Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufalme wa Mungu—Utawala Mpya wa Dunia

Ufalme wa Mungu—Utawala Mpya wa Dunia

Ufalme wa Mungu—Utawala Mpya wa Dunia

“Ufalme . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—DANIELI 2:44.

1. Tunaweza kuwa na uhakika gani katika Biblia?

BIBLIA ni ufunuo wa Mungu kwa wanadamu. Mtume Paulo aliandika: “Mlipopokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Biblia ina habari zile tunazohitaji kujua kuhusu Mungu: habari kuhusu utu wake, makusudi yake, na anayotaka tufanye. Ina ushauri mzuri sana juu ya maisha ya familia na mwenendo wa kila siku. Ina habari nyingi za unabii uliotimizwa wakati uliopita, unaotimizwa sasa, na utakaotimizwa wakati ujao. Naam, “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

2. Yesu alikaziaje kichwa kikuu cha Biblia?

2 Jambo lililo muhimu sana katika Biblia ni kichwa chake kikuu: kutetewa kwa enzi kuu ya Mungu (haki yake ya kutawala) kupitia Ufalme wake wa mbinguni. Yesu alikazia ufalme huo katika huduma yake. “Yesu alianza kuhubiri na kusema: ‘Tubuni, nyinyi watu, kwa maana ufalme wa mbingu umekaribia.’” (Mathayo 4:17) Alionyesha Ufalme unapasa kuwa na umuhimu gani katika maisha yetu, alipohimiza: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Pia alionyesha umuhimu wa ufalme kwa kuwafundisha wafuasi wake kusali kwa Mungu hivi: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:10.

Utawala Mpya wa Dunia

3. Kwa nini Ufalme wa Mungu ni muhimu sana kwetu?

3 Kwa nini Ufalme wa Mungu ni muhimu sana kwa wanadamu? Kwa sababu hivi karibuni utachukua hatua ambayo itabadili milele utawala wa dunia hii. Unabii wa Danieli 2:44 wasema: “Katika siku za wafalme hao [wanaotawala dunia sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali mbinguni] ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote [serikali za kidunia] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Wakati Ufalme wa mbinguni wa Mungu utakapotawala kikamili, wanadamu hawataitawala dunia tena. Utawala wa wanadamu unaosababisha migawanyiko na usioridhisha utatoweka milele.

4, 5. (a) Kwa nini Yesu ndiye anayestahili kabisa kuwa Mfalme wa Ufalme? (b) Yesu atakuwa na mgawo gani hivi karibuni?

4 Mtawala Mkuu wa Ufalme wa mbinguni, Kristo Yesu, ambaye anaelekezwa moja kwa moja na Yehova, ndiye anayestahili kabisa. Kabla ya kuja duniani, Yesu ambaye ndiye wa kwanza kati ya viumbe vyote wa Mungu, aliishi mbinguni akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu. (Mithali 8:22-31) “Yeye ndio mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote; kwa sababu kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa katika mbingu na juu ya dunia.” (Wakolosai 1:15, 16) Na alipotumwa duniani na Mungu, Yesu alifanya mapenzi ya Mungu nyakati zote. Alivumilia majaribu makali sana na kufa akiwa mwaminifu kwa Baba yake.—Yohana 4:34; 15:10.

5 Yesu alithawabishwa kwa sababu ya kuwa mwaminifu kwa Mungu hata kifo. Mungu alimfufua kwenda mbinguni na kumpa haki ya kuwa Mfalme wa Ufalme wa mbinguni. (Matendo 2:32-36) Akiwa Mfalme wa Ufalme huo, Kristo Yesu atapewa na Mungu mgawo wenye kutia kicho wa kuongoza makumi ya maelfu ya viumbe wa roho kuondoa utawala wa wanadamu na uovu wote katika dunia yetu. (Mithali 2:21, 22; 2 Wathesalonike 1:6-9; Ufunuo 19:11-21; 20:1-3) Kisha Ufalme wa mbinguni wa Mungu chini ya Kristo utakuwa ndio mamlaka mpya yenye kutawala, serikali pekee juu ya dunia yote.—Ufunuo 11:15.

