faragha (5:2-6), nyingine zilikuwa dhambi dhidi ya “mambo matakatifu ya BWANA” (5:14-16), na nyingine, japo kwa kadiri fulani zilikuwa za kukusudia, zilikuwa dhambi zilizotokana na tamaa mbaya au udhaifu wa mwili (6:1-3). Mbali na kutubu dhambi hizo, mkosaji alitakiwa kutoa fidia ikihitajika kisha kutoa toleo la hatia kwa Yehova.—Mambo ya Walawi 6:4-7.

Kuja kwa Kitu Bora

19. Kwa nini Waisraeli walikosa kibali cha Mungu wajapokuwa na Sheria na dhabihu zake?

19 Waisraeli walipewa Sheria ya Kimusa, pamoja na dhabihu na matoleo yake mengi, ili waweze kumkaribia Mungu kusudi wapate na kudumisha kibali na baraka zake hadi Mbegu iliyoahidiwa ifike. Mtume Paulo, Myahudi kwa kuzaliwa, alieleza jambo hilo hivi: “Sheria imekuwa mfunzi wetu ikiongoza kwa Kristo, ili tupate kutangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani.” (Wagalatia 3:24) Kwa kusikitisha, Israeli likiwa taifa lilikataa kufunzwa, likatumia vibaya pendeleo hilo. Kwa hiyo, dhabihu zao nyingi zikamchukiza Yehova, aliyesema: “Nimejaa mafuta ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng’ombe wala ya wana-kondoo wala ya mbuzi waume.”—Isaya 1:11.

20. Ni nini kilichotukia mwaka wa 70 W.K. kuhusiana na Sheria na dhabihu zake?

20 Mfumo wa mambo wa Wayahudi, pamoja na hekalu lake na ukuhani, ulikoma mwaka wa 70 W.K. Baada ya hilo, haingewezekana kutoa dhabihu kulingana na matakwa ya Sheria. Je, hilo lamaanisha kwamba dhabihu, zikiwa sehemu muhimu ya Sheria, hazina maana yoyote kwa waabudu wa Yehova leo? Tutachunguza jambo hilo katika makala yafuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kichapo Insight on the Scriptures, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., chaeleza: “Kama litumiwavyo katika Biblia, neno ‘ufuniko’ hasa lamaanisha ‘-funika’ au ‘-badilishana,’ nacho kile kinachotolewa ili kubadilishana na kingine, au kikiwa ‘kifuniko’ cha kingine, lazima kilingane na kinachofunikwa. . . . Ili kufunika ifaavyo kile kilichopotezwa na Adamu, toleo la dhambi lenye thamani inayolingana na uhai mkamilifu wa kibinadamu lingetolewa.”

^ fu. 11 Neno la Kiebrania ambalo mara nyingi hutafsiriwa “toleo” ni qor·banʹ. Alipokuwa akiandika juu ya shutumu la Yesu dhidi ya mazoea fulani mabaya ya waandishi na Mafarisayo, Marko alieleza kwamba “korbani” lamaanisha “zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu.”—Marko 7:11.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini kilichowachochea watu waaminifu wa zamani wamtolee Yehova dhabihu?

• Kwa nini dhabihu zilihitajiwa?

• Ni aina gani kuu za dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria, nazo zilikuwa na makusudi gani?

• Kulingana na Paulo, Sheria na dhabihu zake zilitimiza kusudi gani kuu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Dhabihu ya Abeli ilipendeza kwa sababu ilidhihirisha imani yake katika ahadi ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, unaelewa maana ya mandhari hii?