Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kununua Wakati wa Kusoma na Kujifunza

Kununua Wakati wa Kusoma na Kujifunza

Kununua Wakati wa Kusoma na Kujifunza

“[Jinunulieni] kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu.”—WAEFESO 5:16.

1. Kwa nini ni jambo la hekima kupangia wakati wetu, na namna tunavyotumia wakati wetu yaweza kufunua nini kutuhusu?

IMESEMWA kwamba “kuchagua wakati ni kuokoa wakati.” Mtu ambaye hupangia wakati wake ili kufanya mambo yanayohitaji kufanywa mara nyingi atafaidika zaidi na wakati wake. Mfalme Solomoni mwenye hekima aliandika hivi: “Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” (Mhubiri 3:1) Sote tuna kiasi kilekile cha wakati; ni juu yetu kujua namna tutakavyoutumia. Jinsi tunavyopanga mambo ya kutangulizwa na kupangia wakati wetu hufunua kwa kiasi kikubwa ni nini chenye thamani zaidi moyoni mwetu.—Mathayo 6:21.

2. (a) Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema nini kuhusu uhitaji wetu wa kiroho? (b) Twapaswa kufanya uchunguzi gani wa kibinafsi?

2 Inatubidi tutumie wakati kula na kulala kwa sababu haya ni mahitaji ya kimwili. Lakini vipi juu ya mahitaji yetu ya kiroho? Twajua kwamba lazima yatoshelezwe vilevile. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitangaza hivi: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Hiyo ndiyo sababu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hutukumbusha kwa ukawaida umuhimu wa kutumia wakati kusoma na kujifunza Biblia. (Mathayo 24:45) Huenda ukatambua jinsi ilivyo muhimu kufanya hivyo lakini waweza kuhisi kwamba huna wakati wa kujifunza au kusoma Biblia. Ikiwa ndivyo, acheni tuchunguze njia za kupata wakati zaidi maishani mwetu ili kusoma Neno la Mungu, kufanya funzo la kibinafsi, na kutafakari.

Kutafuta Wakati wa Kusoma na Kujifunza Biblia

3, 4. (a) Mtume Paulo alitoa shauri gani kuhusu kutumia wakati wetu, na hilo latia ndani nini? (b) Paulo alimaanisha nini alipotushauri ‘tujinunulie kabisa wakati unaofaa’?

3 Kwa kufikiria nyakati tunamoishi, sote twahitaji kutii maneno ya mtume Paulo: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu. Kwa ajili ya hili acheni kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.” (Waefeso 5:15-17) Bila shaka, shauri hili lahusu sehemu zote za maisha yetu tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, kutia ndani kutafuta wakati wa kusali, kujifunza, kuhudhuria mikutano, na kutumia wakati mwingi iwezekanavyo kuhubiri “habari njema ya ufalme.”—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

4 Leo watumishi wengi wa Yehova huona ikiwa vigumu kupata wakati wa kusoma Biblia na kuwa na funzo lenye kina. Bila shaka hatuwezi kuirefusha siku, kwa hiyo lazima shauri la Paulo liwe linamaanisha jambo tofauti. Katika Kigiriki, fungu la maneno “kununua kabisa wakati unaofaa” ladokeza kununua kwa kupoteza kitu kingine. Katika kichapo chake Expository Dictionary, W. E. Vine aeleza fungu hilo kuwa lamaanisha “kutumia kila fursa kwa kadiri uwezavyo, kutumia kila fursa kwa njia bora kabisa kwa kuwa ukipoteza fursa yoyote huwezi kuipata tena.” Tutanunua kutoka kwenye nini au kutoka wapi wakati unaofaa ili kusoma na kujifunza Biblia?

Lazima Tupange Mambo ya Kutangulizwa

5. Ni kwa nini na ni kwa njia gani tunaweza “kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi”?

5 Mbali na wajibu wetu wa kimwili, tuna mambo mengi sana ya kiroho tunayohitaji kushughulikia. Tukiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, tuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Kwa sababu hiyo, Paulo aliagiza Wakristo katika Filipi ‘wahakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Hilo lamaanisha kwamba lazima tupange mambo ya kutangulizwa. Sikuzote mambo ya kiroho yapasa kutangulia mambo ya kimwili. (Mathayo 6:31-33) Hata hivyo, lazima tuwe na usawaziko tunapotimiza wajibu wetu wa kiroho. Tunagawanyaje wakati wetu kati ya mambo mbalimbali yahusuyo maisha yetu ya Kikristo? Waangalizi wasafirio wanaripoti kwamba kati ya “mambo yaliyo ya maana zaidi” ambayo Mkristo apaswa kuzingatia, funzo la kibinafsi na usomaji wa Biblia, huelekea kupuuzwa.

