Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furaha ya Milele Mbinguni Au Duniani?

Furaha ya Milele Mbinguni Au Duniani?

Furaha ya Milele Mbinguni Au Duniani?

JE, FURAHA yako hutegemea hasa mahali unapoishi? Watu wengi huenda wakakubali bila kusita kwamba furaha hutegemea mambo kama afya nzuri, kuwa na kusudi maishani, na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Mithali moja ya Biblia yasema hivi: “Chakula cha mboga penye mapendano; ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.”—Mithali 15:17.

Hata hivyo, makao yetu ya kidunia yamekuwa mahali penye chuki, ujeuri, na aina nyingine za maovu kwa muda mrefu. Namna gani mbinguni, mahali penye viumbe wa kiroho ambapo wengi wanatarajia kwenda baada ya kifo? Je, mbinguni pamekuwa sikuzote mahali penye amani, furaha na utulivu, bila mzozo wa aina yoyote, jinsi watu wengi wanavyodhani?

Biblia yafundisha kwamba Mungu anakaa mbinguni pamoja na mamilioni ya viumbe wa roho waitwao malaika. (Mathayo 18:10; Ufunuo 5:11) Hao wanaelezwa kuwa ‘wana [wa roho] wa Mungu’. (Ayubu 38:4, 7) Kama wanadamu, malaika pia wana uhuru wa kuchagua, hao si mashine zifanyazo kazi bila hiari ya kuchagua. Kwa hiyo, wao pia waweza kuchagua kufanya mema au mabaya. Je, malaika wangechagua kufanya mabaya? Huenda baadhi ya watu wakastaajabu kujua kwamba maelfu ya miaka iliyopita, idadi kubwa ya malaika walifanya dhambi dhidi ya Mungu—walimwasi Mungu!—Yuda 6.

Waasi Mbinguni

Dhambi ilianza mbinguni kwa sababu ya uasi wa malaika ambaye alikuja kuitwa Shetani (Mkinzani) na Ibilisi (Mchongezi). Huyo malaika ambaye mwanzoni alikuwa mwaminifu alichagua kwa hiari yake mwenyewe kufanya mabaya. Kuanzia hapo alianza kupotosha viumbe wengine wa kiroho, hivi kwamba katika siku za Noa, kabla ya Gharika, malaika wengi walijiunga naye kumwasi Mungu.—Mwanzo 6:2, NW, kielezi-chini; 2 Petro 2:4.

Malaika hao waliofanya dhambi hawakufukuzwa mbinguni mara moja. Badala yake, kwa maelfu ya miaka malaika hao waliruhusiwa kuingia mbinguni, ijapokuwa yaelekea waliwekewa mipaka fulani. * Hata hivyo, wakati uvumilivu wa Mungu kwa watenda waovu hao ulipokoma, ‘walivurumishwa’ chini kutoka mbinguni ili hatimaye waharibiwe. Kisha sauti mbinguni ikasema hivi: “Kwa ajili ya hili teremeni, nyinyi mbingu nanyi mkaao ndani yazo!” (Ufunuo 12:7-12) Kwa wazi, malaika waaminifu mbinguni walishangilia sana kwamba, mwishowe, wachochezi hao waovu walikuwa wametupwa nje!

Tukizingatia mambo haya ambayo watu wengi hawayajui, ni wazi kwamba hakuwezi kuwa na amani ya kweli wakati wowote ule ambapo viumbe wenye akili wanavunja sheria na kanuni za Mungu. (Isaya 57:20, 21; Yeremia 14:19, 20) Kwa upande mwingine, watu wote wafuatapo sheria za Mungu, amani na utulivu huenea. (Zaburi 119:165; Isaya 48:17, 18) Kwa hiyo ikiwa wanadamu wote wangempenda na kumtii Mungu, na kupendana, je, dunia haingeweza kuwa mahali penye furaha na pa kupendeza kuishi? Biblia yajibu ndiyo!

