Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Saa Imekuja!”

“Saa Imekuja!”

“Saa Imekuja!”

“Saa yake ilikuwa imekuja ya kuhama kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba.” —Yohana 13:1.

1. Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K. ikaribiapo, Yerusalemu limesisimuliwa na uvumi gani, na kwa nini?

ALIPOBATIZWA mwaka wa 29 W.K., Yesu alianza maisha ambayo yangeongoza kwenye “saa” ya kifo, ufufuo na kutukuzwa kwake. Sasa ni masika ya 33 W.K. Ni majuma kadhaa tu ambayo yamepita tangu mahakama kuu ya Wayahudi, Sanhedrini, iliposhauriana kumwua Yesu. Baada ya kujua mpango wao, labda kutoka kwa Nikodemo, mshiriki wa Sanhedrini ambaye amekuwa mwenye urafiki kwake, Yesu ameondoka Yerusalemu na ameenda mashambani, ng’ambo ya Mto Yordani. Msherehekeo wa Sikukuu ya Kupitwa ukaribiapo, watu wengi wanatoka mashambani kwenda Yerusalemu, na jiji limejaa uvumi kuhusu Yesu. “Kauli yenu ni nini?” watu wanaulizana. “Kwamba hatakuja kwenye msherehekeo hata kidogo?” Makuhani wakuu na Mafarisayo wamezidisha msisimuko huo kwa kutoa maagizo kwamba yeyote anayemwona Yesu apaswa kuwapasha habari yeye yuko wapi.—Yohana 11:47-57.

2. Ni tendo gani la Maria linaloleta ubishi, na jibu la Yesu kwa kumtetea laonyesha nini kuhusu ufahamu wake wa “saa yake”?

2 Nisani 8, siku sita kabla ya Sikukuu ya Kupitwa, Yesu amerudi karibu na Yerusalemu. Anakuja Bethania—mji wa nyumbani wa rafiki zake wapendwa Martha, Maria, na Lazaro—ambao uko umbali wa kilometa tatu nje ya Yerusalemu. Ni Ijumaa jioni, na Yesu anakaa huko siku ya Sabato. Jioni inayofuata, wakati Maria anapomhudumia akitumia mafuta ghali yenye marashi, wanafunzi wanapinga jambo hilo. Yesu anawajibu: “Mwacheni, ili ashike mwadhimisho huu kwa kufikiria siku ya maziko yangu. Kwa maana mna maskini pamoja nanyi sikuzote, lakini mimi hamtakuwa nami sikuzote.” (Yohana 12:1-8; Mathayo 26:6-13) Yesu anajua kwamba ‘saa yake imekuja ya kuhama kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba.’ (Yohana 13:1) Baada ya siku tano yeye ‘atatoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Marko 10:45) Tangu wakati huo, Yesu anafundisha na kufanya kila jambo kwa hima. Hicho ni kielelezo kizuri kama nini kwetu tunapongojea kwa hamu mwisho wa mfumo huu wa mambo! Ona yanayompata Yesu siku inayofuata.

Siku Yesu Anapoingia kwa Shangwe ya Ushindi

3. (a) Yesu anaingiaje Yerusalemu Jumapili, Nisani 9, na wengi wa wale wanaomzunguka wanafanyaje? (b) Yesu anawajibuje Mafarisayo wanaolalamika kuhusu umati huo?

3 Jumapili, Nisani 9, Yesu anaingia Yerusalemu kwa shangwe ya ushindi. Anapokaribia jiji—akipanda mwana-punda kwa utimizo wa Zekaria 9:9—watu wengi ambao wamekusanyika kumzunguka wanayatandaza mavazi yao barabarani, huku wengine wakikata matawi ya miti na kuyatandaza chini. “Mbarikiwa ni Yule anayekuja akiwa ndiye Mfalme katika jina la Yehova!” wanapaaza sauti. Mafarisayo fulani katika umati wanataka Yesu awakemee wanafunzi wake. Hata hivyo, Yesu anawajibu: “Mimi nawaambia nyinyi, Kama hawa wangekaa kimya, mawe yangepaaza kilio.”—Luka 19:38-40; Mathayo 21:6-9.

4. Kwa nini jiji la Yerusalemu linasisimuka Yesu anapoingia humo?

4 Majuma kadhaa mapema, wengi katika umati huo walimwona Yesu akimfufua Lazaro. Sasa hawa wanaendelea kuwaambia wengine muujiza huo. Kwa hiyo, Yesu anapoingia Yerusalemu, jiji lote linasisimuka. “Ni nani huyu?” watu wanauliza. Nao umati unaendelea kusema: “Huyu ndiye nabii Yesu, kutoka Nazareti ya Galilaya!” Wanapoona yanayotukia, Mafarisayo wanahuzunika: “Ulimwengu umemfuata.”—Mathayo 21:10, 11; Yohana 12:17-19.

