Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Funzo—Lenye Kuthawabisha na Lenye Kufurahisha

Funzo—Lenye Kuthawabisha na Lenye Kufurahisha

Funzo—Lenye Kuthawabisha na Lenye Kufurahisha

‘Ukiutafuta . . . , utapata kumjua Mungu.’ —Mithali 2:4, 5.

1. Twaweza kupataje furaha nyingi kutokana na usomaji wa kujifurahisha?

WATU wengi husoma ili kujifurahisha tu. Ikiwa habari hiyo ni yenye kujenga, kusoma kwaweza kuwa jambo lifaalo, lenye kuburudisha. Mbali na programu yao ya kawaida ya usomaji wa Biblia, Wakristo fulani hupata furaha ya kweli kwa kusoma bila kupangia Zaburi, Mithali, masimulizi ya Gospeli, au sehemu nyingine za Biblia. Wao hufurahishwa sana na uzuri wa lugha na mawazo. Kwa usomaji wa kujifurahisha wengine huchagua kusoma Yearbook of Jehovah’s Witnesses, gazeti Amkeni!, mambo yaliyoonwa ya maisha yanayochapishwa katika jarida hili, au vichapo vya historia, jiografia, na mambo yanayohusu mimea na viumbe.

2, 3. (a) Ni katika njia gani habari ngumu ya kiroho inaweza kulinganishwa na chakula kigumu? (b) Kujifunza huhusisha nini?

2 Ingawa kusoma ili kujifurahisha kwaweza kuwa namna ya kujiburudisha, kujifunza hutaka jitihada ya akili. Mwanafalsafa Mwingereza Francis Bacon aliandika hivi: “Vitabu fulani vyapasa kuonjwa, vingine kumezwa, na vingine vichache kutafunwa na kumeng’enywa.” Bila shaka Biblia iko katika kikundi cha mwisho. Mtume Paulo aliandika hivi: Kumhusu yeye [Kristo, kama anavyofananishwa kimbele na Mfalme-Kuhani Melkizedeki] tuna mengi ya kusema na yaliyo magumu kufafanuliwa, kwa kuwa mmekuwa wazito katika kusikia kwenu. . . . Chakula kigumu ni cha watu wakomavu, cha wale ambao kupitia utumizi, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.” (Waebrania 5:11, 14) Lazima chakula kigumu kitafunwe kabla hakijamezwa na kumeng’enywa. Habari ngumu ya kiroho hutaka ifikiriwe ili kuweza kuielewa na kuikumbuka.

3 Kamusi moja hufafanua “funzo” kuwa “kitendo au hatua ya kutumia akili ili kujipatia ujuzi au uelewevu, kama kwa kusoma, kufanya uchunguzi, n.k.” Kwa hiyo kusoma kwahusisha mengi zaidi ya kusoma kijuujuu tu, labda kupiga maneno mstari tunaposoma. Kujifunza ni kazi na kwahusisha jitihada ya akili, na kutumia uwezo wa ufahamu. Hata hivyo, ingawa funzo hutaka jitihada, hiyo haimaanishi kwamba haliwezi kufurahisha.

Kufanya Funzo Lipendeze

4. Kulingana na mtunga-zaburi, kujifunza Neno la Mungu kwawezaje kuburudisha na kuthawabisha?

4 Kusoma na kujifunza Neno la Mungu kwaweza kuburudisha na kutia nguvu. Mtunga-zaburi alitangaza hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya BWANA ni safi, huyatia macho nuru.” (Zaburi 19:7, 8) Sheria na vikumbusha vya Yehova huuisha nafsi yetu, huboresha hali yetu ya kiroho, hutupa shangwe ya ndani, na kuyatia macho yetu nuru na hivyo kuona waziwazi makusudi ya ajabu ya Yehova. Inapendeza kama nini!

5. Ni katika njia zipi funzo linaweza kutufurahisha sana?

5 Tunapopata matokeo mazuri ya kazi yetu, tunafurahia kuifanya. Hivyo, ili funzo liwe lenye kupendeza, lazima tuwe wepesi katika kutumia ujuzi mpya tunaojipatia. Yakobo aliandika hivi: “Yeye achunguaye ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyu, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtekelezaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kutenda hiyo.” (Yakobo 1:25) Kutumia mara moja mambo tunayojifunza huleta uradhi mkubwa. Pia kufanya utafiti kwa kusudi la kujibu swali tuliloulizwa katika kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha kutatupa furaha kubwa.