6. Tunaweza kutarajia utawala wa aina gani kutoka kwa Mfalme wa Ufalme?

6 Neno la Mungu lasema hivi kuhusu Mtawala mpya wa dunia: “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.” (Danieli 7:14) Kutakuwa na amani na furaha nyingi chini ya utawala wa Yesu kwa kuwa yeye ataiga upendo wa Mungu. (Mathayo 5:5; Yohana 3:16; 1 Yohana 4:7-10) ‘Utawala wake utastawi daima, amani ya utawala wake haitakoma. Atauimarisha kwa haki na uadilifu.’ (Isaya 9:7, Biblia Habari Njema) Itakuwa ni baraka iliyoje kuwa na Mtawala anayetawala kwa upendo, haki, na uadilifu! Kwa hiyo, andiko la 2 Petro 3:13 latabiri: “Ziko mbingu mpya [Ufalme wa mbinguni wa Mungu] na dunia mpya [jamii mpya ya dunia] ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.”

7. Andiko la Mathayo 24:14 linatimizwaje leo?

7 Kwa kweli Ufalme wa Mungu ni habari njema sana kwa wote wapendao yaliyo haki. Hiyo ndiyo sababu Yesu alitoa unabii ufuatao ukiwa sehemu ya ishara kwamba sasa tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa mambo: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:14) Unabii huo unatimizwa sasa, huku Mashahidi wa Yehova wapatao milioni sita wakitumia muda wa saa zaidi ya bilioni moja kila mwaka, katika nchi 234, kuwajulisha wengine Ufalme wa Mungu. Kwa kufaa, majengo yao ya ibada kwa ajili ya makutaniko 90,000 ulimwenguni pote yanaitwa Majumba ya Ufalme. Watu huenda huko kujifunza juu ya serikali mpya inayokuja.

Watawala-Wenzi

8, 9. (a) Watawala-wenzi wa Kristo wanatoka wapi? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani katika utawala wa Mfalme na watawala wenzake?

8 Kristo Yesu atakuwa na watawala wenzi katika Ufalme wa mbinguni wa Mungu. Andiko la Ufunuo 14:1-4 lilitabiri kuwa watu 144,000 ‘wangenunuliwa kutoka miongoni mwa wanadamu’ na kufufuliwa wakaishi mbinguni. Hao hutia ndani wanaume na wanawake ambao, badala ya kutumikiwa, wanamtumikia Mungu na wanadamu wenzao kwa unyenyekevu. “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.” (Ufunuo 20:6) Hao ni wachache zaidi kuliko ule “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” ambao wataokoka mwisho wa mfumo huu. Hao pia humtolea Mungu “utumishi mtakatifu mchana na usiku,” lakini hawana wito wa mbinguni. (Ufunuo 7:9, 15) Wao ndio kiini cha dunia mpya wakiwa raia wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu.—Zaburi 37:29; Yohana 10:16.

9 Alipochagua wale watakaotawala na Kristo mbinguni, Yehova aliteua wanadamu waaminifu ambao walipatwa na shida zote za maisha. Wafalme-makuhani hao wamepatwa pia na yote ambayo yamewapata wanadamu. Hivyo maisha yao duniani yataboresha uwezo wao wa kuwatawala wanadamu. Hata Yesu mwenyewe “alijifunza utii kutokana na mambo aliyoteseka.” (Waebrania 5:8) Mtume Paulo alisema hivi kumhusu: “Tuna kuhani wa cheo cha juu, si mmoja asiyeweza kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali, bali mmoja ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini asiye na dhambi.” (Waebrania 4:15) Inafariji kama nini kujua kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, wanadamu watatawaliwa na wafalme na makuhani wenye upendo na huruma!

Je, Ufalme Ulikuwa Katika Kusudi la Mungu?

10. Kwa nini Ufalme wa mbinguni haukuwa sehemu ya kusudi la awali la Mungu?

10 Je, Ufalme wa mbinguni ulikuwa sehemu ya kusudi la awali la Mungu alipowaumba Adamu na Hawa? Masimulizi ya uumbaji ya kitabu cha Mwanzo hayataji chochote kuhusu ufalme huo ambao ungetawala wanadamu. Yehova mwenyewe alikuwa Mtawala wao. Maadamu wangemtii, hawangehitaji utawala mwingine. Kitabu cha Mwanzo sura ya 1 chaonyesha kwamba Yehova alishughulika na Adamu na Hawa yamkini kupitia Mwana-mzaliwa wake wa kwanza wa mbinguni. Masimulizi hayo yanatumia semi kama “Mungu akawaambia” na “Mungu akasema” nao.—Mwanzo 1:28, 29; Yohana 1:1.

11. Wanadamu walikuwa na mwanzo gani mkamilifu?

11 Biblia yasema: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Kila kitu katika bustani ya Edeni kilikuwa kikamilifu kabisa. Adamu na Hawa waliishi katika paradiso. Walikuwa na akili na miili mikamilifu. Wangeweza kuwasiliana na Mfanyi wao. Na kwa kudumisha uaminifu, wangezaa watoto wakamilifu. Hakungekuwa na uhitaji wa serikali mpya ya mbinguni.

