Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Uwezavyo Kumkaribia Mungu

Jinsi Uwezavyo Kumkaribia Mungu

Jinsi Uwezavyo Kumkaribia Mungu

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia,” lasema andiko la Yakobo 4:8. Kwa kumtoa Mwanawe kwa ajili yetu, Yehova Mungu alionyesha kwamba anataka sana kuwa na uhusiano wa karibu na wanadamu.

KWA kuzingatia hatua hiyo ya upendo, mtume Yohana aliandika hivi: “Twa[m]penda [Mungu], kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Lakini ili sisi binafsi tumkaribie Mungu, ni lazima tuchukue hatua fulani. Hatua hizi zafanana na zile njia nne za kuwakaribia wanadamu wenzetu, zilizozungumziwa katika makala iliyotangulia. Acheni tuchunguze hatua hizo.

Chunguza Sifa Bora za Mungu

Mungu ana sifa nyingi bora, na baadhi ya sifa zake kuu ni upendo, hekima, haki, na nguvu. Hekima na nguvu zake zaonekana wazi katika mifumo ya sayari iliyoko mbali sana na dunia na vitu vilivyomo duniani, kuanzia makundi makubwa ya nyota hadi atomu ndogo sana. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”—Zaburi 19:1; Waroma 1:20.

Uumbaji pia huonyesha upendo wa Mungu. Kwa mfano, maumbile yetu yaonyesha kwamba Mungu anataka tufurahie maisha. Alitupa uwezo wa kuona rangi mbalimbali, kuonja na kunusa, kupenda muziki, kucheka, kupenda umaridadi, na pia akatupa uwezo na sifa nyingine nyingi ambazo si za lazima ili tuishi. Ndiyo, kwa kweli Mungu ni mkarimu, mwenye fadhili na upendo—sifa ambazo bila shaka zamfanya awe “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11; Matendo 20:35.

Yehova hufurahia kutekeleza enzi yake kuu kwa upendo na viumbe wake wenye akili husukumwa na upendo kuiunga mkono. (1 Yohana 4:8) Yehova ni Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, hata hivyo yeye huwatendea wanadamu, hasa watumishi wake waaminifu, kama baba mwenye upendo awatendeavyo watoto wake. (Mathayo 5:45) Hawanyimi chochote kinachowafaa. (Waroma 8:38, 39) Kama ilivyotajwa mwanzoni, hata alitoa uhai wa Mwana wake mzaliwa-pekee kwa ajili yetu. Naam, upendo ndio uliomsukuma Mungu kutuumba na kutupa tumaini la kuishi milele.—Yohana 3:16.

Yesu alitusaidia kufahamu kindani utu wa Mungu kwa sababu alimwiga Baba yake kikamili. (Yohana 14:9-11) Hakuwa na ubinafsi wowote, na alifikiria mahitaji ya wengine na kuwajali. Wakati mmoja, Yesu alitambulishwa kwa mwanamume kiziwi aliyekuwa pia bubu. Waweza kuwazia wasiwasi ambao huenda mwanamume yule alikuwa nao alipokuwa mahali penye watu wengi. Kwa kupendeza, Yesu alimpeleka mwanamume huyo mahali pa faragha na kumponya. (Marko 7:32-35) Je, wapenda watu wanaofikiria hisia zako na ambao hukustahi? Ikiwa ndivyo, basi kwa hakika utawakaribia zaidi Yehova na Yesu unapoendelea kujifunza mengi zaidi kuwahusu.

Tafakari Sifa za Mungu

Mtu fulani aweza kuwa na sifa bora, lakini twahitaji kutafakari juu yake ili tuvutiwe naye. Hali kadhalika na Yehova. Kutafakari sifa zake ni hatua ya pili yenye maana ili tumkaribie. Mfalme Daudi, mwanamume aliyempenda Yehova kwelikweli na aliyekuwa “mwenye kukubalika kwa moyo [wa Yehova],” alisema hivi: “Nimezikumbuka siku za kale, nimeyatafakari matendo yako yote, naziwaza kazi za mikono yako.”—Matendo 13:22; Zaburi 143:5.

Utazamapo maajabu ya uumbaji au usomapo Neno la Mungu, Biblia, je, kama vile Daudi, unatafakari yale unayoyaona na kusoma? Hebu wazia mwana ambaye ametoka tu kupokea barua kutoka kwa baba ampendaye sana. Angeionaje barua ile? Kwa hakika hangeisoma kijuujuu tu na kuitupa katika dawati. Badala yake, angeisoma ili aelewe kabisa, hata mambo madogo yote. Vilevile, twapaswa kupenda Neno la Mungu, kama alivyolipenda mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”—Zaburi 119:97.