6. Ni nini kinachohusika katika kununua kabisa wakati unaofaa kuhusu kazi ya kimwili au kazi ya nyumbani?

6 Kama tulivyoona, kununua kabisa wakati unaofaa kwatia ndani “kutumia kila fursa kwa kadiri uwezavyo” na “kutumia kila fursa kwa njia bora kabisa.” Kwa hiyo ikiwa hatuna mazoea mazuri ya kusoma na kujifunza Biblia, ingefaa tujichunguze kibinafsi tuone jinsi tunavyotumia wakati wetu. Ikiwa kazi yetu ya kimwili inachukua wakati na nguvu zetu nyingi, twapaswa kusali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. (Zaburi 55:22) Huenda tukafaulu kufanya marekebisho yatakayotuwezesha kuwa na wakati mwingi zaidi kwa ajili ya mambo yaliyo ya maana yanayohusu ibada ya Yehova, kutia ndani funzo na usomaji wa Biblia. Kwa kufaa imesemwa kwamba kazi ya mwanamke haiishi kamwe. Kwa hiyo dada Wakristo pia wapaswa kupanga mambo ya kutangulizwa na kutenga wakati hususa wa kusoma Biblia na kujifunza kwa makini.

7, 8. (a) Mara nyingi twaweza kununua wakati wa kusoma na kujifunza Biblia kutoka kwenye utendaji gani? (b) Kusudi la tafrija ni nini, na kukumbuka hilo kwaweza kutusaidiaje tupange mambo tutakayotanguliza?

7 Kwa ujumla, wengi wetu twaweza kununua kabisa wakati unaofaa kwa ajili ya funzo kwa kupuuza mambo yasiyo ya maana. Twaweza kujiuliza hivi: ‘Mimi hutumia wakati mwingi kadiri gani kusoma magazeti ya kilimwengu, kutazama programu za televisheni, kusikiliza muziki, au kucheza michezo ya vidio? Je, mimi hutumia kompyuta kwa wakati mwingi kuliko ule ninaotumia kusoma Biblia?’ Paulo asema hivi: “Acheni kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.” (Waefeso 5:17) Yaonekana kutazama televisheni kupita kiasi ndiyo sababu kubwa ifanyayo Mashahidi wengi wasipate wakati wa kutosha kujifunza kibinafsi na kusoma Biblia.—Zaburi 101:3; 119:37, 47, 48.

8 Huenda wengine wakasema kwamba hawawezi kujifunza wakati wote, kwamba wanahitaji tafrija. Ingawa hilo ni kweli, huenda ikafaa kufikiria wakati tunaotumia kupumzika na kuulinganisha na wakati tunaotumia hasa kujifunza au kusoma Biblia. Matokeo yaweza kukushangaza. Ingawa tafrija na kupumzika vyahitajika, lazima mambo hayo yafanywe wakati unaofaa. Kusudi la tafrija ni kutuburudisha ili tupate nguvu mpya kwa ajili ya utendaji wa kiroho. Programu nyingi za televisheni na michezo ya vidio humchosha mtu kabisa, ilhali kusoma na kujifunza Neno la Mungu huburudisha na humtia mtu nguvu.—Zaburi 19:7, 8.

Jinsi Ambavyo Wengine Hupata Wakati wa Kujifunza

9. Kuna manufaa gani ya kufuata shauri lipatikanalo katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—1999?

9 Dibaji ya chapa ya 1999 ya kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku yasema hivi: “Litakuwa jambo lenye manufaa zaidi kuchunguza andiko la kila siku na maelezo ya kitabu hiki asubuhi. Utahisi kana kwamba Yehova, yule Mfunzi Mtukufu, anakuamsha na mafundisho yake. Kiunabii Yesu Kristo anasemekana kuwa akinufaika na mafundisho ya Yehova kila asubuhi: ‘[Yehova] huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao.’ Mafundisho hayo yalimpa Yesu ‘ulimi wa hao wafundishwao’ ili aweze ‘kujua jinsi ya kumtegemeza kwa maneno yeye aliyechoka.’ (Isa. 30:20; 50:4; Mt. 11:28-30) Kuamshwa kila asubuhi ili kupata shauri la wakati wake kutoka kwa Neno la Mungu kutakusaidia ukabiliane na matatizo yako mwenyewe na pia kutakuandaa uwe na ‘ulimi wa wafundishwao’ kusaidia wengine.” *

