Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Mtazamo wa Kungoja!

Onyesha Mtazamo wa Kungoja!

Onyesha Mtazamo wa Kungoja!

“Nitamngojea [“Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea,” “NW”] Mungu wa wokovu wangu; Mungu wangu atanisikia.”—MIKA 7:7.

1, 2. (a) Mtazamo usiofaa uliwadhuru Waisraeli nyikani jinsi gani? (b) Mkristo asiyesitawisha mtazamo unaofaa aweza kupatwa na nini?

MAMBO mengi maishani yaweza kuonwa kwa njia nzuri au mbaya, ikitegemea mtazamo wetu. Waisraeli walipokuwa nyikani, walipewa mana kimwujiza. Ingaliwapasa kutazama nchi kame iliyowazunguka na kumshukuru sana Yehova kwa kuwaruzuku. Huo ungekuwa mtazamo mzuri. Badala ya hivyo, walikumbuka vyakula mbalimbali vya Misri na kulalamika kwamba mana si tamu. Mtazamo huo ulikuwa mbaya kama nini!—Hesabu 11:4-6.

2 Hali kadhalika, mtazamo wa Mkristo leo waweza kufanya mambo yaonekane mazuri au mabaya. Pasipo mtazamo unaofaa, Mkristo aweza kupoteza furaha yake kwa urahisi, na hiyo ingekuwa hatari kwa sababu, kama alivyosema Nehemia: “Furaha ya BWANA ni nguvu [zetu].” (Nehemia 8:10) Mtazamo mzuri, wenye furaha, hutusaidia kudumisha nguvu zetu na kuendeleza amani na umoja kutanikoni.—Waroma 15:13; Wafilipi 1:25.

3. Mtazamo unaofaa ulimsaidiaje Yeremia ijapokuwa aliishi nyakati ngumu?

3 Ijapokuwa aliishi nyakati ngumu, Yeremia alidhihirisha mtazamo mzuri. Hata alipoona maafa ya kuanguka kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., bado alitarajia mema. Yehova hangesahau Israeli, na taifa hilo lingeokoka. Yeremia aliandika katika kitabu cha Maombolezo: “Ni huruma za BWANA kwamba hatuangamii, kwa kuwa rehema zake hazikomi. Ni mpya kila siku asubuhi; uaminifu wako ni mkuu.” (Maombolezo 3:22, 23) Tangu kale, watumishi wa Mungu katika hali ngumu zaidi wametafuta kudumisha mtazamo mzuri, wenye furaha.—2 Wakorintho 7:4; 1 Wathesalonike 1:6; Yakobo 1:2.

4. Yesu alidumisha mtazamo gani, nao ulimsaidiaje?

4 Miaka 600 baada ya Yeremia, Yesu alifaulu kuvumilia kwa sababu ya mtazamo wake mzuri. Twasoma hivi: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele [ya Yesu] alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Waebrania 12:2) Bila kujali upinzani au mnyanyaso aliokabili Yesu—hata maumivu ya mti wa mateso—alikaza akili yake kwenye “shangwe iliyowekwa mbele yake.” Shangwe hiyo ilikuwa pendeleo la kutetea enzi kuu ya Yehova na kulitakasa jina lake na vilevile tazamio la kuwaletea wanadamu watiifu baraka nyingi wakati ujao.

Uwe na Mtazamo wa Kungoja

5. Ni katika hali gani hasa mtazamo wa kungoja utatusaidia kudumisha maoni yanayofaa kwa mambo?

5 Tukisitawisha mtazamo wa akili kama wa Yesu, hatutapoteza shangwe ya Yehova hata mambo yasipofanyika vile tunavyotarajia, wakati tunapoyatarajia. Nabii Mika alisema: “Lakini mimi, nitamtazamia BWANA; nitamngojea [“nitaonyesha mtazamo wa kumngojea,” NW] Mungu wa wokovu wangu.” (Mika 7:7; Maombolezo 3:21) Sisi pia twaweza kuonyesha mtazamo wa kungoja. Vipi? Kwa njia nyingi. Kwa mfano, labda tunahisi kuwa ndugu fulani mwenye mamlaka amekosa na kwamba rekebisho la haraka lahitajika. Mtazamo wa kungoja utatupa nafasi ya kufikiria, ‘Je, kweli alikosa, au mimi sikuelewa hali vizuri? Ikiwa alikosa, yawezekana kwamba Yehova anaruhusu mambo yatukie kwa maana anahisi kwamba mtu huyo atafanya mabadiliko na hakuna haja ya kuchukua hatua kali ya kumrekebisha?’

