Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usomaji wa Biblia—Wenye Kufaidi na Wenye Kupendeza

Usomaji wa Biblia—Wenye Kufaidi na Wenye Kupendeza

Usomaji wa Biblia—Wenye Kufaidi na Wenye Kupendeza

“Ni lazima . . . ukisome mchana na usiku.”—YOSHUA 1:8, NW.

1. Ni nini baadhi ya manufaa ya kusoma kwa ujumla na hasa usomaji wa Biblia?

KUSOMA habari zinazofaa ni kazi inayonufaisha. Mwanafalsafa wa siasa Mfaransa (Charles-Louis de Secondat) aliandika hivi: “Sikuzote nimeliona funzo kuwa ponyo la uchovu wa maisha. Sijawahi kupata msononeko ambao nilishindwa kuuondoa baada ya kusoma kwa muda wa saa moja.” Kwa kiwango kikubwa, ndivyo ilivyo na usomaji wa Biblia. Mtunga-zaburi aliyepuliziwa alisema hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo.”—Zaburi 19:7, 8.

2. Kwa nini Yehova ameihifadhi Biblia kwa muda mrefu, naye anatarajia watu wake wafanye nini nayo?

2 Akiwa Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu ameihifadhi kwa muda mrefu licha ya upinzani mkali kutoka kwa maadui wa Biblia wa kidini na wasio wa kidini. Kwa kuwa ni mapenzi yake kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli,” amehakikisha kwamba Neno lake linapatikana kwa wanadamu wote. (1 Timotheo 2:4) Inakadiriwa kwamba karibu asilimia 80 ya watu duniani wanaweza kufikiwa kwa kutumia lugha 100. Biblia nzima hupatikana katika lugha 370, na sehemu za Maandiko hayo zaweza kusomwa katika lugha na lahaja nyingine 1,860. Yehova anataka watu wake wasome Neno lake. Yeye hubariki watumishi wake wanaosikiliza Neno lake, naam, wanaolisoma kila siku.—Zaburi 1:1, 2.

Usomaji wa Biblia Ni Takwa kwa Waangalizi

3, 4. Yehova aliwataka wafalme wa Israeli wafanye nini, na ni kwa sababu gani wazee Wakristo wanatakiwa wafanye hivyo leo?

3 Akifikiria kimbele wakati ambapo Israeli wangekuwa na mfalme wa kibinadamu, Yehova alisema hivi: “Na iwe, zamani aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, kufuata hicho kilicho mbele ya makuhani Walawi; na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya; moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake, wala asikengeuke katika maagizo, kwa mkono wa kuume wala wa kushoto.”—Kumbukumbu la Torati 17:18-20.

4 Ona sababu zilizofanya Yehova awatake wafalme wote ambao wangetawala Israeli wasome kitabu cha sheria yake kila siku: (1) “ili apate kujifunza kumcha BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya”; (2) “moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake”; (3) “asikengeuke katika maagizo, kwa mkono wa kuume wala wa kushoto.” Je, waangalizi Wakristo leo hawahitaji kumcha Yehova, kutii sheria zake, kutojiinua juu ya ndugu zao, na kuepuka kukengeuka katika maagizo ya Yehova? Bila shaka usomaji wa Biblia kila siku ni wa maana sana kwao kama ulivyokuwa kwa wafalme wa Israeli.

5. Ni habari gani ambayo Baraza Linaloongoza liliandikia washiriki wa Halmashauri za Tawi hivi karibuni kuhusu usomaji wa Biblia, na kwa nini ingefaa wazee wote Wakristo kufuata shauri hilo?

5 Leo wazee Wakristo wana shughuli nyingi sana, jambo linalofanya iwe vigumu kusoma Biblia kila siku. Kwa mfano, washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova na washiriki wa Halmashauri za Tawi ulimwenguni pote, ni wanaume wenye shughuli nyingi kwelikweli. Hata hivyo, barua ya hivi majuzi kutoka kwa Baraza Linaloongoza iliyotumwa kwa washiriki wote wa Halmashauri za Tawi ilikazia uhitaji wa kusoma Biblia kila siku na kuwa na mazoea mazuri ya kujifunza. Barua hiyo ilisema kwamba kufanya hivyo kutazidisha upendo wetu kwa Yehova na kwa ile kweli, na “kutatusaidia tudumishe imani, shangwe, na uvumilivu wetu hadi mwisho wenye utukufu.” Wazee wote katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova huona uhitaji wa kufanya hivyo. Kusoma Maandiko kila siku kutawasaidia “kutenda kwa hekima.” (Yoshua 1:7, 8, NW ) Kwao hasa, usomaji wa Biblia ‘wafaa kwa mafundisho, na kwa kuonya makosa, na kwa kuongoza, na kwa kuadibisha katika haki.’—2 Timotheo 3:16, UV.