10. Wengine hupataje wakati wa kusoma na kujifunza Biblia, nao hupata manufaa gani?

10 Wakristo wengi hufuata shauri hilo kwa kusoma andiko la kila siku na maelezo na kwa kusoma Biblia au kujifunza asubuhi mapema. Katika Ufaransa painia mmoja mwaminifu huamka mapema kila siku na hutumia dakika 30 kusoma Biblia. Ni nini ambacho kimemwezesha kufanya hivyo kwa miaka hiyo yote? Asema hivi: “Mimi huchochewa sana, nami hufuata ratiba yangu ya usomaji hata iweje!” Hata tuwe tumechagua wakati gani, jambo muhimu ni kufuata ratiba yetu. René Mica, ambaye amekuwa katika utumishi wa painia kwa zaidi ya miaka 40 katika Ulaya na Afrika Kaskazini, asema hivi: “Tangu 1950 nimekuwa na mradi wa kusoma Biblia nzima kila mwaka, na sasa nimefanya hivyo mara 49. Ninahisi kwamba hilo ni muhimu ili kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Muumba wangu. Kutafakari juu ya Neno la Mungu hunisaidia kuelewa vizuri zaidi haki ya Yehova na sifa zake nyinginezo na kumenitia nguvu sana.” *

“Magawio ya Chakula Kwenye Wakati Ufaao”

11, 12. (a) Ni ‘magawio gani ya chakula’ ambayo yameandaliwa na “msimamizi-nyumba mwaminifu”? (b) “Magawio ya chakula” yameandaliwaje kwa wakati ufaao?

11 Kama vile kula chakula kwa ukawaida huchangia afya nzuri ya kimwili, ratiba ya kawaida ya funzo na usomaji wa Biblia huchangia afya nzuri ya kiroho. Katika Gospeli ya Luka, twasoma maneno haya ya Yesu: “Ni nani kwa kweli aliye msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana-mkubwa wake atamweka rasmi juu ya baraza la mahadimu wake kufuliza kuwapa kipimo chao cha magawio ya chakula kwenye wakati ufaao?” (Luka 12:42) Kwa miaka zaidi ya 120 sasa, “magawio ya chakula [cha kiroho] kwenye wakati ufaao” yameandaliwa katika Mnara wa Mlinzi, na vilevile katika vitabu na vichapo vingine vinavyotegemea Biblia.

12 Ona usemi “kwenye wakati ufaao.” Kwa wakati ufaao, ‘Mfunzi wetu Mtukufu,’ Yehova kupitia Mwana wake na jamii ya mtumwa, ameelekeza watu wake katika mambo yanayohusu mafundisho na mwenendo. Imekuwa ni kana kwamba sote tumesikia sauti ikituambia: “Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.” (Isaya 30:20, 21) Isitoshe, watu mmoja-mmoja wasomapo Biblia na vichapo vyote vya Biblia kwa makini, mara nyingi wanahisi kwamba mawazo yaliyo ndani yanaelekezwa kwao hasa. Naam, shauri la Mungu na mwelekezo wake utakuja kwa wakati ufaao na kutuwezesha tukinze kishawishi au kufanya uamuzi wenye hekima.

Sitawisha Mazoea Mazuri ya Kujilisha

13. Baadhi ya mazoea mabaya ya kujilisha kiroho ni gani?

13 Ili tunufaike kikamili na “magawio ya chakula” yanayoandaliwa kwa wakati ufaao, twahitaji kuwa na mazoea mazuri ya kujilisha. Ni muhimu kuwa na ratiba ya kawaida ya usomaji wa Biblia na funzo la kibinafsi na kuifuata. Je, una mazoea mazuri ya kujilisha kiroho na vipindi vya kawaida vya kufanya funzo la kibinafsi lenye kina? Au je, wewe husoma kijuu-juu tu habari ambayo tumetayarishiwa kwa uangalifu, ukila mbiombio, au hata kukosa kabisa kula milo fulani? Mazoea mabaya ya kujilisha kiroho yamefanya wengine wawe na imani dhaifu—hata kupoteza imani kabisa.—1 Timotheo 1:19; 4:15, 16.

14. Kwa nini inanufaisha kupitia kwa uangalifu habari inayoonekana kuwa tunaifahamu?

14 Huenda wengine wakahisi kwamba tayari wanajua mafundisho ya msingi na kwamba si makala zote huwa na jambo jipya kabisa. Kwa hiyo, si lazima wajifunze kwa ukawaida na kuhudhuria mikutano. Hata hivyo, Biblia huonyesha kwamba twahitaji kukumbushwa mambo ambayo tumejifunza tayari. (Zaburi 119:95, 99; 2 Petro 3:1; Yuda 5) Kama vile mpishi mzuri hupika chakula kilekile kwa njia nyingi zenye kupendeza, ndivyo na jamii ya mtumwa huandaa chakula cha kiroho chenye lishe katika njia nyingi mbalimbali. Hata katika makala ambazo zinazungumzia habari iliyotajwa mara nyingi, mna mambo mazuri ambayo hatungependa kukosa. Ukweli ni kwamba yale ambayo tutapata kutoka kwa habari tunayosoma yategemea sana wakati na jitihada tunayofanya katika kujifunza habari hiyo.