5. Kunatokea nini Yesu anapoenda hekaluni?

5 Kulingana na desturi yake anapozuru Yerusalemu, Yesu, Mwalimu Mkuu, anaenda hekaluni kufundisha. Humo vipofu na vilema wanamwendea, naye anawaponya. Makuhani wakuu na waandishi wanapoona hayo na kuwasikia wavulana hekaluni wakipaaza sauti, “Okoa Mwana wa Daudi, twasihi!” wanakasirika. “Je, wasikia yale wanayosema hawa?” wanateta. “Ndiyo,” Yesu anajibu. “Je, nyinyi hamkusoma kamwe hili, ‘Kutoka kinywani mwa vitoto na watoto wanyonyao umetoa sifa’?” Yesu anatazama kwa makini yale yanayotendeka hekaluni huku akiendelea kufundisha.—Mathayo 21:15, 16; Marko 11:11.

6. Yesu anatendaje tofauti na vile alivyotenda mapema, na kwa nini?

6 Yesu anatenda tofauti jinsi gani na vile alivyotenda miezi sita mapema! Wakati huo aliingia Yerusalemu kwa ajili ya Msherehekeo wa Matabenakulo “si waziwazi bali kama katika siri.” (Yohana 7:10) Naye sikuzote alichukua hatua ya kuondoka salama uhai wake ulipokuwa hatarini. Sasa anaingia waziwazi katika jiji ambamo maagizo yametolewa akamatwe! Pia haikuwa desturi ya Yesu kujitangaza kuwa Mesiya. (Isaya 42:2; Marko 1:40-44) Hakutaka watu wapige mbiu au waeneze ripoti zilizopotoshwa kumhusu. Sasa umati unamtangaza waziwazi kuwa Mfalme na Mwokozi—Mesiya—naye anapuuza maombi ya viongozi wa kidini ya kutaka aunyamazishe umati! Kwa nini amebadilika? Kwa sababu “saa imekuja kwa Mwana wa binadamu kutukuzwa,” kama Yesu anavyotangaza siku inayofuata.—Yohana 12:23.

Kitendo cha Ujasiri—Kisha Mafundisho Yenye Kuokoa Uhai

7, 8. Matendo ya Yesu Nisani 10, 33 W.K., yanafananaje na mambo aliyofanya hekaluni wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 30 W.K.?

7 Anapofika hekaluni Jumatatu, Nisani 10, Yesu anachukua hatua dhidi ya mambo aliyokuwa ameona alasiri iliyotangulia. Anaanza ‘kufukuza nje wale wanaouza na kununua katika hekalu, na kuzipindua meza za wabadili-fedha na mabenchi ya wale wanaouza njiwa; naye haachi yeyote kuchukua chombo kupitia hekalu.’ Anawashutumu wakosaji hao anapotangaza hivi: “Je, haikuandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa ajili ya mataifa yote’? Lakini nyinyi mmeifanya pango la wapokonyaji.”—Marko 11:15-17.

8 Matendo ya Yesu yanafanana na mambo aliyofanya miaka mitatu awali alipozuru hekalu wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 30 W.K. Lakini wakati huu shutumu lake ni kali zaidi. Sasa wafanya-biashara katika hekalu wanaitwa “wapokonyaji.” (Luka 19:45, 46; Yohana 2:13-16) Ni wapokonyaji kwa sababu wanadai bei za juu sana kutoka kwa wale wanaohitaji kununua wanyama wa dhabihu. Makuhani wakuu, waandishi, na walio wakubwa wa watu wanasikia yale Yesu anayofanya na kwa mara nyingine, wanatafuta njia za kumwua. Hata hivyo, hawajui namna ya kumwua Yesu, kwa sababu watu wote, kwa kuwa wamestaajabia mafundisho yake, wanaandamana naye ili wamsikilize.—Marko 11:18; Luka 19:47, 48.

9. Yesu anafundisha somo gani, naye anawapa mwaliko gani wasikilizaji wake kwenye hekalu?

9 Anapoendelea kufundisha hekaluni, Yesu anatangaza: “Saa imekuja kwa Mwana wa binadamu kutukuzwa.” Naam, anajua kwamba ana siku chache tu za kuishi akiwa mwanadamu. Baada ya kusimulia jinsi punje ya ngano inavyopaswa kufa ndipo izae matunda—jambo linalolingana na kufa kwake na kuwa njia ya kuwapa wengine uhai udumuo milele—Yesu anawaalika wasikilizaji wake, akisema: “Ikiwa yeyote angenihudumia, acha anifuate mimi, na nilipo mimi ndipo mhudumu wangu atakuwa pia. Ikiwa yeyote angenihudumia mimi, Baba atamheshimu yeye.”—Yohana 12:23-26.