Jinsi ya Kujifurahisha Sana kwa Neno la Mungu

6. Mwandikaji wa Zaburi ya 119 alijifurahishaje kwa neno la Yehova?

6 Mtungaji wa Zaburi ya 119, ambaye labda ni Hezekia alipokuwa mwana-mfalme mchanga, alijifurahisha sana kwa neno la Yehova. Akitumia lugha ya kishairi alisema hivi: “Nitajifurahisha sana kwa amri zako, sitalisahau neno lako. Shuhuda zako nazo ndizo furaha yangu . . . Nami nitajifurahisha sana kwa maagizo yako, ambayo nimeyapenda. Rehema zako zinijie nipate kuishi, maana sheria yako ni furaha yangu. Ee BWANA nimeutamani wokovu wako, na sheria yako ndiyo furaha yangu.”—Zaburi 119:16, 24, 47, 77, 174.

7, 8. (a) Kulingana na kitabu kimoja cha marejezo, inamaanisha nini ‘kujifurahisha sana’ na Neno la Mungu? (b) Twaweza kuonyeshaje kwamba tunapenda Neno la Yehova? (c) Ezra alijitayarishaje kabla ya kusoma Sheria ya Yehova?

7 Ikieleza maneno yaliyotafsiriwa ‘kujifurahishasana’ katika Zaburi 119, kamusi moja ya Maandiko ya Kiebrania yasema hivi: “Matumizi katika mstari wa 16 yalingana na [vitenzi] vya kushangilia . . . na kutafakari . . . Mwendelezo ni: shangilia, tafakari, pendezwa na . . . Huenda muungano huo unadokeza kwamba kutafakari ukiwa na kusudi hukuwezesha kupendezwa sana na neno la Yahweh. . . . Maana yake huhusisha hisia-moyo.” *

8 Naam, kupenda Neno la Yehova kwapaswa kutoka kwenye moyo, ambao ni msukumo wa hisia-moyo. Twapaswa kupendezwa kurudiarudia mafungu kadhaa ambayo tumetoka tu kusoma. Lazima tutafakari juu ya mambo ya kiroho yenye kina na kuyazingatia. Hilo hutaka kutafakari kwa ukimya pamoja na sala. Kama vile Ezra, twahitaji kutayarisha mioyo yetu kwa ajili ya kusoma na kujifunza Neno la Mungu. Imeandikwa hivi kumhusu: “Huyo Ezra alikuwa ameuelekeza moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda, na kufundisha maagizo na hukumu katika Israeli.” (Ezra 7:10) Ona kwamba Ezra alikusudia kufanya mambo matatu alipokuwa akitayarisha moyo wake: kujifunza, kutumia kibinafsi mambo aliyojifunza, na kufundisha. Twapaswa kufuata kielelezo chake.

Funzo Likiwa Tendo la Ibada

9, 10. (a) Ni katika njia zipi Mtunga-zaburi alifikiri juu ya Neno la Yehova? (b) Kitenzi cha Kiebrania kilichotafsiriwa ‘kufikiria mwenyewe’ chamaanisha nini? (c) Kwa nini ni muhimu tuone funzo la Biblia kuwa “tendo la ibada”?

9 Mtunga-zaburi asema kwamba alifikiria sheria, amri, na vikumbusha vya Yehova. Anaimba hivi: “[“Nitayafikiria mwenyewe,”NW] mausia yako, nami nitaziangalia njia zako. . . . Mikono yangu nitayainulia maagizo yako niliyoyapenda, nami nitazitafakari amri zako. Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa. Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote, maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo.” (Zaburi 119:15, 48, 97, 99) Ni nini kinachodokezwa na ‘kufikiria mwenyewe’ Neno la Mungu?

10 Kitenzi cha Kiebrania kilichotafsiriwa ‘kufikiria mwenyewe’ pia chamaanisha “tafakari, waza” “fikiria jambo.” “Kinatumiwa kuhusu kutafakari kimyakimya kazi za Mungu . . . na Neno la Mungu.” (Theological Wordbook of the Old Testament) Nomino ya neno “kufikiria” yarejezea “kutafakari kwa mtunga-zaburi,” “funzo lake lililochochewa na upendo” kwa sheria ya Mungu, na hivyo likawa “tendo la ibada.” Kuona funzo la Neno la Mungu kuwa sehemu ya ibada yetu huliongezea uzito. Hivyo lapasa kufanywa kwa kudhamiria na kwa sala. Funzo ni sehemu ya ibada yetu nalo hufanywa ili kuboresha ibada yetu.

Kuchimba Ndani Zaidi Katika Neno la Mungu

11. Yehova huwafunuliaje watu wake mawazo ya kiroho yenye kina?

11 Akiwa amevutiwa kwa njia ya staha, mtunga-zaburi alitangaza hivi: “Ee BWANA, jinsi yalivyo makuu matendo yako! Mawazo yako ni mafumbo makubwa.” (Zaburi 92:5) Naye mtume Paulo alizungumza juu ya “mambo yenye kina kirefu ya Mungu,” mawazo magumu kuelewa ambayo Yehova huwafunulia watu wake “kupitia roho yake” inayotenda kwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. (1 Wakorintho 2:10; Mathayo 24:45) Jamii hiyo ya mtumwa huandaa kwa bidii chakula cha kiroho kwa ajili ya wote—“maziwa” kwa ajili ya wapya lakini “chakula kigumu” kwa “watu wakomavu.”—Waebrania 5:11-14.