6. Mtazamo wa kungoja utamsaidiaje mtu anayepambana na tatizo la kibinafsi?

6 Huenda mtazamo wa kungoja ukahitajika wakati jambo fulani la kibinafsi latutatiza au tunapopambana na udhaifu fulani. Tuseme tatizo linaendelea hata baada ya kumwomba Yehova msaada. Nini basi? Sharti tuendelee kufanya yale tuwezayo kulisuluhisha tatizo hilo kisha tuyatumaini maneno ya Yesu: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata; fulizeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa.” (Luka 11:9) Endelea kusali, na umngojee Yehova. Yehova atajibu sala zako kwa njia inayofaa na kwa wakati wake mwenyewe.—1 Wathesalonike 5:17.

7. Mtazamo wa kungoja utatusaidiaje kuwa na maoni ya kupata uelewevu wa Biblia ulioboreshwa hatua kwa hatua?

7 Unabii mbalimbali wa Biblia uendeleapo kutimia, uelewevu wetu wa Maandiko huboreka. Hata hivyo, huenda nyakati nyingine tukaona kwamba wakati wa ufafanuzi fulani umefika. Ikiwa ufafanuzi huo hauji wakati tunapotaka, je, tuko tayari kungoja? Kumbuka kwamba ilimpendeza Yehova kufunua kidogo kidogo “siri takatifu ya Kristo” kwa kipindi cha miaka ipatayo 4,000. (Waefeso 3:3-6) Basi je, tuna sababu yoyote ya kukosa subira? Je, tunashuku kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amewekwa rasmi kuwapa watu wa Yehova “chakula chao kwa wakati unaofaa”? (Mathayo 24:45) Mbona tujinyime furaha ya kimungu kwa sababu tu hatuelewi mambo yote kikamilifu? Kumbuka, Yehova huamua ni lini na jinsi gani azifunue “siri” zake.—Amosi 3:7.

8. Subira ya Yehova imekuja kuwanufaishaje wengi?

8 Huenda wengine wakavunjika moyo kwa sababu wanaona kwamba baada ya miaka mingi ya utumishi mwaminifu, labda watakufa kabla ya “siku ya BWANA [“Yehova,” NW] iliyo kuu na itishayo.” (Yoeli 2:30, 31) Ingawa hivyo, wanaweza kutiwa moyo wanapotazama mambo kwa njia inayofaa. Petro alishauri hivi: “Ioneni subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.” (2 Petro 3:15) Subira ya Yehova imewawezesha mamilioni zaidi ya watu wenye mioyo minyofu wajifunze kweli. Je, hilo si jambo zuri? Na zaidi, kadiri Yehova anavyodhihirisha subira, ndivyo tunavyopata wakati zaidi wa ‘kufuliza kufanyiza wokovu wetu wenyewe kwa hofu na kutetemeka.’—Wafilipi 2:12; 2 Petro 3:11, 12.

9. Ikiwa tuna kizuizi fulani katika yale tunayoweza kufanya katika utumishi wa Yehova, mtazamo wa kungoja utatusaidiaje kuvumilia hali hiyo?

9 Mtazamo wa kungoja hutusaidia tusivunjike moyo wakati upinzani, ugonjwa, uzee, au matatizo mengine yanapotuwekea vikwazo katika utumishi wa Ufalme. Yehova atarajia tumtumikie kwa moyo wote. (Waroma 12:1) Hata hivyo, Mwana wa Mungu, ‘anayemhurumia aliye dhaifu na maskini,’ hadai mengi kuliko yale tuwezayo kutoa, wala Yehova hafanyi hivyo. (Zaburi 72:13) Basi, twatiwa moyo tufanye yale tuwezayo, tukingoja kwa subira hadi hali zibadilike—ama katika mfumo huu wa mambo au ule utakaokuja. Kumbuka: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.