10. Yesu anahisije kuhusu kifo chenye maumivu kinachomngojea?

10 Akifikiria kifo chake chenye maumivu makali ambacho kinatokea siku nne tu baadaye, Yesu anaendelea kusema: “Sasa nafsi yangu yataabika, nami nitasema nini? Baba, niokoe kutoka katika saa hii.” Lakini kinachomngojea Yesu hakiwezi kuepukika. “Hata hivyo,” asema, “hii ndiyo sababu nimekuja kwenye saa hii.” Ni kweli kwamba Yesu anakubaliana kabisa na mpango wote wa Mungu. Ameazimia kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu hadi kifo chake cha kidhabihu. (Yohana 12:27) Alituwekea kielelezo bora kama nini—cha kujitiisha kabisa kwa mapenzi ya Mungu!

11. Yesu anaufundisha mambo gani umati ambao umetoka tu kusikia sauti kutoka mbinguni?

11 Kwa kuhangaikia sana jinsi kifo chake kitakavyoathiri sifa ya Baba yake, Yesu anasali: “Baba, tukuza jina lako.” Kwa mshangao wa umati ambao umekusanyika hekaluni, sauti inatoka mbinguni, ikitangaza: “Mimi nimelitukuza na pia hakika nitalitukuza tena.” Mwalimu Mkuu anatumia fursa hii kuuambia umati ni kwa nini sauti hiyo imesikika, kifo chake kitakuwa na matokeo gani, na ni kwa nini wanahitaji kuwa na imani. (Yohana 12:28-36) Yesu amekuwa na shughuli nyingi sana katika siku mbili ambazo zimepita. Lakini siku muhimu bado inakuja.

Siku ya Mashutumu

12. Viongozi wa kidini wanajaribuje kumnasa Yesu Jumanne, Nisani 11, na matokeo yanakuwa nini?

12 Jumanne, Nisani 11, Yesu anaingia hekaluni tena kufundisha. Wanaomsikiliza ni wenye uhasama. Wakirejezea matendo ya Yesu ya siku iliyotangulia, makuhani wakuu na wazee wa watu wanamwuliza: “Ni kwa mamlaka gani wewe wafanya mambo haya? Na ni nani aliyekupa wewe mamlaka hii?” Mwalimu Mkuu anawatatanisha kwa jibu lake, naye anasimulia mifano mitatu dhahiri—miwili juu ya shamba la mizabibu na mmoja juu ya karamu ya arusi—inayofichua jinsi wapinzani wake walivyo waovu. Wakikasirishwa na yale wanayosikia, viongozi wa kidini wanataka kumkamata. Lakini wanaogopa umati, unaomwona Yesu kuwa nabii. Kwa hiyo, wanajaribu kumhadaa ili aseme kitu kinachoweza kufanya akamatwe. Majibu anayowapa Yesu yanawanyamazisha.—Mathayo 21:23–22:46.

13. Yesu anawapa wasikilizaji wake shauri gani kuhusu waandishi na Mafarisayo?

13 Kwa kuwa waandishi na Mafarisayo wanadai kufundisha Sheria ya Mungu, sasa Yesu anawahimiza wasikilizaji wake: “Mambo yote wawaambiayo nyinyi, yafanyeni na kuyashika, lakini msifanye kulingana na vitendo vyao, kwa maana wao husema lakini hawafanyi.” (Mathayo 23:1-3) Ni shutumu kali la hadharani lililoje! Lakini Yesu hajamaliza kuwashutumu. Hii ndiyo siku yake ya mwisho kwenye hekalu, na kwa ujasiri anafichua unafiki wao mfululizo kama ngurumo ya radi.

14, 15. Yesu anatoa mashutumu gani makali dhidi ya waandishi na Mafarisayo?

