Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Njia Pekee ya Kukomesha Chuki

Njia Pekee ya Kukomesha Chuki

Njia Pekee ya Kukomesha Chuki

“Palipo na hofu hapakosi chuki. . . . Tunachukia kile tunachokiogopa na hivyo palipo na chuki hofu yaotea.”—CYRIL CONNOLLY, MCHAMBUZI WA FASIHI NA MHARIRI.

WANASOSHIOLOJIA wengi wanaamini kwamba chuki imetia mizizi akilini mwa mwanadamu. “Sehemu kubwa ya chuki huenda hata ikawa imetiwa katika mfumo wote wa utendaji wa akili,” imo ndani ya asili ya kibinadamu, akasema mtaalamu mmoja wa siasa.

Yaeleweka ni kwa nini wanafunzi wanaochunguza hali ya kibinadamu hufikia mikataa ya namna hiyo. Somo la pekee katika uchunguzi wao ni wanaume na wanawake ambao wamezaliwa “katika kosa” na “katika dhambi” kulingana na rekodi ya Biblia iliyopuliziwa. (Zaburi 51:5, NW) Hata Muumba mwenyewe, akikadiria mwanadamu asiye mkamilifu katika milenia zilizopita, ‘aliona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.’—Mwanzo 6:5.

Ubaguzi, upendeleo, na matokeo yake ya chuki hutokana na ubinafsi na kutokamilika kwa mwanadamu kulikorithiwa. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Kwa kusikitisha, hapana shirika lolote la kibinadamu au serikali, hata sera yake iwe gani, ambayo imeweza kufanyiza sheria iwezayo kubadilisha moyo wa mwanadamu katika mambo hayo. Mleta-habari wa nchi za kigeni Johanna McGeary alisema: “Hakuna polisi wa ulimwenguni pote, hata awe mwenye uwezo kadiri gani, awezaye kuingilia mambo na kuondoa chuki ambayo imesababisha umwagaji mwingi wa damu katika Bosnia, Somalia, Liberia, Kashmir, na Caucasus.”

Hata hivyo, kabla ya kutafuta utatuzi, lazima tupate kuelewa kiini cha visa vya chuki.

Chuki Yachochewa na Hofu

Chuki hujitokeza kwa njia nyingi. Mwandishi Andrew Sullivan alifafanua hali hiyo vizuri: “Kuna chuki yenye hofu, na chuki yenye kuhisi tu kuchukizwa; kuna chuki ya kuonyesha uwezo, na chuki ya kutokuwa na uwezo; kuna ulipizaji kisasi, na kuna chuki inayotokana na husuda. . . . Kuna chuki ya mwonezi, na chuki ya mwenye kuonewa. Kuna chuki ya kichinichini, na chuki inayokwisha. Na kuna chuki ilipukayo, na chuki isiyopamba moto kamwe.”

Bila shaka, baadhi ya sababu kuu zinazochochea mapambano ya chuki katika siku zetu ni zile za kijamii na kiuchumi. Ubaguzi mbaya sana na milipuko ya chuki mara nyingi hutokea katika maeneo ambamo mna matajiri wachache. Chuki huonekana pia katika mahali ambapo kiwango cha maisha cha sehemu fulani ya jumuiya chatishwa na mmiminiko wa wageni.

Baadhi yao huenda wakahisi kwamba wageni hao watachukua kazi zao, wakilipwa mishahara ya chini, au kusababisha kupungua kwa thamani ya mali. Iwe hofu hiyo ina msingi au la ni jambo jingine. Hofu ya kupata hasara kiuchumi na hofu kwamba viwango vya jamii au mtindo wake wa maisha utazorota ni sababu zenye nguvu zinazotokeza ubaguzi na chuki.

Ni hatua gani yapasa kuwa ya kwanza katika kukomesha chuki? Ni badiliko la mitazamo.

Kubadilisha Mitazamo

“Badiliko la kweli lawezekana tu kutokana na nia ya watu wanaohusika,” akasema McGeary. Na nia ya watu inaweza kubadilishwaje? Imeonekana kwamba jambo lenye nguvu zaidi, lenye kuchochea zaidi, na lenye uvutano wenye kudumu zaidi dhidi ya kusitawisha chuki hupatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Hiyo ni kwa sababu “neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.”—Waebrania 4:12.