10. Mtu mwenye mtazamo wa kungoja aweza kuepuka tabia gani isiyomcha Mungu? Eleza.

10 Mtazamo wa kungoja pia hutusaidia kuepuka kiburi. Watu fulani ambao wameasi imani hawakuwa tayari kungoja. Labda waliona kuna uhitaji wa marekebisho katika uelewevu wa Biblia au katika mambo ya kitengenezo. Lakini, walishindwa kukubali kwamba roho ya Yehova humchochea mtumwa mwaminifu na mwenye busara kufanya marekebisho kwa wakati Wake, wala si wakati tunapofikiri hayo yanahitajika. Na marekebisho yoyote yale lazima yapatane na mapenzi ya Yehova, si mawazo yetu binafsi. Waasi-imani huruhusu mtazamo wa kiburi upotoe fikira zao na kuwakwaza. Lakini kama wangalikuwa na mtazamo wa akili wa Kristo, wangalidumisha shangwe yao na kubaki miongoni mwa watu wa Yehova.—Wafilipi 2:5-8.

11. Twaweza kutumiaje kwa faida wakati wa kungoja, kwa kufuata vielelezo vya akina nani?

11 Bila shaka, kudumisha mtazamo wa kungoja hakumaanishi kuwa mvivu au kukaa bure. Tuna mambo ya kufanya. Kwa mfano, twahitaji kujishughulisha na funzo la Biblia la kibinafsi na hivyo tuonyeshe upendezi uleule wa makini kwa mambo ya kiroho ulioonyeshwa na manabii waaminifu na hata malaika. Akizungumza kuhusu upendezi huo, Petro asema: “Kuhusu wokovu huu wenyewe kuulizia habari kwa bidii yenye kuendelea na utafutaji wa uangalifu sana ulifanywa na manabii . . . Ndani ya mambo hayohayo malaika wanatamani kuchungulia.” (1 Petro 1:10-12) Mbali na funzo la kibinafsi, ni lazima pia tuhudhurie mikutano kwa ukawaida, na kusali. (Yakobo 4:8) Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho kwa kujilisha chakula cha kiroho kwa ukawaida na kushirikiana na Wakristo wenzao huonyesha kwamba wameukubali mtazamo wa akili wa Kristo.—Mathayo 5:3.

Ona Mambo kwa Njia Halisi

12. (a) Adamu na Hawa walitafuta uhuru gani? (b) Wanadamu wamepatwa na nini kwa kufuata matendo ya Adamu na Hawa?

12 Mungu alipowaumba wanadamu wa kwanza wawili, alihifadhi haki ya kuweka viwango vya mema na mabaya. (Mwanzo 2:16, 17) Adamu na Hawa walitaka kujitegemea pasipo mwongozo wa Mungu, na hilo likatokeza ulimwengu tunaouona leo. Mtume Paulo alisema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Miaka elfu sita ya historia ya wanadamu tangu wakati wa Adamu imethibitisha ukweli wa maneno ya Yeremia: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Tunapokiri kwamba maneno ya Yeremia ni ya kweli, hiyo haimaanishi tuna mtazamo wa kushindwa. Ni kuona mambo kihalisi. Hayo yaonyesha sababu gani “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake” kwa karne zote ambazo wanadamu wametawala pasipo kumtegemea Mungu.—Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989.

13. Mashahidi wa Yehova wanaonaje mambo kwa njia halisi kuhusiana na yale ambayo wanadamu waweza kutimiza?

13 Kwa kuzingatia hali ya wanadamu, Mashahidi wa Yehova hutambua kuwa kuna mipaka kwa mambo yanayoweza kutimizwa katika mfumo wa mambo wa sasa. Mtazamo mzuri waweza kutusaidia kudumisha shangwe, lakini huo hausuluhishi kila kitu. Mapema miaka ya 1950, kasisi mmoja wa Marekani alichapisha kitabu kilichouzwa sana kiitwacho The Power of Positive Thinking. Kitabu hicho kilidokeza kwamba vikwazo vingi vyaweza kushindwa mtu akipambana navyo akiwa na mtazamo mzuri. Bila shaka kufikiri kunakofaa hutamanika. Ijapokuwa hivyo, mambo yaliyoonwa yaonyesha kwamba ujuzi, ustadi, mali za kimwili, na mambo mengine mengi huzuia mambo tunayoweza kutimiza sisi binafsi. Na katika ulimwengu kwa jumla, kuna matatizo makubwa mno ambayo wanadamu hawawezi kuyasuluhisha kwa mafanikio, hata kama wana mawazo mazuri!