Ni Jambo la Lazima kwa Wachanga na Wazee

6. Kwa nini Yoshua alisoma kwa sauti kubwa maneno yote ya sheria ya Yehova mbele ya makabila ya Israeli yaliyokusanyika pamoja na wageni?

6 Katika nyakati za kale, watu mmoja-mmoja hawakuwa na nakala za Maandiko, kwa hiyo usomaji wa Biblia ulifanywa mbele za umati uliokusanyika. Baada ya Yehova kumpa ushindi dhidi ya jiji la Ai, Yoshua alikusanya makabila ya Israeli mbele ya Mlima Ebali na Mlima Gerizimu. Kisha simulizi hilo latuambia hivi: “Alisoma maneno yote ya torati, baraka na laana, sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati. Hapakuwa na hata neno moja katika hayo aliyoamuru Musa, ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya kusanyiko lote la Israeli, na mbele ya wanawake, na watoto, na wageni waliokaa nao.” (Yoshua 8:34, 35) Wazee kwa wachanga, wazaliwa kwa wageni, walihitaji kukaziwa katika mioyo yao na akili zao ni mwenendo upi ambao ungeleta baraka za Yehova na ni upi ambao ungewakosesha kibali chake. Kwa hakika usomaji wa Biblia unaofanywa kwa ukawaida utatusaidia kwa habari hii.

7, 8. (a) Ni nani leo walio kama “wageni,” na kwa nini wanahitaji kusoma Biblia kila siku? (b) Ni katika njia zipi “watoto” miongoni mwa watu wa Yehova wanaweza kufuata kielelezo cha Yesu?

7 Leo, mamilioni ya watumishi wa Yehova ni kama “wageni” hao katika maana ya kiroho. Hapo zamani, walikuwa wakiishi kulingana na viwango vya ulimwengu, lakini wamebadili maisha yao. (Waefeso 4:22-24; Wakolosai 3:7, 8) Wanahitaji kujikumbusha daima viwango vya Yehova vya mema na mabaya. (Amosi 5:14, 15) Kusoma Neno la Mungu kila siku huwasaidia wafanye hivyo.—Waebrania 4:12; Yakobo 1:25.

8 Pia kuna “watoto” wengi miongoni mwa watu wa Yehova ambao wamefundishwa viwango vya Yehova na wazazi wao lakini wanahitaji kujisadikishia wao wenyewe kwamba mapenzi yake yanafaa. (Waroma 12:1, 2) Wanaweza kufanyaje hivyo? Katika Israeli, makuhani na wazee waliagizwa hivi: “Uisome torati hii mbele ya Israeli wote masikioni mwao. Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni wako aliyemo malangoni mwako wapate kusikia na kujifunza, na kumcha BWANA, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii; na watoto wao wasiojua, wapate kusikia na kujifunza kumcha BWANA, Mungu wenu.” (Kumbukumbu la Torati 31:11-13) Akiwa anaishi chini ya Sheria, Yesu alipokuwa na umri mdogo wa miaka 12 alipendezwa sana kuelewa sheria za Baba yake. (Luka 2:41-49) Baadaye, ikawa desturi yake kusikiliza na kushiriki kusoma Maandiko katika sinagogi. (Luka 4:16; Matendo 15:21) Leo ingefaa vijana wafuate kielelezo cha Yesu kwa kusoma Neno la Mungu kila siku na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ambapo watu husoma na kujifunza Biblia.

Usomaji wa Biblia —Jambo la Kutangulizwa

9. (a) Kwa nini twahitaji kuwa wateuzi katika mambo tunayosoma? (b) Mhariri-mwanzilishi wa gazeti hili alisema nini kuhusu misaada ya kujifunzia Biblia?

9 Mfalme Solomoni mwenye hekima aliandika hivi: “Kubali maonyo; hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.” (Mhubiri 12:12) Huenda mtu akaongezea kwamba kusoma vitabu vingi vinavyochapishwa leo hakuuchoshi mwili tu, bali ni wazi kwamba kunahatarisha akili. Kwa hiyo ni muhimu kuwa wateuzi. Mbali na kusoma vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia, twahitaji kusoma Biblia yenyewe. Mhariri-mwanzilishi wa gazeti hili aliwaandikia wasomaji wake hivi: “Msisahau kamwe kwamba Biblia ndiyo Kiwango chetu na kwamba hata misaada yetu iwe yenye kubarikiwa na Mungu kadiri gani, hiyo ni ‘misaada’ na haiwi badala ya Biblia.” * Kwa hiyo, ingawa hatupaswi kupuuza vichapo vinavyotegemea Biblia, twahitaji kusoma Biblia yenyewe.

10. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amekaziaje umuhimu wa usomaji wa Biblia?

10 Kwa kuona uhitaji huo, kwa miaka mingi sasa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameratibu usomaji wa Biblia uwe sehemu ya programu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika kila kutaniko. (Mathayo 24:45) Programu ya sasa ya usomaji wa Biblia huchukua muda wa miaka ipatayo saba. Ratiba hii hunufaisha wote hasa wapya ambao hawajapata kusoma Biblia nzima. Wale wanaohudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower ya wamishonari na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na vilevile washiriki wapya wa Betheli wanatakiwa wasome Biblia nzima kwa muda wa mwaka mmoja. Hata uwe unatumia ratiba gani, wewe binafsi au mkiwa familia, kuifuata hutaka mtangulize usomaji wa Biblia.

Mazoea Yako ya Usomaji Huonyesha Nini?

11. Ni jinsi gani na kwa nini inatupasa kujilisha matamko ya Yehova kila siku?

11 Ikiwa una tatizo la kufuatana na ratiba yako ya usomaji wa Biblia, huenda ikafaa kujiuliza hivi: ‘Mazoea yangu ya kusoma au kutazama televisheni huenda yakaathirije uwezo wangu wa kusoma Neno la Yehova?’ Kumbuka yale aliyoandika Musa—na Yesu akayarudia—kwamba “binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4; Kumbukumbu la Torati 8:3) Kama vile tunavyohitaji kula mkate au chakula kingine kila siku maishani mwetu ili kujenga mwili wetu, vivyo hivyo twahitaji kutumia mawazo ya Yehova kila siku ili kudumisha hali yetu ya kiroho. Twaweza kupata mawazo ya Mungu kila siku kwa kusoma Maandiko.

12, 13. (a) Mtume Petro anaelezaje hamu tunayopaswa kuwa nayo ya Neno la Mungu? (b) Paulo atumiaje mfano wa maziwa kwa njia tofauti na Petro?

12 Tukithamini Biblia, “si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu,” tutavutwa kwa Biblia kama vile mtoto hutamani maziwa ya mama yake. (1 Wathesalonike 2:13) Mtume Petro alifanya ulinganisho huo alipoandika hivi: “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni, fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno, ili kupitia hilo mpate kukua kufikia wokovu, mradi mmeonja kwamba Bwana ni mwenye fadhili.” (1 Petro 2:2, 3) Ikiwa tumeonja kikweli, kupitia yale tuliyojionea kibinafsi, kwamba “Bwana ni mwenye fadhili,” tutasitawisha hamu ya kusoma Biblia.

13 Na itambuliwe kwamba katika fungu hili Petro alitumia mfano wa maziwa kwa njia tofauti na mtume Paulo. Maziwa humpa mtoto aliyezaliwa hivi karibuni lishe yote anayohitaji. Mfano wa Petro waonyesha kwamba Neno la Mungu lina mambo yote tunayohitaji ili “kukua kufikia wokovu.” Kwa upande mwingine, Paulo atumia uhitaji wa maziwa ili kueleza mazoea yasiyofaa ya kujilisha ya watu fulani wanaodai kuwa wakomavu kiroho. Katika barua yake kwa Wakristo Waebrania, Paulo aliandika hivi: “Ijapokuwa mwapaswa kuwa walimu kwa kufikiria wakati, nyinyi mwahitaji tena mtu fulani awafundishe tangu mwanzo mambo ya msingi ya matamko matakatifu ya Mungu; nanyi mmekuwa kama wahitajio maziwa, si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu ashirikiye maziwa halijui sana neno la uadilifu, kwa maana yeye ni kitoto. Lakini chakula kigumu ni cha watu wakomavu, cha wale ambao kupitia utumizi, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.” (Waebrania 5:12-14) Usomaji wa Biblia unaofanywa kwa makini waweza kutusaidia sana kusitawisha uwezo wetu wa ufahamu na kuchochea hamu yetu ya mambo ya kiroho.

Jinsi ya Kusoma Biblia

14, 15. (a) Mtungaji wa Biblia hutupa pendeleo gani? (b) Twaweza kunufaikaje na hekima kutoka kwa Mungu? (Toa mifano.)