Ni kweli kwamba ubaguzi na chuki haziwezi kuondolewa bila jitihada zozote, wala jambo hili haliwezi kufanywa kwa usiku mmoja. Lakini linaweza kufanywa. Yesu Kristo, yule mchocheaji mkuu wa moyo na dhamiri, aliweza kuwafanya watu wabadilike. Mamilioni ya watu wamefaulu kwa kufuata shauri hili lenye hekima la Yesu Kristo: “Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi.”—Mathayo 5:44.

Kupatana na mafundisho yake, Yesu alimfanya Mathayo, aliyekuwa hapo zamani mtoza-ushuru mwenye kuchukiwa na kutengwa mbali na jamii ya Kiyahudi, awe mmoja wa rafiki zake aliowaitibari sana. (Mathayo 9:9; 11:19) Zaidi ya hayo, Yesu alianzisha ibada safi ambayo hatimaye ingetia ndani maelfu ya wasio Wayahudi ambao hapo awali walichukiwa na kukataliwa. (Wagalatia 3:28) Watu kutoka pande zote za ulimwengu uliojulikana wakati huo wakawa wafuasi wa Yesu Kristo. (Matendo 10:34, 35) Watu hao walikuja kujulikana kwa sababu ya upendo wao wenye kuzidi sana. (Yohana 13:35) Mwanafunzi wa Yesu, Stefano, alipokuwa akipigwa kwa mawe na watu wenye chuki nyingi, alisema maneno haya kabla ya kufa: “Yehova, usihesabu dhambi hii dhidi yao.” Stefano aliwatakia mema hao waliomchukia.—Matendo 6:8-14; 7:54-60.

Wakristo wa kweli wa siku hizi wameitikia vivyo hivyo shauri la Yesu lenye kuwaagiza wafanye mema, si kwa ndugu Wakristo wenzao tu, bali hata kwa wale wanaowachukia. (Wagalatia 6:10) Wanafanya bidii kuondoa katika maisha yao chuki mbaya. Wakitambua kani zenye nguvu zinazoweza kusababisha chuki ndani yao, wao huchukua hatua nzuri na kufanya upendo uchukue mahali pa chuki. Naam, ni kama alivyosema mtu mmoja mwenye hekima aliyeishi zamani, “kuchukiana huondokesha fitina; bali kupendana husitiri makosa yote.”—Mithali 10:12.

Mtume Yohana alisema hivi: “Kila mtu ambaye huchukia ndugu yake ni muua-binadamu-kikatili, nanyi mwajua kwamba hakuna muua-binadamu-kikatili aliye na uhai udumuo milele ukikaa katika yeye.” (1 Yohana 3:15) Mashahidi wa Yehova wanaamini hilo. Tokeo ni kwamba sasa wao wanaunganishwa—kutoka makabila yote, tamaduni zote, dini zote, na hali zote za kisiasa—kuwa jumuiya moja iliyoungana na isiyo na chuki, udugu halisi wa ulimwenguni pote.—Ona masanduku ambayo yameambatanishwa.

Chuki Itakomeshwa!

Huenda ukasema, ‘lakini hilo linafaa sana watu wanaohusika. Hata hivyo, hilo haliwezi kuondoa chuki duniani.’ Ni kweli kwamba hata kama wewe binafsi huna chuki moyoni mwako, bado unaweza kupatwa na madhara yake. Basi ni lazima tumtegemee Mungu atoe suluhisho halisi kwa tatizo hilo la ulimwenguni pote.

Mungu akusudia kuondoa karibuni masalio yote ya chuki katika dunia. Hilo litafanyika chini ya utawala wa serikali ya mbinguni ambao Yesu alitufundisha kusali juu yake hivi: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.

Wakati sala hiyo ijibiwapo kikamili, hali ambazo huchochea chuki hazitakuwapo tena. Hali zinazotokeza chuki zitaondolewa. Propaganda, kutojua, na ubaguzi hazitakuwapo na badala yake kutakuwa na ujuzi, kweli, na uadilifu. Ndipo kwa kweli, Mungu atakuwa ‘amefuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.’—Ufunuo 21:1-4.

Sasa habari bora hata zaidi! Kuna uthibitisho usioweza kukanushwa kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” Hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba hivi karibuni tutaona chuki mbaya ikitoweka katika dunia. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3-14) Katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi, udugu halisi utakuwepo kwa sababu wanadamu watakuwa wamerudishwa kwenye ukamilifu.—Luka 23:43; 2 Petro 3:13.