14. Je, Mashahidi wa Yehova wana mtazamo mbaya? Eleza.

14 Kwa sababu ya kuona mambo hayo kwa njia halisi, nyakati nyingine Mashahidi wa Yehova hushutumiwa kwamba wana mtazamo mbaya. Kinyume cha hilo, Mashahidi wana hamu ya kuwaambia watu kuhusu Yule awezaye kuboresha hali ya wanadamu kwa njia ya kudumu. Kwa habari hiyo pia, wao huiga mtazamo wa akili wa Kristo. (Waroma 15:2) Na pia wanajishughulisha sana kuwasaidia watu wawe na uhusiano mzuri na Mungu. Wanafahamu kwamba hatimaye, uhusiano huo utaleta manufaa bora zaidi.—Mathayo 28:19, 20; 1 Timotheo 4:16.

15. Kazi ya Mashahidi wa Yehova huboreshaje hali ya watu mmoja-mmoja?

15 Mashahidi wa Yehova hawapuuzi matatizo ya kijamii—hasa matendo machafu yasiyo ya Kimaandiko—yanayowazunguka. Kabla mtu mwenye kupendezwa hajawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yeye hufanya mabadiliko, na mara nyingi inambidi kushinda mazoea maovu yanayomchukiza Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova wamewasaidia watu wanaoitikia ifaavyo waache ulevi, uraibu wa dawa za kulevya, ukosefu wa maadili, na uraibu wa kucheza kamari. Watu hao waliobadili tabia wamejifunza kuruzuku familia zao ifaavyo na kwa unyofu. (1 Timotheo 5:8) Watu mmoja-mmoja na familia zinaposaidiwa hivyo, matatizo hupungua katika jumuiya—idadi ya waraibu wa dawa za kulevya hupungua, visa vya jeuri ya familia hupungua, na kadhalika. Kwa kuwa raia wanaofuata sheria na kwa kuwasaidia wengine kuboresha maisha yao, Mashahidi wa Yehova hupunguza mzigo wa mashirika ambayo yana wajibu wa kushughulikia matatizo ya kijamii.

16. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na vikundi vya kilimwengu vya kuleta mabadiliko ya kijamii?

16 Basi, je, Mashahidi wa Yehova wamebadili hali ya maadili ulimwenguni? Katika miaka kumi iliyopita, idadi ya Mashahidi watendaji iliongezeka kutoka 3,800,000 hivi hadi karibu 6,000,000. Hilo ni ongezeko la karibu watu 2,200,000, na wengi wao waliacha mazoea maovu walipopata kuwa Wakristo. Maisha ya watu wengi yameboreka! Ingawa hivyo, idadi hiyo ni ndogo sana ilinganishwapo na ongezeko la idadi ya watu ulimwenguni wakati huohuo—875,000,000! Mashahidi wa Yehova wamepata furaha kuwasaidia watu mmoja-mmoja wanaoitikia ifaavyo, ingawa wanatambua kuwa ni watu wachache watakaofuata barabara iendayo kwenye uhai. (Mathayo 7:13, 14) Mashahidi wanapongojea mabadiliko ambayo Mungu ataleta ulimwenguni kote ili kuboresha hali, hawajihusishi na vikundi vya kilimwengu vya kuleta mabadiliko ya kijamii, ambavyo mara nyingi huanza kwa makusudio mema lakini huishia kuvunjika moyo na hata jeuri.—2 Petro 3:13.

17. Yesu alifanya nini ili kuwasaidia wale waliokuwa karibu naye, lakini ni nini ambalo hakufanya?

17 Kwa kufuata mwendo huo, Mashahidi wa Yehova huonyesha tumaini lilelile ambalo Yesu alikuwa nalo katika Yehova alipokuwa duniani. Huko nyuma katika karne ya kwanza, Yesu alifanya miujiza ya kuponya. (Luka 6:17-19) Hata alifufua wafu. (Luka 7:11-15; 8:49-56) Lakini hakuondoa tatizo la ugonjwa wala kushinda adui kifo. Alijua kuwa wakati wa Mungu wa kufanya hivyo haukuwa umefika. Yesu, aliyekuwa na uwezo bora mbalimbali akiwa mwanadamu mkamilifu, angalifanya mengi kutatua matatizo mazito ya kisiasa na kijamii. Yaonekana baadhi ya watu wa siku zake walitaka atwae mamlaka na kutatua matatizo hayo, lakini Yesu akakataa. Twasoma hivi: “Watu hao walipoona ishara alizofanya, wakaanza kusema: ‘Kwa hakika huyu ndiye nabii aliyepaswa kuja ulimwenguni.’ Kwa hiyo Yesu, akijua walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye mfalme, akaondoka tena kwenda kuingia mlimani yeye mwenyewe peke yake.”—Yohana 6:14, 15.