12, 13. Kwa nini Mungu bado angeweza kuwasiliana na wanadamu wakamilifu wakati ambapo wangeongezeka?

12 Wakati ambapo familia ya wanadamu ingeongezeka, Mungu angewasilianaje na wote? Fikiria nyota za mbinguni. Zimepangwa pamoja katika makundi yaitwayo magalaksi. Magalaksi fulani yana nyota bilioni moja. Mengine yana nyota zipatazo trilioni moja. Nao wanasayansi wanakadiria kwamba kuna magalaksi yapatayo bilioni 100 katika anga la juu liwezalo kuonekana! Hata hivyo, Muumba asema: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—Isaya 40:26.

13 Kwa kuwa Mungu anajua nyota hizi zote, kwa hakika haingekuwa vigumu kwake kujua hali ya wanadamu ambao idadi yao ni ndogo zaidi. Hata sasa, mamilioni ya watumishi wake husali kwake kila siku. Sala hizo humfikia Mungu mara moja. Kwa hiyo halingekuwa jambo gumu kwake kuwasiliana na wanadamu wote wakamilifu. Hangehitaji Ufalme wa mbinguni ili kuweza kujua hali yao. Ni mpango bora kama nini—kuwa na Yehova akiwa Mtawala, kuwasiliana naye moja kwa moja, na kuwa na matazamio ya kuishi milele katika dunia iliyo paradiso bila kufa kamwe!

“Si Katika Uwezo wa Mwanadamu”

14. Kwa nini wanadamu watahitaji utawala wa Yehova milele?

14 Hata hivyo, wanadamu—hata walio wakamilifu—wangehitaji utawala wa Yehova milele. Kwa nini? Kwa sababu Yehova hakuwaumba wakiwa na uwezo wa kufanikiwa bila utawala wake. Hilo ni jambo la kawaida kwa wanadamu, kama nabii Yeremia alivyokiri: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu. Ee BWANA, unirudi.” (Yeremia 10:23, 24) Ingekuwa ni upumbavu wanadamu kufikiri kwamba wanaweza kuongoza jamii kwa mafanikio bila kutawaliwa na Yehova. Ingekuwa kinyume cha maumbile yao. Bila shaka, kujitegemea pasipo utawala wa Yehova kungetokeza ubinafsi, chuki, ukatili, jeuri, vita, na kifo. ‘Mtu angekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’—Mhubiri 8:9.

15. Uamuzi mbaya wa wazazi wetu wa kwanza ulikuwa na matokeo gani?

15 Kwa kusikitisha, wazazi wetu wa kwanza waliamua kwamba hawakuhitaji Mungu kuwa Mtawala wao, wakaamua kuishi bila kumtegemea. Kwa sababu hiyo, Mungu hakudumisha ukamilifu wao. Sasa walikuwa kama kifaa cha umeme kilichokatiwa umeme. Kwa hiyo, baadaye wangedhoofika na kufa. Walikuwa kama nakshi yenye kasoro, na hali hiyo ndiyo tu wangeweza kupitishia watoto wao. (Waroma 5:12) “Yeye Mwamba [Yehova], kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. . . . Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao.” (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Ni kweli kwamba Adamu na Hawa walishawishiwa na kiumbe mwasi wa roho ambaye alikuja kuwa Shetani, lakini walikuwa na akili kamilifu na wangeweza kukataa mapendekezo yake mabaya.—Mwanzo 3:1-19; Yakobo 4:7.

16. Historia yatoa ushuhuda gani kuhusu matokeo ya kutomtegemea Mungu?

16 Historia yatoa ushuhuda mkubwa kuhusu matokeo ya kutomtegemea Mungu. Kwa maelfu ya miaka, watu wamejaribu kila aina ya serikali, kila mfumo wa kiuchumi na kijamii. Lakini uovu unaendelea “kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.” (2 Timotheo 3:13) Karne ya 20 ilithibitisha jambo hilo. Ilijawa na chuki mbaya, na jeuri, vita, njaa, umaskini, na mateseko mengi sana ambayo hayajawahi kutokea katika historia. Na hata watu wawe wamefanya maendeleo gani kuhusiana na matibabu, kila mmoja anakufa wakati fulani. (Mhubiri 9:5, 10) Kwa kujaribu kuongoza hatua zao, wanadamu wameacha wanaswe na Shetani na roho wake waovu kiasi cha kwamba Biblia inamwita Shetani “mungu wa huu mfumo wa mambo.”—2 Wakorintho 4:4.