Manufaa ya Kiroho Tunayopata kwa Kusoma na Kujifunza

15. Kusoma na kujifunza Biblia hutusaidiaje tuwe wahudumu bora wa Neno la Mungu?

15 Tunapata manufaa mengi kwa kusoma na kujifunza Biblia. Tunasaidiwa kutimiza mojawapo ya madaraka yetu muhimu ya Kikristo, yaani, kila mmoja wetu awe ‘mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, akilitumia sawasawa neno la ile kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Kadiri tuzidivyo kusoma na kujifunza Biblia, ndivyo akili zetu zitakavyozidi kujazwa mawazo ya Mungu. Ndipo, kama Paulo, tutakapoweza ‘kujadiliana na watu kwa kutoa sababu kutokana na Maandiko, tukieleza na kuthibitisha kwa marejezo’ kweli tukufu ya makusudi ya Yehova. (Matendo 17:2, 3) Ustadi wetu wa kufundisha utaboreka, na maongezi, hotuba, na shauri letu litakuwa lenye kujenga sana kiroho.—Mithali 1:5.

16. Ni katika njia gani sisi hunufaika kibinafsi kwa kusoma na kujifunza Neno la Mungu?

16 Kwa kuongezea, wakati tunaotumia kuchunguza Neno la Mungu utatuwezesha kupatanisha maisha yetu kikamili na njia za Yehova. (Zaburi 25:4; 119:9, 10; Mithali 6:20-23) Utaimarisha sifa zetu za kiroho, kama vile unyenyekevu, uaminifu-mshikamanifu, na furaha. (Kumbukumbu la Torati 17:19, 20; Ufunuo 1:3) Tunapotumia ujuzi tunaopata kwa kusoma na kujifunza Biblia, tunafurahia kupokea roho ya Mungu maishani mwetu bila kizuizi chochote, na hivyo kudhihirisha zaidi tunda la roho katika yote tufanyayo.—Wagalatia 5:22, 23.

17. Kiasi na ubora wa usomaji na funzo letu la kibinafsi la Biblia unaathirije uhusiano wetu pamoja na Yehova?

17 Jambo la maana zaidi ni kwamba wakati tunaonunua kutoka katika utendaji mwingine ili kusoma na kujifunza Neno la Mungu utatunufaisha kwa habari ya uhusiano wetu na Mungu. Paulo alisali kwamba Wakristo wenzake ‘wajazwe ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi watembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye.’ (Wakolosai 1:9, 10) Vivyo hivyo, ili nasi ‘tutembee kwa kumstahili Yehova,’ lazima ‘tujazwe ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho.’ Ni wazi kwamba kupokea baraka na kibali cha Yehova kwategemea sana kiasi na ubora wa usomaji na funzo letu la kibinafsi la Biblia.

18. Twaweza kupokea baraka gani tukitii maneno ya Yesu kwenye Yohana 17:3?

18 ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Hilo ni mojawapo ya maandiko yanayotumiwa sana na Mashahidi wa Yehova kusaidia wengine wathamini umuhimu wa kujifunza Neno la Mungu. Ni muhimu pia kwa kila mmoja wetu kufanya hivyo kibinafsi. Tumaini letu la kuishi milele lategemea ukuzi wetu katika kumjua Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Ebu fikiria hilo lamaanisha nini. Hatutakoma kamwe kujifunza zaidi juu ya Yehova—na tutaendelea kujifunza juu yake milele!—Mhubiri 3:11; Waroma 11:33.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

^ fu. 10 Ona makala “Wanapoisoma na Wanavyonufaika,” iliyochapishwa katika toleo la Mei 1, 1995 la Mnara wa Mlinzi, ukurasa wa 20-21.

Maswali ya Kupitia

• Ni nini kinachoonyeshwa na jinsi tutumiavyo wakati wetu?

• Twaweza kununua wakati wa kusoma na kujifunza Biblia kutoka kwenye utendaji gani?

• Kwa nini tuangalie mazoea yetu ya kujilisha kiroho?

• Tunapata manufaa gani kwa kusoma na kujifunza Maandiko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida kutatuwezesha ‘kulitumia sawasawa neno la ile kweli’

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kuwa na usawaziko kati ya shughuli nyingi maishani na ufuatiaji mambo ya kiroho hutokeza manufaa tele