Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Waweza Kumkaribia Mungu Asiyeonekana?

Je, Waweza Kumkaribia Mungu Asiyeonekana?

Je, Waweza Kumkaribia Mungu Asiyeonekana?

‘Nawezaje kusitawisha uhusiano wa karibu na mtu nisiyeweza kumwona?’ huenda ukauliza. Huenda hilo likaonekana kuwa swali zuri. Lakini ebu fikiria:

KUONA ni muhimu kadiri gani ili kusitawisha mahusiano ya kudumu yenye upendo? Je, si mambo usiyoweza kuona ni muhimu kuliko mambo unayoona, au hata ni muhimu zaidi? Kwa hiyo, baadhi ya watu wamesitawisha uhusiano wa karibu pamoja na wengine kwa kuandikiana barua kwa ukawaida, na katika barua zao wao hueleza kwa unyofu yale yanayowapendeza na kuwachukiza, miradi, maadili, ucheshi, na tabia au mapendezi mengine.

Wasioona pia wathibitisha kwamba kuona si kwa lazima ili kusitawisha uhusiano wa karibu na mtu mwingine. Fikiria Edward na Gwen, wenzi wa ndoa wasioona. * Edward alikutana na Gwen walipokuwa wakisoma katika shule moja ya watu wazima wasioona. Alipenda sifa za Gwen, hasa unyofu wa usemi na mwenendo wake, na mtazamo wake bora juu ya kazi. Gwen kwa upande wake, alivutiwa na Edward kwa sababu, kama alivyosema, “yeye alikuwa na sifa zote ambazo nilifundishwa tangu utotoni kuwa ni muhimu.” Walianza kuchumbiana, na baada ya miaka mitatu walioana.

Edward asema hivi: “Mnapokuwa pamoja, kutoweza kuona hakuwezi kuzuia mtu asiweze kusitawisha uhusiano pamoja na mtu mwingine. Huenda msiweze kuonana kwa macho, lakini jambo hilo haliwezi kuzuia mpendane.” Leo, miaka 57 imepita na bado wanapendana sana. Waeleza kwamba uhusiano wao mzuri ajabu wahusisha angalau mambo manne: (1) kutambua sifa za yule mwingine, (2) kutafakari sifa hizo na kuzipenda, (3) kudumisha mawasiliano mazuri, na (4) kufanya mambo pamoja.

Mambo hayo manne ni ya maana katika uhusiano wowote wa karibu, uwe ni kati ya marafiki, wenzi wa ndoa au, muhimu zaidi, kati ya wanadamu na Mungu. Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi mambo hayo yawezavyo kutusaidia kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, ijapokuwa hatuwezi kumwona. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 6 Tofauti na uhusiano baina ya watu, msingi wa uhusiano pamoja na Mungu ni kuamini kwamba yeye yuko. (Waebrania 11:6) Kwa mazungumzo ya kindani juu ya jinsi ya kujenga imani thabiti katika Mungu, tafadhali soma kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.