12. Toa mfano wa “mambo yenye kina kirefu ya Mungu” ambayo yamefafanuliwa na jamii ya mtumwa.

12 Ili kuelewa “mambo [hayo] yenye kina kirefu ya Mungu,” ni muhimu kujifunza kwa sala na kutafakari Neno lake. Kwa mfano, habari nzuri imechapishwa inayoonyesha jinsi Yehova anavyoweza kuwa mwenye haki na mwenye rehema wakati uleule. Yeye hapunguzi uzito wa haki yake kwa kuonyesha rehema; badala yake rehema ya Mungu ni udhihirisho wa haki ya Mungu na vilevile upendo wake. Anapohukumu mkosaji, kwanza Yehova huangalia ili aone kama inawezekana aonyeshe rehema kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Mwanaye. Ikiwa mkosaji haonyeshi toba au ni mwasi, Mungu huruhusu haki itekelezwe kikamili bila kuonyesha rehema isiyostahiliwa. Kwa vyovyote vile, yeye ni mwaminifu kwa kanuni zake za juu. * (Waroma 3:21-26) ‘Lo kina cha hekima ya Mungu!’—Waroma 11:33.

13. Twapaswa kuonyeshaje uthamini kwa “jumla” ya kweli za kiroho tulizofunuliwa kufikia sasa?

13 Kama mtunga-zaburi, twasisimuka kwamba Yehova hutujulisha mawazo yake mengi. Daudi aliandika hivi: “Fikira zako zina thamani nyingi kwangu; jinsi ilivyo kubwa jumla yake! Kama ningezihesabu ni nyingi kuliko mchanga.” (Zaburi 139:17, 18) Ijapokuwa leo tunajua sehemu ndogo tu ya mawazo yasiyohesabika ambayo Yehova ataendelea kufunua milele, twathamini sana “jumla” ya kweli za kiroho zenye thamani zilizofunuliwa kufikia sasa na kuendelea kuchimba hata ndani zaidi kwenye msingi wa Neno la Mungu.—Zaburi 119:160, NW kielezi-chini.

Jitihada na Vifaa Vyenye Matokeo Vyahitajiwa

14. Mithali 2:1-6 hukaziaje uhitaji wa jitihada katika kujifunza Neno la Mungu?

14 Funzo la Biblia lenye kina hutaka jitihada. Twaona jambo hilo waziwazi tusomapo kwa uangalifu Mithali 2:1-6. Ona vitenzi vinavyoashiria tendo ambavyo Mfalme Solomoni alitumia ili kukazia jitihada inayohitajiwa kujipatia ujuzi, hekima, na uelewevu wa Mungu. Aliandika hivi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.” (Italiki ni zetu.) Naam, funzo lenye kuthawabisha hutaka utafiti, kuchimba, kana kwamba unatafuta hazina iliyositirika.

15. Ni kielezi gani cha Biblia kinachokazia uhitaji wa kuwa na njia nzuri za kujifunza?

15 Ili kuwa na funzo lenye kujenga kiroho tunahitaji kuwa na njia nzuri za kujifunza. Solomoni aliandika hivi: “Iwapo chuma hakipati, wala mtu hakinoi; ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi.” (Mhubiri 10:10) Mfanyakazi akitumia kifaa cha kukatia ambacho si kikali au asipokitumia kwa ustadi, atapoteza nguvu zake na kazi yake itakuwa duni. Hali kadhalika, huenda tukapata manufaa ya aina mbalimbali kwa muda tunaotumia kujifunza, ikitegemea njia zetu za kujifunza. Madokezo bora kabisa tunayoweza kutumia ili kuboresha namna tunavyojifunza yaweza kupatikana katika Somo la 7 la kitabu Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. *

16. Tumepewa madokezo gani tunayoweza kutumia ili kutusaidia kuwa na funzo lenye kina?

16 Msanii anapoanza kazi yake, yeye hutayarisha vifaa atakavyohitaji. Vivyo hivyo, tunapoanza kujifunza, twapaswa kuteua vifaa vya kujifunzia tutakavyohitaji katika maktaba yetu ya kibinafsi. Tunapokumbuka kwamba funzo ni kazi na hutaka jitihada ya akili, ni vizuri pia tuketi ifaavyo. Ikiwa twataka kubaki chonjo kiakili, huenda ikafaa zaidi kuketi kwenye kiti mezani au kwenye dawati badala ya kulala kitandani au kuketi katika kiti chenye kustarehesha. Baada ya kukaza fikira kwa muda fulani, huenda ukaona inafaa kujinyoosha kidogo au kutoka nje ili kupata hewa safi.