Lakini si lazima kungojea hadi wakati ujao ili ufurahie udugu halisi. Kwa kweli, kama inavyoonyeshwa katika masimulizi yanayofuata, upendo wa Kikristo unatenda sasa ndani ya mioyo ya mamilioni ya watu ambayo ingekuwa imejawa na chuki. Wewe pia unakaribishwa uwe sehemu ya udugu huo wenye upendo!

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

“Yesu Angalifanya Nini?”

Mnamo Juni 1998, katika sehemu za mashambani za Texas, Marekani, wazungu watatu walimshambulia mtu mmoja mweusi James Byrd, Jr. Walimpeleka mbali, mahali pasipo na watu, wakampiga na kufunga miguu yake kwa mnyororo. Halafu wakamfunga nyuma ya gari aina ya pickup na kumburuta kilometa tano barabarani mpaka mwili wake ulipogonga mtaro. Kisa hiki kimetajwa kuwa uhalifu wenye kuchochewa na chuki wenye kuogofya zaidi katika miaka ya 1990.

Dada watatu wa James Byrd ni Mashahidi wa Yehova. Wanawaonaje wale waliotenda kitendo hicho chenye kuogofya? Katika taarifa ya pamoja walisema hivi: “Kuteswa vibaya na kuuawa kwa mtu mpendwa kulituumiza sana na kutuhuzunisha sana. Mtu apaswa kuitikiaje kitendo cha ukatili wa jinsi hiyo? Hatukuwahi kufikiria kulipiza kisasi, kuwa na usemi wenye kujaa chuki, au kuanzisha propaganda ya chuki. Tuliwaza hivi: ‘Yesu angalifanya nini? Angeitikiaje?’ Jibu lilikuwa wazi sana. Ujumbe wake ungekuwa wa amani na tumaini.”

Kati ya marejezo ya Maandiko yaliyowasaidia wasisitawishe chuki ndani ya mioyo yao ni Waroma 12:17-19. Mtume Paulo aliandika hivi: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. . . . Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’”

Wakaendelea kusema: “Tunakumbuka taarifa halisi zinazopatikana kwenye vichapo vyetu ambazo zaonyesha kwamba baadhi ya udhalimu au uhalifu ni mbaya sana hivi kwamba ingekuwa vigumu kusema tu ‘nimekusamehe’ na kuondoka. Kusamehe katika hali kama hizo huenda ni kuondoa tu kinyongo moyoni na kuendelea mbele na maisha ili kuepuka kuwa mgonjwa kimwili au kiakili kwa sababu ya kufungia kinyongo.” Ni ushuhuda ulio dhahiri kama nini wa uwezo wa Biblia wa kuzuia chuki yenye nguvu isikue!

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Chuki Yageuzwa Kuwa Urafiki

Katika miaka ya karibuni, maelfu ya wahamiaji wamemiminika Ugiriki kutafuta kazi. Hata hivyo, hali ya uchumi inayozidi kuzorota imepunguza fursa za kupata kazi, na hilo limezidisha ushindani kati ya wanaotaka kuajiriwa. Tokeo limekuwa uhasama mkubwa miongoni mwa watu wa jamii tofauti-tofauti. Mashindano kati ya wahamiaji kutoka Albania na wale wa kutoka Bulgaria ni mfano halisi. Katika sehemu nyingi za Ugiriki, kumekuwa na ushindani mkali kati ya watu wa jamii hizo mbili.

Katika mji wa Kiato, kaskazini-mashariki mwa Peloponnisos, familia moja kutoka Bulgaria na mtu mmoja kutoka Albania walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na wakajuana. Kutumia kanuni za Biblia kulimaliza chuki iliyoko kati ya wengi wa jamii hizo mbili. Pia kulichangia urafiki halisi wa kidugu kati ya watu hao. Ivan, ambaye ni Mbulgaria hata alimsaidia Loulis yule Mualbania, apate makao kando ya nyumba ya Ivan. Mara nyingi familia hizi mbili hushiriki pamoja milo na vitu vichache vya kimwili walivyo navyo. Wanaume hawa wawili sasa ni Mashahidi wa Yehova waliobatizwa na wanashirikiana sana katika kuhubiri habari njema. Ni wazi kwamba majirani wanaona urafiki huu wa Kikristo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Chini ya Ufalme wa Mungu masalio yote ya chuki yataondolewa duniani