14 Usomaji wa Biblia unaofaidi zaidi huanza, si kwa kusoma, bali kwa kusali. Sala ni pendeleo lisilo na kifani. Ni kana kwamba unaanza kusoma kitabu chenye habari ngumu kwa kumwomba mtungaji wa kitabu hicho akusaidie kuelewa habari unayotaka kusoma. Kufanya hivyo kwaweza kukunufaisha kama nini! Mtungaji wa Biblia, Yehova, anakupa pendeleo hilo. Mshiriki mmoja wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza aliandikia ndugu zake hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo. Lakini acheni afulize kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo.” (Yakobo 1:5, 6) Baraza Linaloongoza la kisasa hutuhimiza daima tufanye usomaji wa Biblia kwa sala.

15 Hekima ni kutumia ujuzi kwa busara. Kwa hiyo kabla ya kufungua Biblia yako, mwombe Yehova akusaidie kutambua mambo fulani katika usomaji wako unayohitaji kutumia katika maisha yako ya kibinafsi. Linganisha mambo mapya uliyojifunza na ujuzi uliopata hapo awali. Yatumie pamoja na “kiolezo cha maneno yenye afya” ambayo umefahamu. (2 Timotheo 1:13) Fikiria kwa uzito visa vya maisha ya watumishi wa Yehova wa kale, na ujiulize ungetendaje chini ya hali zinazofanana na hizo.—Mwanzo 39:7-9; Danieli 3:3-6, 16-18; Matendo 4:18-20.

16. Tumepewa madokezo gani tunayoweza kutumia ili kutuwezesha kufanya usomaji wetu wa Biblia unufaishe na uwe wa maana zaidi?

16 Usisome tu ili kumaliza kurasa ulizopangia. Usiwe na haraka. Tafakari yale unayosoma. Ukitatanishwa na jambo fulani, angalia marejezo yanayolingana ikiwa Biblia yako inayo. Ikiwa bado huelewi jambo hilo, litie alama ili kufanya utafiti zaidi baadaye. Unaposoma, tia alama au yanakili maandiko ambayo ungependa hasa kuyakumbuka. Pia waweza kuandika pambizoni mambo na marejezo yanayolingana. Andika maneno makuu ya maandiko unayohisi utayahitaji siku fulani katika kazi ya kuhubiri na kufundisha, na kutazama faharisi ya maneno ya Biblia upande wa nyuma wa Biblia yako. *

Fanya Usomaji wa Biblia Upendeze

17. Kwa nini twapasa kupendezwa kusoma Biblia?

17 Mtunga-zaburi alizungumza juu ya mtu mwenye furaha ambaye “sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” (Zaburi 1:2) Usomaji wetu wa Biblia kila siku haupaswi kuwa kama kazi bali wapaswa kupendeza kwelikweli. Njia moja ya kuufanya upendeze ni kutambua daima thamani ya mambo tunayojifunza. Mfalme Solomoni mwenye hekima aliandika hivi: “Heri mtu yule aonaye hekima . . . Njia zake ni njia za kupendeza sana, na mapito yake yote ni amani. Yeye ni mti wa uzima kwao wamshikao sana; ana heri kila mtu ashikamanaye naye.” (Mithali 3:13, 17, 18) Jitihada inayohitajiwa ili kujipatia hekima inafaa kwelikweli, kwa kuwa njia zake ni njia za kupendeza, amani, furaha, na hatimaye, uhai.

18. Ni nini kingine kinachohitajika mbali na usomaji wa Biblia, na tutajifunza nini katika makala inayofuata?

18 Naam, usomaji wa Biblia ni wenye kufaidi na wenye kupendeza. Lakini je, unatosha? Washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wamekuwa wakiisoma Biblia kwa karne nyingi, “sikuzote wakijifunza na bado hawawezi kamwe kufikia ujuzi sahihi juu ya kweli.” (2 Timotheo 3:7) Ili usomaji wa Biblia uwe na matokeo, lazima tuufanye tukiwa na lengo la kutumia ujuzi tunaojipatia katika maisha yetu ya kibinafsi na kuutumia katika kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Hilo lataka jitihada na njia nzuri za kujifunza, ambazo pia zaweza kufurahisha na kuthawabisha, kama tutakavyoona katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Soma kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., ukurasa wa 241.

^ fu. 16 Ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1995, ukurasa wa 16-17, “Madokezo ya Kuboresha Usomaji Wako wa Biblia.”

Maswali ya Kupitia

• Ni shauri gani walilopewa wafalme wa Israeli linalotumika leo kwa waangalizi, na kwa nini?

• Ni nani leo walio kama “wageni” na “watoto,” na kwa nini wanahitaji kusoma Biblia kila siku?

• Ni katika njia gani zenye kutumika ambazo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametusaidia kusoma Biblia kwa ukawaida?

• Twaweza kunufaikaje na kupendezwa kabisa na usomaji wetu wa Biblia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wazee hasa, wapaswa kusoma Biblia kila siku

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alikuwa na desturi ya kushiriki kusoma Maandiko katika sinagogi