17, 18. Toa mifano ya jinsi ya kutumia vifaa bora vya kujifunzia ulivyo navyo.

17 Pia tuna vifaa vingi vya kujifunzia visivyo na kifani. Cha kwanza kabisa ni Biblia ya New World Translation, ambayo sasa hupatikana kwa sehemu au ikiwa nzima katika lugha 37. Chapa ya kawaida ya New World Translation ina marejezo yanayolingana na pia “Jedwali ya Vitabu vya Biblia” yenye jina la mwandishi, mahali kilipoandikiwa, na muda uliotumika. Pia ina faharisi ya maneno ya Biblia, nyongeza, na ramani. Katika lugha fulani, Biblia hii imechapishwa katika chapa kubwa zaidi, inayoitwa Reference Bible. Ina sehemu hizo zote zilizotajwa juu na nyingine zaidi, kutia ndani vielezi-chini vingi sana, ambavyo pia vimepangwa katika faharisi. Je, wewe hutumia kikamili vifaa vinavyopatikana katika lugha yako ili kukusaidia kuchimba ndani zaidi ya Neno la Mungu?

18 Kifaa kingine cha kujifunzia chenye thamani kubwa ni ensaiklopedia ya Biblia yenye mabuku mawili Insight on the Scriptures. Ikiwa una kitabu hiki katika lugha unayoweza kuelewa, wapaswa kuwa nacho kila wakati unapojifunza. Kitakupa habari muhimu ili kuelewa kiini cha habari nyingi za Biblia. Vivyo hivyo, kifaa kingine chenye kusaidia ni kitabu “Kila Andiko Lenye Pumzi ya Mungu Lafaa.” Tunapoanza kusoma kitabu kipya cha Biblia, ni vizuri kuchunguza sehemu inayozungumzia kitabu hicho katika kitabu “Kila Andiko” ili tuelewe hali ya kihistoria na ya kijiografia na pia kupata muhtasari wa habari za kitabu hicho cha Biblia na kuona jinsi ulivyo wenye thamani kwetu. Kwa kuongezea vitabu vingi vya kujifunzia tulivyo navyo, hivi karibuni tumepokea Watchtower Library katika kompyuta, ambayo sasa yapatikana katika lugha tisa.

19. (a) Kwa nini Yehova ametuandalia vifaa bora kwa ajili ya funzo la Biblia? (b) Ni nini kinachohitajiwa ili kusoma na kujifunza Biblia ifaavyo?

19 Yehova ameandaa vifaa hivi vyote kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kuwezesha watumishi wake duniani ‘watafute na wapate kumjua Mungu.’ (Mithali 2:4, 5) Mazoea mazuri ya kujifunza hutuwezesha kumfahamu Yehova vizuri zaidi na kufurahia uhusiano wa karibu pamoja naye. (Zaburi 63:1-8) Naam, funzo ni kazi, lakini ni kazi yenye kufurahisha na inayothawabisha. Hata hivyo, linahitaji wakati, na labda unafikiria, ‘Nitatoa wapi wakati ili kukazia fikira vya kutosha usomaji wangu wa Biblia na funzo langu la kibinafsi?’ Jambo hili litazungumziwa katika makala ya kumalizia ya mfululizo huu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 New International Dictionary of Old Testament Theology & Exegesis, Buku la 4, ukurasa wa 205-207.

^ fu. 12 Ona Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 1998, ukurasa wa 13, fungu la 7. Ukiwa mradi wa funzo la Biblia, waweza kurudia makala za funzo katika toleo hilo na vilevile makala ya “Justice,” “Mercy,” na “Righteousness” katika ensaiklopedia ya Biblia Insight on the Scriptures, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. Ikiwa kitabu hiki hakipatikani katika lugha yako, shauri zuri kuhusu njia za kujifunza laweza kupatikana katika matoleo yafuatayo ya Mnara wa Mlinzi: Agosti 15, 1993, ukurasa wa 13-17; Mei 15, 1986, ukurasa wa 19-20.

Maswali ya Kupitia

• Twawezaje kufanya funzo letu la kibinafsi liwe lenye kuburudisha na lenye kuthawabisha?

• Kama mtunga-zaburi, twaweza ‘kujifurahishaje sana’ na pia ‘kufikiria’ Neno la Yehova?

Mithali 2:1-6 huonyeshaje uhitaji wa jitihada katika kujifunza Neno la Mungu?

• Yehova ameandaa vifaa gani bora vya kujifunzia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kutafakari kwa ukimya pamoja na sala hutusaidia tusitawishe upendo kwa Neno la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, wewe hutumia kikamili vifaa vya kujifunzia ulivyo navyo ili kuchimba ndani zaidi katika Neno la Mungu?