Dumisha Mawasiliano Mazuri

Mawasiliano mazuri ni ya lazima katika mahusiano yoyote. Hayo yatia ndani kusema na kusikiliza—si kwa akili tu bali kwa moyo vilevile. Twasema na Muumba kupitia sala, ambayo yamaanisha kusema na Mungu kwa heshima. Yehova hufurahishwa na sala za wale wanaompenda na kumtumikia, na kukubali kwamba Yesu Kristo ni mwakilishi Wake mkuu.—Zaburi 65:2; Yohana 14:6, 14.

Zamani, Mungu alisema na wanadamu kwa njia mbalimbali, kutia ndani njozi, ndoto, na kupitia malaika. Hata hivyo, siku hizi anasema kupitia Biblia Takatifu, Neno lake lililoandikwa. (2 Timotheo 3:16) Neno lililoandikwa ni bora kwa njia nyingi. Ushauri wake wapatikana wakati wowote. Kama barua, laweza kusomwa tena na tena. Na halibadiliki kama vile habari zinazopashwa kwa mdomo. Kwa hiyo, ione Biblia kama barua nyingi kutoka kwa Baba mpendwa wa mbinguni, na umruhusu aseme nawe kila siku kupitia barua hizo.—Mathayo 4:4.

Kwa mfano, Biblia yatueleza maoni ya Yehova juu ya mema na mabaya. Yaeleza kusudi lake kwa wanadamu na kwa dunia. Na yafunua jinsi anavyoshughulika na watu na mataifa mbalimbali, kuanzia waabudu waaminifu hadi adui wenye chuki. Kwa kuandika katika Biblia jinsi ambavyo ameshughulika na wanadamu, Yehova ametupatia ufafanuzi wa kindani wa utu wake. Anafafanua upendo wake, shangwe, huzuni, kukatishwa tamaa, hasira, rehema, ufikirio—naam, mawazo na hisia zake zote, na kile kinachosababisha mawazo na hisia hizo—kwa njia ambayo wanadamu waweza kuelewa kwa urahisi.—Zaburi 78:3-7.

Baada ya kusoma sehemu fulani katika Neno la Mungu, wawezaje kunufaika kutokana na yale unayosoma? Na unawezaje hasa kumkaribia Mungu? Kwanza, tafakari kile ambacho umesoma na kujifunza juu ya Mungu binafsi, ukiruhusu mambo hayo yaingie moyoni. Halafu umwambie Yehova kupitia sala mawazo yako na jinsi unavyohisi moyoni juu ya yale ambayo umesoma na jinsi utakavyojitahidi kunufaishwa nayo. Hayo ndiyo mawasiliano. Ikiwa kuna mambo mengine yakusumbuayo, bila shaka unaweza kuyataja katika sala yako.

Tenda Pamoja na Mungu

Biblia yasema kwamba wanaume fulani waaminifu wa siku za kale walikwenda pamoja na, au mbele za, Mungu wa kweli. (Mwanzo 6:9; 1 Wafalme 8:25) Hilo lamaanisha nini? Kimsingi lamaanisha kwamba waliishi kila siku kana kwamba Mungu alikuwapo papo hapo pamoja nao. Ni kweli kwamba walikuwa wenye dhambi. Hata hivyo walipenda sheria na kanuni za Mungu, na kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Yehova anapendezwa na huwatunza watu wa aina hiyo, kama vile Zaburi 32:8 inavyoonyesha: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.”

Yehova aweza kuwa rafiki yako wa karibu pia—rafiki atembeaye nawe, akutunzaye, na kukushauri kama baba anavyofanya. Nabii Isaya alimfafanua Yehova kuwa yule ‘akufundishaye ili upate faida, akuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.’ (Isaya 48:17) Tunapopata faida hizo, tunahisi kana kwamba Yehova yupo “kuumeni [kwetu],” kama alivyohisi Daudi.—Zaburi 16:8.

Jina la Mungu Lakazia Sifa Zake

Dini nyingi na vilevile tafsiri nyingi za Biblia hazitumii wala hazijulishi jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Hata hivyo, katika maandishi ya Kiebrania ya awali, jina hilo—Yehova—lapatikana mara 7,000 hivi! (Huku watafsiri wengi wa Biblia wakiliondoa jina la Mungu na kuacha majina ya miungu mingi ya uwongo yanayotajwa katika maandishi ya awali, kama vile Baali, Beli, Merodaki, na hata Shetani!)

Baadhi ya watu wanapuuza umuhimu wa kutotumia jina la Mungu. Lakini fikiria: Je, ni rahisi au ni vigumu kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na mtu asiye na jina? Majina ya cheo kama Mungu na Bwana (yanayotumiwa pia kwa miungu ya uwongo) huenda yakakazia uwezo, mamlaka, au cheo cha Yehova, lakini ni jina lake binafsi tu linalomtambulisha waziwazi. (Kutoka 3:15; 1 Wakorintho 8:5, 6) Jina la kibinafsi la Mungu wa kweli lakazia sifa zake na utu wake. Maneno haya ya mwanatheolojia Walter Lowrie ni ya kweli: “Mtu asiyemjua Mungu kwa jina hamfahamu Mungu kikweli.”