Namna gani wale wanaokataa kwa choyo kubadili njia zao mbaya? Je, wataendelea milele kuvuruga amani ya wale wanaotaka kwa moyo kufanya mapenzi ya Mungu? La hasha, Mungu alichukua hatua dhidi ya malaika waovu mbinguni, na atachukua hatua vilevile dhidi ya watu waovu hapa duniani.

Dunia Safi

“Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu,” Mungu akasema. (Isaya 66:1) Kwa sababu Mungu ndiye upeo wa utakatifu, hataruhusu “mahali pa kuweka miguu” yake pachafuliwe na uovu milele na milele. (Isaya 6:1-3; Ufunuo 4:8) Sawasawa na jinsi alivyosafisha mbingu wasiwepo roho waovu, ndivyo atakavyosafisha dunia wasiwepo wanadamu waovu, kama yaonyeshavyo maandiko ya Biblia yafuatayo:

“Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi.”—Zaburi 37:9.

“Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:21, 22.

“Ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu kulipa dhiki kwa wale wawafanyiao nyinyi dhiki, lakini, kwenu nyinyi mpatwao na dhiki, kitulizo pamoja nasi kwenye ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika moto wenye kuwaka mwali, aletapo kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu. Hawahawa watapatwa na adhabu ya kihukumu ya uharibifu udumuo milele kutoka mbele ya Bwana na kutoka katika utukufu wa nguvu yake.”—2 Wathesalonike 1:6-9.

“Ulimwengu [wa wanadamu waovu] unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17.

Je, Amani Itadumu Duniani?

Ijapokuwa Maandiko yaonyesha wazi kwamba Mungu hataruhusu waovu kuwapo milele, twawezaje kuwa na uhakika kwamba uovu utakapoondolewa, hautatokea tena? Twajua ya kwamba baada ya Gharika ya siku za Noa, uovu ulitokea tena upesi na kwa wingi hivi kwamba Mungu aliamua kuzuia miradi miovu ya wanadamu kwa kuvuruga lugha yao.—Mwanzo 11:1-8.

Sababu yetu kuu ya kuwa na uhakika kwamba uovu hautazuka tena ni kwamba dunia haitatawaliwa tena na wanadamu kama ilivyotawaliwa muda mfupi tu baada ya Gharika. Badala yake, Ufalme wa Mungu ndio utakaoitawala. Ufalme huo utakuwa serikali pekee ya dunia itakayoitawala kutoka mbinguni. (Danieli 2:44; 7:13, 14) Utachukua hatua bila kukawia dhidi ya yeyote ajaribuye kuanzisha uovu tena. (Isaya 65:20) Hatimaye utamharibu yule aliyeanzisha uovu—Shetani Ibilisi—pamoja na roho waovu, malaika waovu waliomfuata.—Waroma 16:20.

Mbali na hayo, wanadamu hawatakuwa na wasiwasi juu ya chakula, mavazi, makao, na kazi. Kukosa mambo hayo hufanya baadhi ya watu wawe wahalifu leo. Naam, dunia nzima itakuwa paradiso inayotoa mazao ya kutosha kwa wote.—Isaya 65:21-23; Luka 23:43.

Hata zaidi, Ufalme utawaelimisha raia zake katika njia ya maisha yenye amani, huku ukiwafanya wawe wakamilifu kabisa. (Yohana 17:3; Waroma 8:21) Baadaye, wanadamu wataweza kumtii Mungu kwa ukamilifu na kwa furaha, kama mtu mkamilifu Yesu alivyofanya, kwa sababu hawatahitaji tena kamwe kupambana na udhaifu mbalimbali na mielekeo ya kufanya dhambi. (Isaya 11:3) Yesu alibaki mwaminifu hata chini ya ushawishi mkubwa na hata mateso—mambo ambayo hayatakuwapo kabisa katika Paradiso.—Waebrania 7:26.

Kwa Nini Watu Kadhaa Wanakwenda Mbinguni?

Hata hivyo, wasomaji wengi wa Biblia wanayajua maneno yafuatayo ya Yesu: ‘Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. . . . ninashika njia yangu kwenda kuwatayarishia nyinyi mahali.’ (Yohana 14:2, 3) Je, maneno hayo yanapinga tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani?

