Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umependezwa kusoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Basi, ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba utimizo wa unabii wa “mbingu mpya na nchi mpya” kwenye Isaya 65:17-19 ulitia ndani mengi zaidi ya kurudi kwa Wayahudi kutoka utekwani?

Kwa sababu mitume Petro na Yohana, walioandika katika karne ya kwanza W.K., walirejezea utimizo wa wakati ujao, unaohusisha baraka ambazo zitakuja baadaye. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4)—4/15, ukurasa wa 10-12.

Huenda hekaya za kale za Kigiriki juu ya miungu-wanadamu wenye jeuri zilitokana na nini?

Huenda ikawa hekaya hizo ni habari zilizoongezwa chumvi na zilizopotoshwa kwamba kabla ya Furiko baadhi ya malaika walijivika miili ya kibinadamu na kuishi maisha yenye jeuri na yasiyo ya adili humu duniani. (Mwanzo 6:1, 2)—4/15, ukurasa wa 27.

Wakristo wakomavu wapaswa kujihadhari na hatari zipi kwenye arusi?

Ni muhimu kuepuka sherehe yenye kelele za ulevi na ugomvi unaoweza kutokea ikiwa pombe nyingi inanywewa, na watu wanacheza dansi bila kujidhibiti huku muziki ukiimba kwa sauti kubwa. Isipotajwa waziwazi kwamba kila mtu amekaribishwa kwenye karamu, wale wasioalikwa hawapaswi kuhudhuria. Bwana-arusi apaswa kuhakikisha kwamba wasimamizi Wakristo wanaostahili watakuwepo hadi sherehe hiyo iishe kwa wakati mzuri.—5/1, ukurasa wa 19-22.

Andiko la Zaburi 128:3 linadokeza nini linapotaja wana kuwa “miche ya mizeituni” inayozunguka meza ya mtu?

Mara nyingi machipukizi mapya huchipuka kutoka kwenye shina la mzeituni. Wakati shina kuu la mti wa zamani liachapo kuzaa matunda kwa wingi, linaweza kuzungukwa na machipukizi mapya yenye kusitawi. Vivyo hivyo, wazazi wanaweza kufurahi kuwa na watoto wenye kuzaa matunda wakimtumikia Yehova pamoja nao.—5/15, ukurasa wa 27.

Watoto hupata manufaa gani kutokana na hali nzuri ya kifamilia?

Hiyo hutokeza maoni mazuri juu ya mamlaka, uthamini wa maadili yafaayo, na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Hali kama hiyo inaweza kuwasaidia wawe na urafiki na Mungu.—6/1, ukurasa wa 18.

Katika nchi moja huko Mashariki ya Mbali, ni nini kilichofanywa ili kuwatia moyo akina ndugu waelewe kwamba Wakristo wote ni ndugu?

Makutaniko yote yalihimizwa yasitumie jina la cheo kwa ndugu fulani. Badala yake, wote wanapaswa kuitwa ndugu.—6/15, ukurasa wa 21, 22.

Je, Mashahidi wa Yehova hukubali dawa zinazotokana na damu?

Tunaamini kwamba amri ya Biblia ya ‘kujiepusha na damu’ hukataza kutia mishipani damu au mojawapo ya sehemu zake kuu nne (plazima ya damu, chembe nyekundu au chembe nyeupe, au vigandisha-damu). (Matendo 15:28, 29) Kuhusu visehemu vinavyotokana na zile sehemu kuu za damu, kila Mkristo huamua kibinafsi, akikumbuka yale Biblia isemayo na uhusiano wake pamoja na Mungu.—6/15, ukurasa wa 29-31.

Je, kweli inawezekana kupata amani ya akili leo?

Ndiyo. Kwa kutumia Biblia, Yesu Kristo anawaongoza watu kwenye njia ya ibada safi na amani inayofafanuliwa kwenye Isaya 32:18. Isitoshe, wale wanaopata amani hiyo wanatarajia kufurahia amani yenye kudumu duniani kwa utimizo wa Zaburi 37:11, 29.—7/1, ukurasa wa 7.

George Young alitimiza nini katika historia ya kitheokrasi ya siku hizi?

Kuanzia mwaka wa 1917, yeye alikuwa mchukua-nuru wa habari njema za Ufalme katika nchi nyingi. Huduma yake ilifanya asafiri kotekote Kanada, visiwa vya Karibea, Brazili na nchi nyinginezo za Amerika ya Kusini, Amerika ya Kati, Hispania, Ureno, na ule uliokuwa zamani Muungano wa Sovieti, na Marekani.—7/1, ukurasa wa 22-27.

Andiko la 1 Wakorintho 15:29 lamaanisha nini linaposema kwamba watu fulani ‘wanabatizwa kwa kusudi la kuwa wafu’?

Linamaanisha kwamba wakati Wakristo wanapotiwa mafuta na roho takatifu, wao hufuatia sana maisha ambayo huongoza kwenye kifo na baadaye ufufuo kwenye uhai wa mbinguni.—7/15, ukurasa wa 17.

Mtume Paulo alikuwa akifanya nini katika ile ambayo imeelezwa kuwa miaka yake ya kufuliza kukaa kimya?

Huenda ikawa alisaidia kuanzisha na kuimarisha makutaniko huko Siria na Kilikia. Ni lazima magumu mengi yanayotajwa kwenye 2 Wakorintho 11:23-27 yawe yalitokea wakati huo, ikionyesha kwamba alikuwa anaendelea na huduma yake kwa bidii.—7/15, ukurasa wa 26, 27.

Ni nini kiwezacho kutusaidia tuwe wenye kiasi katika matarajio yetu?

Kumbuka kwamba Yehova anaelewa hisia zetu. Sala kwake inaweza kutusaidia kuwa na usawaziko wa akili, nayo huonyesha kwamba tuna kiasi. Msaada mwingine watokana na kutafuta maoni zaidi kwa kuzungumza na rafiki aliyekomaa.—8/1, ukurasa wa 29, 30.