14 “Ole wenu nyinyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki!” Yesu anatangaza mara sita. Ni wanafiki kwa sababu, kama aelezavyo, wanawafungia watu Ufalme wa mbinguni na hawaruhusu wale wanaotaka kuingia waingie. Wanafiki hao huvuka bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mgeuzwa-imani, kisha wanamfanya astahili kuharibiwa milele. Wanazingatia sana sehemu ya kumi huku wakipuuza “mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.” Kwa kweli, wanasafisha “upande wa nje wa kikombe na wa sahani, lakini upande wa ndani vimejaa vitu vilivyoporwa na upitaji-kiasi,” yaani sura yao ya nje, inayoonyesha wao ni wachaji Mungu, inaficha namna ambavyo wameoza ndani. Isitoshe, ili watu waone matendo yao ya hisani, wanakuwa tayari kuwajengea manabii makaburi na kuyapamba, hata ingawa wao “ni wana wa wale waliowaua manabii kimakusudi.”—Mathayo 23:13-15, 23-31.

15 Akiwashutumu wapinzani wake kwa ukosefu wa maadili ya kiroho, Yesu anasema: “Ole wenu nyinyi, viongozi vipofu.” Wao ni vipofu kiadili kwa sababu wanazingatia zaidi dhahabu ya hekalu kuliko thamani ya kiroho ya mahali hapo pa ibada. Akiendelea, Yesu anatoa shutumu lake lililo kali zaidi. “Nyoka, uzao wa nyoka-vipiri,” anasema, “nyinyi mtaikimbiaje hukumu ya Gehena?” Naam, Yesu anawaambia kwamba kwa kufuatia mwenendo wao mwovu, wataharibiwa milele. (Mathayo 23:16-22, 33) Sisi pia na tuonyeshe ujasiri katika kutangaza ujumbe wa Ufalme, hata inapomaanisha kufichua dini isiyo ya kweli.

16. Anapoketi juu ya Mlima wa Mzeituni, Yesu anawatolea wanafunzi wake unabii gani muhimu?

16 Yesu sasa anaondoka hekaluni. Yeye na mitume wake wanapanda Mlima wa Mzeituni huku mwangaza wa jua la alasiri ukififia. Wanapoketi huko, Yesu anatoa unabii kuhusu kuhabiriwa kwa hekalu na ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo. Maana ya unabii huo yahusu hata wakati wetu. Jioni hiyo, Yesu pia anawaambia wanafunzi wake: “Mwajua kwamba siku mbili tangu sasa kutakuwa sikukuu ya kupitwa, naye Mwana wa binadamu apaswa kukabidhiwa ili atundikwe mtini.”—Mathayo 24:1-14; 26:1, 2.

Yesu ‘Anawapenda Walio Wake Mwenyewe Hadi Mwisho’

17. (a) Yesu anawafundisha somo gani wale 12 wakati wa Sikukuu ya Kupitwa siku ya Nisani 14? (b) Yesu anaanzisha ukumbusho gani baada ya kumwambia Yudasi Iskariote aende?

17 Kwa siku mbili zinazofuata—Nisani 12 na 13—Yesu hajionyeshi hadharani katika ekalu. Viongozi wa kidini wanataka kumwua, naye hataki chochote kimzuie asisherehekee Sikukuu ya Kupitwa pamoja na mitume wake. Siku ya Nisani 14 inaanza Alhamisi baada ya jua kutua—siku ya mwisho ya maisha ya Yesu duniani akiwa mwanadamu. Jioni hiyo, Yesu na mitume wake wako pamoja katika nyumba moja huko Yerusalemu ambapo matayarisho yamefanywa ili washerehekee Sikukuu ya Kupitwa. Wanapofurahia Sikukuu ya Kupitwa pamoja, anawafundisha wale 12 somo zuri la unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. Baada ya kumwambia Yudasi Iskariote aende, ambaye amekubali kumsaliti Bwana-Mkubwa wake kwa vipande 30 vya fedha—bei ya mtumwa kulingana na Sheria ya Kimusa—Yesu anaanzisha Ukumbusho wa kifo chake.—Kutoka 21:32; Mathayo 26:14, 15, 26-29; Yohana 13:2-30.

18. Ni mambo gani zaidi ambayo Yesu anawafundisha kwa upendo mitume wake waaminifu 11, naye anawatayarishaje kwa ajili ya kuondoka kwake kunakokaribia?