Fikiria Maria, aliyekuwa Mkatoliki mwaminifu aishiye Australia. Wakati Mashahidi wa Yehova walipokutana naye mara ya kwanza, Maria aliwaruhusu Mashahidi hao wamwonyeshe jina la Mungu katika Biblia. Aliitikiaje? “Nilipoona jina la Mungu katika Biblia mara ya kwanza, nililia machozi. Niliguswa sana kujua kwamba niliweza kulijua na kulitumia jina la kibinafsi la Mungu.” Maria aliendelea kujifunza Biblia, na kwa mara ya kwanza maishani mwake, alipata kufahamu kuwa Yehova ni mtu, na kuweza kusitawisha uhusiano wa kudumu naye.

Naam, twaweza ‘kumkaribia Mungu,’ ijapokuwa hatuwezi kumwona kwa macho. Twaweza “kuuona” utu wake bora sana katika mioyo na akili zetu na kwa njia hiyo kuzidi kumpenda. Upendo wa aina hiyo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Yehova Atakupenda Ukimpenda

MAHUSIANO yote yanahusisha pande mbili. Tunapomkaribia Mungu, yeye anazidi kutukaribia pia. Hebu fikiria hisia zake kwa wazee Simeoni na Ana, ambao wote wasifiwa katika Biblia. Mwandikaji wa Gospeli, Luka, atuambia kwamba Simeoni alikuwa “mwadilifu na mwenye kumstahi Mungu,” na alimngojea Mesiya. Yehova alitambua sifa hizo nzuri za Simeoni na alimwonyesha upendo mzee huyo mpendwa kwa kumfunulia kwamba “hangeona kifo kabla ya kuwa amemwona Kristo.” Yehova alitimiza ahadi yake na kumwelekeza Simeoni kwa mtoto mchanga Yesu, aliyepelekwa na wazazi Wake hekaluni Yerusalemu. Kwa msisimuko na uthamini mwingi, Simeoni alimpokea mtoto huyo mchanga mikononi mwake na kusali hivi: “Sasa, Bwana Mwenye Enzi Kuu, unamwacha mtumwa wako aende huru katika amani kulingana na tangazo lako; kwa sababu macho yangu yameona njia yako ya kuokoa.”—Luka 2:25-35.

“Saa hiyohiyo,” Yehova alionyesha upendo wake kwa Ana mwenye umri wa miaka 84 kwa kumwelekeza kwa Yesu pia. Biblia yasema kwamba mjane huyo mpendwa alikuwa hekaluni daima “akitoa utumishi mtakatifu” kwa Yehova. Alikuwa amejawa na uthamini, na kama Simeoni, akamshukuru Yehova kwa fadhili yake ya pekee, na baadaye akasema juu ya mtoto “kwa wale wote wenye kungojea ukombozi wa Yerusalemu.”—Luka 2:36-38.

Naam, Yehova alitambua kwamba Simeoni na Ana walimpenda kwa moyo na kumcha, na kuwa walipendezwa kindani na utimizo wa kusudi lake. Je, masimulizi kama hayo ya Biblia yanafanya umkaribie Yehova?

Kama vile Baba yake, Yesu pia alitambua mtu wa ndani. Alipokuwa akifundisha hekaluni, alimwona “mjane . . . mwenye uhitaji” aliyetoa tu “sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana.” Kwa watazamaji wengine, mchango wake ulikuwa wenye thamani ndogo sana, lakini haikuwa hivyo kwa Yesu. Alimsifu mwanamke huyo kwa kuwa alitoa yote aliyokuwa nayo. (Luka 21:1-4) Kwa hiyo, twaweza kuwa na hakika kwamba Yehova na Yesu watatupenda tukiwatolea kilicho bora, mchango wetu uwe mkubwa au mdogo.

Ingawa Mungu hufurahishwa na wanaompenda, yeye huhuzunika watu wanapomwasi na kutenda maovu. Mwanzo 6:6 hutuambia kuwa Yehova ‘alihuzunika moyo’ kwa sababu ya uovu wa wanadamu kabla ya Gharika ya siku za Noa. Baadaye Waisraeli wasiotii ‘walimjaribu Mungu [tena na tena]; wakampa mpaka [“wakamhuzunisha,” NW] Mtakatifu wa Israeli,’ yasema Zaburi 78:41. Naam, Mungu si “Chanzo cha Ulimwengu” tu asiyejali na asiye na hisia. Yeye ni mtu, na hisia zake ni timamu, wala hazijakufa ganzi kama zetu, kwa sababu ya kutokamilika.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kutafakari uumbaji wa Yehova ni njia moja ya kumkaribia