Mafundisho hayo hayapingani. Badala yake, yaungana mkono. Kwanza, Biblia yasema kwamba ni Wakristo waaminifu wachache tu, yaani 144,000, watakaofufuliwa kama viumbe wa roho kuishi mbinguni. Kwa nini hao wanapewa zawadi hiyo nzuri ajabu? Kwa sababu wao ndio kikundi ambacho Yohana alikiona katika njozi, nao ‘walikuja kwenye uhai wakatawala wakiwa wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu.’ (Ufunuo 14:1, 3; 20:4-6) Wakilinganishwa na mabilioni ya watu waliomo duniani, wale 144,000 ni “kundi dogo” kwelikweli. (Luka 12:32) Zaidi ya hayo, kwa sababu wameishi duniani na kupatwa na matatizo ya kawaida ya wanadamu, wataweza “kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali” kama Yesu alivyofanya, wanapoongoza kazi ya kurudisha dunia na wanadamu katika hali kamilifu.—Waebrania 4:15.

Dunia—Makao ya Milele ya Wanadamu

Alipoandaa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, Mungu alianza kukusanya wale 144,000 karibu miaka 2,000 iliyopita, na yaelekea kwamba kikundi hiki ni kamili sasa. (Matendo 2:1-4; Wagalatia 4:4-7) Hata hivyo, dhabihu ya Yesu haikutolewa kwa ajili ya dhambi za wale 144,000 pekee, “bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:2) Kwa hiyo, wote wamwaminio Yesu wana tumaini la kuishi milele. (Yohana 3:16) Wale wanaolala kaburini ambao wamo katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa, si kuishi mbinguni, bali wataishi katika dunia iliyosafishwa. (Mhubiri 9:5; Yohana 11:11-13, 25; Matendo 24:15) Wanatarajia kupata nini humo?

Andiko la Ufunuo 21:1-4 lajibu likisema: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Hebu wazia—wanadamu wanawekwa huru na kifo, na maumivu na kilio zisababishwazo na kifo hazipo tena kamwe! Mwishowe, kusudi la awali la Yehova kwa dunia na wanadamu litakuwa limefikia utimizo wake mtukufu.—Mwanzo 1:27, 28.

Chaguo Letu—Uhai au Kifo

Adamu na Hawa hawakupewa kamwe uchaguzi wa kwenda mbinguni. Walikuwa wachague kati ya kumtii Mungu na kuishi milele katika paradiso duniani au kutomtii na kufa. Jambo la kusikitisha ni kwamba walichagua kutotii na kwa hiyo wakarudi “mavumbini.” (Mwanzo 2:16, 17; 3:2-5, 19) Kusudi la Mungu halikuwa kamwe kwamba wengi wa wanadamu wafe na kujaza mbingu kupitia kwa ufufuo wa wafu. Mungu aliumba maelfu ya malaika waishi mbinguni; viumbe hao wa roho si wanadamu waliokufa ambao wamefufuliwa kuishi mbinguni.—Zaburi 104:1, 4; Danieli 7:10.

Ni lazima tufanye nini ili tupate baraka za kuishi milele katika Paradiso duniani? Hatua ya kwanza ni kujifunza Neno la Mungu, Biblia Takatifu. ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo,’ Yesu akasema katika sala.—Yohana 17:3.

Kutumia ujuzi huo katika maisha ni hatua nyingine ya kupata furaha ya milele katika Paradiso. (Yakobo 1:22-24) Wanaoishi kwa kupatana na Neno la Mungu wanalo tumaini la kuona kwa macho yao wenyewe utimizo wa unabii mbalimbali kama ule wa Isaya 11:9 ambao husema hivi: “Hawatadhuru [wanadamu] wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Italiki ni zetu.)

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ukitaka kujua ni kwa nini Mungu ameruhusu uovu kuwapo mbinguni na duniani, soma kitabu cha Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., ukurasa wa 70-79.

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” —Zaburi 37:29