18. (a) Yesu ameonyeshaje mtazamo wa kungoja sikuzote? (b) Utendaji wa Yesu umebadilikaje tangu mwaka wa 1914?

18 Yesu alikataa kujihusisha katika siasa au katika kazi iliyohusisha tu jamii kwa sababu alijua kwamba wakati wake wa kutwaa mamlaka ya kifalme na kufanya kazi za kuponya kila mtu kila mahali haukuwa umefika. Hata baada ya kupaa mbinguni kwenye uhai wa kiroho usioweza kufa, alikuwa tayari kungoja wakati rasmi wa Yehova kabla ya kuchukua hatua. (Zaburi 110:1; Matendo 2:34, 35) Lakini tangu alipotawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914, anasonga mbele “akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufunuo 6:2; 12:10) Tunashukuru kama nini kwamba tunajitiisha kwa utawala wake, ilhali wengine wanaodai kuwa Wakristo wameamua kupuuza mafundisho ya Biblia kuhusu Ufalme!

Kungoja—Huvunja Moyo au Huleta Shangwe?

19. Ni wakati gani kungoja hufanya ‘moyo uugue,’ na ni wakati gani kunapoleta shangwe?

19 Solomoni alijua kwamba kungoja kwaweza kuvunja moyo. Aliandika hivi: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” (Mithali 13:12) Kwa hakika, mtu akiwa na matarajio yasiyo na msingi, moyo waweza kuugua kwa kukata tamaa. Hata hivyo, kungojea matukio yenye furaha—labda arusi, kuzaliwa kwa mtoto, au kuungana tena na watu tuwapendao—kwaweza kutujaza shangwe ya kuyatazamia matukio hayo muda mrefu kabla ya siku kufika. Shangwe hiyo huzidishwa tunapotumia kwa hekima wakati wa kungoja, tukifanya matayarisho kwa ajili ya matukio hayo yanayokuja.

20. (a) Tunatarajia kwa uhakika kuona matukio gani mazuri? (b) Twaweza kupataje shangwe tunapongojea makusudi ya Yehova yatimie?

20 Tunapotumaini kikamilifu kwamba matarajio yetu yatatimia—hata tusipojua ni lini yatatimia—si lazima kipindi cha kungoja kiufanye ‘moyo uugue.’ Waabudu waaminifu wa Mungu wanajua kuwa Utawala wa Milenia wa Kristo u karibu. Wana uhakika kwamba wataona ukomo wa kifo na ugonjwa. Kwa hamu kubwa, wanangojea kwa shangwe wakati ambapo watawakaribisha mabilioni kutoka kwa wafu, wakiwemo wapendwa wao waliokufa. (Ufunuo 20:1-3, 6; 21:3, 4) Katika nyakati hizi za uharibifu wa mazingira, wanashangilia tazamio hakika la kuona Paradiso ikianzishwa duniani. (Isaya 35:1, 2, 7) Basi, ni jambo la hekima kama nini kutumia kwa busara wakati wa kungoja, ‘sikuzote tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana’! (1 Wakorintho 15:58) Endelea kujilisha chakula cha kiroho. Endelea kujenga uhusiano wa karibu zaidi na Yehova. Tafuta wengine ambao mioyo yao huwachochea kumtumikia Yehova. Watie moyo waamini wenzako. Tumia kikamilifu wakati wowote ule ambao huenda Yehova akaruhusu. Ndipo kumngojea Yehova hakutaufanya ‘moyo wako uugue kamwe.’ Badala yake, kutakujaza shangwe!

Unaweza Kueleza?

• Yesu alionyeshaje mtazamo wa kungoja?

• Ni katika hali gani Wakristo wanahitaji mtazamo wa kungoja?

• Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanaridhika kumngojea Yehova?

• Kumngojea Yehova kwawezaje kuwa jambo lenye kuleta shangwe?

[Maswalu ya funzos]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yesu alivumilia kwa sababu ya shangwe iliyowekwa mbele yake

[Picha katika ukurasa wa 13]

Hata baada ya miaka mingi ya utumishi, twaweza kudumisha shangwe yetu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mamilioni wameboresha maisha yao kwa kuwa Mashahidi wa Yehova