18 Baada ya Ukumbusho kuanzishwa, mitume wanaanza mabishano makali juu ya ni nani kati yao aliye mkubwa zaidi. Badala ya kuwakemea, Yesu anawafundisha kwa subira manufaa ya kuwahudumia wengine. Yeye anafanya agano pamoja nao kwa ajili ya ufalme kwa kuthamini kwamba wameshikamana naye wakati wa majaribu yake. (Luka 22:24-30) Yesu pia anawaamuru wapendane kama alivyowapenda. (Yohana 13:34) Yesu anakawia katika chumba hicho, huku akiwatayarisha kwa upendo kwa ajili ya kuondoka kwake kunakokaribia. Anawahakikishia kwamba yeye ni rafiki yao, anawatia moyo wawe na imani, na kuwaahidi msaada wa roho takatifu. (Yohana 14:1-17; 15:15) Kabla ya kuondoka katika nyumba hiyo, Yesu anamwomba Baba yake: “Baba, saa imekuja; mtukuze mwana wako, ili mwana wako apate kukutukuza wewe.” Kwa kweli, Yesu amewatayarisha mitume wake kwa ajili ya kuondoka kwake, na kwa hakika ‘anawapenda walio wake mwenyewe hadi mwisho.’—Yohana 13:1; 17:1.

19. Kwa nini Yesu ana maumivu makali kwenye bustani ya Gethsemane?

19 Huenda ni usiku wa manane wakati Yesu na mitume wake waaminifu 11 wanapofika katika bustani ya Gethsemane. Amekuwa akienda hapo mara nyingi pamoja na mitume wake. (Yohana 18:1, 2) Baada ya saa chache, Yesu atakufa kama mhalifu mwenye kudharauliwa. Maumivu anayopata kwa kutarajia kifo hicho na pia suto ambalo huenda kikaletea Baba yake, ni makali sana hivi kwamba anaposali, jasho lake linakuwa kama matone ya damu yanayoanguka chini. (Luka 22:41-44) “Saa imekuja!” Yesu anawaambia mitume wake. “Tazameni! Msaliti wangu amekaribia.” Wakati anapozungumza, Yudasi Iskariote anakaribia, akiandamana na umati mkubwa unaobeba mienge na taa na silaha. Wamekuja kumkamata Yesu. Naye hatoi upinzani wowote. “Katika kisa hicho,” anaeleza, “Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke kwa njia hii?”—Marko 14:41-43; Mathayo 26:48-54.

Mwana wa Binadamu Atukuzwa!

20. (a) Ni ukatili gani unaompata Yesu baada ya kukamatwa? (b) Kwa nini muda mfupi tu kabla ya kufa Yesu anapaaza sauti: “Imetimizwa”?

20 Baada ya kukamatwa, Yesu anashtakiwa na mashahidi wasio wa kweli, mahakimu wasiofuata haki wanampata na hatia, anahukumiwa na Pontio Pilato, anadharauliwa na makuhani na watu wenye ghasia, nao askari wanamdhihaki na kumtesa. (Marko 14:53-65; 15:1, 15; Yohana 19:1-3) Kufikia Ijumaa adhuhuri, Yesu anatundikwa kwenye mti wa mateso na kupatwa na maumivu makali sana wakati uzito wa mwili wake unapofanya majeraha ya misumari kwenye mikono yake na miguu yake, yawe makubwa hata zaidi. (Yohana 19:17, 18) Saa tisa hivi alasiri, Yesu anapaaza sauti: “Imetimizwa!” Naam, ametimiza yote aliyokuja kufanya duniani. Akimkabidhi Mungu roho yake, anainamisha kichwa na kufa. (Yohana 19:28, 30; Mathayo 27:45, 46; Luka 23:46) Siku ya tatu baadaye, Yehova anamfufua Mwana wake. (Marko 16:1-6) Siku arobaini baada ya kufufuliwa, Yesu anapaa mbinguni na anatukuzwa.—Yohana 17:5; Matendo 1:3, 9-12; Wafilipi 2:8-11.

21. Tunaweza kumwigaje Yesu?

21 Tunaweza ‘kufuataje hatua za Yesu kwa ukaribu’? (1 Petro 2:21) Kama yeye, acheni tujikakamue kisulubu katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi na tuwe jasiri na wenye moyo mkuu katika kusema neno la Mungu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 4:29-31; Wafilipi 1:14) Na tusisahau kamwe tuko wapi kwenye mkondo wa wakati wala tusishindwe kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora. (Marko 13:28-33; Waebrania 10:24, 25) Na tuache matendo yetu yote yaongozwe na mapenzi ya Yehova Mungu na kule kufahamu kwamba tunaishi “wakati wa mwisho.”—Danieli 12:4.

Ungejibuje?

• Yesu alitekelezaje huduma yake kwenye hekalu huko Yerusalemu alipojua kwamba kifo chake kiko karibu?

• Ni nini kionyeshacho kwamba Yesu ‘aliwapenda walio wake hadi mwisho’?

• Matukio ya saa chache za mwisho za maisha ya Yesu yanaonyesha nini kumhusu?

• Tunaweza kumwigaje Kristo Yesu katika huduma yetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu“aliwapenda hadi mwisho”