Zawadi ya Hiari

17. Zawadi ya Mungu ya hiari ingetumiwaje?

17 Kwa nini Yehova angewaruhusu wanadamu wafanye watakavyo? Kwa sababu aliwaumba wakiwa na zawadi ya ajabu ya hiari, uhuru wa kuchagua. “Iliko roho ya Yehova, kuna uhuru,” akasema mtume Paulo. (2 Wakorintho 3:17) Hakuna mtu ambaye angependa kufanya mambo bila kufikiri, akiacha mtu mwingine amwamulie kila wakati atakayosema na kufanya. Lakini Yehova alitaka wanadamu watumie zawadi hiyo ya hiari kwa kuwajibika, waone hekima ya kufanya mapenzi yake na kudumu wakiwa watiifu kwake. (Wagalatia 5:13) Kwa hiyo uhuru haungekuwa bila mipaka, kwa kuwa jambo hilo lingetokeza machafuko. Sheria njema za Mungu zingetumiwa kudhibiti uhuru huo.

18. Mungu amedhihirisha nini kwa kumruhusu mwanadamu atumie uhuru wa kuchagua?

18 Kwa kuiruhusu familia ya wanadamu ifanye itakavyo, Mungu amedhihirisha, mara moja kwa wakati wote kwamba tunahitaji utawala wake. Njia yake ya kutawala, enzi kuu yake, ndiyo njia pekee iliyo ya haki. Inatokeza furaha kubwa sana, uradhi, na ufanisi. Sababu ni kwamba akili na miili yetu zilibuniwa na Yehova kwa njia ya kwamba zinafanya kazi vema zaidi zinapotumiwa kupatana na sheria zake. “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” (Isaya 48:17) Uhuru wa kuchagua haungekuwa jambo gumu ukitumiwa kupatana na sheria za Mungu, badala yake ungetokeza vyakula mbalimbali vitamu, makao, sanaa, na muziki. Ikitumiwa vizuri, sikuzote hiari ingetokeza maisha mazuri yenye kupendeza sana katika dunia paradiso.

19. Mungu anatumia nini kupatanisha wanadamu naye?

19 Kwa sababu ya kuchagua vibaya, wanadamu walijitenga na Yehova, wakawa wasiokamilika, wenye kudhoofika, na kufa. Kwa hiyo wangehitaji kukombolewa kutokana na hali hiyo yenye kusikitisha na kurudishwa kwenye uhusiano ufaao pamoja na Mungu wakiwa wana na binti zake. Mungu alitumia Ufalme kutimiza jambo hilo, naye Yesu Kristo ndiye Mkombozi. (Yohana 3:16) Kupitia mpango huo, wale ambao wametubu kikweli—kama mwana mpotevu katika mfano wa Yesu—watapatanishwa na Mungu na kukubaliwa tena kuwa watoto wake.—Luka 15:11-24; Waroma 8:21; 2 Wakorintho 6:18.

20. Kusudi la Mungu litatimizwaje na Ufalme?

20 Bila shaka, mapenzi ya Yehova yatatimizwa duniani. (Isaya 14:24, 27; 55:11) Kupitia Ufalme wake chini ya Kristo, Mungu atatetea (atathibitisha) haki yake ya kuwa Mwenye Enzi Kuu wetu. Ufalme huo utakomesha utawala wa wanadamu na roho waovu juu ya dunia, nao pekee utawale kutoka mbinguni kwa miaka elfu moja. (Waroma 16:20; Ufunuo 20:1-6) Lakini ubora wa njia ya Yehova ya kutawala utadhihirishwaje wakati huo? Na baada ya miaka elfu, Ufalme utakuwa na wajibu gani? Makala inayofuata itazungumzia maswali hayo.

Mambo ya Kupitia

• Kichwa kikuu cha Biblia ni nini?

• Ni nani wanaofanyiza utawala mpya wa dunia?

• Kwa nini utawala wa wanadamu bila kumtegemea Mungu hauwezi kamwe kufanikiwa?

• Hiari yapasa kutumiwaje?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mafundisho ya Yesu yalikazia utawala wa Mungu kupitia Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mashahidi wa Yehova hufanya Ufalme kuwa fundisho lao kuu katika kila nchi

[Picha katika ukurasa wa 14]

Historia yatoa ushuhuda kuhusu matokeo mabaya ya kutomtegemea Mungu

[Hisani]

Askari wa WWI: U.S. National Archives photo; kambi ya mateso: Oświęcim Museum; mtoto: UN PHOTO 186156/J. Isaac